Je! Biblia Irekebishwe Ikubalie Watu Kuoa Wake Wengi?
KATIKA gazeti Bijeen (maana yake, Pamoja), ambalo ni gazeti la Kikatoliki nchini Uholanzi, Sjef Donders anayeandika safu za magazeti alizungumza juu ya mgongano ulio katika nchi fulani za Afrika kati ya amri ya Kibiblia inayohusu kuwa na mke mmoja na ile desturi inayokubaliwa ya kuoa wanawake wengi. Mgongano huo umemalizwa, kwa “kutangaza tu kwamba fundisho la kanisa [juu ya kuoa mke mmoja tu] halifai.”
Akionyesha kwamba maoni ya kanisa hayana uhakika, Donders alitaja maneno yaliyosemwa na padri Mwamerika Eugene Hillman, aliye mshiriki wa chama cha Kikatoliki kinachoitwa Mababa wa Roho Mtakatifu ambacho kimeendesha sana umisionari wa Kikatoliki katika Afrika. Katika kitabu kinachoshughulika na kuoa wanawake wengi, Hillman aliandika hivi: “Ikiwa, kwa sababu ya maafa fulani ya asili au mabaya yenye kusababishwa na wanadamu, hesabu ya wanaume ingekaribia kwisha, iwe ni kama wanawake tu ndio wamebaki, hakika zingepatikana sababu katika Biblia za kuruhusu wanaume hao waliobaki wafanye ngono na wanawake wengi.”
Je! sababu zingepatikana? Hata maoni ya padri huyo yawe ni ya kulegeza mambo kadiri gani, ndoa yenye wanawake wengi haipasi kuruhusiwa kwa Mkristo ye yote hata awe ni wa taifa gani au ana hali gani. Ndoa yenye mke mmoja tu ndiyo iliyokuwa mpango wa Mungu kwa wanadamu katika Edeni, na Yesu Kristo alionyesha kwamba watu wanapaswa kurudia mpango huo katika kundi la Kikristo. (Mathayo 19:4-6) Chini ya uongozi wa Mungu mtume Paulo aliandika hivi: “Imempasa mwangalizi awe bila lawama, mume wa mke mmoja.” (1 Timotheo 3:2) Na kwa habari ya Wakristo wote, alishauri hivi: “Kwa sababu ya kuenea sana kwa uasherati, kila mwanamume na awe na mke wake mwenyewe na kila mwanamke awe na mume wake mwenyewe.” (1 Wakorintho 7:2, NW) Jambo hilo haliwaachii Wakristo wa kweli nafasi ya kuoa wanawake wengi.