Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 12/15 kur. 557-562
  • Mtumaini Yehova, Si Mwanadamu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mtumaini Yehova, Si Mwanadamu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • VITU VILIVYOTUMAINIWA BURE NA WANASAYANSI
  • YEHOVA ANASTAHILI TUMTUMAINI
  • Kuwatumaini Wengine Ni Muhimu kwa Maisha Yenye Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Katika Nyakati Zetu Zenye Hofu Ni Nani Unayeweza Kuitibari Kikweli?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Fanya Yehova Awe Itibari Yako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Waweza Kuitumaini Sayansi Kadiri Gani?
    Amkeni!—1998
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 12/15 kur. 557-562

Mtumaini Yehova, Si Mwanadamu

“Ni heri kumkimbilia [Yehova] kuliko kuwatumainia wanadamu.”​—Zab. 118:8.

1, 2. (a) Ni watu wangapi wanaoendelea kumtumaini sana Yehova bila kuacha, na kwa sababu gani? (b) Ni nani wanaomtumaini Yehova alete hali bora?

NI WATU wachache leo wanaoendelea kumtumaini sana Yehova Mungu bila kuacha. Wengine hata hawaamini kwamba yuko. Wengine wanakubali kwamba Mungu yuko, lakini hawataki kufanya mapenzi yake. Hata wale wanaofuata sana dini za ulimwengu huu wanatumaini sana-sana mapokeo yao ya kidini au viongozi wao wa dini, badala ya Yehova. Wanafanana sana na wale ambao mtume Paulo alisema hivi juu yao: “Nawashuhudia kwamba wana juhudi kwa ajili ya Mungu, lakini si katika maarifa. Kwa maana, wakiwa hawaijui haki ya Mungu, na wakitaka kuithibitisha haki yao wenyewe, hawakujitia chini ya haki ya Mungu.”​—Rum. 10:2, 3.

2 Watu wanatumaini nani aletee jamaa ya kibinadamu hali bora wakati ujao? Wengi wao wanatumaini jitihada za mwanadamu, wala hawatumaini vile Yehova amekusudia kufanyia wanadamu. Ni hesabu ndogo sana kati ya wakaaji bilioni nne wa dunia ambao wamechunguza kwa uangalifu ushuhuda unaoonyesha kwamba Yehova yuko, kisha wakakubali kutimiza wajibu walio nao kwake, na kuishi maisha ya kutii sheria zake. Watu hao wanamtumaini kabisa, nao wanajua kwamba atatimiza ahadi yake ya kuanzia wanadamu taratibu mpya yenye haki. Wanasema kama mtunga zaburi wa kale: “Mimi nakutumaini Wewe, [Yehova], nimesema, Wewe ndiwe Mungu wangu.” (Zab. 31:14) Tena wanatii onyo la Mungu linalosema: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake.”​—Zab. 146:3.

3. Kwa sababu gani haitupasi kuvunjika moyo kwa sababu watu wengi hawamtumaini Yehova?

3 Je! inapasa wale wanaomtumaini Yehova wavunjike moyo kwa sababu ni wachache wakilinganishwa na watu bilioni nne walio duniani? Hapana, kwa maana jambo haliwi la haki kamwe kwa sababu tu linafuatwa na watu wengi. Yesu Kristo alisema: “Ingieni kwa kupitia mlango ulio mwembamba; maana mlango ni mpana, na njia ni pana iendayo upotevuni, nao ni wengi waingiao kwa mlango huo. Bali mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani, nao waionao ni wachache.” (Mt. 7:13, 14) Basi, njia ya kupitia “mlango ulio mwembamba” unaoleta uzima kamili si kutumaini uamuzi unaofanywa na wingi wa watu. Historia inaonyesha ahadi nyingi sana zimefanywa na wanadamu zisitimizwe kamwe, kisha watu wengi walioziamini kwa upumbavu wakaumia.

