Ufahamu Kutokana na Vitabu Viwili vya Wafalme
KATIKA pindi moja Yesu alipokuwa akihutubu katika mji wa nyumbani kwao Nazareti, alisema jambo fulani lililotokeza itikio kali kwa njia ya kushangaza. Wakaaji wa Nazareti walielekea kustaajabu ni kwa sababu gani hakuwa amefanya miujiza mingi huko kama alivyokuwa amefanya katika miji mingine. Akiwaambia sababu, Yesu alitumia mifano miwili ya Kimaandiko. Hivi ndivyo alivyosema:
“Amin, nawaambia ya kwamba, Hakuna nabii mwenye kukubaliwa katika nchi yake mwenyewe. Lakini, kwa hakika nawaambia, Palikuwa na wajane wengi katika nchi ya Israeli zamani za Eliya, wakati mbingu zilipofungwa miaka mitatu na miezi sita, njaa kuu ikaingia nchi nzima; wala Eliya hakutumwa kwa mmojawapo, ila kwa mjane mmoja wa Sarepta katika nchi ya Sidoni. Tena, palikuwa na wenye ukoma wengi katika Israeli zamani za nabii Elisha, wala hapana aliyetakaswa ila Naamani, mtu wa Shaibu.”’ (Luka 4:24-27) Aliposema hayo, wenye kusikiliza walijawa na hasira wakajaribu kumuua Yesu. Kwa sababu gani waliitikia kwa jeuri sana?
Ili kupata jibu, inatupasa kurudi nyuma katika Maandiko ya Kiebrania kisha tusome historia za Eliya na Elisha. Wakristo wa karne ya kwanza walifahamu sana sana habari zilizo katika vitabu hivyo, na ndivyo wasikilizaji wao wa Kiyahudi. Pindi nyingi sana waandikaji wa Biblia wa nyakati za Kikristo walitaja matukio na watu walio katika vitabu hivyo vya zamani kidogo ili kuonyesha maana ya jambo fulani, kama Yesu alivyofanya hapa. Mitajo hiyo ilitambuliwa mara moja na kufahamiwa na wasikilizaji. Ili tupate maana kamili ya mafundisho ya Yesu, tunahitaji hata sisi kuitambua mitajo hiyo.
Ukweli ni kwamba, haiwezekani kufahamu kabisa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo tusipokuwa tumefahamu vizuri Maandiko ya Kiebrania. Historia za manabii ambao Yesu alitaja, Eliya na Elisha, zimeandikwa katika vitabu vile viwili vya Wafalme. Acheni tufikirie vitabu viwili hivyo ili kuonyesha maana ya jambo hilo kisha tuone namna maarifa ya kuvijua yanavyotupa ufahamu wa ndani zaidi na ulio wazi zaidi juu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.
Ulinganisho Usiofaa
Kwanza kabisa, kwa sababu gani wakaaji wa Nazareti waliudhika sana wakati Yesu alipotaja miujiza miwili iliyofanywa na Eliya na Elisha miaka zaidi ya 900 kabla ya hapo? Basi, kwa wazi Yesu alikuwa akiwalinganisha na Wanazareti na Waisraeli wa ufalme wa Israeli wa kaskazini wakati wa siku za Eliya na Elisha, na kulingana na vitabu vile viwili vya Wafalme, Israeli hawakuwa na hali nzuri ya kiroho wakati huo. Waisraeli walikuwa wamegeuka wakaingia moja kwa moja katika ibada ya Baali na walikuwa wakitesa manabii wa Yehova. Kwa kweli Eliya alikuwa akiwakimbia wananchi wenzake wakati mjane wa Sarepta, katika nchi ya kigeni, alipomkaribisha nyumbani mwake na kumlisha. Hapo ndipo alipoufanya muujiza alioutaja Yesu. (1 Wafalme 17:17-24) Bado Israeli walikuwa wamejitia sana katika ibada ya Baali alipoponya Naamani mkuu wa jeshi la Shamu ukoma wake.—2 Wafalme 5:8-14.
Wakaaji wa Nazareti hawakufurahia kulinganishwa na Wayahudi wa siku hizo. Je! Yesu alikuwa na haki ya kuwalinganisha hivyo? Kwa wazi ndivyo. Sawa na vile uhai wa Eliya ulivyokuwa hatarini katika Israeli, ndivyo sasa uhai wa Yesu ulivyokuwa hatarini. Maandishi yanatuambia hivi: “Wakajaa ghadhabu wote waliokuwa katika sinagogi walipoyasikia hayo. Wakaondoka wakamtoa nje ya mji, wakampeleka katika ukingo wa kilima ambacho mji wao umejengwa juu yake, wapate kumtupa chini.” Lakini Yehova alimlinda Yesu, kama alivyokuwa amelinda Eliya kabla ya hapo.—Luka 4:28-30.
Utukufu wa Mfalme Sulemani
Huo ni mfano mmoja wa namna vitabu vile viwili vya Wafalme vinavyoonyesha uhakika wa maneno ya Yesu na Wakristo wa karne ya kwanza. Fikiria mfano mwingine. Katika Mahubiri ya Mlimani yake, Yesu aliwatia moyo wenye kumsikiliza wategemee Yehova katika shauri la kupata mahitaji ya kimwili. Kati ya mambo mengine, alisema: “Na mavazi, ya nini kuyasumbukia? Fikirini maua ya mashamba, jinsi yameavyo; hayafanyi kazi, wala hayasokoti; nami nawaambia, ya kwamba hata Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama mojawapo la hayo.” (Mathayo 6:28, 29) Kwa sababu gani Yesu akataja Sulemani hapo?
Wasikilizaji wake wa Kiyahudi wangeijua sababu kwa kuwa walifahamu habari za utukufu wa Sulemani. Umesimuliwa kwa urefu kidogo katika Kitabu cha Kwanza cha Wafalme (na pia katika Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati). Kwa mfano, inaelekea kuwa wangekumbuka kwamba vyakula vya nyumba ya Sulemani kila siku “vilikuwa kori thelathini za unga mzuri, na kori sita za ngano, na ng’ombe kumi walionona, na ng’ombe ishirini za malisho, na kondoo mia, pamoja na ayala, na paa, na kulungu, na kuku walionona.” (1 Wafalme 4:22, 23) Hicho kilikuwa chakula kingi.
Zaidi ya hilo, uzito wa dhahabu iliyomjia Sulemani katika mwaka mmoja ilikuwa “talanta mia sita sitini na sita,” hicho kikiwa ni kiasi cha zaidi ya shilingi milioni 3,750 (Kshs.) kulingana na thamani ya sasa ya pesa. Na vitu vyote vilivyotumiwa kupamba nyumba ya Sulemani vilikuwa vya dhahabu. “Hakuna vya fedha, fedha haikuhesabiwa kuwa kitu siku za Sulemani.” (1 Wafalme 10:14, 21) Yesu alipoamsha kumbukumbu zao juu ya mambo hayo, wasikilizaji wake walifahamu upesi maana ya aliyokuwa akisema.
Yesu alimtaja Sulemani katika habari yenye maana nyingine. Waandishi na Mafarisayao fulani walikuwa wamedai afanye ishara, naye Yesu alijibu: “Malkia wa kusini atasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu yeye alikuja kutoka pande za mwisho za dunia ili asikie hekima ya Sulemani, na hapa yupo aliye mkuu kuliko Sulemani.” (Mathayo 12:42) Kwa sababu gani mtajo huo ulikuwa kemeo kali kwa viongozi wa kidini waliokuwa wakisikiliza?
Ikiwa tunafahamu vizuri habari za kitabu cha kwanza cha Wafalme, tunajua kwamba “malkia wa kusini” alikuwa malkia wa Sheba. Kwa wazi yeye alikuwa bibi mkuu, maIkia wa milki tajiri. Alipomtembelea Sulemani, alikuja akiwa na “wafuasi wengi sana,” mafuta ya bei kubwa na “dhahabu nyingi sana, na vito vya thamani.” (1 Wafalme 10:1, 2) Kwa kawaida mawasiliano yenye amani kati ya watawala wa kitaifa yanafanywa kwa kutumia mabalozi. Kwa hiyo, lilikuwa jambo lisilo la kawaida malkia wa Sheba, mkuu mwenye kutawala, asafiri yeye binafsi njia yote hiyo mpaka Yerusalemu akamwone Mfalme Sulemani. Kwa sababu gani alifanya hivyo?
Mfalme Sulemani alikuwa tajiri sana, lakini hata malkia wa Sheba alikuwa tajiri. Hangesafiri mwendo wote huo kwa sababu tu ya kutaka kuona mtawala tajiri. Lakini, Sulemani hakuwa tajiri tu, bali pia ‘aliwapita wafalme wote wa dunia kwa mali, na kwa hekima.’ (1 Wafalme 10:23) Chini ya utawala wake wa hekima “Yuda na Israeli wakakaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, tokea Dani mpaka Beersheba, siku zote za Sulemani.”—1 Wafalme 4:25.
Hekima ya Sulemani ndiyo iliyovuta malkia wa Sheba. Yeye alikuwa ‘akisikia habari za Sulemani juu ya jina la Yehova, akaja ili amjaribu kwa maswali ya fumbo.’ Alipofika Yerusalemu, ‘alimfikilia Sulemani, akazungumza naye mambo yote aliyokuwa nayo moyoni. Naye Sulemani akamfumbulia maswali yake yote; wala hakukuwa na neno alilofichiwa mfalme asimwambie.’—1 Wafalme 10:1-3.
Yesu, pia, alikuwa na hekima ya ajabu sana ‘juu ya jina la Yehova.’ Kwa kweli, yeye alikuwa “mkubwa kuliko Sulemani.” (Luka 11:31) Malkia wa Sheba, ambaye hakuwa Myahudi, alifunga safari ndefu ya shida ili tu yeye mwenyewe ajionee Sulemani na kufaidika kutokana na hekima yake. Hivyo, kwa uhakika waandishi na Mafarisayo wangalipaswa kusikiliza kwa kuthamini yule aliye “mkubwa kuliko Sulemani” wakati alipokuwa pale pale mbele yao. Lakini hawakufanya hivyo. “Malkia wa kusini” alithamini hekima iliyotolewa na Mungu kuliko wao.
Kutaja Manabii kwa Njia Isiyo ya Moja kwa Moja
Wakati wa kipindi cha historia kinachozungumzwa katika vitabu vya Kwanza na Pili vya Wafalme, watawala katika ufalme wa makabila 12—na baadaye katika falme zilizogawanyika za Israeli na Yuda—walikuwa wafalme. Wakati huo manabii wa Yehova walikuwa wenye bidii sana kati ya watu Wake. Wenye kutokeza sana kati yao walikuwa Eliya na Elisha ambao tayari tumewataja. Mtajo wa Yesu juu yao katika Nazareti sio wakati wa peke yake ambao walitajwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.
Mtume Paulo katika barua aliyoandikia Wakristo Waebrania alisema juu ya imani ya watumishi wa Mungu wa nyakati za zamani. Kwa mfano, alisema: “Wanawake walipokea wafu wao waliofufuliwa.” (Waebrania 11:35) Bila shaka alikuwa akiwafikiria Eliya na Elisha, nao wote wawili walitumiwa kufanya miujiza. (1 Wafalme 17:17-24; 2 Wafalme 4:32-37) Wakati watatu wa mitume wa Yesu walipokuwa ‘wameona wenyewe ukuu wa Yesu’ wakati wa njozi ile ya kugeuka sura, walimwona Yesu akiongea na Musa na Eliya. (2 Petro 1:16-18; Mathayo 17:1-9) Kwa sababu gani Eliya akachaguliwa kuwakilisha mstari wa manabii wa nyakati zilizotangulia Ukristo ambao walitoa ushuhuda juu ya Yesu? Ukisoma masimulizi ya Kitabu cha Kwanza cha Wafalme na kuona imani yake kuu na njia hodari ambayo kwayo alitumiwa na Yehova, utafahamu jibu.
Hata hivyo, kwa kweli Eliya alikuwa mtu wa kikawaida tu kama sisi. Yakobo alitaja tukio jingine katika Kitabu cha Kwanza cha Wafalme wakati alipoandika: “Kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana’, akiomba kwa bidii. Eliya alikuwa mwanadamu mwenye tabia moja na sisi, akaomba kwa bidii mvua isinye; na mvua haikunya juu ya nchi muda wa miaka mitatu na miezi sita. Akaomba tena, mbingu zikatoa mvua, nayo nchi ikazaa matunda yake.”—Yakobo 5:16-18; 1 Wafalme 17:1; 18:41-46.
Mawazo Mengine Ambayo Yametolewa Katika Wafalme
Mitajo mingine mingi katika Maandiko ya Kigikiri ya Kikristo yana mawazo yaliyotolewa katika vitabu vile viwili vya Wafalme. Stefano alikumbusha Mahakama Kuu ya Kiyahudi kwamba Sulemani alijengea Yehova nyumba katika Yerusalemu. (Matendo 7:47) Mengi ya maelezo marefu yanayohusu ujenzi huo yamo katika kitabu cha kwanza cha Wafalme. (1 Wafalme 6:1-38) Yesu aliposema na mwanamke katika Samaria, mwanamke huyo alimwambia hivi kwa kushangaa: “Imekuwaje wewe Myahudi kutaka maji kwangu, nami ni mwanamke Msamaria? (maana Wayahudi hawachangamani na Wasamaria).” (Yohana 4:9) Kwa sababu gani Wayahudi hawakuwa na uhusiano na Wasamaria? Masimulizi katika Kitabu cha Pili cha Wafalme yanayoeleza chanzo cha watu hao yanatoa mwangaza wa shauri hilo.—2 Wafalme 17:24-34.
Barua inayopatikana katika kitabu cha Ufunuo liliyoandikiwa kundi la Thiatira ina shauri kali hili: “Lakini nina neno juu yako, ya kwamba wamridhia yule mwanamke Yezebeli. yeye ajiitaye nabii na kuwafundisha watumishi wangu na kuwapoteza, ili wazini na kula vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu.” (Ufunuo 2:20) Yezebeli alikuwa nani? Alikuwa binti ya kuhani wa Baali katika Tiro. Kama vile kitabu cha kwanza cha Wafalme kinavyotuambia, aliolewa na Mfalme Ahabu wa Israeli kisha akawa malkia wa Israeli. Alimtawala mume wake, akaanzisha ibada ya Baali ndani ya Israeli waasi-imani, akaingiza makuhani wengi wa Baali nchini na kutesa manabii wa Yehova. Mwishowe, aliuawa kwa jeuri.—1 Wafalme 16:30-33; 18:13; 2 Wafalme 9:30-34.
Kwa wazi mwanamke aliyekuwa akionyesha roho ya Yezebeli katika kundi la Thiatira alikuwa akijaribu kufundisha kundi lizoee uasherati na kuvunja sheria za Mungu. Roho ya namna hiyo ilipasa kuondolewa kabisa kundini, sawa na vile jamaa ya Yezebeli ilivyopaswa kuondolewa kabisa katika taifa la Kiisraeli.
Ndiyo, tunahitaji Maandiko ya Kiebrania ili kufahamu Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kuwa na maelezo mengi kungekuwa hakuna faida bila yale mambo ya msingi yanayoonyeshwa na Maandiko ya Kiebrania. Yesu na Wakristo wa kwanza, na pia Wayahudi waliowazungumzia, walifahamu vizuri maandiko hayo. Kwa sababu gani usichukue wakati ili wewe mwenyewe pia ujifahamishe maandiko hayo kama wao? Hivyo utajipatia faida kamili ya “kila andiko,” ambalo ni “lenye pumzi ya Mungu [na] lafaa kwa mafundisho.”—2 Timotheo 3:16.