Iweni Waaminifu kwa Mungu “Aonaye Sirini”
“Usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.”—MATHAYO 6:6.
1, 2. Inaweza kuonyeshwaje kwamba yanayoelekea kuwa mambo ya siri yanaweza kujulikana na watu wote? (1 Samweli 21:7; 22:9)
MIAKA kadha iliyopita, mwanamke, mmoja wa Mashahidi wa Yehova alimpigia simu nduguye katika Long Island, New York. Kwa kuwa yeye alikuwa wa dini tofauti, alimwambia juu ya ahadi ya Mungu ya kuondoa uovu duniani na kurudisha hali za paradiso. Mazungumzo yalipokwisha na nduguye akaweka simu chini, alishangazwa kusikia sauti ikisema, “Ngoja kidogo, nataka kukuuliza ulizo.”
2 Ilikuwa sauti ya opareta wa simu. Alikuwa amesikiliza, kwa kuwezeshwa na vyombo vya simu vya wakati huo, ingawa halikuwa jambo la adili kufanya hivyo na ilikuwa kinyume cha mwongozo wa shirika. Shahidi huyo alipendezwa kwamba maneno yake yalikuwa yametokeza kupendezwa kama huko, naye akafanya mipango ya kufuatia mwanamke huyo mwenye kupendezwa, ingawa aligutushwa kwamba mazungumzo yake hayakuwa ya siri. Ndiyo, nyakati nyingine wengine wanaona na kusikia mambo tunayofikiri ni ya siri.—Mhubiri 10:20.
3. Ni katika maana gani maisha za Wakristo sikuzote ziko mbele ya macho ya watu?
3 Jambo hilo halipasi kutokeza matatizo makubwa kwa Wakristo, ambao wanajitahidi kuwa waaminifu kwa Mungu nyakati zote. Mtume Paulo alisema: “Tumekuwa tamasha kwa dunia; kwa malaika na wanadamu.” (1 Wakorintho 4:9) Alikuwa akihusianisha hilo na zoea moja kwenye uwanja wa kupigana. Kabla ya tukio la mwisho wale ambao wangepigana na labda wafe waliwekwa mbele ya macho ya watu waonwe wakiwa uchi. Leo Wakristo pia wako mbele ya macho ya watu wa ukoo wasioamini, wafanya kazi wenzi, majirani, na wanashule wenzi. Wenye kutazama wanaweza kusitawisha maoni mazuri au mabaya juu ya Ukristo kwa kutegemea wanayoona kwetu.—1 Petro 2:12.
4. Ufahamu wa kwamba wengine wanamtazama mtu unaweza kuwa na matokeo gani juu yake?
4 Tunapojua kwamba wengine wanatazama, huenda tukawa na maelekeo ya kutenda tunavyopaswa, tukiwa na tamaa kama ya Paulo: “Tusiwe kwazo la namna yo yote katika jambo lo lote, ili utumishi wetu usilaumiwe.” (2 Wakorintho 6:3) Kujua kwetu kwamba wengine wanatazama huenda kukaimarisha azimio letu la kufanya yaliyo haki. Lakini, iweje, tukikabili jaribu la kanuni za Kikristo kama hatuonwi na watu?
Yeye Anatazama Zaidi ya Sura ya Nje
5. Maisha mbele ya watu na maisha ya faraghani ya viongozi Wayahudi yalitofautianaje?
5 Viongozi wengi wa kidini Wayahudi katika karne ya kwanza walikuwa mtu tofauti nje, na mtu mwingine ndani. Yesu alionya katika Mahubiri ya Mlimani: “Angalieni msifanye wema wenu machoni pa watu, kusudi mtazamwe na wao.” (Mathayo 6:1, 2) Viongozi wa kidini walikuwa kama vikombe vilivyokuwa safi nje lakini ‘ndani yake vimejaa kutokuwa na kiasi,’ kama “makaburi yaliyopakwa chokaa, nayo kwa nje yaonekana kuwa mazuri, bali ndani yamejaa mifupa ya wafu, na uchafu wote.”—Mathayo 23:25-28; linganisha Zaburi 26:4.
6. Yehova anaweza kuona nini kuhusu sisi?
6 Maneno hayo yanapasa kutusaidia tuthamini kwamba Yehova anapendezwa na mengi zaidi ya yale ambayo huenda yakaonwa na wanadamu wengine. Yesu alishauri hivi: “Wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.” (Mathayo 6:6) Ndiyo, Mungu anaweza kusikia sala zetu zinazotolewa wakati tunapokuwa tumejitenga na wanadamu wengine. Hakuna jambo lisiloonwa na Mungu. Anaweza kuona mtu akiumbika awe kiinitete katika tumbo la uzazi, labda akisoma habari zilizomo ndani ya chembe ambazo baadaye zitaamua vile sifa za mtu huyo zitakavyokuwa. (Zaburi 139:15, 16; Mwanzo 25:23) Hata anaweza kusoma maelekeo ya siri ya mioyo yetu. (1 Samweli 16:7; 1 Wafalme 8:39; Yeremia 17:10; Matendo 1:24) Fikiria jinsi mambo hayo yanavyopasa kuwa na matokeo juu yetu.
7. Ni wapi Mkristo anaweza kuhitaji kufanya maendeleo?
7 Ili kuwa Wakristo wa kweli tulipaswa kujitahidi kushinda kasoro kubwa-kubwa na dhambi, kama vile Wakristo wa kwanza. (1 Wakorintho 6:9-11; Matendo 26:20; 1 Petro 4:1-4) Lakini namna gani makosa ambayo huenda yasiwe yanajulikana na wanadamu wengine? Kwa kuwa makosa hayo hayajulikani na watu hakuyafanyi yawe madogo. Jambo hilo linaonyeshwa na maneno ya Daudi: “Amsingiziaye jirani yake kwa siri, huyo nitamharibu. Mwenye macho ya kiburi na moyo wa majivuno, huyo sitavumilia naye.” (Zaburi 101:5) Hata kama kulifanywa sirini, kwa msikiaji mmoja, kusingizia ni kosa. Kwa hiyo Daudi hangeruhusu dhambi hiyo ya “siri.”
8. Tunajuaje kwamba makosa yaliyofichwa hayakosi kuonwa na Yehova?
8 Wala mtendaji-dhambi asijipumbaze kwa kufikiri kwamba kosa hilo litakosa kuonwa na Mungu “aonaye sirini.” Kwa kweli, Mungu amethibitisha kwamba anapendezwa na wanadamu kuwa waaminifu hata matendo yao yanapokuwa hayajulikani na watu. Kumbuka kisa cha Akani. Waisraeli walipaswa wauharibu Yeriko na wakaaji wake, Wakanaani waovu. Fedha, dhahabu na shaba ndizo peke yake hazingeharibiwa. Zingekuwa za hazina ya patakatifu pa Mungu. (Yoshua 6:17-19) Lakini, Akani, alishawishika akachukua vazi la bei kubwa, vipande kadha vya fedha na dhahabu. Alificha hivyo chini ya hema lake, labda akiwa na maoni kwamba hakuna ye yote angejua. Lakini je, alimdanganya Yule “aonaye sirini”? Hapana. Mungu alihakikisha kwamba dhambi ya Akani ilifunuliwa mbele ya watu, na kumletea kifo yeye na jamaa yake.—Yoshua 7:1, 16-26.
9. Tunapaswa kufanya nini ili tuwe na kibali ya Mungu na kuendelea kuwa nayo?
9 Elihu alieleza kwa hekima juu ya Yehova: “Kwani macho yake ya juu ya njia za mtu, naye huiona miendo yake yote. Hapana weusi, wala hilo giza tupu, wawezapo kujificha watendao udhalimu.” (Ayubu 34:21, 22) Ikiwa, basi, tunatamani kuwa na kibali ya Yehova Mungu na kuidumisha, ni lazima tutake kuishi kulingana na kanuni zake wakati tunapojua wengine wanatutazama sisi na wakati inapoonekana kwamba mwenendo wetu ni wa sirini. Nyakati zote “macho yake yako juu ya njia za mwanadamu.”
10. (a) Paulo aliweka mfano gani mzuri kwa habari ya mwenendo wa sirini? (b) Tunastahili kuchunguza uwezekano wa makosa ya sirini katika maeneo gani?
10 Huenda Mkristo akapatwa na jaribu fulani ambalo ni siri kwa waabudu wenzake. Jambo hilo lilitokea kwa Paulo alipokuwa gerezani. Wayahudi walikuwa wamemshtaki kuwa “mwanzilishi wa fitina” na mwenye ‘kujaribu kulitia hekalu unajisi.’ (Matendo 24:1-6) Paulo alitoa ushuhuda juu ya kutokuwa kwake na hatia mbele ya mwakilishi wa Roma, Feliki, ambaye wanahistoria wanasema alikuwa mkatili na mwenye kukosa adili. Feliki alimzuia Paulo gerezani ‘akitaraji kwamba atapewa fedha na Paulo.’ (Matendo 24:10-21, 26) Ingawa mtume huyo alijua shauri la Biblia la kutotoa au kukubali zawadi za kubadili hukumu, yeye angaliweza kuwaza kwamba kutoa hongo kungalikuwa njia ya kumsaidia awe huru. Kwa kuwa hongo hilo lingaliweza kufanywa sirini, Paulo hangalikuwa na wasiwasi wa kukwaza wengine. (Kutoka 23:8; Zaburi 15:1, 5; Mithali 17:23) Hata hivyo Paulo hakuwaza hivyo. Wengi wa watu wa Yehova katika nyakati za kisasa wamekabili majaribu mengine, kama yale yanayohusu sheria ya Mungu juu ya damu, kupiga punyeto, na kutumia vibaya kileo. Na tufikirie jinsi majaribu hayo yangeweza kukukabili wewe au wapendwa wako.
Utii Wajaribiwa Kuhusiana na Damu
11. Msingi wa msimamo wa Kikristo juu ya matumizi ya damu ni nini?
11 Kwa hakika sheria ya Mungu inayokataza damu si mpya wala isiyo wazi. Kupitia babu yetu sote, Noa, Yehova aliamuru wanadamu wote hivi: “Bali nyama pamoja na uhai, yaani, damu yake, msile.” (Mwanzo 9:4) Utakatifu wa damu, unaowakilisha uhai kutoka kwa Mungu, ulikaziwa katika Torati ya Musa. Damu ingeweza kutumiwa kwenye madhabahu, la sivyo ilipasa ‘kumwagwa juu ya nchi kama maji.’ (Mambo ya Walawi 17:11-14; Kumbukumbu la Torati 12:23-25) Je! katazo la kutoendeleza maisha kwa kutumia damu liliendelea baada ya Torati ya Musa kumalizika? Liliendelea kabisa. Kwenye lile ambalo wengine huenda wakaita baraza la kwanza la Kikristo, mitume na wanaume wazee (ambao walifanyiza baraza linaloongoza) walikata kauli kwamba Wakristo wanapaswa ‘kujiepusha na unajisi wa sanamu, na uasherati, na nyama zilizosongolewa [zikiwa zina damu iliyobaki ndani], na damu.’ Kutumia vibaya damu kulikuwa jambo zito sawa na dhambi ya kukosa adili kama vile ngono haramu.—Matendo 15:20, 21, 28, 29.
12. Wakristo wa kwanza walichukua msimamo gani juu ya damu?
12 Wakristo wa kwanza walitii sheria ya Mungu juu ya damu. Ingawa watu wengine wakati huo walikunywa damu ya watu waliopigana katika wanja za mawonyesho kuwa ni “dawa” ya kifafa, Wakristo wa kweli hawakufanya hivyo. Wala hawakula chakula chenye damu, hata wakati kukataa kwao kulimaanisha kifo kwao na kwa watoto wao. Tangu wakati huo, wanachuo fulani wa dini na wengine wamekubali kwamba Wakristo wako chini ya sheria ya Mungu inayokataza kuendeleza uhai kwa kutumia damu.
13. (a) Ni kwa sababu gani huenda wakati fulani ukakabiliwa na jaribu linalohusu damu? (b) Ni sababu gani kubwa ya Wakristo kukataa damu tunayopaswa kuendelea kukumbuka?
13 Katika nyakati za karibuni kutia damu mishipani kumekuwa dawa yenye kupendwa na wengi. Kwa hiyo huenda Mkristo akakabili jaribu linalohusu damu. Madaktari, wauguzi, na hata watu wa ukoo huenda wakamsihi sana akubali damu. Bila shaka, watu wenye ufahamu, wanajua kwamba kutiwa damu mishipani kwenyewe kunatokeza hatari kubwa. Gazeti Time (Novemba 5, 1984) lilisema kwamba “Waamerika 100,000 hivi wanapatwa na ugonjwa wa ini kila mwaka kutokana na kutiwa damu mishipani.” Pia Time liliripoti hivi juu ya visa zaidi ya 6,500 vya AIDS (ugonjwa unaotoa nguvu za mwili za kujikinga na maradhi), vingine vya visa hivyo vikiwa “vinahusiana na kutiwa damu mishipani.” Ripoti hiyo ilisema: “Karibu nusu ya wagonjwa hao wamekufa, ingawa hatimaye hesabu ya vifo huenda ikawa 90% au zaidi.” Bila shaka, Mashahidi wa Yehova hawakatai kwa msingi wa kwamba damu ni dawa mbaya. Hata kama madaktari wangeweza kuwapa uhakikisho kwamba kutiwa damu kungekuwa salama kabisa, Neno la Mungu linatuamuru ‘tujiepushe na damu.’—Matendo 21:25.
14. Huenda ukakabili jaribu gani la “siri” linalohusu damu?
14 Wazia kama wewe ungeambiwa kwamba unahitaji sana kutiwa damu mishipani. Ungekumbuka sheria ya Mungu inayokataza damu, sivyo? Na inaelekea azimio lako la kumtii Mungu, hata matokeo ambayo huenda yakafuata wakati huo yawe nini, lingetiwa nguvu kama Wakristo wenzi wangekuwapo. (Linganisha Danieli 3:13-18.) Lakini, vipi kama faraghani daktari au hakimu angekukaza ukubali damu, hata akuambie yeye atakuwa mwenye daraka mbele za Mungu?
15. Madaktari na maofisa fulani wana maoni gani yenye kosa juu ya msimamo wetu kuhusu damu?
15 Ripoti kutoka nchi mbalimbali zinaonyesha kwamba nyakati nyingine madaktari, maofisa wa hospitali, na mahakimu wanawaza kwa makosa kwamba Mashahidi wa Yehova wanakataa kutiwa damu mishipani mbele ya watu lakini kisiri au kindani wana maoni tofauti. Katika kisa kimoja hakimu alikata maneno yeye binafsi “kwamba shaka juu ya tatizo hilo, si imani za kidini [za mgonjwa], bali ni kukataa kwake kutia sahihi kibali iliyotangulia kuandikwa ya kutoa ruhusa ya kutiwa damu mishipani. [Mwanamke huyo mgonjwa] hakukataa utibabu huo wenye kuhusika—hata hivyo, [mwanamke huyo] hakuagiza utumiwe.” Tofauti na hilo, badala ya Mashahidi wa Yehova kujifanya hawataki ‘kutia sahihi kibali ya kutoa ruhusa ya kutiwa damu mishipani’ na kumbe wanataka, maandishi yanathibitisha kwamba wao wana tamaa yenye nguvu ya kutia sahihi hati za kisheria zinazoondolea wafanya kazi wa utibabu daraka lo lote linalohusiana na kukataa damu.
16. Ikiwa mtu sirini angekusihi ukubali damu, hupaswi kusahau nini?
16 Madaktari na mahakimu huenda wakajaribu kukushawishi ukubali damu kwa sababu wameona watu wa dini zile nyingine wakikataa hatua fulani ya utibabu lakini ndipo wanakubali sirini. Maofisa wengine hata wamedai wanajua Shahidi fulani aliyekubali kutiwa damu mishipani siri-siri. Ikiwa hilo lilitokea, huenda ikawa lilihusu mtu ambaye alikuwa ametoka tu kufahamiana na Mashahidi wa Yehova. Watumishi wa Mungu waliojitoa wanajua vema kwamba kukubali kuvunja sheria yake hivyo kusingekosa kuonwa na yeye. Kumbuka wakati Daudi alipotenda dhambi kuhusiana na Bathsheba na Uria. Yehova aliona akampeleka Nathani akiwa na ujumbe huu: “Maana wewe [Daudi] ulifanya jambo lile kwa siri; bali mimi nitalifanya jambo hili mbele ya Israeli wote na mbele ya jua.” Kama Mungu alivyosema, baadaye Daudi alipatwa na matokeo yenye huzuni ya dhambi yake ya “siri.”—2 Samweli 11:27–12:12; 16:21.
17. (a) Kukubali kutiwa damu mishipani kisiri kungeweza kuwaleteaje wengine shida? (b) Eleza jinsi dada mmoja alivyosimama akiwa imara katika suala la damu hata sirini, na matokeo ya hilo yalikuwa nini?
17 Upendo kwa ajili ya nduguzo wa Kikristo wapasa pia kukusaidia upinge mkazo wa kukubali kisiri kuvunja sheria ya Mungu ya kukataza damu. Jinsi gani? Kama daktari au hakimu anajaribu kukushawishi ukubali damu, hata kisiri, unapaswa kufikiria shida zaidi ambayo kufanya hivyo kungeletea Shahidi atakayefuata. Angalia jambo hili lililoonwa:
Dada Rodriguez alikuwa akitibiwa ambukizo fulani. Halafu akawa mgonjwa sana; daktari wake akagundua alikuwa anatokwa na damu ndani ya mwili na kumshauri aende haraka kwenye hospitali kubwa. Dada Rodriguez akaambia wafanya kazi wa chumba cha dharura: “Hata iweje, siwezi kukubali kutiwa damu mishipani.” Alishikilia hivyo baadaye wakati wauguzi walipomkaza kwa kudai kwamba Mashahidi wengine walikuwa wametiwa damu. Kwa siku nyingi dada huyu aliendelea kupoteza damu na kudhoofika, mwishowe akahamishwa kwenye chumba cha wagonjwa walio mahututi. Halafu hospitali hiyo ikamwita hakimu wa Mahakama Kuu ya taifa.
Miezi fulani baadaye katika jumba la hospitali hiyo, hakimu alizungumza na madaktari zaidi ya 150 juu ya habari hii “Ingawaje, Ni Uhai wa Nani?” Yeye, pia, alisema alikuwa amekutana na watu ambao hapo kwanza walikataa damu lakini wakakubali mara hakimu alipohusika. Lakini namna gani juu ya Dada Rodriguez? Hakimu huyo alisimulia kwamba alijaribu kisiri-siri kumsadikisha Dada Rodriguez amruhusu ‘achukue daraka’ la kutiwa kwake damu mishipani kwa agizo la mahakama. Dada Rodriguez alifanya nini? Hakimu huyo aliwaambia madaktari hao waliokusanyika kwamba kwa nguvu zote alizokuwa nazo, Bi. Rodriguez alimwambia kwamba hatakubali damu na kwamba anapaswa kumwacha na kwenda zake kutoka chumba hicho. Kwa hiyo, hakimu huyo akaeleza, hakuwa na msingi wo wote wa kuagiza atiwe damu kinyume cha alivyotaka Dada Rodriguez.
18. Ni azimio gani tunalopaswa kufanya liwe wazi kuhusu suala la damu, na inaelekea matokeo yatakuwa nini?
18 Jambo hilo linakazia umaana wa kuonyesha wazi kabisa kwamba msimamo wetu juu ya damu si wa kujadiliwa. Mitume walichukua msimamo hakika hivyo, wakatangaza: “Imetupasa kumtii Mungu kuliko wanadamu.” (Matendo 5:29) Kisa cha Dada Rodriguez pia kinaonyesha matokeo ambayo kuvunja kwa Shahidi mmoja sheria ya Mungu kwaweza kuwa nayo juu ya wengine. Alipokuwa mgonjwa na amedhoofika kimwili, alilazimika kukabili mkazo wa ziada kwa sababu tu mtu fulani mapema huenda akawa alikuwa amevunja sheria ya Mungu kisiri. Bila shaka, kuvunja huko hakuwezi kuwa siri kwa “Mhukumu ulimwengu wote.” (Mwanzo 18:25) Kwa furaha, Dada Rodriguez hakuvunja sheria ya Mungu sirini sawa na asivyoivunja mbele ya watu. Na baadaye, akiwa na afya njema, alieleza kusanyiko lilo hilo la watibabu juu ya azimio lake la kuendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu.
19. Nyakati zote, tunapaswa kukumbuka uhakika gani?
19 Sisi, pia, twapaswa kuwa waaminifu, matendo yetu yawe au yasiwe mbele ya watu. Yehova anafurahia uaminifu huo naye atauthawabisha; kwa haki atajibu kazi—zilizofanywa mbele ya watu au faraghani—za wale wasio waaminifu kwa viwango vyake. (Zaburi 51:6; Ayubu 34:24) Kwa upendo anatoa shauri kamilifu litakalotusaidia tushinde makosa yo yote yaliyofichwa tuliyo nayo, kama tutakavyochunguza halafu.
(Itaendelezwa)
[Sanduku katika ukurasa wa 27]
Sheria ya Mungu Juu ya Damu Yatambuliwa Ingali ya Kweli
JOSEPH PRIESTLEY (1733-1804) anatambuliwa sana kuwa mwanasayansi aliyevumbua hewa ya oksijeni, lakini yeye pia alikuwa mwanachuo wa dini. Aliandika hivi:
“Katazo la kula damu, alilopewa Noa, laonekana kuwa ni takwa la kufuatwa na wazao wake wote.” Kuhusu dai la kwamba katazo la Kikristo juu ya damu lilikuwa la muda tu, Priestley aliongeza hivi: “Hakuna kiwazo, au kidokezo, kuwa ni la muda, wala mtajo wo wote wa wakati ambao katazo hilo lingekwisha. . . . Tukifafanua katazo hilo la mitume kwa msingi wa zoea la Wakristo wa kwanza, ambao hatuwezi kuwazia hata kidogo hawakufahamu asili na wakati ambao lingeendelea, tunakata maneno, kwamba lilikusudiwa liwe hakika na la kudumu.”
Mwaka wa 1646 kichapo A Bloody Tenet Confuted, or, Blood Forbidden kilichapishwa. Kwenye ukurasa wa 8 kilimalizia hivi: “Na tuache mila hii ya ukatili ya kula uhai wa wanyama, kwa maana inatumiwa katika Uingereza yote, katika vitumbua vyeusi [yaani, vyenye damu], kwa kuwa tutajionyesha wenyewe ni watu wenye rehema, wala si watu wa kinyama; kwa kuwa hatutakutwa kuwa sisi ni waasi Mungu katika amri zilizo wazi, bali wenye kutii mapenzi yake, na watendaji wa mambo ambayo ni haki machoni pake, kwa kuwa tungekuwa na kibali ya Mungu, . . . wala tusikatiliwe mbali kutoka kwa watu wetu, na kuwa na uso wa Mungu daima ukiwa kinyume chetu kwa sababu ya uovu.”
Thomas Bartholin alikuwa profesa wa jinsi viumbe walivyo wa karne ya 17 kwenye Chuo Kikuu cha Copenhagen. Akiandika juu ya ‘Matumizi Mabaya ya Damu,’ alisema: ‘Wanaotumia damu ya kibinadamu kwa ajili ya kuponya maradhi ya kindani yaonekana wanaitumia vibaya na wanakosea vibaya sana. Walaji-watu wanalaaniwa. Kwa nini hatuchukii wanaotia doa koo lao kwa damu ya wanadamu? Ni hali moja na kupokea damu ya mwingine kutoka mshipa uliokatwa, ama kupitia kinywani au kwa vyombo vya kutia damu. Wabuni wa tendo hilo wanavunja sana sheria ya kimungu, inayokataza kula damu.’
Kichapo Revelation Examined with Candour (1745) kilizungumza amri za Mungu juu ya damu. Kilitoa sababu hii: “Amri iliyotolewa na Mungu mwenyewe kwa Noa, ikarudiwa kwa Musa, na kuthibitishwa na mitume wa Yesu Kristo; ilitolewa mara tu baada ya gharika, wakati ulimwengu, kama ulivyo, ulipoanza upya; na ndiyo pekee iliyotolewa wakati wa pindi hiyo kubwa; ilirudiwa kwa uzito wenye kutisha, kwa watu hao ambao Mungu alitenganisha na wanadamu wengineo, wawe watakatifu kwake; ilirudiwa kwa hukumu za kisasi cha kimungu zenye kuogopesha, dhidi ya Myahudi na mgeni ambaye angethubutu kuivunja; na ilithibitishwa na baraza lenye kuzungumza kwa uzito sana na lililo takatifu zaidi, lililopata kukusanyika duniani; likiwa linatenda moja kwa moja chini ya uongozi wa Roho ya Mungu! ikapokezwa kutoka kwa kusanyiko hilo takatifu mpaka kwa makanisa kadha ya mataifa jirani, kwa mikono ya wajumbe wasiopungua cheo cha maaskofu wawili, na mitume wawili . . . Je! mtu ye yote, baada ya haya, atathubutu kupunguza uzito wa amri hiyo? Je! mtu ye yote mwenye akili atasema amri, iliyotolewa kwa njia hiyo, iliyorudiwa kwa njia hiyo, na iliyothibitishwa kwa njia hiyo na Mungu mwenyewe, kuwa haifai kitu na haina maana?”