4. Sasa tuko katika hali bora ya kuamua nini, na kwa sababu gani?

4 Hasa karne iliyopita imeonekana kwamba ni upumbavu kuitumaini hekima ya mwanadamu. Sasa, kwa kuwa tumepata ujuzi zaidi kwa kukiona kizazi hiki cha kisasa chenye ufundi mwingi wa sayansi, tuko katika hali bora ya kuchunguza matokeo ya vitu ambavyo mwanadamu amevumbua. Tunaweza kuvilinganisha na vitu vilivyofanywa na Yehova, tuone waziwazi inapasa tutumaini nani.

VITU VILIVYOTUMAINIWA BURE NA WANASAYANSI

5. Maendeleo ya kisayansi yaliwapaje watu wengi matumaini ya kuwa na ulimwengu bora?

5 Wanadamu walizidi kutumaini kwamba zingekuwako hali bora ulimwenguni kwa sababu ya maendeleo ya kisayansi karne moja hivi iliyopita. Watu wengi walidhani kwamba wanadamu wameanza kuingia katika kipindi chenye mambo mazuri sana. Mwishowe, ilidhaniwa kwamba matatizo kama umaskini, njaa, ukosefu wa kazi, magonjwa, uzee na vita yangeweza sasa kutatuliwa na wanadamu. Mwandikaji Lewis Mumford anaeleza yafuatayo juu ya matumaini makubwa ambayo watu walikuwa nayo:

“Ilidhaniwa kwamba, kwa sababu mashine ziliundwa kwa njia nzuri zaidi zikawa zikifanya kazi vizuri sana, ndizo zilizoanzia mwanadamu njia mpya za kutimizia mambo . . .

“Ilisemekana kwamba kila udhaifu au ugonjwa wa mwili wa mwanadamu ungeweza kuponywa upesi kwa kutumia mashine au dawa. Hata wakati taa ya kwanza ya umeme ilipotengenezwa, watu waliishangilia wakiwa na hakika kwamba ingezuia uvunjaji sheria usifanywe nyakati za usiku.”

6. Ni kwa kadiri gani sayansi ilitokeza vitu vyenye kusaidia jamaa ya kibinadamu?

6 Bila shaka sayansi imewezesha watu watengeneze vifaa vingi. Katika nchi nyingi, siku hizi akina mama wanaotunza nyumba hawatumii wakati mwingi wakifua nguo na kuzishona kwa mikono, hawapiki kwa kutumia kuni, hawatumii muda mwingi wakihifadhi chakula cha miezi yenye baridi nyingi, wala hawachoti maji katika kisima au kijito. Sayansi imewezesha watu watokeze nguvu za umeme kwa kutumia mafuta yanayochimbwa, makaa ya mawe na mvuke ili kuendesha mashine mpya za kufulia na kushonea nguo, kuwasha meko ya kupikia, kuendesha mashine za barafu, vyombo vya kupashia nyumba joto, kuwasha taa na vifaa vinginevyo. Mabomba ya maji yamewekwa ndani ya nyumba na kuwezesha watu waepuke kwenda nje mahali penye kuharibu afya, wanapokuwa na haja. Tingatinga zimetengenezwa zikaweza kuvuta vitu ambavyo vingeweza kuvutwa na farasi 50. Mashine za kukama ng’ombe zimefanya wakulima wawe na kazi nyepesi. Maendeleo ya udaktari yamesaidia kupunguza magonjwa mbalimbali. Hata ufundi umeongezeka, kukawa na mashine kubwa za hesabu na roketi ambazo zimesaidia kupeleka wanadamu mwezini.

7. Sayansi imeletaje matatizo mengi?

7 Lakini ingawa sayansi imesaidia kutatua matatizo fulani, imeongeza mengine mengi. Kwa mfano, ingawa motokaa inasafirisha watu upesi na kuwafaa kwa njia fulani, imeleta matatizo yasiyotatulika. Motokaa zinasongamana sana na kuleta mvurugo katika miji mikubwa. Moshi pia unatoka viwandani na kuchafua hewa katika miji mingi. Nayo motokaa imekuwa kimojawapo vitu vyenye hatari zaidi vilivyopata kuvumbuliwa. Kulingana na yaliyosemwa katika gazeti World Health la Umoja wa Mataifa, karibu watu 250,000 wanakufa kila mwaka katika mikasa ya barabarani. Mamilioni wengine wanaumia.

8. Wanasayansi wameleta matokeo gani kwa sababu ya kufanya kazi ya vita katika karne yetu?

8 Tunda jingine baya ambalo limetokana na sayansi linatajwa na kitabu Great Events of the 20th Century, kinaposema hivi: “Bila shaka, jambo ambalo limebadili sana karne ya 20 ni kuongezeka sana kwa maarifa ya kisayansi​—nayo maarifa hayo yametumiwa sana nyakati za vita kuliko nyakati nyinginezo.” Vifaru, ndege, mizinga yenye kulipua moto, bunduki zenye kumimina risasi kama maji, manowari, fataki, makombora ya atomu na silaha nyingi zimetengenezwa na wanasayansi. Zimeua watu zaidi ya milioni 100 katika kizazi hiki, na hao ni wengi kuliko waliouawa katika kizazi kinginecho chote. Neno la Mungu lilitaja kweli liliposema, “Ole wao . . . watumainio magari kwa kuwa ni mengi, na wapanda farasi kwa kuwa ni hodari sana; lakini hawamwangalii Mtakatifu wa Israeli, wala hawamtafuti [Yehova]!” (Isa. 31:1) Ingawa silaha zinazotengenezwa kwa maarifa ya kisayansi zimeleta msiba mkubwa, mataifa sasa yanatumia dola bilioni 300 (shilingi bilioni 2,400 au Zaire karibu bilioni 258) kila mwaka kutayarisha zana za vita. Karibu kiasi cha 25 kwa mia cha wanasayansi wote katika United States na Urusi wanafanya kazi ya vita; kiasi kidogo sana kuliko mmoja kati ya kila wanasayansi mia moja ndio wanaopinga utengenezaji wa silaha za vita.

9. Je! sayansi imesaidia kutatua matatizo yanayotaabisha sana jamaa ya kibinadamu?

9 Je! sayansi imesaidia kuzuia uvunjaji sheria usienee ulimwenguni pote? Hapana, kwa maana umeongezeka kama Neno la Mungu lilivyotabiri ungeongezeka ‘siku hizi za mwisho? (Mt. 24:12; 2 Tim. 3:1-5, 13) Katika United States peke yake, uchunguzi mmoja unaonyesha kwamba matendo makubwa milioni 37 ya kuvunja sheria yanatendwa kila mwaka, lakini theluthi moja tu ndiyo inayoripotiwa kwa polisi. Tena, ingawa sayansi ya udaktari imesaidia kupunguza magonjwa, mengine yameongezeka sana yakaishinda nguvu. Ugonjwa wa moyo umeongezeka sana, na vilevile kisonono na kaswende; nayo cancer imekuwa ikiua watu wengi. Matatizo ya afya yameongezeka kwa sababu mwanadamu amechafua hewa, nchi na maji, na vilevile akawa akitia dawa katika vyakula ili kuvizuia visiharibiwe na viini. Sayansi iko hoi kabisa, wala haiwezi kuondoa uzee na kifo. Hali ya wanadamu imeendelea kuwa kama vile Neno la Mungu linavyosema: “Kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote.” (Rum. 5:12) Zaidi ya hilo, ijapokuwa sayansi ya kisasa imefanya maendeleo, gazeti Parade linasema hivi: “Watu wanaokufa njaa, walio maskini, wasio na elimu wala kazi katika ulimwengu ni wengi sasa kuliko wakati wo wote uliotangulia.”

10, 11. (a) Wakuu fulani wa ulimwengu wamesema nini kuonyesha wanajua kwamba sayansi imeshindwa? (b) Biblia ilisema nini kwa usahihi juu ya jitihada za mwanadamu?

10 Hivyo, matokeo ya kizazi hiki cha kisayansi yameonekana wazi. Sisi wenyewe tumeyaona. Tunaweza kukata maneno kama kitabu Environmental Ethics’. “Ufundi wa siku hizi umekwisha shindwa.” Mwandikaji Lewis Mumford pia alisema hivi: “Lile wazo la kusema kwamba wanadamu watapata faida zinazolingana na maendeleo yatakayopatikana katika ufundi wa mashine na sayansi . . . sasa limepingwa kabisa.” Naye mwanahistoria Arnold Toynbee alisema: “Tumejaribu kuziacha mashine zituongoze, mambo yakawa mabaya sana. . . . Mwanadamu asiyefanya maendeleo hawezi kutumainiwa anapotumia vitu hatari ambavyo vimetengenezwa katika viwanda vyake vya ufundi.”

11 Sasa tunaweza kuona waziwazi jambo ambalo limeipata jamaa ya kibinadamu kwa sababu ya. kumtumaini mwanadamu. Ni kama vile Yeremia nabii wa Mungu alivyotabiri: “Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake, na moyoni mwake amemwacha [Yehova]” (Yer. 17:5) Vilevile maneno yafuatayo ya mtunga zaburi aliyeongozwa na Mungu yanatumainika: “[Yehova] asipoijenga nyumba waijengao wafanya kazi bure.”​—Zab. 127:1.

YEHOVA ANASTAHILI TUMTUMAINI

12. Ni nani peke yake anayestahili tumtumaini atutimizie mambo yaliyo ya lazima maishani?

12 Kama vile ujuzi wa kibinadamu umeonyesha, ni upumbavu kutumaini hekima ya kibinadamu itusaidie katika mambo yaliyo ya lazima maishani. Hatuwezi kumtumaini mwanadamu atutatulie matatizo makubwa sana yanayopata jamaa ya kibinadamu. Yehova peke yake, Muumba Mwenye Nguvu Zote, ndiye anayeweza kuyatatua. Kwa hiyo inatupasa tumgeukie Yehova atuongoze nyakati hizi zenye hatari, maana hilo ni jambo la maana sana. Je! kama ungetaka ramani ya kukuongoza katika safari yenye hatari, ungetumaini kitoto kidogo kikuchoree-choree vitu visivyoeleweka? Au ungetegemea maongozi ya mtu stadi anayejua sana njia ya kuendea? Hekima ya kibinadamu haifai kabisa kutuongoza katika safari yetu ya ‘siku hizi za mwisho’ zenye hatari tunapojitahidi kupata uzima wa milele katika taratibu mpya ya Mungu. Ndiyo sababu Biblia inasema hivi: “Amebarikiwa mtu yule anayemtegemea [Yehova], ambaye [Yehova] ni tumaini lake.”​—Yer. 17:7.

13-15. (a) Ulimwengu mzima unaonyeshaje kwamba Yehova ni mwenye hekima na uweza? (b) Kwa sababu gani inapasa jambo hilo litufanye tuzidi kumtumaini Yehova? (Isa. 40:28, 29)

13 Tunapewa matumaini zaidi na vitu vilivyofanywa na Yehova pamoja na hekima na uwezo wake. Tunapoona vitu ambavyo amekwisha fanya, pamoja na vile anavyoweza kufanya, tunapata ufahamu zaidi kwamba ana uwezo wa kuongoza maisha yetu na kutayarisha taratibu mpya yenye haki. Mfano wa uwezo wa Yehova unaonekana katika ulimwengu alioumba. Kabla darubini hazijavumbuliwa, watu walidhani kwamba hakukuwa na nyota nyingine isipokuwa maelfu machache tu ya nyota ambazo wangeweza kuona kwa macho yao wenyewe. Lakini darubini za kwanza zilipotokea, nyota nyingine nyingi zilionekana. Nazo darubini za ki-siku-hizi zimeona sehemu za mbali za ulimwengu wa anga za juu, zikaonyesha kwamba kuna mabilioni mengi sana ya nyota kiasi cha kwamba, “jeshi la mbinguni haliwezi kuhesabiwa” na mwanadamu, kama Yeremia alivyosema.​—Yer. 33:22, tafsiri ya American Standard.

14 Iligunduliwa kwamba nyota za mbinguni haziko katika hali ya kutawanyika ovyo tu, bila mpango. Zimepangwa pamoja katika makundi yanayoitwa galaxy (galaksi) na kila mojawapo lina mabilioni ya nyota na vitu vingine. Kundi la nyota tunamoishi linaitwa Milky Way, na inakadiriwa kwamba ina nyota mabilioni 100 zinazolingana na jua letu. Imehesabiwa ikaonekana kwamba, tukisafiri upesi kama nuru, inaweza kutuchukua karibu miaka 100,000 kuivuka galaksi yetu; nayo nuru inasafiri karibu maili trilioni sita (kilomita 9,600,000,000,000) kwa mwaka mmoja tu! Isitoshe. Gazeti Nationai Geographic linasema kwamba uchunguzi ambao mwanadamu amefanya karibuni ‘umemfanya aduwae.’ Galaksi nyingi sana zimeonekana, hata wachunguzi wakakadiri kwamba hesabu yazo ni bilioni kumi; mchunguzi mwingine anakadiri kwamba ni bilioni 100! Tena, imechunguzwa ikaonekana kwamba galaksi hizo nazo hazikutawanyika ovyo-ovyo tu, bali zimepangwa vizuri. Zimepangwa makundi makundi, kila kundi likiwa na galaksi kadha.

15 Ukubwa wa ulimwengu, utaratibu wake, na kawaida zinazoongoza madude ya mbinguni kwa njia nzuri sana, umeshangaza wanasayansi wengine. Ni kama vile lisemavyo gazeti Science News: “Wachunguzi wa ulimwengu mzima wanavurugika akili wanapofikiria mambo hayo, kwa maana haionekani kwamba vitu hivyo vyenye kufuata utaratibu mzuri kabisa vilitokea vivi hivi tu.” Bila shaka, ulimwengu mzima haukutokea “vivi hivi tu.” Hekima, uwezo, utaratibu na kawaida zinazoonekana katika ulimwengu mzima zilitokana na Muumba mkuu, Yehova Mungu: “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake.” (Zab. 19:1) Uwezo wa Yehova ni mwingi sana hivi kwamba, yeye anafanya kwa wepesi mambo ambayo wanadamu wanaona hayawezekani, hata “huihesabu idadi ya nyota, huzipa zote majina.”​—Zab. 147:4.

16. Inatupasa tukate maneno namna gani kwa sababu ya mambo mapya yanayogunduliwa?

16 Wanasayansi wengi wanazidi kushangaa sana kwa sababu ya jinsi vitu vilivyo hai duniani vimeumbwa kwa hekima na kwa njia iliyo ngumu sana kufahamika. Kitabu Science Digest kilisema hivi: “Kwa kuwa habari mpya zinajulikana wakati chembe za vitu vilivyo hai zinapochunguzwa, inazidi kuonekana kwamba uhai usingeweza kujitokeza wenyewe.” Wanasayansi wanakadiri kwamba, ili kueleza mambo yote yanayofanyika katika chembe moja ya mwili wa mwanadamu, ingehitajiwa encyclopedia yenye vitabu 1,000 iandikwe. Vitu vyote hivyo vilitoka wapi? Ukiona encyclopedia nyingi katika rafu unajua kwamba kuna mtu mwenye akili aliyeziandika. Basi, mambo mengi sana tunayoona katika vitu vilivyo hai, pamoja na hekima tunayoona katika maumbo yavyo yaliyo magumu sana kufahamika, yanatuonyesha kwamba vitu hivyo viliumbwa na mtu mwenye akili. Basi, kwa ufupi na kwa ukweli, Biblia inasema juu ya Yehova Mungu hivi: “Kwako Wewe iko chemchemi ya uzima.”​—Zab. 36:9.

17. Wanyenyekevu watakubali nini?

17 Wanyenyekevu watakubali vile wanasayansi wengi na watu wengine wasivyokubali, kwamba Yehova ndiye “aliyeziumba mbingu, na kuzitanda; yeye aliyeitandaza nchi na mazao yake; yeye awapaye pumzi watu walio juu yake; yeye awapaye roho wao waendao ndani yake.” (Isa. 42:5) Hakika Muumba huyo mtukufu, anayeonyesha uwezo na hekima nyingi hivyo, anastahili tumtumaini. Ni kama walivyosema wale wazee 24 katika njozi: “Umestahili wewe, Bwana wetu na Mungu wetu, kuupokea utukufu na heshima na uweza; kwa kuwa wewe ndiwe uliyeviumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako, navyo vikaumbwa.”​—Ufu. 4:11.

18, 19. (a) Vitu vilivyofanywa na Mungu vinaonekanaje vikilinganishwa na vya mwanadamu? (b) Tutatumaini Mungu au mwanadamu?

18 Kwa hiyo, tunapolinganisha vitu vilivyofanywa na Mungu na vile vilivyofanywa na mwanadamu, tunaweza kuuliza hivi: Ni nani anayestahili tumtumaini? Hakika haitupasi kumtumaini mwanadamu, hata ikiwa amefanya maendeleo mengi ya kisayansi. Uharibifu mwingi na mvurugo ambao amekwisha letea dunia unaonyesha kwamba hawezi kutatua matatizo ya maisha, wala hatuwezi kumtumaini afanye hivyo. Ni kama vile kisemavyo kitabu World Book Encyclopedia:

“Ijapokuwa maendeleo makubwa yamefanywa katika sayansi, wanasayansi wangali hawajatatua matatizo mengi. . . .

“Wachunguzi wa miti na mimea mingineyo hawajui habari zote juu ya jinsi mimea inavyotengeneza wanga na sukari kwa kusaidiwa na mwanga wa jua, hewa na maji. Wachunguzi wa ukuzi wa vitu vilivyo hai na mazingira yavyo hawajafahamu bado jinsi uhai ulivyoanza. Wachunguzi wa anga za juu hawajafahamu vizuri jinsi ulimwengu mzima ulivyotokea. Madaktari na wachunguzi wa mambo yanayofanywa na vitu vilivyo hai hawajui kinachoanza cancer wala kinachoweza kuiponya, wala hawajui jinsi ya kuponya magonjwa mbalimbali yenye kuambukia watu. . . . Wachunguzi wa akili hawajui vitu vyote vinavyoleta ugonjwa wa akili.”

19 Yehova anajua majibu ya mambo yote hayo. Hakika yeye ana hekima na uwezo wa kutatua matatizo yanayopata wanadamu kwa wingi. Kwa hiyo, onyo la Biblia lifuatalo linafaa: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake.” (Zab. 146:3) Wale wanaopenda haki, wanaopenda uzima, na wanaotaka kuona hali bora wakati ujao, watakuwa kati ya wale wanaoelezwa na mtunga zaburi: “Nao wakujuao jina lako wakutumaini Wewe, maana Wewe, [Yehova], hukuwaacha wakutafutao.”​—Zab. 9:10.

[Picha katika ukurasa wa 558]

Yanayoitwa “maendeleo” ya kisayansi na wanadamu yanaleta msongamano, uchafu, mvurugo na vifo vingi visivyo vya wakati wake

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki