Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 4/15 kur. 9-14
  • Imani na Wakati Ujao Wako

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Imani na Wakati Ujao Wako
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wakati Uliopita Ulikuwaje?
  • Hakuna Utatuzi wa Kibinadamu
  • Jinsi Mashahidi wa Yehova Huuona Wakati Ujao
  • Wakati Ujao wa Utawala wa Kibinadamu
  • Weka Imani Katika Ahadi za Yehova
  • Mtumaini Yehova Atimize Kusudi Lake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Karibuni Kusudi la Mungu Kutimizwa
    Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai?
  • Ufalme wa Mungu—Utawala Mpya wa Dunia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Yehova Hutimiza Ahadi Zake kwa Waaminifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 4/15 kur. 9-14

Imani na Wakati Ujao Wako

“Imani ni taraja lililohakikishwa la mambo yatumainiwayo.”—WAEBRANIA 11:1.

1. Watu walio wengi hutaka wakati ujao wa aina gani?

JE, WAPENDEZWA na wakati ujao? Watu wengi wanapendezwa. Watarajialo ni wakati ujao wenye amani, usio na hofu, wenye hali nzuri za kuishi, wenye kazi yenye matokeo na yenye kuonewa shangwe, wenye afya nzuri, na wenye maisha marefu. Bila shaka kila kizazi katika historia kimetaka mambo hayo. Na leo, katika ulimwengu huu uliojaa taabu sana, hali hizo zatamanika zaidi kuliko wakati mwingine wowote.

2. Mwanasiasa mmoja alionyeshaje maoni ya aina moja juu ya wakati ujao?

2 Wanadamu wasongapo kuelekea karne ya 21, je, kuna njia yoyote ya kupambanua jinsi wakati ujao utakavyokuwa? Njia moja ilielezwa na mwanasiasa Mmarekani Patrick Henry zaidi ya miaka 200 iliyopita. Alisema hivi: “Sijui njia nyingineyo ya kuamua kuhusu wakati ujao ila kupitia wakati uliopita.” Kulingana na maoni hayo wakati ujao wa familia ya kibinadamu waweza kujulikana kwa kiwango fulani kwa kutegemea yale ambayo mwanadamu alifanya wakati uliopita. Watu wengi hukubaliana na wazo hilo.

Wakati Uliopita Ulikuwaje?

3. Rekodi ya historia huonyesha nini kuhusu matazamio ya wakati ujao?

3 Ikiwa wakati ujao utafanana na wakati uliopita, je, waona hilo kuwa lenye kutia moyo? Je, wakati ujao wa vizazi vilivyotangulia uliboreka katika enzi zote zilizopita? Kwa kweli sivyo. Yajapokuwa matumaini ambayo watu wamekuwa nayo kwa maelfu ya miaka, na yajapokuwa maendeleo ya vitu vya kimwili katika mahali fulani-fulani, historia imejawa na uonevu, uhalifu, ujeuri, vita, na umaskini. Ulimwengu huu umepatwa na msiba mmoja baada ya mwingine, ambayo imeletwa hasa na utawala wa kibinadamu usiotosheleza. Biblia hutaarifu hivi kwa usahihi: ‘Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.’—Mhubiri 8:9.

4, 5. (a) Kwa nini watu walijawa na matumaini mapema katika karne ya 20? (b) Matumaini yao ya wakati ujao yalipatwa na nini?

4 Jambo lililo la hakika ni kwamba, historia mbaya ya kibinadamu ya wakati uliopita huendelea kujirudia yenyewe—lakini kwa kiwango kikubwa zaidi na chenye kuharibu zaidi. Karne hii ya 20 ni ithibati ya hilo. Je, wanadamu walijifunza kutokana na makosa ya wakati uliopita na kuyaepuka? Mwanzoni mwa karne hii, watu wengi waliamini juu ya wakati ujao ulio bora zaidi kwa sababu kwa kulinganishwa kulikuwa kumekuwa na kipindi kirefu cha amani na kwa sababu ya maendeleo ya kiviwanda, sayansi, na elimu. Mapema miaka ya 1900, akasema profesa wa chuo, iliaminiwa kwamba vita havingewezekana tena kwa sababu, “watu walikuwa wastaarabu sana.” Aliyekuwa waziri mkuu wa Uingereza hapo zamani alisema hivi kuhusu maoni ambayo watu walikuwa nayo nyuma huko wakati huo: “Kila kitu kingeendelea kuwa bora zaidi na zaidi. Huo ndio ulimwengu nilimozaliwa.” Lakini akataarifu hivi: “Ghafula, bila kutazamiwa, asubuhi moja katika 1914 mambo yote yakakoma.”

5 Ijapokuwa wakati huo watu wengi waliamini juu ya wakati ujao ulio bora, karne mpya ilikuwa imeanza tu wakati ambapo ulimwengu ulikumbwa na msiba mkubwa na mbaya zaidi uliopata kutokezwa na watu—Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Kikiwa kielelezo cha hali yake, fikiria kilichotukia mwaka wa 1916 katika pigano moja wakati ambapo vikosi vya Uingereza vilivamia majeshi ya Ujerumani karibu na Mto Somme, Ufaransa. Kwa saa kadhaa tu Uingereza ilipoteza wanajeshi 20,000, na wengi waliuawa upande wa Ujerumani. Katika miaka minne ya uchinjaji, askari wapatao milioni kumi na raia wengi walikufa. Idadi ya watu wa Ufaransa ilipungua kwa muda kwa sababu ya wanaume wengi sana waliokufa. Uchumi mbalimbali uliharibiwa, ukiongoza kwenye Mshuko Mkubwa wa Kiuchumi wa miaka ya 1930. Si ajabu kwamba watu fulani wamesema kwamba siku ambayo Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilianza ndiyo siku ambayo ulimwengu ulipata kichaa!

6. Je, maisha yalipata kuwa afadhali baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza?

6 Je, huo ndio wakati ujao uliotumainiwa na kizazi hicho? Bila shaka la. Matumaini yao yalivunjwa kabisa; wala yote hayo hayakuongoza kwenye jambo lolote bora zaidi. Miaka 21 tu baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, au mwaka wa 1939, msiba mkubwa ulio mbaya hata zaidi uliotokezwa na watu ulianza—Vita ya Ulimwengu ya Pili. Iliua wanaume, wanawake, na watoto wapatao milioni 50. Kulipuliwa kwa mabomu mengi kulibomoa majiji. Katika Vita ya Ulimwengu ya Kwanza maelfu kadhaa ya askari waliuawa katika pigano moja katika muda wa saa kadhaa tu, ilhali katika Vita ya Ulimwengu ya Pili, mabomu mawili tu ya atomu yaliua watu zaidi ya 100,000 katika muda wa sekunde chache tu. Watu waliuona ule mfumo wa uuaji-kimakusudi wa mamilioni ya watu katika kambi za mateso za Nazi kuwa mbaya hata zaidi.

7. Uhalisi wa karne yote hii ni nini?

7 Vyanzo kadhaa vyataarifu kwamba tukitia ndani vita kati ya mataifa, mapambano ya kiraia, na serikali ambazo zimeua raia wake wenyewe, wale waliouawa katika karne hii watajumlika kuwa watu wapatao milioni 200. Hata chanzo kimoja chasema idadi hiyo yapata milioni 360. Wazia chukizo la mambo hayo yote—ule uchungu, yale machozi, yale maumivu makali, na yale maisha yaliyoangamizwa! Kwa kuongezea, kwa wastani, watu wapatao 40,000, hasa watoto, hufa kila siku kutokana na visababishi vihusianavyo na umaskini. Mara tatu ya idadi hiyo huuawa kwa kutoa mimba kila siku. Pia, watu wapatao bilioni moja ni maskini sana hata wasiweze kupata chakula kihitajiwacho ili kufanya kazi ya kawaida ya siku. Hali zote hizo ni uthibitisho wa yale yaliyotabiriwa katika unabii wa Biblia wa kwamba twaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu mwovu wa mambo.—2 Timotheo 3:1-5, 13; Mathayo 24:3-12; Luka 21:10, 11; Ufunuo 6:3-8.

Hakuna Utatuzi wa Kibinadamu

8. Kwa nini viongozi wa kibinadamu hawawezi kutatua matatizo ya ulimwengu?

8 Karne hii ya 20 ikaribiapo mwisho wake, twaweza kuongezea mambo ambayo yameipata kwa yale ya karne zilizotangulia. Nayo historia hiyo yatuambia nini? Yatuambia kwamba viongozi wa kibinadamu hawajapata kamwe kutatua matatizo makubwa ya ulimwengu, kwamba hawayatatui sasa, na kwamba hawatayatatua wakati ujao. Hawana uwezo wa kuandaa aina ya wakati ujao tunaotaka, hata wawe na makusudio mazuri kama nini. Na baadhi ya watu wenye mamlaka hawana makusudio mazuri; watafuta nyadhifa na mamlaka ili kupata sifa na mali wala si kwa manufaa ya wengine.

9. Kwa nini kuna sababu ya kushuku kwamba sayansi ina majibu kwa matatizo ya mwanadamu?

9 Je, sayansi ina majibu? La, tukichunguza wakati uliopita. Wanasayansi wa serikali wametumia fedha, wakati, na jitihada nyingi wakitengeneza silaha za kikemikali, za kibiolojia, na za aina nyinginezo zenye kusababisha uharibifu mbaya sana. Mataifa, kutia na yale yaliyo maskini zaidi, hutumia dola bilioni 700! Pia, ‘maendeleo ya kisayansi’ yalaumika kwa kadiri fulani kwa sababu ya zile kemikali ambazo zimechangia kuchafuliwa kwa hewa, ardhi, maji, na chakula.

10. Kwa nini hata elimu haihakikishii wakati ujao ulio bora?

10 Je, twaweza kutarajia kwamba mashirika ya kielimu ya ulimwengu yatasaidia kujenga wakati ujao ulio bora zaidi kwa kufundisha viwango vya juu zaidi vya maadili, kuwafikiria wengine, na kupenda jirani? La. Badala ya hivyo, hayo hukazia kazi-maisha, kupata fedha. Hukuza roho kubwa sana ya ushindani, wala si ya kushirikiana, wala shule hazifundishi maadili. Badala ya hivyo, nyingi za shule hizo huruhusu uhuru wa kingono, ambao umetokeza ongezeko kubwa la mimba za utineja na maradhi ya kuambukiza kingono.

11. Rekodi ya shughuli za kibiashara zatokezaje shaka juu ya wakati ujao?

11 Je, biashara kubwakubwa za ulimwengu zitachochewa ghafula kutunza vizuri sayari yetu na kuwaonyesha wengine upendo kwa kutengeneza bidhaa ambazo zitakuwa za manufaa ya kweli wala si kwa ajili ya faida tu? Haielekei kuwa hivyo. Je, wataacha kutayarisha vipindi vya televisheni vyenye kujaa ujeuri na ukosefu wa adili ambavyo huchangia kufisidi akili za watu, hasa vijana? Wakati wa karibuni ambao umepita hautii moyo hata kidogo, kwa sababu, kwa sehemu iliyo kubwa, televisheni imejaa ukosefu wa adili, na ujeuri.

12. Binadamu wana hali gani kuhusiana na ugonjwa na kifo?

12 Zaidi ya hayo, hata madaktari wawe wenye moyo mweupe kama nini, hawawezi kushinda ugonjwa na kifo. Mathalani, mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, hawakuweza kuzuia kuenea kwa homa ya Kihispania; iliua watu wapatao milioni 20 ulimwenguni pote. Leo, maradhi ya moyo, kansa, na magonjwa mengine yenye kuua yameenea sana. Wala ulimwengu wa kitiba haujashinda tauni ya kisasa ya UKIMWI. Kinyume cha hilo, ripoti ya Umoja wa Mataifa iliyotangazwa hadharani Novemba 1997 ilikata kauli kwamba kiwango ambacho kirusi cha UKIMWI chaenea ni maradufu ya makadirio ya wakati uliopita. Tayari, mamilioni ya watu wamekufa kutokana na UKIMWI. Katika mwaka wa majuzi, watu wengine milioni tatu waliambukizwa.

Jinsi Mashahidi wa Yehova Huuona Wakati Ujao

13, 14. (a) Mashahidi wa Yehova huuonaje wakati ujao? (b) Kwa nini wanadamu hawawezi kutokeza wakati ujao ulio bora?

13 Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova huamini kwamba wanadamu wana wakati ujao mwangavu, ulio bora kabisa! Lakini hawatarajii wakati ujao huo ulio bora zaidi uje kupitia jitihada za kibinadamu. Badala ya hivyo, wao humtegemea Muumba, Yehova Mungu. Yeye ajua wakati ujao utakuwaje, nao utakuwa wa ajabu! Ajua pia kwamba wanadamu hawawezi kuleta wakati ujao kama huo. Kwa kuwa Mungu aliwaumba, ajua mipaka yao zaidi ya mtu mwingine yeyote. Katika Neno lake, atuambia waziwazi kwamba hakuwaumba wanadamu wakiwa na uwezo wa kutawala kwa mafanikio bila uongozi wa kimungu. Mungu amewaruhusu wanadamu watawale kwa muda mrefu bila kumtegemea. Kufanya hivyo kumedhihirisha pasipo shaka kwamba hawezi kutawala bila kumtegemea Mungu. Mtungaji mmoja alikiri hivi: “Akili ya mwanadamu imejaribu aina zote ziwezekanazo za serikali, nayo imefanya hivyo kwa ubatili.”

14 Kwenye Yeremia 10:23, twasoma maneno haya ya nabii aliyepuliziwa: “Ee BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” Pia, Zaburi 146:3 hutaarifu hivi: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake.” Kwa hakika, kwa sababu sisi huzaliwa tukiwa wasio wakamilifu, kama vile Waroma 5:12 huonyesha, Neno la Mungu hutuonya tusijitumainie hata sisi wenyewe. Yeremia 17:9 husema hivi: “Moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha.” Kwa sababu hiyo, Mithali 28:26 hujulisha hivi: “Mwenye kujitumainia moyo wake ni mjinga; bali yeye aendaye kwa busara ataokolewa.”

15. Twaweza kupata wapi hekima ya kutuongoza?

15 Twaweza kupata wapi hekima hiyo? “Kumcha BWANA ni mwanzo wa hekima; na kumjua Mtakatifu ni ufahamu.” (Mithali 9:10) Yehova tu ndiye aliye na hekima iwezayo kutuongoza katika nyakati hizi zenye kutia hofu. Naye ametupatia uwezo wa kupata hekima yake kupitia kwa Maandiko Matakatifu, ambayo yamepuliziwa ili yatuongoze.—Mithali 2:1-9; 3:1-6; 2 Timotheo 3:16, 17.

Wakati Ujao wa Utawala wa Kibinadamu

16. Ni nani ambaye ameamua juu ya wakati ujao?

16 Neno la Mungu hutuambia nini juu ya wakati ujao? Hutuambia kwamba bila shaka wakati ujao hautadhihirisha mambo ambayo wanadamu wamefanya wakati uliopita. Kwa hiyo maoni ya Patrick Henry yalikuwa yenye kosa. Wakati ujao wa dunia hii na wa watu walio duniani utaamuliwa na Yehova Mungu, wala si wanadamu. Mapenzi yake yatafanywa duniani, wala si mapenzi ya wanadamu wowote au mataifa yoyote ya ulimwengu huu. “Mna hila nyingi moyoni mwa mtu; lakini shauri la BWANA ndilo litakalosimama.”—Mithali 19:21.

17, 18. Mapenzi ya Mungu kwa wakati wetu ni nini?

17 Mapenzi ya Mungu kwa wakati wetu ni nini? Amekusudia kukomesha mfumo wa mambo uliopo wenye ujeuri, na usio wa adili. Karibuni mahali pa utawala mbaya wa karne nyingi wa kibinadamu patachukuliwa na utawala uliofanyizwa na Mungu. Unabii kwenye Danieli 2:44 hutaarifu hivi: “Katika siku za wafalme hao [walioko leo] Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme [mbinguni] ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” Ufalme huo pia utaondoa uvutano mwovu wa Shetani Ibilisi, jambo ambalo wanadamu hawawezi kamwe kufanya. Utawala wake wa dunia hii utakoma milele.—Waroma 16:20; 2 Wakorintho 4:4; 1 Yohana 5:19.

18 Ona kwamba serikali hiyo ya kimbingu itaharibu aina zote za utawala wa kibinadamu. Na kazi ya kutawala dunia hii hawataachiwa tena kamwe wanadamu. Wale wafanyizao Ufalme wa Mungu mbinguni, wataongoza mambo yote ya kidunia kwa faida ya wanadamu. (Ufunuo 5:10; 20:4-6) Duniani, wanadamu waaminifu watashirikiana na mielekezo ya Ufalme wa Mungu. Huo ndio utawala ambao Yesu alitufundisha kusali kwa ajili yao aliposema hivi: “Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.”—Mathayo 6:10.

19, 20. (a) Biblia hufafanuaje mpango wa Ufalme? (b) Utawala wake utafanyia wanadamu nini?

19 Mashahidi wa Yehova huweka imani yao katika Ufalme wa Mungu. Huo ni zile “mbingu mpya” ambazo mtume Petro aliandika kuzihusu: “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) “Dunia mpya” ni jamii mpya ya kibinadamu ambayo itatawaliwa na mbingu mpya, Ufalme wa Mungu. Huo ndio mpango ambao Mungu alimfunulia mtume Yohana katika ono. Yohana aliandika hivi: “Nikaona mbingu mpya na dunia mpya; kwa maana mbingu ya kwanza na dunia ya kwanza zilikuwa zimepitilia mbali . . . Naye [Mungu] atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:1, 4.

20 Ona kwamba dunia mpya itakuwa adilifu. Mambo yote yasiyo ya uadilifu yataondolewa kwa tendo la Mungu, pigano la Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14, 16) Unabii kwenye Mithali 2:21, 22 wasema hivi: “Maana wanyofu watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu watatengwa na nchi.” Na andiko la Zaburi 37:9 laahidi hivi: “Maana watenda mabaya wataharibiwa, bali wamngojao BWANA ndio watakaoirithi nchi.” Je, hungependa kuishi katika ulimwengu mpya huo?

Weka Imani Katika Ahadi za Yehova

21. Kwa nini twaweza kuweka imani katika ahadi za Yehova?

21 Je, twaweza kuweka imani katika ahadi za Yehova? Sikiliza ambayo ataarifu kupitia nabii wake Isaya: “Kumbukeni mambo ya zamani za kale; maana mimi ni Mungu, wala hapana mwingine; mimi ni Mungu, wala hapana aliye kama mimi; nitangazaye mwisho tangu mwanzo, na tangu zamani za kale mambo yasiyotendeka bado; nikisema, Shauri langu litasimama, nami nitatenda mapenzi yangu yote.” Sehemu ya mwisho ya mstari wa 11 yasema hivi: “Nimenena, nami nitatekeleza; nimekusudia, nami nitafanya.” (Isaya 46:9-11) Ndiyo, twaweza kuwa na imani katika Yehova na ahadi zake kana kwamba kwa hakika ahadi hizo zimetimia tayari. Biblia huonyesha hilo hivi: “Imani ni taraja lililohakikishwa la mambo yatumainiwayo, wonyesho dhahiri wa mambo halisi ingawa hayaonwi.”—Waebrania 11:1.

22. Kwa nini twaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatimiza ahadi zake?

22 Watu wanyenyekevu huonyesha imani hiyo kwa sababu wajua Mungu atatimiza ahadi zake. Kwa kielelezo, kwenye Zaburi 37:29 twasoma hivi: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” Je, twaweza kuamini hilo? Ndiyo, kwa sababu andiko la Waebrania 6:18 lasema: “Haiwezekani Mungu kusema uwongo.” Je, ulimwengu ni wa Mungu, hivi kwamba aweza kuwapa wanyenyekevu? Andiko la Ufunuo 4:11 latangaza hivi: “Uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako na vikaumbwa.” Hivyo, andiko la Zaburi 24:1 lasema hivi: “Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya BWANA.” Yehova aliiumba dunia, ni yake, naye huwapa walio na imani kwake. Ili kusaidia kukuza uhakika wetu katika hilo, makala inayofuata itaonyesha jinsi ambavyo Yehova ametimiza ahadi zake kwa watu wake katika nyakati zilizopita na pia katika siku yetu na kwa nini twaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba atafanya hivyo wakati ujao.

Hoja za Kupitia

◻ Kotekote katika historia, matumaini ya watu yamepatwa na nini?

◻ Kwa nini tusiwategemee binadamu ili kupata wakati ujao ulio bora?

◻ Mapenzi ya Mungu kuhusu wakati ujao ni nini?

◻ Kwa nini tuna uhakika kwamba Mungu atatimiza ahadi zake?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Biblia hutaarifu hivi kwa usahihi: “Kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.”—Yeremia 10:23

[Hisani]

Bomu: Picha ya Hifadhi za Nyaraka za Kitaifa ya Marekani; watoto wenye njaa: WHO/OXFAM; wakimbizi: PICHA ya UM 186763/J. Isaac; Mussolini na Hitler: Picha ya Hifadhi za Nyaraka za Kitaifa ya Marekani

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki