Ni Jambo Gani Linalopata Maisha ya Jamaa?
“TAFADHALI nisaidieni. Mume wangu ananitenda vibaya nami sasa nashindwa kuvumilia. Sina mtu wa kuendea anisaidie. Sina mtu mwingine wa kushinda naye isipokuwa mwana wangu mwenye umri wa mwaka mmoja. Mume wangu ni mtu wa hasira kali-kali na nyakati nyingine mikono yangu imegeuka rangi kwa kunipiga ngumi. Majuma mawili yaliyopita alinigonga kwa kichwa puani nikatokwa na damu nyingi. Kisha usiku mmoja tulipokuwa kitandani akaanza kuninyonga, halafu nilipozimia ndipo tu alipotambua amefanya nini. Ikawa vigumu kwangu kumeza vitu muda wa siku nyingi. . . .
“Mume wangu ananipiga kwa ukawaida na kuvunja vitu ndani ya nyumba na kumshtua mtoto wetu mchanga. Mume wangu alipokwisha kuniangusha sakafuni usiku mmoja, mtoto alipiga ukelele kwa hofu nami nikawa nimeumia na kushtuka mno nisiweze kufanya lo lote. . . . Nimemwambia mume wangu nataka talaka. Sasa sijaribu kusema nataka kwenda au sivyo maana nikifanya hivyo yeye anaanza mambo yake nami naogopa kwamba uhai wangu au wa mwanangu umo hatarini.”—Kutoka kitabu Scream Quietly or the Neighbours Will Hear (Lia Polepole au Sivyo Jirani Watasikia), cha Erin Prizzey.
Hicho ni kisa cha mahali pamoja tu? Hata kidogo! Inakadiriwa kwamba katika United States (Amerika) peke yake, kila mwaka wake karibu milioni 1.8 wanapigwa na waume wao, yaani, wanapigwa mateke, wanaumwa, wanapigwa ngumi, wanagongwa kwa kitu fulani, wanatishwa au kushambuliwa kwa kisu au bunduki. Ukiongeza kwenye mambo hayo visa vya kutumia watoto vibaya katika ngono na kutokujali maoni yao ya moyoni, kuwatumia vibaya wazazi, mababu na nyanya, utaona hali ikionekana kuwa ya kusikitisha zaidi. Kwa hiyo, ulizo hili linatokea: Ni jambo gani linalopata maisha ya jamaa?
Kuna sababu ya kukufanya utake kujua. ‘Kwa sababu gani mimi? ’ huenda ukauliza. ‘Mimi nakuambia kweli kwamba mambo hayo hayatendeki katika jamaa yangu! ’ Hata hivyo, matatizo hayo ya jamaa yanapasa kufikiriwa nawe. Kwa sababu gani? Kwa sababu zamani za kale Biblia ilitabiri kwamba kuwako kwa mambo hayo yenye kuvuruga jamaa kungekuwa sehemu ya ushuhuda wa kuonyesha wazi kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu mzima wa mambo ya ulimwenguni pote.a Angalia aliyotabiri mtume Paulo: “Ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, . . . wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao.”—2 Timotheo 3:1-3.
Kweli maneno ya Paulo yanatimizwa leo? Ugomvi ulio katika jamaa ni wa kadiri gani? Je! umetosha kuunga mkono utimizo wa unabii wa Paulo unaoonyesha kwamba kweli tunaishi katika “siku za mwisho”?
[Maelezo ya Chini]
a Na iangaliwe kwamba unabii mbalimbali wa Biblia unaohusu “siku za mwisho” unajumlika pamoja kuwa ishara yenye mambo mengi ndani yake. Ndiyo kusema, wakati mambo yote yaliyotabiriwa yangepata kizazi kimoja, huo ungekuwa uthibitisho wa kwamba tunaishi katika wakati wa mwisho. Katika mfululizo wa makala hizi, tutakaza fikira juu ya upande mmoja wa unabii mbalimbali, yaani, matokeo ya ‘nyakati zetu za hatari’ juu ya jamaa.