Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 7/1 kur. 30-31
  • Ziara Iliyothawabishwa Sana

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ziara Iliyothawabishwa Sana
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ripoti Yenye Kuvutia
  • Maswali ya Fumbo, Majibu Yenye Kuridhisha
  • Somo Kwetu
  • Ukarimu Unapokuwa Mwingi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Sulemani Atawala kwa Hekima
    Biblia—Ina Ujumbe Gani?
  • Ufahamu Kutokana na Vitabu Viwili vya Wafalme
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Alithamini Hekima
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2023
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 7/1 kur. 30-31

Walifanya Mapenzi ya Yehova

Ziara Iliyothawabishwa Sana

LAZIMA malkia awe alichoshwa sana na safari ya kutoka Sheba hadi Yerusalemu. Alikuwa amezoea kuishi maisha ya anasa. Sasa alikuwa akisafiri kwa mwendo wa ngamia safari iliyokuwa na urefu wa kilometa 2,400, sehemu kubwa ikiwa katika jangwa lenye joto jingi. Kulingana na kadirio moja, huenda safari yake, ya kwenda tu hadi huko, ilichukua siku zipatazo 75 kuikamilisha!a

Ni kwa nini malkia huyo mwenye mali nyingi aliacha makao yake yenye starehe katika Sheba na kufunga safari ngumu hivyo?

Ripoti Yenye Kuvutia

Malkia wa Sheba alikuja Yerusalemu baada ya “[ku]sikia habari za Sulemani juu ya jina la BWANA.” (1 Wafalme 10:1) Habari kamili ambayo malkia alisikia haijaelezwa. Hata hivyo, twajua kwamba Yehova alimpa Solomoni baraka ya hekima, mali, na heshima kwa njia ya pekee. (2 Mambo ya Nyakati 1:11, 12) Malkia alikuja kujuaje hayo? Kwa kuwa Sheba ilikuwa kitovu cha biashara, huenda alisikia juu ya umaarufu wa Solomoni kupitia wafanyabiashara waliozuru nchi yake. Labda baadhi ya watu hao walikuwa wamezuru Ofiri, nchi ambayo Solomoni alifanya nayo biashara nyingi.—1 Wafalme 9:26-28.

Kwa vyovyote vile, malkia huyo aliwasili Yerusalemu “na wafuasi wengi sana, na ngamia wachukuao manukato, na dhahabu nyingi sana, na vito vya thamani.” (1 Wafalme 10:2a) Watu fulani husema kuwa hao “wafuasi wengi sana” walikuwa ni pamoja na kikosi chenye silaha. Hilo laeleweka, ukikumbuka kwamba malkia huyo alikuwa mheshimiwa mwenye nguvu, akisafiri na mali zenye thamani kubwa sana.b

Hata hivyo, ona kwamba malkia alisikia umaarufu wa Solomoni “juu ya jina la BWANA.” Hivyo, safari hiyo haikuwa ya kibiashara tu. Yamkini, malkia alikuja hasa kusikiliza hekima ya Solomoni—labda hata kujifunza jambo fulani kuhusu Mungu wa Solomoni, Yehova. Kwa vile yawezekana alikuwa wa uzao wa Shemu ama Hamu, waliokuwa waabudu wa Yehova, huenda alikuwa mdadisi kuhusu dini ya mababu wake.

Maswali ya Fumbo, Majibu Yenye Kuridhisha

Alipokutana na Solomoni, malkia akaanza kumjaribu kwa “maswali ya fumbo.” (1 Wafalme 10:1) Neno la Kiebrania lililotumiwa hapo laweza kutafsiriwa “vitendawili.” Lakini hilo halimaanishi kwamba malkia alimwingiza Solomoni katika michezo isiyo na maana. Kwa kupendeza, katika Zaburi 49:4 (BHN), neno hilohilo la Kiebrania limetumiwa kufafanua maswali mazito yanayohusu dhambi, kifo, na ukombozi. Basi, yaonekana kuwa malkia wa Sheba alikuwa akizungumza na Solomoni habari nzito zilizojaribu kina cha hekima yake. Biblia yataarifu kwamba malkia “a[li]zungumza naye mambo yote aliyokuwa nayo moyoni.” Solomoni naye “akamfumbulia maswali yake yote; wala hakukuwa na neno alilofichiwa mfalme asimwambie.”—1 Wafalme 10:2b, 3.

Malkia wa Sheba alivutiwa sana na hekima ya Solomoni na ufanisi wa ufalme wake hivi kwamba “roho yake ilizimia.” (1 Wafalme 10:4, 5) Wengine husema kuwa fungu hilo lamaanisha malkia “alihemahema.” Msomi mmoja hata adokeza kwamba alizimia! Hata iweje, malkia alishangazwa na yale aliyoona na kusikia. Aliwatangaza watumishi wa Solomoni kuwa wenye furaha kwa kusikiliza hekima ya mfalme huyo, naye akamtukuza Yehova kwa kumweka Solomoni kwenye kiti cha ufalme. Kisha akampa mfalme zawadi zenye thamani kubwa, dhahabu pekee ilifikia, kwa bei ya sasa, dola 40,000,000 hivi. Naye Solomoni akamtunukia zawadi, akampa malkia “haja yake yote, kila alilotaka.”c—1 Wafalme 10:6-13.

Somo Kwetu

Yesu alitumia malkia wa Sheba kama tukio lenye funzo kwa waandishi na Mafarisayo. “Malkia wa kusini atainuliwa katika hukumu pamoja na kizazi hiki naye atakilaumu; kwa sababu alikuja kutoka miisho ya dunia kuisikia hekima ya Solomoni, lakini, tazama! kitu fulani zaidi ya Solomoni kipo hapa.” (Mathayo 12:42) Naam, malkia wa Sheba alionyesha uthamini mkubwa kwa hekima iliyotoka kwa Mungu. Ikiwa alisafiri kilometa 2,400 ili kumsikiliza Solomoni, kwa hakika waandishi na Mafarisayo walipaswa kumsikiliza Yesu, aliyekuwa hapohapo mbele yao, kwa makini.

Sisi leo twaweza kuonyesha uthamini mkubwa kwa Solomoni Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo. Kwa njia gani? Njia moja ni kwa kufuata mwelekezo wake kuhusu “[kufanya] wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” (Mathayo 28:19) Njia nyingine ni kwa kutafakari kielelezo na mtazamo wa akili wa Yesu na kisha kuiga sifa hizo.—Wafilipi 2:5; Waebrania 12:2, 3.

Ni kweli kwamba twahitaji kujitahidi sana ili kufuata kielelezo cha Solomoni Mkubwa Zaidi. Hata hivyo, tutapata thawabu tele. Kwa kweli, Yehova awaahidi watu wake kwamba wakionyesha roho ya kujidhabihu, ‘atawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagia baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha.’—Malaki 3:10.

[Maelezo ya Chini]

a Wasomi wengi huamini kuwa Sheba ilikuwa kusini-magharibi mwa Arabia, katika nchi ambayo leo ni Jamhuri ya Yemeni.

b Kulingana na Strabo, mwanajiografia wa kale Mgiriki, watu wa Sheba walikuwa na mali nyingi mno. Yeye asema kwamba walitumia dhahabu kwa wingi katika fanicha zao, vyombo, na hata katika kuta, milango, na paa za nyumba zao.

c Watu fulani husema kwamba fungu hilo lamaanisha kuwa malkia alifanya ngono na Solomoni. Ngano zasema kwamba hata walipata mwana. Hata hivyo, hakuna uthibitisho unaounga mkono lolote la madai hayo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki