Endeleeni Kuepuka Mtego wa Pupa
“Jihadharini na pupa ya kila aina, kwa maana hata mtu anapokuwa na vingi, utajiri wake haumpi uzima.”—LUKA 12:15, The New English Bible.
1. Kwa sababu gani onyo la Paulo juu ya pupa ni la wakati unaofaa?
TUNAISHI katika ulimwengu unaoabudu ufanisi wa mali. Faida za kibiashara daima zinavutia pupa ya watu ya kutaka kujitajirisha. Kufanikiwa kwa kawaida kunapimwa kwa kulingana na ukubwa wa mshahara. Kwa hiyo, maonyo mengi ya Biblia dhidi ya pupa na uovu unaohusiana nayo wa kutamani yanafaa kabisa. (Wakolosai 3:5; 1 Timotheo 6:10) Kulingana na kamusi, pupa na kutamani yote yanahusu “kuwa na au kuonyesha tamaa kubwa ya mali na hasa vitu vya kimwili. “Pupa yaweza kuwa jambo lenye uzito kama vile uasherati au ibada ya sanamu, kwa maana Paulo alionya hivi: “Msichangamane na mtu aitwaye ndugu, akiwa ni mzinzi au mwenye kutamani au mwenye kuabudu sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi; mtu wa namna hii msikubali hata kula naye.”—1 Wakorintho 5:11; Waefeso 5:3, 5.
2. Ni maonyo gani ambayo Yesu na Yehova wanatupa juu ya kutamani?
2 Yesu aliwaonya wafuasi wake hivi: “Jihadharini na kila aina ya tamaa.” (Luka 12:15, HNWW) Na Yehova mwenyewe alitia amri hiyo ya kuonya juu ya uovu huo kati ya zile Amri Kumi: “Usiitamani nyumba ya jirani yako, usimtamani mke wa jirani yako; wala mtumwa wake, wala mjakazi wake, wala cho chote alicho nacho jirani yako.”—Kutoka 20:17; Warumi 13:9.
Hakuna Ye Yote Anayeweza Kujikalia Kizembe Tu
3. Pupa ilimshindaje Hawa na baadaye Waisraeli?
3 Ukweli ni kwamba hakuna ye yote anayeweza kuacha kujihadhari na pupa na tamaa. Hawa alipofanya dhambi katika bustani ya Edeni, ilikuwa ni kwa sababu ya pupa: “Mwanamke [aliona] ya kuwa ule mti wafaa kwa chakula, wapendeza macho, nao ni mti wa kutamanika.” (Mwanzo 3:6) Katika pindi moja jangwani, Waisraeli walionyesha pupa yenye kuchukiza. Katika kujibu malalamiko yao juu ya kula mana peke yake, Yehova alipotoa kware kwa utele, walitenda kama walafi wakaadhibiwa vikali.—Hesabu 11:4-6, 31-33.
4. Ni mifano gani mingine ya kihistoria inayoonyesha hatari za pupa?
4 Baadaye, kwenye pigano la Yeriko, ni pupa iliyomsukuma Akani aibe fedha na dhahabu na vazi la thamani kutoka kati ya nyara za mji huo. (Yoshua 7:20, 21) Pupa ilimfanya Gehazi, mtumishi wa Elisha, ajaribu kujifaidi kifedha kwa maponesho ya kimuujiza ya ukoma wa Naamani. (2 Wafalme 5:20-27) Mfalme Ahabu alikuwa mtu mwingine mwenye pupa. Aliruhusu Yezebeli, mkeye mpagani, afanye hila ya kuuawa kwa Nabothi, jirani yake, ili anyakue shamba la mizabibu la Nabothi. (1 Wafalme 21:1-19) Mwishowe, Yuda Iskariote, mshiriki wa karibu sana wa Yesu, alitumia kwa pupa cheo chake kuiba pesa za shirika. Na pupa ilimwongoza amsaliti Yesu kwa ajili ya vipande 30 vya fedha.—Mathayo 26:14-16; Yohana 12:6.
5. Tunajifunza nini kwa mambo yaliyowapata watu wa aina tofauti walioanguka katika mtego wa pupa?
5 Wote hao wenye pupa waliadhibiwa. Lakini je, umeona aina tofauti tofauti za watu walioangukia mtego wa pupa? Hawa alikuwa mwanamke mkamilifu aliyekuwa akiishi katika Paradiso. Akani na Waisraeli walikuwa wameshuhudia kibinafsi miujiza ya Yehova. Ahabu alikuwa mfalme, labda akiwa ndiye mwanamume mwenye utajiri zaidi katika nchi hiyo. Gehazi na Yuda walikuwa wamebarikiwa na ushirika wenye utajiri mwingi wa kiroho na mapendeleo makubwa ya utumishi. Lakini wote wakawa wenye pupa. Kwa hiyo ye yote—hata awe tajiri namna gani, hata awe mwenye pendeleo kubwa la utumishi namna gani, hata awe ni mwenye ujuzi gani—anaweza kuanguka katika mtego huo. Basi si ajabu Yesu alionya hivi: “Jihadharini na kila aina ya tamaa”!—Luka 12:15, HNWW.
6. Ni nini kinahitajiwa iwapo tutaepuka mtego wa pupa?
6 Lakini tunaweza kufanyaje hivyo? Ni kwa kujiweza tu na kujichunguza daima binafsi. Pupa inaanzia moyoni. Ili kuepuka mtego wa pupa, ni lazima tuchunguze mioyo yetu daima tuone kama wonyesho fulani wa pupa unatia mizizi humo. Biblia inatusaidia kufanya hivyo. Jinsi gani? Kwanza, ina maandishi ya mambo yaliyosemwa na Yesu na wanafunzi wake juu ya pupa. Tunapochunguza maelezo hayo, yanatudokezea tujiulize maswali fulani ya kindani tuone msimamo wetu ni nini kwa habari ya pupa.
Kuchunguza Nia Zetu
7. Jibu la Yesu kwa mwanamume yule aliyekuwa na ugomvi wa urithi linatusaidiaje kujichunguza?
7 Onyo la Yesu juu ya tamaa lilitokezwa na ombi hili la mmoja wa wasikilizaji wake: “Mwalimu, mwambie ndugu yangu anigawie urithi wetu.” Yesu alijibu: “Mtu wewe, ni nani aliyeniweka mimi kuwa mwamuzi au mgawanyi juu yenu?” (Luka 12:13, 14) Halafu akaendelea kuonya juu ya tamaa. Yesu hakutaka kujiingiza katika ugomvi wa mambo ya kimwili, kwa sababu ya kazi ya kiroho yenye maana aliyokuwa amekuja hapa kuitimiza. (Yohana 18:37) Lakini mazungumzo hayo yanadokeza maswali yenye kuchunguza mambo kindani ambayo tungeweza kujiuliza wenyewe. Tuseme hatuna uhitaji fulani, lakini tuwe na maoni ya kwamba tuna haki ya mali au utajiri fulani wenye kugombaniwa. Tungepigana kwa kadiri gani ili tushinde kesi yetu? Tungetoa kadiri gani ya utumishi wetu kwa Yehova au ya uhusiano wetu na ndugu zetu ili tushinde tunazoona kuwa ni haki zetu?—Mithali 20:21; 1 Wakorintho 6:7.
8. Tunaweza kuepukaje kuwa kama waandishi waliotajwa na Yesu katika Luka 20:46, 47?
8 Fikiria maelezo mengine ya Yesu. Aliwaonya wafuasi wake hivi: “Jilindeni na waandishi . . . [wanaokula] nyumba za wajane.” (Luka 20:46, 47) Huo ulikuwa wonyesho wa pupa wenye ukatili namna gani! Bila shaka, Wakristo wana daraka la kutunza wajane, wala si kuwala. (Yakobo 1:27) Lakini, tuseme unamjua mjane aliyelipwa na bima kiasi kikubwa, nawe unahitaji haraka pesa za dharura. Je! wazo lako la kwanza lingekuwa kumwendea mjane huyo, ukiwa na maoni kwamba ndiye rahisi kushawishwa, au kwamba anapaswa kusaidia kwa sababu ‘yeye ana mapesa’? Au tuseme umekwisha kukopa pesa, na sasa una shida ya kuzilipa. Je! ungehisi una haki ya kungojea kabla ya kulipa mjane huyo, kwa sababu ‘hataleta matata,’ au labda kwa sababu unafikiri ‘hahitaji pesa hizo sana’? Tunapaswa kuwa waangalifu tusiruhusu kanuni zetu zipotolewe tunapokabili matatizo ya kifedha.
9. Tunaweza kuangukaje katika mtego wa ‘kupendelea watu wenye cheo kwa faida ya kibinafsi’?
9 Pia Yuda alieleza njia moja ambayo pupa yaweza kututega. Alizungumza juu ya watu ambao walikuwa wamejiingiza katika kundi la Kikristo na walikuwa wakilichafua kwa pupa yao na mwenendo wao mpotovu, na “kuthibitika kuwa wawongo kwa Mwenyewe wetu mmoja tu na Bwana, Yesu Kristo.” (Yuda 4, NW) Pia, walikuwa “wakipendelea watu wenye cheo kwa ajili ya faida [ya kibinafsi].” (Yuda 16) Hatungependa kuwa kama wao. Lakini ebu fikiria: Je! tunajikuta tukipendelea kuutumia wakati pamoja na Wakristo wenye utajiri zaidi na kutoshughulika sana na walio maskini zaidi katika kundi? Ikiwa ndivyo, je, yaweza ikawa tunatumaini kufaidika kwa njia fulani? (Linganisha Matendo 20:33; 1 Wathesalonike 2:5.) Tunapokaribisha walio na madaraka katika tengenezo, je, tunafanya hivyo kwa sababu ya upendo au ni kwa sababu tunatumaini kupata mapendeleo fulani kama malipo? Kama tunafanya hivyo ili tulipwe, labda sisi pia ‘tunapendelea watu wenye cheo kwa ajili ya faida ya kibinafsi.’
10. Ni katika njia gani inawezekana kujipatia faida ya kifedha kupitia ibada yetu kwa Yehova? Tukifanya hivyo, tunafuata mfano wa nani?
10 Wonyesho mmoja wa pupa uliomuudhi sana Yesu ulikuwa wakati alipoona “pale hekaluni watu waliokuwa wakiuza ng’ombe na kondoo na njiwa, na wenye kuvunja fedha wameketi.” Bidii kwa ajili ya nyumba ya Yehova ilimsukuma awafukuze watoke hekaluni na kusema: “Msiifanye nyumba ya Baba yangu kuwa nyumba ya biashara.” (Yohana 2:13-17) Je! tuna bidii kama hiyo? Basi ingekuwa vema kujiuliza hivi: Je! mimi ningezungumza mambo ya kibiashara kwenye Jumba la Ufalme? Je! mimi ninatia moyo shughuli za kibiashara kati ya Wakristo wenzangu kwa sababu kuwa kwao ndugu za kiroho kunafanya iwe vigumu zaidi kwao kukataa? Je! mimi ninatumia marafiki wengi nilio nao katika tengenezo ili niwe na watu wengi zaidi wa kufanya biashara nao? Hakika sisi hatupaswi kutengeneza faida kwa pupa kwa kuutumia vibaya uhusiano wetu pamoja na ndugu zetu.
11. Ni kanuni gani za Kikristo zinazotusaidia tudumishe maoni yanayofaa tunapoendesha biashara sisi kwa sisi?
11 Je! hiyo maana yake ni kwamba Wakristo hawawezi kufanya biashara pamoja? La. Maana yake ni kwamba kuna wakati na mahali pa kufanyia biashara, na wakati mwingine na mahali pengine pa kufanyia ibada. (Mhubiri 3:1) Lakini, Wakristo wanapokuwa na ushirikiano wa kibiashara, hawapaswi kusahau kanuni za Biblia. Mkristo anapofanya mapatano ya biashara, hapaswi kutafuta njia za kuepa kutimiza madaraka yake yanayompasa kisheria. (Mathayo 5:37) Wala hatakuwa asiyetaka kusamehe au mwenye kutaka kulipa kisasi biashara ikiharibika na kuleta hasara. Mtume Paulo aliwaandikia Wakorintho hivi: “Basi imekuwa upungufu kwenu kabisa kwamba mnashitakiana ninyi kwa ninyi. Maana si afadhali kudhulumiwa? Maana si afadhali kunyang’anywa mali zenu?” (1 Wakorintho 6:7) Je! wewe, kwa ajili ya kundi, ungechagua kunyang’anywa (kupunjwa) badala ya kwenda mahakamani?
12. Ni kanuni gani za Biblia zitakazosaidia wale wanaoshughulika na biashara waepuke mtego wa pupa?
12 Mkristo ye yote anayeshughulika na biashara apaswa kuwa mwangalifu sana. Leo mazoea mengi ya kibiashara ni yenye ukatili mwingi, lakini Mkristo hawezi kutenda hivyo. Hapaswi kusahau kamwe kwamba yeye ni mwanafunzi wa Kristo. Yeye hataki kuwa na sifa mbaya kwamba yeye si mnyofu wala mwenye mazoea ya ukatili. (Linganisha Mithali 20:14; Isaya 33:15.) Naye hapaswi kusahau kamwe onyo la Yesu dhidi ya kufanya utajiri uwe mungu, wala onyo la Yohana dhidi ya “tamaa ya mwili na tamaa ya macho na kujionyesha kwa mtu mali yake.” (1 Yohana 2:16, NW; Mathayo 6:24) Wewe ukiwa mfanyi biashara Mkristo, je, unaweza kupinga kishawishi cha kuamsha pupa ya watu wengine ili uuze bidhaa nyingi? Au ungejifaidi kwa hali yao ya kufuatia upepo au kiburi chao ili kuendeleza biashara yako? Je! wewe unaiendesha kazi yako ya kimwili kwa njia ambayo huoni aibu kusema na Yehova juu ya kazi hiyo katika sala zako?—Mathayo 6:11; Wafilipi 4:6, 7.
13, 14. (a) Wakristo matajiri wanapaswa kudumisha usawaziko gani? Na wale ambao si matajiri wanapaswa kudumisha usawaziko gani? (b) Sala iliyo katika Mithali 30:8 inatusaidiaje tujifunze kuwa wenye kiasi kwa habari ya utajiri?
13 Hatimaye, Paulo alimwandikia Timotheo hivi: “Hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu.” (1 Timotheo 6:9) Kuwa tajiri si dhambi, ingawa utajiri unatokeza matatizo yake na vishawishi vyake. (Mathayo 19:24-26) Hatari iko katika ‘kutaka (‘kuazimia,’ NW) kuwa tajiri.’ Kwa mfano, mzee mmoja alisema: “Tatizo mara nyingi linatokea wakati mtu anapomwangalia nduguye Mkristo aliye tajiri na kusema: ‘Mbona mimi nisiwe kama yeye?’ “
14 Biblia inasihi hivi: “Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo; kwa kuwa yeye mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.” (Waebrania 13:5) Ikiwa wewe ni tajiri, je, unaliona hilo kuwa zawadi, jambo ambalo unaweza kutumia katika utumishi wa Yehova? Katika pindi moja, Yesu alimwambia mwanamume mmoja kijana kwamba kama alitaka kumfuata, angepaswa kutoa utajiri wake wote awape wengine. Kama Yesu angalikuambia wewe hayo, je, ungalichagua kubaki na utajiri wako au kumfuata Yesu? (Mathayo 19:20-23) Ikiwa wewe si tajiri, unaweza kuridhika na hali yako? Je! unaweza kuepuka mtego wa kutamani? Je! una nia ya kuitumaini ahadi ya Yehova: “Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa”?—Ona pia Mithali 30:8.
Jitajirishe kwa Mungu
15, 16. (a) Yesu alitumia mfano gani kukazia shauri lake juu ya kutotamani? (b) Tatizo la msingi la mwanamume yule katika mfano wa Yesu lilikuwa nini?
15 Yesu alipowaonya wasikilizaji wake ‘wajihadhari na kila aina ya tamaa,’ aliendelea kueleza juu ya mkulima mmoja ambaye mashamba yake yalizaa kwa utele. Mtu huyo “akaanza kuwaza moyoni mwake, akisema, Nifanyeje? maana sina pa kuyaweka akiba mavuno yangu. Akasema, Nitafanya hivi; nitazivunja ghala zangu, nijenge nyingine kubwa zaidi, na humo nitaweka nafaka yangu yote na vitu vyangu. Kisha, nitajiambia, Ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi.” Lakini, usiku uo huo, mtu huyo akafa. Utajiri wote huo uliorundikwa haukumsaidia hata kidogo. Yesu alimalizia hivi: “Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu.”—Luka 12:16-21.
16 Je! mtu huyo alitenda dhambi nzito yo yote, kama vile kunyang’anya au kuiba? Mfano huo hausemi hivyo. Lakini bado alikuwa na tatizo. Alitegemea utajiri wake ili awe na wakati ujao salama akasahau jambo la maana zaidi: ‘kujitajirisha kwa Mungu.’ Wakristo wa kweli wanaweza kuepuka mtego wa pupa na hivyo kutokuwa sehemu ya ulimwengu hasa kwa sababu wanafanya uhusiano wao na Mungu kuwa jambo la maana zaidi.—Yohana 17:16.
17. Mkristo mwenye usawaziko analionaje tatizo la kujiruzuku?
17 Wakati mmoja Yesu alishauri hivi: “Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? au Tunywe nini? au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta.” (Mathayo 6:31, 32) Ni kweli kwamba sisi sote tunakabili matatizo yale yale ambayo “Mataifa” wanakabili. Wengi wetu tunalazimika kufanya kazi kwa bidii ili tupate kujiruzuku kwa kununua vitu vya lazima vya kula, kunywa, na kuvaa. (2 Wathesalonike 3:10-12) Lakini haturuhusu mahangaiko hayo yawe ya maana kuliko ‘kujitajirisha kwa Mungu.’
18. Kumtumaini Yehova kutatusaidiaje tuepuke mtego wa pupa?
18 Yehova ndiye chanzo cha utajiri wote. (Matendo 14:15, 17) Yeye ameahidi kuwaangalia kipekee watumishi wake. Yesu alisema: “Kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” (Mathayo 6:32, 33; Zaburi 37:25) Je! wewe unaiamini ahadi hiyo? Je! una uhakika kwamba Yehova ataitimiza? Je! utaridhika na maandalizi ya Yehova? Ikiwa ndivyo, utaweza kuepuka mtego wa pupa. (Wakolosai 3:5) Utumishi wako kwa Yehova na uhusiano wako naye sikuzote utakuwa wa kwanza, na njia yako yote ya maisha itakuwa wonyesho wa imani yako kwake.
Unakumbuka?
◻ Ni watu wa aina zipi wanaopatwa na matokeo ya pupa?
◻ Tunaweza kujilindaje na pupa?
◻ Wakati mwingine pupa inajionyeshaje?
◻ Ni maulizo gani yanayotusaidia tujue kama tunaepuka mtego wa pupa au la?
◻ Ulinzi mkubwa dhidi ya pupa ni nini?
[Blabu katika ukurasa wa 29]
Wakati wa kufanya biashara pamoja, Wakristo hawapaswi kusahau kanuni za Biblia