Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 6/15 kur. 15-20
  • Serikali Inayotimiza Mambo Asiyoweza Mwanadamu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Serikali Inayotimiza Mambo Asiyoweza Mwanadamu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kanuni ya Ukombozi
  • Elimu Katika Utaratibu Mpya
  • Kujenga Paradiso
  • Jamaa ya Duniani Pote Yenye Umoja
  • Kukusanywa Kwenye Ibada ya Kweli
  • “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya”
    “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya”
  • Uhuru wa Kweli Chini ya Utawala wa Ufalme
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Namna Ufalme wa Mungu Unavyoweza Kukufaidi Wewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Serikali ya Ufalme wa Mungu Ni Halisi Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 6/15 kur. 15-20

Serikali Inayotimiza Mambo Asiyoweza Mwanadamu

“Njoni yatazameni matendo ya Mungu; hutisha kwa mambo awatendayo wanadamu.”​—Zaburi 66:5.

1, 2. (a) Ulimwengu mzima unaoonekana unaonyeshaje uwezo wa kutisha wa Muumba? (b) Kwa sababu gani inatupasa tuamini yale ambayo Neno la Yehova la unabii linasema juu ya wakati wetu?

YEHOVA ana uwezo wa kufanya asiyoweza mwanadamu. Kwa mfano: Wanadamu wanaogopa sana kwa sababu ya nguvu za kombora la nyukilia; lakini nguvu zalo ni kitu kidogo sana zinapolinganishwa na nguvu zilizo katika jua letu. Na hata hivyo jua ni moja tu ya nyota karibu bilioni 200 zilizo katika galaksi yetu pekee (kundi la nyota) inayoitwa Njia ya Kimaziwa. Wachunguzi wa anga za juu wanakadiri kwamba katika ulimwengu mzima huenda kukawa kuna galaksi bilioni 100, kila moja yazo ikiwa na mabilioni ya nyota. Ilichukua nguvu nyingi kama nini kuumba vyote hivyo! (Isaya 40:26) Nguvu hizo za kutisha alizo nazo Muumba zinafanya nguvu za wanadamu ziwe ni kama haziko.​—Isaya 40:15.

2 Hivyo hakuna mtu anayepaswa kutia shaka kwamba Yehova anaweza kutimiza mambo anayosema atafanya. (Isaya 46:9,10; 55:11) Inatupasa tuamini wakati Neno lake la kiunabii linapotuambia kwamba tunakaribia mwisho wa kikomo cha wakati ambacho ameruhusu wanadamu wafuate njia yao ya kujitegemea. Historia inaonyesha kwamba mambo ambayo watu wametenda wanadamu wenzao na wanyama, na pia dunia yenyewe, ni aibu, doa juu ya ulimwengu mzima wa Mungu. Hivyo, Yehova ana haki kamili ya kufuta doa hilo mara moja kwa nyakati zote.​—Hosea 4:1-3; Yuda 14, 15.

3. Unabii wa Biblia unasema nini juu ya wakati ujao ulio karibu?

3 Mambo yanayotendeka ulimwenguni leo ni ushuhuda wa wazi kwamba mfumo huu wa mambo umo katika sehemu ya mwisho kabisa ya “siku za mwisho” zilizotabiriwa kwenye 2 Timotheo sura ya 3. Karibuni Yehova atauponda mfumo huu upotelee mbali, na kumlemaza aliye kichwa chao, Shetani Ibilisi. Jambo hilo litafuatwa na mfumo mpya kabisa wa mambo duniani, wenye kusimamiwa na serikali ya kimbingu ambayo Yesu alifundisha wafuasi wake kuomba wakati aliposema hivi: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”​—Mathayo 6:9, 10; Danieli 2:44; Warumi 16:20.

Kanuni ya Ukombozi

4. Yehova alitumiaje kanuni ya ukombozi katika Israeli wa kale?

4 Serikali za kibinadamu haziwezi kuondolea mbali dhambi, magonjwa, na kifo. Lakini, serikali ya Mungu itafanya mambo wasiyoweza wanadamu. Tunapata ufahamu fulani juu ya jinsi hilo litakavyowezekana kwa kuchunguza matendo ya Mungu pamoja na watu wake wa kale wa Israeli. Huko nyuma, Mungu alitumia kanuni ya ukombozi. Kwa mfano, ikiwa Mwisraeli aliingia katika umaskini, labda angalilazimika kujiuza awe mtumwa wa mtu asiye Mwisraeli. Lakini mtu wa ukoo wa karibu angeweza kumkomboa kama alikuwa na bei ya ukombozi inayotosha.​—Mambo ya Walawi 25:47-49.

5, 6. (a) Kanuni ya ukombozi inatumikaje katika kuondolea wanadamu dhambi ya kurithi? (b) Je! kila mtu anawekwa huru asiwe na dhambi hata bila ya yeye kuchukua hatua yo yote?

5 Vivyo hivyo, Mungu ameandaa njia ya kukomboa wanadamu watoke katika utumwa wa dhambi. Bei ilipasa kulingana na kile kilichopotezwa. (Kumbukumbu la Torati 19:21) Adamu alipoteza uhai wa kibinadamu ulio mkamilifu na wa milele. Kwa kuwa hakuna cho chote walicho nacho wanadamu kinaweza kulingana na uhai huo kwa ubora, hawawezi ‘kumkomboa hata ndugu yao.’ (Zaburi 49:7) Lakini, Biblia ilitabiri kuja kwa mmoja ambaye angeweza. Huyo akawa ni Yesu Kristo. Ilifunuliwa kwamba Yesu alitangulia kuishi mbinguni kabla hajawa mwanadamu. Lakini kwa nguvu za Yehova uhai wake ulihamishwa ukaletwa kwenye tumbo la uzazi la Mariamu. Kwa njia hiyo alizaliwa akiwa mwanadamu. Lakini hakurithi udhambi uliokuwa umelemaza wanadamu wengine wote, kwa kuwa Mungu ndiye aliyekuwa Baba yake.​—Mathayo 1:18-21; Yohana 1:1, 14; 1 Petro 2:22.

6 Hivyo, Yesu alikuwa na kitu kile cha pekee kilicholingana ubora na uhai mkamilifu wa kibinadamu​—uhai mwingine mkamilifu wa kibinadamu. Lakini tofauti na Adamu asiyetii, Yesu aliendelea kuwa mtiifu kwa Mungu. Naye alipotoa uhai wake kwa ajili ya jamaa ya kibinadamu, Yehova aliukubali kuwa ndiyo bei ya ukombozi iliyofaa. (Wagalatia 1:4) Lakini je, maana yake ni kwamba kila mtu anawekwa huru kutoka utumwa wa dhambi na atapata ukamilifu chini ya utawala wa Ufalme bila kuchukua hatua yo yote? Hapana, kwa maana Yohana 3:16 inasema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hata akamtoa Mwana wake mzaliwa wa pekee, ili kila mtu anayejizoeza imani katika yeye asipate kuharibiwa bali awe na uzima wa milele.” (NW) Tukiukubali uandalizi wa ukombozi na kuchukua hatua, hapo tu ndipo miili na akili zetu zitakaporudishwa kwenye ukamilifu katika Paradiso.​—Ufunuo 21:4.

Elimu Katika Utaratibu Mpya

7, 8. Ni uwezekano gani wa kujifunza wakati ujao unaokaa ndani ya ubongo wa kibinadamu?

7 Akili ina uwezo mkubwa sana wa kujifunza, hata katika hali yetu ya sasa ya kutokamilika. Lakini hicho ni kisehemu kidogo sana cha mambo itakayoweza kujifunza katika Utaratibu Mpya, ambamo dhambi haitauzuia kufanya kazi. Katika kichapo kinachoitwa The Brain Book, mtungaji anasema: “Ndani ya vichwa vyetu wenyewe unakaa mmoja wa mifumo iliyo migumu sana kufahamika katika ulimwengu mzima wa vitu vinavyojulikana. Uwezo na ustadi wake unapita kwa mbali ule wa kompyuta yo yote iliyofanywa na mwanadamu.” Anaongeza hivi: “Mara nyingi inasemwa kwamba tunatumia asilimia 10 tu ya uwezo kamili wa akili yetu. Sasa hilo linaonekana ni kadirio la juu kupita kiasi. Labda hata hatutumii asilimia 1—inaelekea zaidi kuwa tunatumia asilimia 0.1 au kidogo kuliko hapo.”

8 Wazia ubongo wa kibinadamu utawezesha wanadamu kutimiza nini wakati utakapofikia uwezo wao kamili katika Utaratibu Mpya. Fikiria vitu vyote vya kusisimua ambavyo Yehova ameweka juu ya dunia hii ambavyo tunaweza kujifunza juu yavyo, kama vile wanyama, viumbe vya baharini, na mimea. Fikiria, pia, juu ya kujifunza habari za ulimwengu mzima unaostaajabisha sana pamoja na mabilioni yake ya galaksi za nyota. Fikiria ustadi wa namna zote tutakazoweza kujifunza vizuri katika uchoraji, muziki, sanaa, na mambo mengine mengi.

9. Ni elimu ya namna gani itakayoleta faida zilizo kubwa zaidi katika Utaratibu Mpya?

9 Kuna namna nyingine ya elimu katika Utaratibu Mpya itakayoleta faida iliyo kubwa kupita zote. Yesu alisema: “Wote watafundishwa na Yehova.” (Yohana 6:45, NW) Hiyo ndiyo elimu ya kiwango cha juu zaidi. Nayo itafanywa iweze kupatikana kwa raia wote wa Ufalme wa Mungu, kutia ndani wale watakaookoka mwisho wa mfumo huu wa mambo. (Ufunuo 7:9, 14) Raia wengine wa Ufalme wametajwa penye Yohana 5:28 na 29, ambapo Yesu alisema: “Saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini [makaburi ya ukumbusho, NW] wataisikia sauti yake. Nao watatoka.” Ufufuo huo wa mabilioni ya wafu​—usiowezekana kabisa kutimizwa na wanadamu​—unamaanisha kwamba itakuwa lazima kazi kubwa sana ya elimu ifanywe kwa ajili yao.

10. Elimu itaendeleaje katika Utaratibu Mpya?

10 Leo kuna mifumo mingi ya elimu inayopingana. Lakini katika Utaratibu Mpya, serikali ya kimbingu ya Mungu itaandaa mfumo mmoja wa elimu ulimwenguni pote ili kufundisha watu ukweli juu ya Yehova kwa njia yenye umoja. Sehemu moja ya mfumo huo itakuwa ni kufundisha watu juu ya uhusiano unaofaa wa kibinadamu. Hakutakuwa kufundisha watu kiburi cha ukabila, utaifa, au cheo cha mtu katika jamii. Bali, wakaaji wa dunia watajifunza kupendana, kila mtu kuheshimu fahari ya mwingine. Elimu hiyo itabadili vizuri pia nyutu za watu ili zifanane na sifa bora za Yehova.​—Matendo 10:34, 35; Wakolosai 3:9-12.

11, 12. Tunaweza kuwaje na uhakika kwamba elimu hiyo katika Utaratibu Mpya itafanikiwa katika kusudi lake?

11 Je! kweli elimu ya namna hiyo inaweza kuwa na matokeo mazuri? Tuna uhakika kwamba inaweza na itakuwa nayo. Sababu moja ni kwamba Yehova, ambaye hawezi kunena uwongo, anasema kwamba ndivyo itakavyokuwa. (Tito 1:2) Tena, elimu ya namna hiyo inakuwa na matokeo mazuri sasa hivi! Tayari Yehova ana tengenezo linalofundisha mamilioni ya watu ulimwenguni pote juu ya serikali yake ya Ufalme na matakwa yake. Hilo linatukia kwa sababu utawala wa Ufalme umekuwa ukifanya kazi tangu “siku za mwisho” zilipoanza katika mwaka wa 1914.

12 Tangu wakati huo, unabii wa Mathayo sura ya 25 umekuwa ukitimizwa. Unaonyesha kwamba Yesu anakuja kwenye mamlaka ya Ufalme katika mbingu na huku adui za Mungu wakiwa bado duniani. Mstari wa 32 unasema: “Mataifa yote watakusanyika mbele zake; naye atawabagua kama vile mchungaji abaguavyo kondoo na mbuzi.” Watu hao wenye mfano wa kondoo wanafundishwa na Yehova sasa kupitia tengenezo lake lionekanalo, linaloendelea kukua. Kwa kuthamini wanayojifunza, wanajitahidi kubadili nyutu zao zipatane na mfano wa Mungu. Nalo jambo la kwamba elimu hiyo inageuza vizuri mamilioni ya watu sasa ni wonyesho hakika kwamba itafanya hivyo kwa kadiri kubwa zaidi katika Utaratibu Mpya wa Mungu.

Kujenga Paradiso

13. Ni ujenzi gani mkubwa utakaofanyika chini ya utawala wa Ufalme?

13 Kazi ya namna nyingine itakayofanywa chini ya utawala wa Ufalme itakuwa ile ya kugeuza dunia hii iwe paradiso. Na paradiso haingeweza kuwa na mitaa michafu-michafu wala umaskini. Watu wanataka nyumba nzuri na shamba la kiasi fulani lenye miti, maua, na bustani. Wale walio na nia ya kufundishwa na Mungu watapata vitu hivyo. Andiko la Isaya 65:21 na 22 linatabiri hivi: “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine . . . Wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.”

14, 15. Kwa sababu gani tunaweza kuwa na uhakika kwamba watumishi wa Yehova wataweza kujenga paradiso?

14 Usitie shaka juu ya yale ambayo Yehova atatimiza katika Utaratibu Mpya kwa kutumia mioyo yenye nia na mikono ya watu wake. Hata leo mafundi wa ujenzi wanastaajabia mambo yanayotimizwa na Mashahidi wa Yehova katika kujenga majengo, kama Majumba ya Ufalme yanayojengwa kwa haraka. Baada ya moja la hayo kujengwa katika United States (Amerika), makala ya mhariri katika gazeti moja ilisema: ‘Kitu chenye thamani zaidi ya jengo kilifanyizwa na watu hao 2,000 wenye kujitolea. Viongozi wa kiserikali wanapaswa kuchungulia lililotimizwa mwisho-juma uliopita. Shauku, kujitoa na tamaa ya kutimiza mradi ni mambo yaliyotumiwa kwa matokeo ya kustaajabisha. Kama vikundi vya mitaa yetu vingeweza kutumia mambo ayo hayo, mradi wo wote​—iwe ni kugeuza vitu vilivyotumika viwe vya manufaa nyingine, kuzuia uhalifu au kuleta maendeleo ya jamii​—ungeweza kufikiwa. Jeshi la wafanya kazi lilithibitisha kwamba mwanadamu anaweza kufanya mengi wakati jumuiya inapokuwa na umoja. Tunatumaini Jumba la Ufalme ndipo mahali palipo na chemchemi ya kuchochea kundi la Mashahidi. Tayari kuwapo kwalo ni kichocheo kwetu sote.’

15 Moyo wa kupenda na ufundi huo wa watumishi wa Yehova utatumiwa kwa faida zilizo kubwa hata zaidi katika Utaratibu Mpya wa Mungu. Nalo litakuwa jambo la kufurahika namna gani kuondolea mbali maeneo yote yasiyopendeza na kuweka badala yake nyumba na mazingira ya kupendeza! Litakuwa jambo la kuridhisha namna gani kujua kwamba kila siku jitihada zako zitaifanya dunia hii ikaribie zaidi kwa siku moja kuwa Paradiso!

Jamaa ya Duniani Pote Yenye Umoja

16. Kwa sababu gani wakaaji wa Utaratibu Mpya hawatajisikia kamwe wakitishwa na jeuri?

16 Wala wakaaji wa Utaratibu Mpya hawatajisikia tena wakielekewa na tisho la uhalifu, fujo za wenye ghasia, wala vita. Zaburi 46:9 inasema: “[Mungu] avikomesha vita hata mwisho wa dunia.” “Mwana-Mfalme wa Amani,” Yesu Kristo, atahakikisha kumekuwa na amani ya kudumu duniani pote, kwa maana “kwa wingi wa utawala huo wa mwana-mfalme na kwa amani hakutakuwako mwisho.” (Isaya 9:6, 7, NW) Kukiwa na amani ya kweli, na jamaa nzima ya kibinadamu ikiwa imeelimishwa katika viwango bora vya namna moja, watu wote watakuwa na umoja katika kifungo cha upendo kisichovunjika. Hivyo, hakutakuwa tena na mipaka yo yote ya kitaifa yenye kuleta migawanyiko.

17. Amani na umoja ambao watumishi wa Mungu wanao hata sasa ni wa kadiri gani?

17 Je! ahadi hizo zimekolezwa chumvi tu? Hapana, kwa sababu amani na umoja ni mambo ambayo tayari yako kati ya wale wanaounyenyekea utawala wa Ufalme kwa ushikamanifu! Fikiria hili: Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni mbili na nusu wametapakaa kwenye sehemu zote za dunia. Hata hivyo, tayari wanatimiza andiko la Isaya 2:4, linalosema: “Nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” Hata wawe chini ya hali yo yote ile katika nchi yo yote ile, Mashahidi wa Yehova hawataua ndugu zao, au mtu mwingineye yote, kwa kukusudia. Ni kama vile kichapo cha Kiitalia II Corriere di Trieste kilivyosema: “Wako tayari kufa badala ya kuvunja wazo lile la msingi . . . USIUE!” Kwa sababu ya kufuata sana viwango vya Mungu, Mashahidi wa Yehova wana amani ya kweli na umoja, ambao hauwezi kupatikana na ulimwengu huu. Na uhakika wa kwamba mamilioni yao wanafurahia hali hiyo katikati ya ulimwengu wenye kujawa na ugomvi unashuhudia jambo litakalotukia wakati Ufalme wa Mungu utakaposimamia mambo yote ya dunia.​—Yohana 13:34, 35; 1 Yohana 3:10-12.

18, 19. Faida nyingine zinazowajia wale wanaofuata sana viwango vya juu vya Mungu ni zipi?

18 Zaidi ya amani na umoja huo ulio kati ya watu wa mataifa yote, kufuata sana viwango bora vya Mungu kunatokeza watu wanaojali jirani yao na mali ya jirani yao. Hivyo ‘wanajiendesha kwa unyofu katika mambo yote.’ (Waebrania 13:18, NW) Akiandika kuhusu jambo hilo, katika jarida Le Journal de Montreal, mwandikaji wa safu za mazeti aliye Mkanada-Mfaransa, alisema hivi juu ya Mashahidi wa Yehova: “Kama wao peke yao ndio wangekuwa katika ulimwengu, haingekuwa lazima tufunge milango yetu wala kuweka king’ora cha kutujulisha kuna wevi wakati wa usiku.”

19 Raia hao washikamanifu wa serikali ya Mungu hawana tatizo la uhalifu kati yao wenyewe, ingawa huo umekuwa usiozuilika katika ulimwengu. Pia, kwa kuwa wanafuata sana viwango vya juu vya Biblia kuhusu maadili, wao hawapigwi na magonjwa yanayopata watu kwa kufanya ngono za ovyoovyo, wala na utoaji wa mimba ulioenea sana katika kila taifa. Tena watumishi wa Yehova wanaheshimu sana ndoa, tofauti na maoni ya ulimwengu yenye kuachilia watu wafanye vyo vyote tu wanavyotaka katika mpango wa ndoa. Kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wanaweza kuendeleza viwango hivyo? Kwa sababu Yehova anaongoza waabudu wake washikamanifu, na “kwa Mungu yote yawezekana.”​—Mathayo 19:26.

Kukusanywa Kwenye Ibada ya Kweli

20. Ni shughuli gani iliyo ya maana kuliko zote nyakati za kisasa?

20 Watu wawe au wasiwe wanatambua, mkusanyo wa duniani pote wa kuingiza watu wenye mfano wa kondoo ndani ya tengenezo la Yehova ndiyo shughuli kubwa zaidi ya zote inayoendelea nyakati za kisasa. Hiyo inatimiza unabii wa ajabu wa Isaya 2:2, 3: “Na itakuwa katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya [Yehova, yaani, ibada yake ya kweli iliyoinuliwa] utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote watauendea makundi makundi. Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova], . . . naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.”

21. Watu wenye mioyo minyofu wanatiwa moyo wafanye nini?

21 Tunawatia moyo watu wote wenye mioyo minyofu wawe sehemu ya shughuli hiyo inayosisimua ulimwenguni pote ya kuelekea kwenye ibada ya kweli na serikali ya uadilifu. Furahia baraka ambazo zinakuja sasa kwa kushirikiana na kundi la watu linaloelimishwa katika sheria na kanuni za Mungu. Nyenyekea kwa ushikamanifu serikali ya Ufalme ambayo karibuni itaanza kugeuza dunia hii iwe paradiso. Utumaini Ufalme huo wala si mipango ya ulimwengu huu, kwa maana kama vile Zaburi 127:1 inavyosema: “[Yehova] asipoijenga nyumba waijengao wafanya kazi bure.” Itikia ukaribishaji wa Zaburi 66:5: “Njoni yatazameni matendo ya Mungu; hutisha kwa mambo awatendayo wanadamu.” Kwa hiyo njoni kwa Mungu anayetoa uhakikisho thabiti juu ya serikali iliyo bora kabisa kwa wanadamu, serikali itakayotimiza mambo asiyoweza mwanadmu, serikali ambayo karibuni sana itakuwa ndiyo peke yake itakayokuwa hapa duniani.​—Kutoka ml/15/85.

Wewe Ungejibuje?

◻ Kwa sababu gani tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatimiza makusudi yake?

◻ Kanuni ya ukombozi inatumikaje kuondolea mtu dhambi?

◻ Ni kazi gani kubwa za elimu na ujenzi zitakazokuwa katika Utaratibu Mpya?

◻ Kuna ushuhuda gani sasa wa kwamba amani, umoja, na upendo utakuwa duniani pote katika Utaratibu Mpya?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Chini ya utawala wa Ufalme, watu wote wanaopenda ukweli ‘watafundishwa na Yehova’

[Picha katika ukurasa wa 19]

Amani na umoja tayari ni mambo halisi kati ya wale wanaonyenyekea serikali ya Ufalme

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki