Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 8/1 kur. 10-15
  • Fanikiwa Katika Kuepuka Mtego wa Pupa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Fanikiwa Katika Kuepuka Mtego wa Pupa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Yehova Hutuonya Juu ya Hatari
  • Kunaswa na Pupa ya Kupata Utajiri au Mali
  • Pupa Katika Sehemu Nyingine za Maisha
  • Endelea Kuazimia Kuepuka Pupa
  • Endeleeni Kuepuka Mtego wa Pupa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • “Enzi ya Pupa”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Wazia Ulimwengu Usio na Pupa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Unaweza Kutoka Kwenye Mitego ya Shetani!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 8/1 kur. 10-15

Fanikiwa Katika Kuepuka Mtego wa Pupa

“Hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi [Mtego, NW].”—1 TIMOTHEO 6:9.

1. Kwa nini tuhangaikie mitego?

NENO “mtego” laweza kukukumbusha juu ya mwindaji anayeweka kifaa kilichofunikwa ili kukamata mawindo yasiyokuwa na habari. Hata hivyo, Mungu huelewesha wazi kwamba kwetu sisi mitego iliyo ya hatari zaidi, si vifaa halisi, bali ni lile liwezalo kutunasa kiroho au kiadili. Ibilisi ni fundi stadi katika kuweka mitego kama hiyo.—2 Wakorintho 2:11; 2 Timotheo 2:24-26.

2. (a) Yehova hutusaidaje tuepuke mitego yenye hatari? (b) Ni aina gani hasa ya mtego inayokaziwa sasa?

2 Yehova hutusaidia kwa kutambulisha baadhi ya mitego mingi na ya unamna-namna ya Shetani. Kwa kielelezo, Mungu hutuonya kwamba midomo yetu, au kinywa, yaweza kuwa mtego tukisema bila hekima, bila msingi, au juu ya yale ambayo hatupaswi kusema. (Mithali 18:7; 20:25) Kiburi chaweza kuwa mtego, kama vile kushirikiana na watu wenye mwelekeo wa hasira. (Mithali 22:24, 25; 29:25) Lakini acheni tugeukie mtego mwingine: “Hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi [mtego, NW], na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu.” (1 Timotheo 6:9) Chanzo au msingi wa mtego huo waweza kutajwa kifupi katika neno moja, “pupa.” Ingawa mara nyingi pupa hudhihirishwa kwa bidii ya kuwa tajiri, kwa kweli pupa ni mtego wenye sehemu nyingi.

Yehova Hutuonya Juu ya Hatari

3, 4. Historia ya kale ya kibinadamu ina somo jipi juu ya pupa?

3 Kwa msingi, pupa ni tamaa nyingi mno au ya kupita kiasi ya kuwa na zaidi, iwe ni fedha, mali, mamlaka, ngono, au mambo mengine. Sisi si wa kwanza kuhatarishwa na mtego wa pupa. Zamani za kale katika bustani ya Edeni, pupa ilimnasa Hawa kisha Adamu. Mwenzi wa Hawa, aliyekuwa na uzoefu zaidi maishani kuliko yeye, alikuwa ameagizwa na Yehova kibinafsi. Mungu alikuwa amewaandalia makao ya paradiso. Wangeweza kufurahia wingi wa chakula kizuri na cha unamna-namna kilichopandwa kwenye ardhi isiyochafuzwa. Wangeweza kutazamia kuwa na watoto wakamilifu, ambao pamoja nao wangeweza kuishi na kumtumikia Mungu milele. (Mwanzo 1:27-31; 2:15) Je! hayo yasingeonekana kuwa ya kutosha ili kumridhisha mwanadamu yeyote?

4 Lakini, hata mtu akiwa na ya kutosha hilo halizuii pupa isiwe mtego. Hawa alinaswa na taraja la kuwa kama Mungu, kuwa na uwezo wa kujitegemea zaidi na kujiwekea viwango vyake mwenyewe. Yaonekana kwamba Adamu alitaka ushirika wenye kuendelea na mwenzi wake mrembo, hata iwe ingegharimu nini. Kwa kuwa hata wanadamu hao wakamilifu walinaswa na pupa, unaweza kutambua kwa nini pupa yaweza kuwa hatari kwetu.

5. Ni jambo la maana jinsi gani kwetu kuepuka mtego wa pupa?

5 Ni lazima tujilinde dhidi ya kunaswa na pupa kwa sababu mtume Paulo atuonya hivi: “Hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio [wenye pupa, NW].” (1 Wakorintho 6:9, 10) Paulo alituambia hivi pia: “Uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote wala kutamani [pupa, NW].” (Waefeso 5:3) Kwa hiyo pupa haipasi hata kuwa kichwa cha mazungumzo kwa kusudi la kuridhisha mwili wetu usio mkamilifu.

6, 7. (a) Ni vielelezo vipi vya Biblia vinavyokazia jinsi pupa iwezavyo kuwa yenye nguvu? (b) Kwa nini vielelezo hivyo viwe onyo kwetu?

6 Yehova amerekodi vielelezo vingi vya kutuweka macho kwa hatari ya pupa. Kumbuka pupa ya Akani. Mungu alisema kwamba Yeriko lilipasa liharibiwe, lakini dhahabu, fedha, shaba, na chuma vyalo vilikuwa vya hazina Yake. Mwanzoni huenda ikawa Akani alikusudia kufuata amri hiyo, lakini pupa ikamnasa. Mara alipokuwa katika Yeriko, ilikuwa kana kwamba alikuwa kwenye ziara ya kununua vitu ambako aliona bei za chini zisizoaminika, kutia na vazi zuri lililoonekana kumfaa kabisa. Akiokota dhahabu na fedha zenye thamani ya maelfu ya dola, angaliweza kufikiri, ‘Huu ni utajiri ulioje! Ni wa rahisi sana, kama kwamba kuiba.’ Kwa kweli hilo lilikuwa tendo la kuiba! Kwa kutamani kile kilichopasa kuharibiwa au kukabidhiwa, alimwibia Mungu, na hilo liligharimu uhai wa Akani. (Yoshua 6:17-19; 7:20-26) Ebu fikiria pia, vile vielelezo vya Gehazi na Yuda Iskariote.—2 Wafalme 5:8-27; Yohana 6:64; 12:2-6.

7 Hatupaswi kupuuza jambo la kwamba wale watatu waliotajwa juu hawakuwa wapagani wasiojua viwango vya Yehova. Bali, walikuwa katika uhusiano wa kujiweka wakfu kwa Mungu. Wote walikuwa wameshuhudia miujiza ambayo ingepasa ikaze juu yao nguvu za Mungu na umaana wa kubaki na upendeleo wake. Bado, mtego wa pupa ulikuwa angamizo lao. Sisi tunaweza pia kuharibu uhusiano wetu na Mungu tukijiruhusu tunaswe na pupa ya namna yoyote. Ni aina au namna zipi za pupa ambazo huenda hasa zikawa zenye hatari kwetu?

Kunaswa na Pupa ya Kupata Utajiri au Mali

8. Biblia hutoa onyo jipi kuhusu utajiri?

8 Wakristo wengi wamesikia maonyo ya wazi kutoka katika Biblia dhidi ya kusitawisha upendo wa mali, kutamani utajiri. Kwa nini usipitie baadhi yayo, kama yanavyopatikana kwenye Mathayo 6:24-33; Luka 12:13-21; na 1 Timotheo 6:9, 10? Ingawa huenda ukahisi kwamba unakubali na kufuata shauri hilo, je, haielekei kwamba Akani, Gehazi, na Yuda wangalisema kwamba walikubaliana nalo? Kwa wazi, hatupaswi kukubali kiakili tu. Ni lazima tuwe waangalifu kwamba mtego wa pupa wa kupata utajiri au mali hauathiri maisha yetu ya kila siku.

9. Kwa nini tuchunguze mtazamo wetu kuelekea kununua vitu?

9 Katika maisha ya kila siku, mara nyingi tunapaswa kununua vitu—chakula, mavazi, vifaa vya nyumbani. (Mwanzo 42:1-3; 2 Wafalme 12:11, 12; Mithali 31:14, 16; Luka 9:13; 17:28; 22:36) Lakini ulimwengu wa biashara huchochea tamaa ya kupata vitu zaidi na ambavyo ni vipya zaidi. Matangazo mengi yanayojaza magazeti ya habari, majarida, na televisheni ni masingizio ya kuchochea pupa. Jitihada hizo za kuchochea pupa zaweza pia kuwako kwenye maduka yenye mbao za kuangikia blauzi, koti, marinda, na fulana, pamoja na rafu zenye viatu vipya, vifaa vya kielektroni, na kamera. Lingekuwa jambo la busara kwa Wakristo kujiuliza wenyewe, ‘Je! kununua vitu kumekuwa jambo kuu au lenye kupendeza zaidi maishani mwangu?’ ‘Je! kweli ninahitaji vitu vipya ninavyoona, au ulimwengu wa biashara unachochea tu mbegu za pupa ndani yangu?’—1 Yohana 2:16.

10. Ni mtego gani wa pupa ulio wa hatari hasa kwa wanaume?

10 Ikiwa kununua vitu kunaonekana kuwa mtego wa kawaida kwa wanawake, kupata fedha zaidi ni mtego kwa wanaume wengi. Yesu alitolea kielezi mtego huo kwa kutumia mwanamume tajiri aliyekuwa na mshahara mzuri lakini akaazimia ‘kuzivunja ghala zake, ajenge nyingine kubwa zaidi aweke nafaka yake yote na vitu vyake.’ Yesu alionyesha kwa wazi hatari ya hiyo: “Angalieni, jilindeni na choyo [kila aina ya kutamani, NW]” au pupa. (Luka 12:15-21) Tuwe matajiri au la, tunapaswa kutii shauri hilo.

11. Mkristo anaweza kunaswaje na pupa ya kupata fedha zaidi?

11 Mara nyingi pupa ya kupata fedha zaidi, au vitu viwezavyo kununuliwa kwa fedha, hukuzwa kwa njia isionekane rahisi. Mpango wa kuwa tajiri upesi unaweza ikatolewa—labda fursa ya mara moja maishani ya kupata usalama wa kifedha kupitia mradi wa kifedha wenye mashaka. Au huenda mtu akashawishwa kuchuma fedha kwa mazoea ya biashara yenye kutilika shaka au yasiyo halali. Tamaa hiyo yenye uchoyo yaweza kumshinda mtu nguvu, na kumnasa. (Zaburi 62:10; Mithali 11:1; 20:10) Wengine katika kutaniko la Kikristo wameanza biashara wakitazamia kwamba ndugu zao wenye kutumainika wangekuwa wateja wakuu. Ikiwa kusudi lao si kuandaa tu kifaa au utumishi unaohitajiwa kwa ‘juhudi, wakitenda kazi iliyo nzuri kwa mikono yao wenyewe,’ bali ni kuchuma fedha upesi kwa hasara ya Wakristo wenzao, basi wanatenda kwa sababu ya pupa. (Waefeso 4:28; Mithali 20:21; 31:17-19, 24; 2 Wathesalonike 3:8-12) Pupa ya kupata fedha imewaongoza wengine wacheze kamari kupitia changanya-changanya, pata-potea, au tikiti za bahati-nasibu. Wengine, wakipuuza hisia-mwenzi na kusababu ifaavyo, wamekimbilia kushtaki mahakamani wakituamini kulipwa ridhaa au kupata malipo makubwa.

12. Kwa nini tunajua kwamba pupa ya kupata utajiri inaweza kushindwa?

12 Yanayotangulia ni maeneo ambamo inafaa tujichunguze wenyewe ili tuweze kuona kikweli kama pupa yaweza kuwa inafanya kazi ndani yetu. Hata kama ni hivyo, tunaweza kubadilika. Kumbuka kwamba Zakayo alibadilika. (Luka 19:1-10) Mtu yeyote akipata kwamba pupa ya kupata utajiri au mali ni tatizo, anapaswa kuazimia kama vile Zakayo kuepuka mtego huo.—Yeremia 17:9.

Pupa Katika Sehemu Nyingine za Maisha

13. Zaburi 10:18 yaelekeza fikira yetu kwenye mtego gani mwingine wa pupa?

13 Wengine huona kwamba ni rahisi zaidi kuona hatari ya pupa kuhusiana na fedha au mali kuliko njia nyingine inayotokea. Kamusi moja ya Kigiriki inasema kwamba fungu la maneno linalofasiriwa “pupa” au “kutamani” lina maana ya “‘kutaka zaidi,’ kuhusiana na mamlaka na kadhalika, pamoja na mali.” Naam, tungeweza kunaswa kwa kutaka kwa njia ya pupa kuwa na uwezo juu ya wengine, labda kuwafanya watetemeke chini ya mamlaka yetu.—Zaburi 10:18.

14. Tamaa ya kupata mamlaka imekuwa yenye madhara katika sehemu zipi?

14 Tangu siku za mapema wanadamu wasio wakamilifu wamefurahia kuwa na mamlaka juu ya wengine. Mungu aliona kimbele kwamba tokeo lenye huzuni la dhambi ya kibinadamu lingekuwa kwamba waume wengi ‘wangewatawala’ wake zao. (Mwanzo 3:16) Hata hivyo, kosa hilo halikuathiri ndoa tu. Maelfu ya miaka baadaye, mwandishi mmoja wa Biblia alisema “mwanadamu ametawala mwanadamu kwa kumwumiza.” (Mhubiri 8:9, NW) Yaelekea wajua jinsi ambavyo hilo limekuwa kweli katika mambo ya kisiasa na ya kijeshi, lakini je, yaweza ikawa kwamba katika mazingira yetu wenyewe, tunajitahidi kupata mamlaka au uwezo zaidi wa binafsi?

15, 16. Mkristo anaweza kunaswa kwa njia zipi na tamaa ya kupata mamlaka zaidi? (Wafilipi 2:3)

15 Sisi sote tuna uhusiano na wanadamu wengine—katika familia zetu za karibu au za nje, kazini au shuleni mwetu, miongoni mwa rafiki, na katika kutaniko. Pindi kwa pindi, au mara nyingi, huenda tukawa na daraka la kuamua lile litakalofanywa, na pia jinsi au wakati litakalofanywa. Hilo lenyewe si jambo lisilofaa au lililo baya. Lakini je, sisi tunafurahia kupita kiasi kutumia mamlaka yoyote tuliyo nayo? Je! yawezekana kwamba tunapenda kufanya uamuzi wa mwisho na twataka kufanya hivyo zaidi na zaidi? Mara nyingi meneja au mabwana wakubwa walimwengu huonyesha mtazamo huo kwa kujikusanyia watu wa kuwaunga mkono, ambao hawatoi maoni yenye kupinga na ambao hawapingi jitihada (pupa) za kilimwengu za wakubwa wao za kupata mamlaka.

16 Huo ni mtego unaopasa kuepukwa katika kushughulikia Wakristo wenzetu. Yesu alisema: “Mwajua ya kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha. Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu ye yote anayetaka kuwa mkubwa kwenu, na awe mtumishi wenu.” (Mathayo 20:25, 26) Unyenyekevu kama huo wapaswa uonekane wazi wakati wazee Wakristo wanaposhughulika na wazee wenzao, na watumishi wa huduma, na kutaniko. Kwa mfano, je, tamaa ya kuwa na mamlaka yaweza kuonyeshwa na mwangalizi msimamizi anayeshauriana na wazee wenzake katika mambo madogo tu lakini afanya maamuzi yote makubwa peke yake? Je! kwa kweli ana nia ya kukabidhi kazi? Matatizo yangeweza kutokea ikiwa mtumishi wa huduma anayeshughulikia mkutano kwa ajili ya utumishi wa shambani hakutaka kusikia maoni ya wengine katika mipango yake, hata kufanyiza kanuni nyingi.—1 Wakorintho 4:21; 9:18; 2 Wakorintho 10:8; 13:10; 1 Wathesalonike 2:6, 7.

17. Kwa nini inafaa kufikiria chakula tunapozungumzia mtego wa pupa?

17 Chakula ni sehemu nyingine ambamo wengi hunaswa na pupa. Bila shaka, ni jambo la asili kupata furaha katika kula na kunywa; Biblia hukubali hilo. (Mhubiri 5:18) Hata hivyo, kuhusiana na hilo, ni jambo la kawaida kwa tamaa kukua kwa kipindi fulani cha wakati, kupita kabisa kiasi chenye kufurahisha na kinachotosha. Ikiwa haifai kwa watumishi wa Mungu kuhangaikia hilo, kwa nini Neno la Yehova liseme hivi kwenye Mithali 23:20: “Usiwe miongoni mwao wanywao mvinyo; miongoni mwao walao nyama kwa pupa”? Lakini, tunaepukaje mtego huo?

18. Tunaweza kujichunguzaje kuhusu chakula na kinywaji?

18 Mungu hadokezi kwamba watu wawe na taratibu fulani ya kujinyima chakula. (Mhubiri 2:24, 25) Wala hakubali tufanye chakula na kinywaji viwe sehemu kuu ya mazungumzo na mipango yetu. Twaweza kujiuliza wenyewe hivi ‘Je! mara nyingi mimi huwa mwenye idili ya kupita kiasi ninaposimulia mlo fulani niliokula au ninaopanga kula?’ ‘Je! sikuzote ninaongea juu ya chakula na kinywaji?’ Onyesho jingine laweza kuwa jinsi tunavyoitikia tunapokuwa na mlo ambao hatukutayarisha au hatukulipia, labda tunapokuwa mgeni katika nyumba ya mtu mwingine au wakati chakula kinapopatikana kwenye kusanyiko la Kikristo. Je! yawezekana kwamba wakati huo tunaelekea kula zaidi kuliko kawaida? Twakumbuka kwamba Esau aliruhusu chakula kiwe cha maana isivyofaa, kwa madhara yake ya kudumu.—Waebrania 12:16.

19. Pupa ingewezaje kuwa tatizo kuhusiana na raha ya ngono?

19 Paulo atupa sisi mwono-ndani katika mtego mwingine: “Uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote wala kutamani [pupa, NW], kama iwastahilivyo watakatifu.” (Waefeso 4:17-19; 5:3) Kwa kweli, pupa ya kupata raha ya kingono yaweza kukua. Bila shaka, raha hiyo inaonyeshwa ifaavyo ndani ya vifungo vya ndoa. Shauku hiyo ya karibu inayohusianishwa na raha hiyo inashiriki sehemu katika kuwasaidia mume na mke waendelee kujitoa kwa mmoja na mwenzake kupitia miaka mingi ya ndoa. Lakini, ni watu wachache ambao wangekanusha kwamba ulimwengu wa leo umekazia ngono kupita kiasi, ukionyesha kuwa la kawaida lile jambo ambalo kwa kweli Paulo alitaja kuwa ni pupa. Maoni hayo yasiyofaa ya raha ya ngono hufuatwa hasa kwa urahisi na wale wanaojifunua wazi waingiwe na ukosefu wa maadili na maonyesho ya uchi wa mwili ulio kawaida katika sinema, vidio, na magazeti mengi, na pia mahali-mahali pa vitumbuizo.

20. Wakristo wanaweza kujionyeshaje kuwa wenye macho kwa hatari ya pupa katika mambo ya kingono?

20 Simulizi la dhambi ya Daudi pamoja na Bath-sheba waonyesha kwamba mmoja wa watumishi wa Mungu anaweza kunaswa na pupa ya ngono. Ingawa alikuwa huru kufurahia raha ndani ya ndoa yake mwenyewe, Daudi aliruhusu tamaa ya ngono haramu ikue. Akiona jinsi mke wa Uria alivyokuwa mwenye kuvutia, hakudhibiti mawazo—na matendo yake—ya kupata raha haramu naye. (2 Samweli 11:2-4; Yakobo 1:14, 15) Kwa hakika ni lazima tuepuke namna hiyo ya pupa. Inafaa kuepuka pupa hata katika ndoa. Hilo lingetia ndani kukatalia mbali mazoea ya ngono ya kupita kiasi. Mume anayeazimia kuepuka pupa katika eneo hilo angependezwa kikweli na mwenzi wake, hivi kwamba chaguo lolote ambalo wote wawili walifanya kuhusu kupanga uzazi lisingeweka raha yake kuwa ya maana kuliko afya ya mke wake ya wakati huu na ya wakati ujao.—Wafilipi 2:4.

Endelea Kuazimia Kuepuka Pupa

21. Kwa nini mazungumzo yetu juu ya pupa yasituvunje moyo?

21 Yehova haandai tahadhari au maonyo kwa sababu ya kutotumaini. Yeye ajua kwamba watumishi wake wenye kujitoa wanataka kumtumikia kwa uaminifu-mshikamanifu, na ana uhakika kwamba wengi sana wataendelea kufanya hivyo. Kuhusu watu wake kwa ujumla, anaweza kusema kama vile alivyosema juu ya Ayubu alipokuwa akisema na Shetani: “Je! umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu? kwa kuwa hapana mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na uelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu.” (Ayubu 1:8) Baba yetu mwenye upendo, na mwenye kutumaini hututahadharisha kwa mitego yenye hatari, kama vile ile inayohusiana na namna za pupa, kwa sababu ataka tuendelee kuwa bila lawama na waaminifu kwake.

22. Tunapaswa kufanya nini ikiwa funzo letu limefunua sehemu fulani ya hatari au udhaifu wa binafsi?

22 Kila mmoja wetu amerithi mbetuko kuelekea pupa, na huenda ikawa tumeusitawisha zaidi chini ya uvutano wa ulimwengu mbovu. Namna gani ikiwa katika funzo letu juu ya pupa—kuhusiana na utajiri, mali, uwezo na mamlaka, chakula, au raha ya ngono—uliona sehemu fulani yenye udhaifu? Basi zingatia moyoni shauri hili la Yesu: “Mkono wako ukikukosesha, ukate; ni afadhali kuingia katika uzima u kigutu, kuliko kuwa na mikono miwili, na kwenda zako jehanum.” (Marko 9:43) Fanya mabadiliko yanayohitajiwa katika mtazamo au katika mambo yanayokupendeza. Epuka mtego wa pupa ulio hatari sana. Hivyo kwa msaada wa Mungu, waweza “kuingia katika uzima.”

Nimejifunza Nini?

◻ Kwa nini tuhangaikie mtego wa pupa?

◻ Pupa ya kupata utajiri au mali inaweza kutunasa katika njia zipi?

◻ Pupa katika maeneo mengine ya maisha inaweza kutokezaje hatari halisi?

◻ Mtazamo wetu wapasa uwe nini kuelekea udhaifu wowote tulio nao kuhusiana na pupa?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki