Je! Mambo Yaliyotimizwa na Wanadamu Yanaweza Kuondosha Msiba?
“Kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.”—YEREMIA 10:23.
1, 2. Ni nini mengine ya mambo yaliyotimizwa na wanadamu katika karne hii ya 20?
KATIKA karne yetu ya 20, wanadamu wametimiza mambo ya kustaajabisha. Maendeleo makubwa yamefanywa katika elimu, katika sayansi, na katika mambo ya kiufundi. Leo watu wengi wanavuna faida za jambo hilo katika maisha zao za kila siku. Katika nchi mbalimbali kuna vitu vingi vya kisasa vinavyorahisisha maisha, kama taa za umeme ndani ya nyumba, mabomba yenye kuleta maji na vyombo vingine vyenye mafaa. Pia, sayansi ya tiba inasaidia kuzuia magonjwa fulani yaliyokuwa mapigo makubwa, kama ugonjwa wa ndui.
2 Mawasiliano na usafirishaji, pia, yamekuwa na maendeleo makubwa. Kwa kutumia simu, motakaa, magari-moshi, na ndege tunawasiliana au kufika tunakokwenda kwa haraka kuliko vile baba zetu wa zamani walivyowazia. Leo, matukio yanayotendekea upande ule mwingine wa dunia yanaweza kujulishwa kwetu mara iyo hiyo kwa kutumia vyombo vya angani vya upashaji-habari.
Mambo ya Lazima Yasiyotimizwa
3, 4. Ni mambo gani ya maana sana ambayo wanadamu hawajatimiza, kama ilivyotabiriwa kwa usahihi katika unabii wa Biblia?
3 Hata hivyo, msiba wenye kuletwa na silaha za nyukilia unatisha-tisha daima kuangukia wanadamu, na kuna mambo ya lazima kabisa ambayo wanadamu hawajaweza bado kutimiza. Kwa mfano, je! maendeleo katika elimu yameleta maendeleo pia katika kuelimisha watu wawe wanyofu zaidi, wasema-kweli zaidi, na wenye kufuata zaidi maadili? Katika United States (Amerika), kodi inayoepwa kulipwa kwa kutumia udanganyifu ni dola zaidi ya bilioni 100 kila mwaka. Katika nchi nyingine, katika jiji moja tu, maafisa wa polisi 17,000 wanasemwa kuwa waliondolewa kazini kwa sababu ya ufisadi muda wa miaka saba. Udanganyifu huo unakumbusha mtu unabii wa Biblia kwenye 2 Timotheo sura ya 3 ambapo unatabiri kwamba katika “siku za mwisho” hizi watu wangekuwa ‘wenye kujipenda wenyewe, wapenda fedha, wasio safi [wasio washikamanifu, NW], wasiopenda mema.’
4 Halafu kuna uchafu wa mambo ya ngono. Uzinzi na uasherati unafanywa sana hivi kwamba katika mahali pengi si kawaida kuona jamaa zinazofuata maadili zikionyeshwa katika sinema, vipindi vya televisheni, michezo ya kuigizwa, au vitabu vya hadithi. Na uchafu wa mambo ya ngono kila mwaka unasababisha wanawake karibu milioni 55 kutoa mimba ulimwenguni pote! Huo ni uharibifu wa idadi ya watu iliyo kubwa kuliko ile ya Kenya, au Tanzania, au Zaire, au Uganda, au mataifa mengine 145—kila mwaka! Kwa hiyo ingawa tawi moja la sayansi ya tiba linashangilia maendeleo yanayookoa maisha ya watoto wengine, tawi jingine la sayansi ya tiba linaua mamilioni ya wengine wasiozaliwa. Sawa na vile Biblia ilivyotabiri, katika “siku za mwisho” hizi watu wengi ni “wasiojizuia” na “wasiowapenda wa kwao.”—2 Timotheo 3:3.
5. Matokeo ya afya yamekuwa nini kwa sababu ya uasherati ulioenea sana leo?
5 Uasherati unaleta kipuku cha magonjwa yanayoambukia watu wanapofanya ngono za ovyoovyo. Namna nyingi za magonjwa hayo sasa zinashinda nguvu za dawa. Ugonjwa ule ulioenea kote kote wa malengelenge ya ngozi katika viungo vya uzazi hauna dawa ya kuutibu mpaka sasa. Tena kuna ongezeko kubwa sana katika hesabu ya watoto wachanga walio nao. Wanaupata kwa akina mama walioambukiwa. Karibu nusu ya watoto hao wanakufa, na kati ya wale wengine wanaobaki, nusu yao wanakuwa na madhara ya mwili au akili. Wala maponyo hayajapatikana mpaka sasa kwa ugonjwa wa AIDS (mchanganyiko wa viini vibaya vinavyoondoa nguvu za mwili za kujikinga na magonjwa), ugonjwa unaoua ambao umeduwaza madaktari wasijue la kufanya. AIDS umetokea katika nchi zisizopungua 33 “na sasa ni tisho kwa afya duniani pote,” kinasema kichapo Associated Press. Umewapata hasa watu wanaolalana na wengine wa jinsia yao, hiyo ikikumbusha mtu Warumi 1:27.
6. Je! sayansi ya tiba imezuia ongezeko la magonjwa katika sehemu zote za ulimwengu?
6 Sayansi ya tiba haiwezi kukomesha ongezeko kubwa la magonjwa mengine mengi. Katika Afrika peke yake, mamilioni ya watu wana maleria, ugonjwa wa malale, ukoma, na magonjwa mengine. Katika mataifa yenye maendeleo kansa, ugonjwa wa moyo, ugonjwa wa sukari, kufura ini, na magonjwa mengi yanayotokana na hali zinazovuruga maoni ya moyoni yanaongezeka. Mengine ya hayo yanaletwa, au kuzidishwa, na mahangaiko au madhara yasiyotazamiwa yanayosababishwa na jamii ya kisasa yenye viwanda. Mengine yanatokana na maisha ya kuachilia watu waishi vyo vyote tu watakavyo.
7. Je! inaelekea kuwa kwamba maendeleo katika elimu ya tiba yangeweza kutuweka katika afya nzuri milele?
7 Kama magonjwa mengi zaidi yangezuiwa, je! sayansi ya tiba ingetuweka katika afya nzuri milele? Wanasayansi wengi wanasema, Hapana. Wanaonyesha kwamba ingawa huenda urefu wa maisha ukaongezwa kwa miaka michache, magonjwa mengine yangepata nguvu yaue watu wengi. Mwanasayansi mmoja alikata maneno hivi: “Hakuna uwezekano mkubwa wa kwamba tutaongeza sana muda wa kuishi au tuahirishe uzee hivi karibuni.” Zamani za kale Biblia ilisema hivi kwa usahihi kwenye Zaburi 90:10: “Siku za miaka yetu ni miaka sabini, na ikiwa tuna nguvu miaka themanini; na kiburi chake ni taabu na ubatili, maana chapita upesi tukatokomea mara.”
Tatizo la Umaskini Halijatatuliwa
8. Biblia ilitabirije kwa usahihi kwamba elimu ya ufundi haingetatua tatizo la umaskini?
8 Ni kweli kwamba elimu ya ufundi imefanya maisha yawe rahisi zaidi kwa watu wengi. Lakini wengine wengi hawana pesa za kutosha kununua bidhaa zinazotokana na ufundi wenyewe. Kichapo World Military and Social Expenditures 1983 kilitaarifu hivi: “Watu 2,000,000,000 wanaishi kwa kutegemea mapato yaliyo chini ya dola 500 [za United States] kwa mwaka.” Kiliendelea kusema: “Mtu asiyepungua mmoja kati ya watano amenaswa katika umaskini wa kupindukia, hali ya ufukara mwingi sana hivi kwamba huo unakuwa uuaji wa watu wengi pole kwa pole.” Halafu kichapo hicho kikasema kwamba kila mwaka “watoto wachanga 11,000,000 wanakufa kabla ya kuishi mwaka mmoja,” sababu ikiwa ni ukosefu wa chakula kinachofaa au ugonjwa.—Ufunuo 6:5-8.
9. Ni hali gani ya kuhuzunisha iliyo katika nchi nyingi?
9 Katika nchi fulani-fulani, linasema gazeti The Detroit News, “wanawake wengi wanajikuta wakiwa na watoto wengi mno bila njia ya kuwatunza. . . . Mara nyingi mno, akina mama wa namna hiyo wanamtupa mtoto ambaye hawamtaki . . . barabarani.” Kuna mamilioni ya watoto wa namna hiyo. Mahali pengine, watoto wanaacha wazazi wakiwa peke yao. Mwandikaji mmoja wa habari za jarida katika Esia anasema: “Maelfu ya watu wazee wanakatazwa kukaa katika nyumba zao kwa sababu jamaa zao haziwezi kuendelea kuwalisha. Hakuna mashirika yanayotolea watu msaada wa pesa. Mara nyingi watoto wa wazee hao wanawapandisha gari-moshi kisha wanawashushia mahali fulani au wanawaacha kwenye vituo vya magari-moshi.” Mwandikaji huyo anaongeza hivi: “Hilo ni badiliko la kushtua sana katika utamaduni uliokuwa ukiheshimu sana wazee-wazee.” Kwa hiyo kizazi chetu kinaona ukweli wa andiko la Mithali 30:11, linalosema: “Kuna kizazi cha watu wamlaanio baba yao; wala hawambariki mama yao.”
10. Hali ya kiuchumi ya ulimwengu ina usalama, na hiyo inakumbusha mtu unabii gani wa Yesu?
10 Serikali za kibinadamu haziwezi kutatua tatizo la umaskini wa duniani pote. Nchi zinazositawi zinalemewa na mzigo mzito wa madeni yenye kuongezeka zisiyoweza kulipa. Hata nchi zilizositawi zina madeni mengi mno. Kuonyesha hivyo, benki nyingi zilifilisika katika United States (Amerika) mwaka jana. Wakati moja ya zilizo kubwa zaidi ilipoelekea kufilisika, serikali tu ndiyo iliyoiokoa kwa kuipa mabilioni ya dola. Ilihofiwa kwamba kama benki kubwa namna hiyo ingefilisika, “ambukizo lingalienea kwenye benki zile nyingine pia, hivyo mfumo mzima wa kifedha uwe hatarini,” likaripoti gazeti The New York Times. Hivyo, inazidi kuwa vigumu kuondosha kando msiba. Kwa kweli, kila mwaka unapoendelea kupita maoni ya gazeti Guardian la Uingereza yanapata nguvu zaidi: “Ulimwengu uko karibu na maangamizi ya kibinadamu na msiba wa kisiasa. . . . Bara nzima-nzima zimeona matumaini yao kwa wakati ujao yakitoweka.”—Luka 21:25, 26.
Matokeo ya Elimu ya Ufundi Juu ya Vita
11. Ni tatizo gani jingine ambalo serikali haziwezi kutatua limeongezwa na elimu ya ufundi?
11 Elimu ya ufundi imeharibu zaidi jambo jingine ambalo serikali haziwezi kukomesha: vita. Elimu ya ufundi ndiyo iliyofanya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilete machinjo makubwa ya kutumia sana bunduki zenye kumimina risasi kama maji, nyambizi (sabmarini), ndege za vita, vifaru, na silaha za kutupia watu moto. Mtungaji Mwingereza Richard Rees alisema: “Vita ya 1914-1918 ilifunua wazi mambo mawili: kwanza, kwamba elimu ya ufundi ilikuwa imefikia kiasi ambacho ingeweza kuendelea bila msiba katika ulimwengu wenye umoja peke yake na, pili, kwamba matengenezo ya kisiasa na ya kijamii yaliyo katika ulimwengu yalifanya umoja huo usiwezekane.” Vita ya Ulimwengu ya Pili ilithibitisha maneno yake, kwa kuwa silaha mpya zaidi ziliua watu karibu milioni 55.
12. Ni matisho gani yanayoelekea jamaa ya kibinadamu leo?
12 Leo silaha za vita zinatisha zaidi, na serikali hazina umoja hata kidogo. Kwa habari ya silaha za nyukilia, mtungaji Herman Wouk alisema: “Ustadi, kazi, na hazina zinazotumiwa kwa wingi juu ya . . . uwazimu huu hakika zinastaajabisha sana. Kama mataifa hayangejifunza vita tena kamwe, hakuna jambo ambalo wanadamu hawangeweza kufanya.” Mchunguzi wa anga za juu Carl Sagan alisema hivi juu ya vita ya nyukilia: “Hakuna shaka kwamba ustaarabu wetu wa duniani pote ungeharibiwa.” Na wakati msiba huo wa duniani pote unapoelekea sana kupata jamaa ya kibinadamu, mapigano mengine mengi yanaua watu wasiohesabika. Makao ya Habari za Ulinzi katika United States yaliripoti kwamba mwaka wa 1984 vita mbalimbali na maasi 42 yalikuwa yakiendelea wakati ule ule mmoja! Serikali haziwezi hata kukomesha wimbi la uhalifu na jeuri katika nchi zao zenyewe, achia mbali kuleta amani ya duniani pote.
13. Je! jeuri iliyo duniani pote katika wakati wetu inalingana na unabii wa Biblia?
13 Hayo yote yanalingana na unabii kwenye Ufunuo 6:4 juu ya uendeshaji wa mmoja wa wale ‘wapanda-farasi wanne wa kitabu cha Ufunuo’ tangu mwaka wa 1914: “Akatoka farasi mwingine, mwekundu sana, na yeye aliyempanda alipewa kuiondoa amani katika [dunia], ili watu wauane, naye akapewa upanga mkubwa.”
Sababu ya Jitihada za Kibinadamu Kushindwa
14, 15. Ni nini sababu moja kubwa inayofanya wanadamu wasiweze kutimiza shabaha zao sasa?
14 Kwa nini kuna sababu ya kuogopa kwamba mambo yaliyotimizwa na wanadamu hayataondosha kando msiba? Kwa kweli, mbona wanadamu hawawezi kutimiza shabaha zao? Biblia inaonyesha sababu moja kubwa: “Kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.” (Warumi 5:12) Wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, waliumbwa wakiwa wakamilifu katika mwili na akili. Lakini ukamilifu huo ulitegemea kubaki kwao katika mipaka ya sheria za Mungu zenye kuwafaidi. Ndani ya sheria hizo walipewa uhuru mwingi wa hiari. Lakini Mwanzo sura ya 3 inaonyesha kwamba wazazi wetu wa kwanza waliruka mipaka ya uhuru wa hiari. Walitamani waache kumtegemea Mungu na sheria zake, kutaka kujiamulia wenyewe mema na mabaya, hali ni Mungu tu mwenye mamlaka ya kufanya hivyo. Baada ya wao kufanya uchaguzi huo, waliachwa wajitegemee. Biblia inasema: “[Yehova] yu pamoja nanyi, mkiwa pamoja naye; . . . lakini mkimwacha atawaacha ninyi.” (2 Mambo ya Nyakati 15:2) Wakiwa wametenganishwa na Mungu, Adamu na Hawa walianza kudhoofika. Magonjwa, huzuni, na mwishowe kifo kikawafikia.—Mwanzo 2:16, 17.
15 Baada ya wazazi wetu wa kwanza kupoteza ukamilifu, sheria za urithi katika chembe za mwili zilihakikisha kwamba wazao wao walirithi kutokamilika. Mtunga zaburi alikiri hivi: “Mimi naliumbwa katika hali ya uovu; mama yangu alinichukua mimba hatiani.” (Zaburi 51:5) Hakuna njia iwayo yote ambayo sayansi ya tiba inaweza kushinda matokeo ya kutokamilika kulikorithiwa. Kutafuta njia ya tiba ya kuondoa magonjwa na kifo ni kutafuta kitu ambacho wanadamu hawawezi kutimiza—hata wafanye nini.
16. Hali ya kutokamilika imehusuje hali ya akilini ya wanadamu?
16 Kutokamilika kulikorithiwa kunaipata pia hali yetu ya akilini. Sote tumezaliwa tukiwa na maelekeo ya kufanya ubaya. Sasa, hiyo haimaanishi kwamba wanadamu hawawezi kuongoza vitendo vyao. Wanaweza wakichukua hatua za kujirekebisha. Andiko la Mithali 3:6 linaonyesha hivyo, likisema: “Katika njia zako zote mkiri yeye [Yehova], naye atayanyosha mapito yako.” Lakini, wakati wanadamu wanapopuuza marekebisho mazuri wanayopewa, basi hapo wanaingia katika matata makubwa. Na kadiri watu mmoja mmoja na mataifa wanavyozidi kuacha sheria za Mungu, ndivyo wanavyotenda kwa uharibifu zaidi, wa kukuza maelekeo ya kichoyo waliyozaliwa nayo. Kwa habari hiyo makala ya mhariri ya gazeti New York Times ilisema: “Hata unapotupia jicho vichwa vya magazeti leo kwa kiasi kidogo tu, unashangaa ulimwengu unaelekea wapi. . . . Ona vile inavyokuwa wakati wanadamu, vyama na mataifa wanapoweka faida zao za kichoyo mbele ya kila kitu kingine. . . . Uhakika ulio wazi katika nchi zote ni kwamba kufanya uchoyo hakuna mafanikio.”
Mavutano ya Kishetani
17, 18. Ni jambo gani jingine kubwa linalosaidia kueleza sababu inayofanya wanadamu wasiweze kutimiza shabaha zao?
17 Jambo jingine kubwa linalosaidia kueleza kwa nini wanadamu hawawezi kutimiza shabaha zao na kuondosha kando msiba ni mavutano yaliyoandikwa kwenye (2 Wakorintho 4:4 NW), ambapo panasema juu ya “mungu wa huu mfumo wa mambo.” Huenda watu fulani wasiofahamu sana habari za Biblia wakafikiri kwamba mungu anayetajwa hapo ni Mungu Mweza Yote. Lakini mstari uo huo unaongeza kwamba mungu huyo “amepofusha akili za wasio waamini.” Kwa uhakika, Muumba mwenye upendo hangefanya hivyo. Mungu anayetajwa ndiye yule yule anayesemwa kwenye 1 Yohana 5:19 (NW) panaposema: “Ulimwengu mzima uko katika nguvu za yule mwovu.”
18 Mungu anayeongoza ulimwengu huu wa sasa anatambulishwa kwenye Ufunuo 12:9 kuwa “aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote.” Jina Shetani linamaanisha “Mpinzani” au “Hasimu.” Jina Ibilisi linamaanisha “Mshitaki wa uwongo,” au “Mchongezi.” Hayo ni maneno yanayofaa, kwa maana uasi wa Adamu na Hawa ulichochewa na mwasi huyo akiwa katika makao ya kiroho. Yeye ndiye aliyeambia Hawa jambo kama hili: ‘Huna haja ya kutii sheria za Mungu. Unaweza kujiamulia mwenyewe lililo jema na lililo kosa.’ Lakini, kwa kujiondoa upande wa Mungu, Shetani akawa na akili yenye kukosa adili. Hilo linaweza kuonekana kutokana na kazi zake, kwa maana ebu tazama jinsi ulivyo ulimwengu anaouongoza! Historia mbovu na isiyopendeza ya wanadamu inathibitisha kwamba kuna uvutano mbovu unaoongoza ulimwengu.
Kuna Tumaini Gani?
19. Watazamaji wengine wamependekeza nini kuwa dawa za matatizo ya ulimwengu huu?
19 Watu fulani wenye kuutazama ulimwengu huu uliovurugika wametoa maoni ya kupendeza juu ya kinachoweza kuwa dawa ya matatizo ya wanadamu. The Gazette la Montreal lilisema: “Karibu vikundi 150 vya wanasiasa wa kitaifa wanaelekeza jitihada zao pande zinazotofautiana, wakielekeza dunia-sayari kwenye mvurugo. Hata hivyo mengi zaidi ya matatizo makubwa ya ulimwengu yanapatikana duniani pote kwa sababu ufundi wa usafirishaji na mawasiliano umefupisha ulimwengu ukawa mtaa mmoja au kijiji kimoja.” Ndipo lilipopendekeza hivi: “Namna fulani ya serikali ya ulimwengu itahitajiwa kabisa.” Erich Fromm aliye mchunguzi wa mambo ya kijamii alisema kwamba mabaya ya ulimwengu huu yanaweza kuondolewa “ikiwa tu mfumo mzima [wa kijamii na kisiasa] ambao umekuwako wakati wa miaka 6000 iliyopita unaweza kubadilishwa na mwingine ulio tofauti kabisa.”—Italiki ni zetu.
20. (a) Ni kwa sababu gani miradi inayotamaniwa haiwezi kufikiwa kwa jitihada za kibinadamu? (b) Inatupasa tutumaini nani kuhusu wakati ujao?
20 Watazamaji hao hawatambui, lakini mfumo mzima wa kijamii na kisiasa kwa uhakika utabadilishwa na “mwingine ulio tofauti kabisa”! Kwa uhakika kutakuwako karibuni serikali ya ulimwengu, moja tu, kwa wanadamu wote. Lakini haitakuja kwa jitihada za kibinadamu. Wanadamu wakiwa peke yao hawawezi kuondosha kando msiba. Hawawezi kubadilisha mfumo huu wa mambo ya sasa walete ulio bora, kama historia ilivyothibitisha. Hawawezi kuondolea mbali kutokamilika kulikorithiwa, magonjwa, na kifo. Tena hawawezi kuondolea mbali Shetani na mashetani wake. Bali, matukio ya kibinadamu ya wakati uliopita yamethibitisha ukweli wa maneno haya yaliyoongozwa na roho ya Mungu: “Kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Hivyo Neno la Mungu linashauri hivi: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake.” (Zaburi 146:3) Basi, inakupasa utumainie nani? Mithali 3:5 inahimiza hivi: “Mtumaini [Yehova] kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe.” Kwa sababu gani tumtumainie Yehova hivyo? Kwa sababu yeye anaweza kufanya asiyoweza mwanadamu, kama vile makala inayofuata itakavyothibitisha.
Maulizo ya Kurudia
◻ Ni mambo gani ya maana kabisa ambayo wanadamu wameshindwa kutimiza?
◻ Elimu ya ufundi imeongezaje madhara ya vita?
◻ Kwa sababu gani jitihada za kibinadamu zinashindwa mara nyingi sana?
◻ Kwa sababu ya matendo ambayo mwanadamu amekuwa nayo muda wote, mwendo wa hekima ni nini?
[Picha katika ukurasa wa 11]
Sayansi ya tiba haikukomesha ongezeko kubwa la magonjwa na kifo
[Picha katika ukurasa wa 12]
Serikali za kibinadamu haziwezi kuondolea mbali umaskini wa duniani pote