Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 7/1 kur. 13-18
  • Kuiona “Ishara” kwa Ufahamu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuiona “Ishara” kwa Ufahamu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kukusanya Wale Waliopewa Kibali ya Wokovu
  • Kazi Tukufu Inayofuata Uendeshaji wa Wapanda-Farasi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Ishara ya Siku za Mwisho
    Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
  • Hakuna “Upungufu wa Nguvu” wa Kiroho kwa Wenye Busara
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Kulinda Wakati wa “Umalizio wa Mfumo wa Mambo”
    Usalama Ulimwenguni Pote Chini ya “Mwana-Mfalme wa Amani”
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 7/1 kur. 13-18

Kuiona “Ishara” kwa Ufahamu

“Wakati alipokuwa akiketi juu ya Mlima wa Mizeituni, wanafunzi walimkaribia kwa faragha, wakisema: ‘Tuambie, Mambo hayo yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?’ “—MATHAYO 24:3, New World Translation.

1. Ni kwa sababu gani matukio yenye kuutikisa ulimwengu tangu mwaka wa 1914 hayakujitokeza yenyewe tu, na wanafunzi wa Yesu walimuuliza nini?

MATUKIO yenye kushtua ulimwengu tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ya 1914-1918 hayakujitokeza yenyewe tu. Yalitabiriwa karne 19 zilizopita na Yesu Kristo. Alikuwa amewaambia wanafunzi wake juu ya mambo mengi yenye kushtua ambayo yangekuja, na kwa sababu hiyo wakamuuliza: “Tuambie, Mambo hayo yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?”​—Mathayo 24:3, NW.

2. Ni kwa sababu gani mitume walitaka kujua zaidi ya mambo yale ambayo yangetokea kabla ya kuharibiwa kwa Yerusalemu mwaka wa 70 W.K.?

2 Mitume hao walitaka kujua zaidi ya yale ambayo yangetokea kati ya wakati huo na kuharibiwa kwa Yerusalemu. Yesu hakurudi ama kwa kuonekana au kwa kutokuonekana katika pindi hiyo yenye msiba. Wala mfumo wa mambo ambao ulikuwa umekuwako tangu Gharika haukumalizika wakati wa kuharibiwa kwa Yerusalemu mwaka wa 70 W.K. Kwa kweli, “ishara ya kuwapo [kwa Yesu kusikoonekana] na ya umalizio wa mfumo wa mambo” ingetokea muda mrefu baada ya uzima wa kidunia wa mitume wake.

3. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba “habari njema hizi za Ufalme” hazikuhubiriwa na dini za Jumuiya ya Wakristo wakati wa kufuatia uasi-imani wa baada ya mitume? (b) Je! Ufalme wa Mungu utashindwa wakati Umoja wa Mataifa utakaposhindwa?

3 Kupitia mifano ya kiunabii inayohusu Ufalme wa Mungu, Yesu alikuwa amewaambia mitume wake juu ya uasi wa kidini ambao ungetokea baada ya kurudi kwake mbinguni na kufa kwao. Katika muda wote wa uasi-imani huo, je, kungekuwako kuhubiri ko kote kwa “habari njema hizi za ufalme” ulimwenguni pote? (Mathayo 24:14, NW) Kwa hakika kama kungekuwako hakungefanywa na dini za Jumuiya ya Wakristo, na hali baadaye sana katika Desemba 1918 Muungano wa Baraza la Makanisa ya Kristo katika Amerika ulishangilia Ushirika wa Mataifa uliopendekezwa wakati huo kuwa “wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu duniani.” Kujapokuwa kuunga mkono huko kwa kidini, hata hivyo, Ushirika huo ulishindwa wakati Vita ya Ulimwengu ya Pili ilipotokea mwaka wa 1939. Lakini kwa Ushirika huo kushindwa hivyo, je, Ufalme wa Mungu wa kweli kweli ulishindwa? Hata! Wala hautashindwa wakati mrithi wa Ushirika huo, Umoja wa Mataifa, ushindwapo hivi karibuni. Badala yake, Ufalme huo wa kimungu utauharibu Umoja wa Mataifa, hata kuwe kunahitajiwa malaika wangapi wa kimbingu ili kutimiza hilo!

4. Ni kwa sababu gani kazi ya kuuhubiri Ufalme ingekuwa sehemu ya “ishara” hiyo?

4 Yote hayo yaliyotangulia yanasaidia kuleta ufahamu ulio wazi zaidi wa jambo hili la maana: Ilikuwa katika kujibu ombi la “ishara” la kwamba Yesu akawaambia wafuasi wake hivi: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14, NW) Hilo linaonyesha kwamba kuhubiriwa huko kwa Ufalme duniani pote kungekuwa sehemu ya “ishara” yenye sehemu nyingi ambayo ingetia alama ya “umalizio wa mfumo wa mambo.” Pia kungekuwa ushuhuda wenye kuonekana wa “kuwapo” kusikoonekana kwa Yesu Kristo. Ni jambo linalostahili kuangaliwa jinsi Yesu alivyopanga mfululizo wa matukio kabla ya unabii wake unaohusu kazi ya kuuhubiri Ufalme. Kwa sehemu alisema:

5. Ni zipi nyingine za sehemu za “ishara” ambayo Yesu alitaja kabla hajatabiri kuhubiriwa kwa Ufalme ulimwenguni pote?

5 “Mtasikia habari za vita na ripoti za vita; angalieni msitishwe. Kwa maana ni lazima mambo hayo yatukie, lakini ule mwisho bado. Kwa maana taifa litainuka juu ya taifa na ufalme juu ya ufalme, na kutakuwako upungufu wa chakula na matetemeko ya ardhi mahali hapa na mahali hapa. . . . Na kwa sababu ya kuongezeka kwa kutokutii sheria upendo wa wengi zaidi utapoa. Lakini yeye ambaye amevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.”​—Mathayo 24:6-13, NW.

6. Ni kwa sababu gani sehemu za “ishara” hiyo si mwendelezo tu wa kielelezo tu cha mambo yaliyotangulia?

6 Ni kweli kwamba kabla ya hapo kulikuwa kumekuwako vita, upungufu wa chakula, matetemeko ya ardhi, na magonjwa ya kuambukia katika karne zote za Wakati wa Kawaida wetu mpaka 1914. (Luka 21:11) Hata hivyo, hakukuwa kumekuwako cho chote cha kulinganika na mambo ambayo yametokea tangu Nyakati za Mataifa kumalizika katika mwaka huo wa maana sana. Ugomvi wa kimataifa uliochochewa kwa mshangao katika kiangazi cha mwaka wa 1914 uliongezeka ukawa pambano la kijeshi ambalo hatimaye lilishirikiwa na mataifa 28. Matetemeko ya ardhi ya asili yaliambatana na msukosuko huo wa kibinadamu. Kulikuwako upungufu wa chakula, au njaa kubwa, na katika mwaka wa mwisho wa vita hiyo ya ulimwengu kukaja magonjwa ya kuambukia yaliyo mfano wa mwivi yanayoitwa homa kali ya Hispania iliyoua watu zaidi ya 20,000,000. Yote hayo hayakuwa mwendelezo tu wa kielelezo cha mambo yaliyokuwa yakitokea hapo mbele. Ulikuwa mwanzo wa mfululizo wa matukio yanayoifanyiza “ishara” ya kwamba mfumo wa mambo huu umo katika ‘wakati wake wa mwisho’ uliotabiriwa. (Danieli 12:4) Kitabu cha mwisho cha Biblia​—Ufunuo​—kinahakikisha jambo hilo.

7. Ni kwa sababu gani kitabu cha Ufunuo kiliandikwa, na mambo mengi yaliyomo ‘ambayo yalitolewa katika ishara’ yangeonyesha nini?

7 Mtume Yohana, aliyepewa Ufunuo huo, aliamriwa auandike kwa kusudi la pekee. Kwa kusudi gani? Hili: ‘Ili kuonyesha watumwa wa Mungu mambo ambayo hayana budi kuwako upesi.’ Na kwenye umalizio wa Ufunuo Bwana Yesu Kristo anasema: “Naam; naja upesi.” Kisha Yohana anajibu: “Amina; na uje, Bwana Yesu.” Kwa hiyo mambo mengi ‘yaliyotolewa katika ishara’ (NW), yakitokea katika historia, yangeonyesha kwamba tunaishi “wakati wa mwisho” wa huu mfumo wa mambo. (Ufunuo 1:1; 22:20) Ndiyo, yangetusaidia tuone kwa ufahamu “ishara” yenye sehemu nyingi.

8. Mpandaji wa “farasi mweupe” ni nani, na Mungu alimpa mamlaka ya kutoka kwenda dhidi ya maadui wake wakati gani?

8 Katika Ufunuo sura ya 6 kuna masimulizi ya mambo ambayo yameitwa “wapanda farasi wa kitabu cha Ufunuo.” Anayeonekana kwanza ni mpanda “farasi mweupe,” Yesu Kristo aliyetukuzwa, akisonga mbele akafanye vita dhidi ya adui zake. Alipewa mamlaka ya kufanya hivyo na Mungu mwishoni mwa Nyakati za Mataifa, wakati adui za Yesu mbinguni na duniani walipaswa kujitiisha kwa utawala wake.​—Zaburi 2:1-12.

9. Ni nini kinachofananishwa na mpandaji wa (a) farasi “mwekundu sana”? (b) “farasi mweusi”? (c) “farasi wa rangi ya kijivujivu”?

9 Mpandaji yule farasi wa pili “mwekundu sana” alifananisha vita ya mataifa yote, kwa maana alipewa silaha ya kijeshi, “upanga mkubwa.” Juu ya farasi wa tatu, “farasi mweusi,” kulikuwa mpandaji mwenye kufananisha upungufu wa chakula. Twajuaje hilo? Kwa maana alibeba ratili ya kupimia chakula kilicho kawaida ya watu wengi kikiwa cha bei kubwa sana. Mpandaji wa nne, akiwa juu ya “farasi wa rangi ya kijivujivu” mwenye kuonekana mgonjwa-mgonjwa, alifananisha magonjwa ya kuambukia, kwa maana masimulizi hayo yanasema: “Na yeye aliyemupanda jina lake ni mauti, na Hadeze [kaburi] akafuatana naye.” (ZSB) Ni kweli kwamba mpandaji huyo wa nne alipewa mamlaka aue “kwa upanga mrefu” (NW) wa vita “na kwa njaa . . . na kwa hayawani wa nchi.” Hata hivyo, ni jambo linalofaa kuangaliwa kwamba yeye pia alipewa mamlaka aitumie kuua watu waingie katika kaburi (Hadesi) kupitia “tauni [“tauni yenye kuua,” NW].”​—Ufunuo 6:1-8.

10. Ni mambo gani yangetokea baada ya muhuri wa tano na sita kufunguliwa, na wakaaji wa dunia wangelazimika kukubali nini?

10 Baada ya mtume Yohana kuona maono hayo ya mambo ambayo yangetia alama “umalizio wa mfumo wa mambo,” aliona muhuri ya tano na sita za kitabu cha kukunjwa zikifunguliwa. Hapo aliona maono ya matukio ya kiasili yenye kushtua sana, yakianza kwa “tetemeko kuu la ardhi.” Mwishowe, wakaaji wa dunia wakalazimika kukubali hivi: “Siku iliyo kuu, ya hasira yao [Yehova Mungu na Yesu Kristo], imekuja.” Kumalizika kwa siku hiyo ya mfano ya hasira kungeonyesha kwamba mwisho wa wategemezaji wa ulimwengu huu ulikuwa umefika hatimaye.​—Ufunuo 6:9-17.

Kukusanya Wale Waliopewa Kibali ya Wokovu

11. Yesu alitumia mfano gani kuonyesha uhakika wa yale aliyotabiri kuhusu “kuwapo” kwake na “umalizio wa mfumo wa mambo”?

11 Akitoa “ishara” ya “kuwapo” kwake “na ya umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu alisema: “Basi kwa mtini jifunzeni mfano; tawi lake likiisha kuchipuka na kuchanua majani, mwatambua ya kuwa wakati wa mavuno u karibu; nanyi kadhalika, myaonapo hayo yote, tambueni ya kuwa yu karibu, milangoni. Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia. Mbingu na [dunia] zitapita; lakini maneno yangu hayatapita kamwe.”​—Mathayo 24:32-35.

12, 13. (a) Msiba wa taifa zima la Kiyahudi wa 70 W.K. ulifananisha nini? (b) Msiba huo ulikuwa mfano wa kiunabii wa nini? (c) Kwa hiyo, Yesu aliendelea kutabiri nini kuhusu kuja kwake?

12 Wakati Waroma walipouharibu Yerusalemu na hekalu lake mwaka wa 70 W.K. sawa na alivyokuwa ametabiri Yesu, dhiki hiyo mbaya sana juu ya Wayahudi haikuonyesha kwamba alikuwa amekuja mara ya pili na kwamba kuwapo wake kusikoonekana kulikuwa kumeanza. (Mathayo 24:15-21) Kwa kuwa Biblia inatumia Yerusalemu wa kale kuwa mfano, msiba huo wenye kushtua wa mwaka wa 70 W.K. ulikuwa mfano wa kiunabii hasa. Ulionyesha kwa njia ndogo mambo ambayo yangetokea ulimwenguni pote baada ya Nyakati za Mataifa kumalizika mwaka wa 1914 na kwa hiyo baada ya Yesu Kristo kuanza hasa kuwapo kwake kusikoonekana. Ndiyo sababu Yesu alisema hivi pia:

13 “Lakini mara, baada ya dhiki ya siku zile, jua litatiwa giza, na mwezi hautatoa mwanga wake, na nyota zitaanguka mbinguni, na nguvu za mbinguni zitatikisika; ndipo itakapoonekana ishara yake Mwana wa Adamu mbinguni; ndipo mataifa yote ya ulimwengu watakapoomboleza, nao watamwona Mwana wa Adamu akija juu ya mawingu ya mbinguni pamoja na nguvu na utukufu mwingi. Naye atawatuma malaika zake pamoja na sauti kuu ya parapanda, nao watawakusanya wateule wake toka pepo nne, toka mwisho huu wa mbingu mpaka mwisho huu.”​—Mathayo 24:29-31.

14. Ni agano gani na dhabihu gani inayotajwa katika Zaburi 50:5?

14 Kukusanywa kulikotabiriwa kwa “wateule” hao wakati wa umalizio wa huu mfumo wa mambo ni utimizo wa amri ya Mungu: “Nikusanyieni wacha Mungu wangu waliofanya agano nami kwa dhabihu.” (Zaburi 50:5) Kwa kuwa Yehova analiita ni “agano lake” (NW), haiwezi ikawa ni wakfu ambao mtu binafsi anajiweka kwa Mungu akiisha kuwa Mkristo na ambao angeweza kujifunga kwao kwa kujitoa dhabihu yeye binafsi. La, agano hilo lililofanywa kati ya Yehova na “wacha Mungu” ni “agano jipya” la Mungu aliloahidi kufanya na nyumba ya kiroho ya Israeli. Dhabihu ambayo ni msingi wa agano jipya hilo ni dhabihu ya ukombozi ya “Mwana wa Adamu,” Yesu Kristo.​—Yeremia 31:31-34; Mathayo 24:30.

15. “Wacha Mungu” ni nani, na sasa wanatumika wakiwa kama nini kwa ulimwengu?

15 “Wacha Mungu” wanaoingizwa kwenye agano jipya hilo wanafanywa kuwa Waisraeli wa kiroho. (Luka 22:19, 20) Mungu anaagiza kukusanywa huko kufanywe ili aweze kuchunguza hao waliokusanywa, awape kibali walio washikamanifu na kukataa wale wasioishi kulingana na madai yao kuwa ndani ya agano lake, agano jipya. (Zaburi 50:16) Tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, ushuhuda ni kwamba Jumuiya ya Wakristo, inayodai kuwa imo ndani ya agano jipya, haijawa yenye kukubalika kwa Yehova Mungu. Tofauti sana nayo kuna baki dogo la wanafunzi wa Mpatanishi wa agano jipya, Yesu Kristo ambalo li wakfu kikweli na kubatizwa. Wamejithibitisha kuwa Waisraeli wa kiroho. Washikaji hao wa agano jipya walio washikamanifu ndio “wateule” ambao Mwana wa Adamu anajikusanyia kupitia malaika zake. Wanatimiza matakwa ya agano jipya, “agano langu” (NW), kama anavyoliita Mungu. Kwa sababu ya utendaji wao katika kuunga mkono Ufalme wa Mungu mikononi mwa Yesu Kristo, wamekuwa ‘ishara’ kwa ulimwengu wote.​—Isaya 8:18; Waebrania 2:12, 14.

16. (a) Ni wakati gani kulipokuwa kuamka kwa kiroho kwa mabaki ya “wacha Mungu”? (b) Katika mfano wa wanawali kumi, Bwana-arusi ni nani, na ni nani wanaofanyiza bibi-arusi wake wa mfano?

16 Baki hilo la “wacha Mungu,” lilipasa kuamka kiroho wakati wa sehemu ya kwanza ya “umalizio wa mfumo wa mambo.” Hiyo ilikuwa sehemu yenye kutokeza ya “ishara” ambayo Yesu alitabiri katika unabii wake mkuu. Kwa baki hilo, wakati huo wa kuamka ulikuwa wa furaha kubwa, furaha kama ile ya wanawali wenye akili watano, au wenye hekima, walioamshwa na kilio cha usiku wa manane: “Haya, bwana arusi; tokeni mwende kumlaki.” (Mathayo 25:1-6) Kuamka huko kwenye furaha kulitokea katika masika ya 1919, wakati mabaki wapakwa mafuta walipoanza kupata nafuu kutokana na matokeo ya mateso na vipingamizi vya ulimwenguni pote walivyokuwa wamepatwa navyo wakati wa kipindi chenye taabu cha Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Bwana-arusi wa mfano huo wa wanawali kumi, bila shaka ni Yesu Kristo, na bibi-arusi wake wa mfano ni kundi lake lenye ushikamanifu la washiriki 144,000 ambao watashirikiana naye katika Ufalme wa kimbingu. (Ufunuo 14:1-4) Elimu ya tarehe za Biblia na ulingani mbalimbali wa kisasa vinaonyesha kwamba Mfalme Bwana-harusi alikuja kwenye hekalu la kiroho katika masika ya 1918. Halafu akaanza kuwafufua washiriki waaminifu waliokufa wa bibi-arusi wa kiroho na kuwaunganisha na yeye mwenyewe katika Ufalme wa kimbingu. Ukiwa ndio usemi wa mabaki ya bibi-arusi, wanaofananishwa na wanawali wenye akili, andiko la Ufunuo 19:7 linasema: “Na tufurahi, tukashangilie, tukampe utukufu wake; kwa kuwa arusi ya Mwana-Kondoo imekuja, na mkewe amejiweka tayari.”

17. (a) Ni kwa sababu gani jamii ya ‘wanawali wenye akili’ ingeweza kufurahi? (b) Wanawali wenye akili walibeba nini, na kwa hiyo wangeweza kufanya nini?

17 Ndiyo, wakati wa kuamka kiroho kwa jamii ya wale ‘wanawali wenye akili’ na kupata kwao kuelewa maana ya “ishara” iliyoanza kuonekana mwaka wa 1914 ilikuwa pindi ya furaha kubwa. Ndipo maneno haya yakawahusu: “[Wenye furaha ni] walioalikwa karamu ya arusi ya Mwana-Kondoo.” (Ufunuo 19:9) Katika mfano wa Yesu, wale wanawali watano wenye akili walibeba akiba ya mafuta ya taa ili waweze kuwasha taa zao tena na hivyo wajiunge na mwandamano wenye furaha wa ndoa wakiwa na taa zilizowaka. Bwana-arusi alipofika, “[wanawali] waliokuwa tayari wakaingia pamoja naye arusini; mlango ukafungwa.”​—Mathayo 25:1-10.

18. (a) Baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, mabaki ya wapakwa mafuta wangali walikuwa na Neno la Mungu lenye kutoa nuru ya maarifa na roho takatifu yake ndani yao kuwezeshwa kufanya nini? (b) Ni nini kilichotangazwa kwenye kusanyiko lao la kwanza la baada ya vita?

18 Kwa utimizo wa mfano wa wale wanawali wenye akili watano, mabaki wapakwa mafuta walimkaribisha kwa shangwe na furaha Bwana-arusi wao wa kimbingu, ambaye wakati wake wa kufunga ndoa na kundi lake la bibi-arusi ulikuwa umefika. Baada ya mambo yaliyowapata yenye kuhuzunisha kiroho wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, walikuwa wangali wana Neno la Mungu lenye kutoa nuru ya maarifa ya kutosha na roho takatifu yake ndani yao wakiwa “vyombo vya udongo” ili kuanzisha tena kazi yao ya kuwapa wanadamu nuru ya maarifa kuhusu Ufalme wa Mungu mikononi mwa Mfalme-Bwana-arusi wake. (2 Wakorintho 4:7) Kwa hiyo, katika Septemba 1-8, 1919, jamii ya ‘wanawali wenye akili’ ilifanya kusanyiko lao la kwanza la mataifa yote katika Cedar Point, Ohio. Huko tangazo lilitolewa la kusudio la kuchapishwa gazeti jipya kuongezea Mnara wa Mlinzi. Gazeti hilo jipya lingeitwa The Golden Age, jina ambalo lilieleza aina ya kipindi ambacho wanadamu waliorudishwa watafurahia wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Mfalme-Bwana-arusi Yesu Kristo. Gazeti hilo lingali linachapishwa, sasa likiwa linaitwa Amkeni!

19. (a) Jamii ya ‘wanawali wenye akili’ ilikuwaje sehemu yenye kutokeza ya “ishara” ya “kuwapo” kwa Yesu? (b) Ni nani sasa walio wenye furaha duniani?

19 Muda mfupi baada ya kusanyiko hilo, toleo la kwanza la The Golden Age​—lile la Oktoba 1, 1919—lilichapishwa. Kwa gazeti hilo na vichapo vingine vya Sosaiti, ‘jamii ya wanawali’ washikamanifu ilisonga mbele na mgawo wao wa kuangazia ulimwengu. Walianzisha kazi ya baada ya vita ya ‘kuhubiri habari njema hizi za ufalme kwa ushuhuda kwa mataifa yote’ kabla ya mwisho wa huu mfumo wa mambo kuja. (Mathayo 24:14, NW) Kwa njia hiyo mabaki wapakwa mafuta, jamii ya ‘wanawali wenye akili,’ ikawa sehemu yenye kutokeza ya “ishara” yenye sehemu nyingi yenye kutia alama “kuwapo” kwa Yesu kusikoonekana akiwa Mfalme mwenye uwezo na “umalizio wa mfumo wa mambo.” Kazi hiyo ya kutoa nuru ya maarifa ni uthibitisho zaidi kwamba “wakati wa mwisho” ulianza mwishoni mwa Nyakati za Mataifa mwaka wa 1914. Wenye furaha ni wale wote ambao wakiwa na ufahamu wanaona sehemu hiyo iliyotabiriwa ya “ishara” hiyo katika umaana wayo wote!

Wewe Ungejibuje?

◻ Kazi ya kuuhubiri Ufalme ni sehemu ya nini?

◻Ni nani au ni nini kinachofananishwa na mpandaji farasi mweupe; farasi mwekundu sana; farasi mweusi; farasi wa kijivujivu?

◻ Msiba wa taifa zima la Kiyahudi mwaka wa 70 W.K. ulikuwa mfano wa kiunabii wa nini?

◻ Ni nani wanaofanyiza jamii ya ‘wanawali wenye akili,’ na ni kwa sababu gani wanaweza kufurahi?

[Picha katika ukurasa wa 14]

‘Tuambie, ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako?’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki