Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 8/1 kur. 13-18
  • Fundisha kwa Ustadi na Bidii

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Fundisha kwa Ustadi na Bidii
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Angalia Mafundisho Yako’
  • Jitahidi Kuwa Mwalimu Bora
  • Mikutano Inaweza Kutufanya Tuwe Wastadi Zaidi
  • Mazoezi kwa Ajili ya Kufundisha kwa Bidii
  • Endelea Kusitawisha Ustadi
  • “Mnapaswa Kuwa Walimu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Uwe Stadi Katika Huduma Yako
    Huduma Yetu ya Ufalme—1990
  • Kutayarishwa Kusema Maneno Yapendezayo ya Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Kufundishwa na Yehova Hadi Siku Hii
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 8/1 kur. 13-18

Fundisha kwa Ustadi na Bidii

“Kwa hiyo, nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”​—MATHAYO 28:19, 20, NW.

1. Ni jambo gani ambalo Mithali 22:29 inatia moyo lisitawishwe, na jinsi gani hivyo?

NENO LA YEHOVA linatia moyo kuwa na ustadi na kufanya kazi kwa juhudi. Kwa mfano, linasema: “Je! wamwona mtu mwenye bidii katika kazi zake? Huyo atasimama mbele ya wafalme; hatasimama mbele ya watu wasio na cheo.” (Mithali 22:29) Bila shaka, si kushushwa cheo kufanyia kazi “watu wasio na cheo.” Lakini kazi njema ya fundi stadi haitabaki sirini. Kwa kuwa habari za ufundi wake zaweza kusikiwa na mfalme, ambaye huenda akataka kutumikiwa naye!

2. (a) Ili kusitawisha ustadi katika kazi yo yote, ni jambo gani la lazima? (b) Ni kwa sababu gani kuwa kwa mhudumu wa Kikristo mwenye matokeo ni kwa maana sana?

2 Maarifa na ustadi yanahitajiwa katika kazi yo yote. Huenda mtu akajifunza useremala na huenda pia akajifunza mengi kwa kuangalia wale wenye ustadi wa kazi hiyo. Lakini ili yeye mwenyewe akuze ustadi huo ni lazima atumie katika kazi hiyo maarifa aliyojipatia. Daktari wa upasuaji anahitaji kuwa ameelimishwa. Lakini ili kuwa fundi, ni lazima atumie maarifa yake katika chumba cha upasuaji. Na katika kazi hiyo ustadi unahitajiwa, kwa maana ufundi mara nyingi unaweza kumaanisha uhai au kifo kwa mgonjwa. Lakini, wa maana zaidi ni ustadi wa kuwa mhudumu. Kwa sababu gani? Kwa sababu kuwa kwa mhudumu na matokeo akiwa mwalimu kwaweza kuongoza namna watu wanavyoitikia habari njema. Nalo itikio lao laweza kumaanisha uzima wa milele au kifo cha milele kwao.​—Kumbukumbu la Torati 30:19, 20; Yohana 17:3.

3. Kufanya wanafunzi kunataka nini?

3 Mgawo ambao Yesu Kristo aliwapa wafuasi wake unatia ndani kufundisha. Alisema: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi. Na, tazama! mimi nipo pamoja na ninyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:19, 20, NW) Bila shaka, ustadi unahitajiwa ili kufundisha wenye mioyo minyofu mambo yote aliyoamuru Yesu.

4. (a) Kufundisha kwa ustadi kwapasa kufanywa kwa nia gani? (b) Apolo alifaidikaje kwa kushirikiana na Akila na Prisila?

4 Ufundishaji huo wa ustadi wapasa kufanywa kwa bidii. Ndiyo, Wakristo wanapaswa kuwa “wenye bidii kwa ajili ya kazi njema,” na bila shaka kazi hizo ni kutia na kutoa maagizo ya kiroho katika huduma na kundi. (Tito 2:14, NW) Wakiwa walimu stadi, Akila na Prisila ‘walimchukua Apolo kwao, wakaanza kushinda pamoja naye huko Efeso na kumweleza njia ya Mungu kwa usahihi zaidi.’ Jambo hilo lilimfaidi sana Apolo, kwa maana baadaye katika Akaya “kwa bidii yenye joto jingi aliwathibitishia Wayahudi kweli kweli kuwa ni wenye kosa mbele ya watu wote, huku akionyesha kulingana na Maandiko kwamba Yesu ndiye Kristo.” (Matendo 18:24-28, NW) Kwa wazi, Apolo alifundisha kwa ustadi na bidii.

‘Angalia Mafundisho Yako’

5. Kulingana na 1 Timotheo 4:16, ni kwa sababu gani tunapaswa kufundisha kwa ustadi na bidii?

5 Mtume Paulo alimwambia mwenzi wake Mkristo Timotheo hivi: “Jitunze [‘Jiangalie,’ NW] nafsi yako, na mafundisho yako. Dumu katika mambo hayo; maana kwa kufanya hivyo utajiokoa nafsi yako na wale wakusikiao pia.” (1 Timotheo 4:16) Kwa kuwa wokovu wenyewe wa mwalimu na mwanafunzi unahusika sana, bila shaka maagizo hayo yanapasa kutolewa kwa ustadi na kwa bidii.

6. Unaweza kuwaje fundi wa kutumia Maandiko, na ni maswali gani yanayofaa ambayo yanaweza kufikiriwa?

6 Maseremala na madaktari wa upasuaji hakika ni lazima wajiangalie. Ni lazima waweze kutumia vyombo vyao kwa ufundi. Ni hali moja na mhudumu Mkristo, ambaye chombo chake kikuu ni ‘upanga wa roho, neno la Mungu.’ (Waefeso 6:17) Unaweza kuwaje fundi wa kutumia Maandiko? Bila shaka, ni kwa kujifunza kwa ukawaida na kutumia unayojifunza. Kwa hiyo, je, umekwisha kuisoma Biblia toka jalada mpaka jalada, ukichukua wakati kutafakari mashauri yayo yaliyo mazuri sana? Je! wewe unaisoma kila siku? Je! wewe unaitumia kwa ukawaida katika huduma ya shambani? Na je, unajifaidi kwa ukamili na chakula kingi cha kiroho kinachotolewa na Yehova kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili”?​—Mathayo 24:45-47.

7. Ni mapendekezo gani yanayotolewa kuhusu wakati wa funzo, na uhitaji wa funzo unaweza kuonyeshwaje Kimaandiko?

7 Hakikisha kuweka kando wakati wa kujifunza Neno la Mungu na vichapo vya kweli vya Kikristo. Kufanya hivyo kutajaza akili yako na habari yenye kujenga itakayokufaidi wewe na inayoweza kutumiwa kujibu watu wenye kutaka kujua kwa moyo mweupe. (1 Petro 3:15; Wakolosai 4:6) Nyakati za funzo na kutafakari zinatofautiana kati ya jamaa hii na hii na mtu huyu na huyu. Huenda wengine wakaona inafaidi kujifunza mwishoni mwa siku. Huenda wengine wakawa chonjo zaidi wanapoamka. Na bado wengine huenda wakaona adhuhuri kuwa wakati unaowafaa zaidi. Vyo vyote iwavyo, ukawaida na bidii ni mambo ya maana sana. Yoshua na wafalme wa Israeli walipaswa kusoma Neno la Mungu kila siku,—Yoshua 1:7, 8; Kumbukumbu la Torati 17:18-20.

Jitahidi Kuwa Mwalimu Bora

8. Kushirikisha akili kunaweza kufanyaje ustadi wako wa kufundisha uwe bora zaidi?

8 Kufanyia maendeleo ustadi wa kufundisha kunataka kazi ya bidii. Njia moja ya kufanya uwezo wako uwe bora zaidi ukiwa mwalimu ni kutumia akili kushirikisha mambo unapojifunza Biblia au vichapo vya Kikristo. Shirikisha mawazo mapya na yale unayojua tayari. Kufanya hivyo kutasaidia habari hiyo isimame akilini mwako ili uweze kueleza mambo waziwazi unapofundisha wengine. Kwa mfano, wakati mmoja huenda ukawa hukujua kwamba Wakristo wanapaswa kutii kwa kadiri “mamlaka kuu” za kiserikali. Lakini sasa unajua kwamba kumtii Mungu ni lazima kuwe ndilo jambo la kwanza. (Warumi 13:1-8; Marko 12:17; Matendo 5:29) Unafahamu hayo kwa sababu umeshirikisha mambo mapya na yale uliyojua tayari.

9. Onyesha jinsi unavyoweza kupiga picha akilini tukio fulani lililoandikwa katika Biblia.

9 Njia nyingine ya kuongeza uwezo wako wa kufundisha ni kupiga picha akilini visa vilivyoripotiwa katika Biblia. Kwa nini usifanye hivyo sasa kwa kusoma Waamuzi 7:19-22? Kwa kufichwa na giza, Gideoni na wanaume 300 wanazingira kambi ya Wamidiani ambako walinzi wametoka tu kuwekwa. Ghafula, unasikia kikundi kidogo cha Gideoni chenye watu 100 kikipiga tarumbeta zao, halafu unawaona wakigonganisha mitungi ya maji ambayo wamekuwa wakiichukua. Wale Waisraeli wengine 200 wafanya vivyo hivyo. Na wote wanapoinua mwanga wa moto, sikia wakipiga kelele hii kubwa: ‘Upanga wa Yehova na wa Gideoni!’ Wamidiani waliopigwa hofu wanapoanza kutoroka, vile vikundi vitatu vya Gideoni vinaendelea kupiga tarumbeta zao, na kuona kwamba Yehova amefanya maadui wanaotoroka wauane kwa panga zao. Kwa sababu umepiga picha akilini tukio hilo, bila shaka utalikumbuka vizuri na utaweza kutumia jambo hilo unapofundisha wengine. Bila shaka, somo moja la jambo hilo ni kwamba Yehova anaweza kuokoa watu wake bila kuwa na jeshi lenye nguvu la kibinadamu.​—Zaburi 94:14.

10. Katika kufundisha, unaweza kutumiaje mfano ulioko katika Waamuzi 9:8-15?

10 Mifano mizuri, kutia ile iliyomo ndani ya Maandiko, pia inaweza kufanya ustadi wako ukiwa mwalimu uwe bora zaidi. Kwa mfano, fikiria Waamuzi 9:8-15. Mwana wa Gideoni, Yothamu, alieleza juu ya wakati ambapo miti ilienda kupaka mafuta mtawala wayo. Ingawa mzeituni, mtini, na mzabibu ilikataa cheo cha utawala, mti wa miiba wa hali ya chini ulikubali cheo hicho kwa shauku. Miti hiyo yenye thamani ilifananisha watu waliostahili ambao hawakutafuta kuwa wafalme juu ya Waisraeli wenzao. Lakini, mti wa miiba, wa aina yenye kufaa kutumiwa kwa mafuta tu, ulifananisha ufaIme wa Abimeleki muuaji, mwenye kichwa kikubwa, aliyetaka kutawala wengine lakini akapatwa na mwisho mbaya uliotimiza unabii wa Yothamu. (Waamuzi 9:50-57) Mfano huo unaweza kutumiwa kukazia uhitaji wa kufanya yaliyo haki na kuwa wanyenyekevu, si wenye kichwa kikubwa.​—Zaburi 18:26, 27; 1 Petro 5:5.

11. (a) Ni mambo gani yanayokaziwa na mfano wa Yesu ulioandikwa katika Mathayo 13:45, 46? (b) Jinsi ulivyo mfano huo inaonyesha nini juu ya mifano inayotumiwa na walimu Wakristo?

11 Mwalimu Mkuu, Yesu Kristo, anajulikana sana kwa sababu ya mifano yake bora sana. Kwa mfano, fikiria maneno haya yake: “Ufalme wa mbinguni umefanana na mfanya biashara, mwenye kutafuta lulu nzuri; naye alipoona lulu moja ya thamani kubwa, alikwenda akauza alivyo navyo vyote, akainunua.” (Mathayo 13:45, 46) Kwa mfano huo Yesu alionyesha thamani ya Ufalme na kuonyesha kwamba mtu anayethamini thamani halisi ya kuupata angekuwa na nia ya kutoa cho chote ili aupate. Mfano huo haukuwa mgumu, na walimu Wakristo yawafaa kukumbuka kiwango hicho wanapotumia mifano kuwa msaada wa kufundisha.

Mikutano Inaweza Kutufanya Tuwe Wastadi Zaidi

12. Kuhudhuria hotuba za watu wote kunaweza kukusaidiaje ufanye uwezo wako wa kufundisha uwe bora zaidi?

12 Mikutano ya Kikristo inatimiza sehemu ya maana kuwafanya watumishi wa Yehova wawe walimu stadi na wenye bidii. Kama Mahubiri ya Mlimani ya Yesu yanavyoonyesha, hotuba za watu wote ni njia nzuri ya kutoa maagizo ya kiroho. (Mathayo 5:1–7:29) Kwa hiyo, hotuba za watu wote ni sehemu ya mikutano ya Mashahidi wa Yehova leo. Je! wewe unahudhuria kwa ukawaida? Je! wewe ni msikilizaji mzuri? Je! unafungua Biblia yako maandiko yanaposomwa na msemaji? Je! una zoea la kuandika mambo? Hizo ni njia za kufanya uwezo wako ukiwa mwalimu uwe bora zaidi, na maagizo hayo mazuri ya Kimaandiko yanapasa kuongeza ustadi na bidii yako pia ukiwa mfanya wanafunzi.

13, 14. (a) Ni wakati gani kazi ya kufanya wanafunzi ilipochukua umaana maalum kati ya watumishi wa Yehova? (b) Ni maulizo gani yanayoweza kuulizwa kwa kufaa juu ya Funzo la Mnara wa Mlinzi na Funzo la Kitabu la Kundi?

13 Kazi ya kufanya wanafunzi ilichukua umaana maalum kati ya watumishi wa Yehova wakati mwito ulipotolewa wa ‘Kumtangaza Mfalme na Ufalme,’ ambao ulitangazwa kwanza wakati wa kusanyiko lao katika Cedar Point, Ohio, mwaka wa 1922. Pia katika mwaka huo, mafunzo ya vikundi-vikundi ya Sosaiti yetu yalipangwa kwa mara ya kwanza. Hakika gazeti hili limetanguliza ufundishaji wa Biblia na kuhubiri Ufalme. Jina lenyewe la gazeti hili ni Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova. Je! wewe ni msomaji mwenye hamu sana wa Neno la Mungu pamoja na Mnara wa Mlinzi unaotumika kuwa msaada? Je! wewe unashiriki kwa bidii katika Funzo la Mnara wa Mlinzi la kila juma?

14 Pia Funzo la Kitabu la Kundi la kila juma linatoa nafasi za kufanya uwezo wako ukiwa mwalimu wa habari njema uwe bora. Unapotoa majibu kwenye mikusanyiko midogo hiyo, pia kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi, je! unaeleza mambo kwa maneno yako mwenyewe? Je! maelezo yako yanaonyesha mambo unayosadiki moyoni mwako?

15. Kusudi la Mkutano wa Utumishi ni nini, na uongozi kwa ajili yayo unatolewaje?

15 Kabla ya mwaka wa 1922, ilikuwa desturi kwa watumishi wa Yehova kukusanyika kwa ajili ya mkutano wa Sala, Sifa, na Ushuhuda katikati ya juma. Hiyo ilikuwa pindi ya kuimba, kutoa shuhuda, na kushiriki katika sala. Lakini kwa sababu ya mkazo kuongezwa juu ya utangazaji wa Ufalme nyumba kwa nyumba, mkusanyiko huko uliendelea ukawa Mkutano wa Utumishi, unaokazia kazi ya kuhubiri. Kichapo Bulletin kilisaidia zaidi. Kilikuwa na maagizo na ushuhuda wa utumishi wa shambani ambao ungeweza kutumiwa katika huduma. Leo, Huduma ya Ufalme Yetu inatoa msaada kama huo, pamoja na uongozi wa “Mikutano Inayotusaidia Kufanya Wanafunzi” ya kila juma. Je! wewe unafuata mashauri yaliyokusudiwa kukusaidia ufundishe kwa ustadi na bidii?

16. Kama ilivyosemwa wakati wa kuanzishwa kwayo, kusudi la Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ni nini?

16 Ili kuendeleza ufundishaji wa ustadi, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ilianzishwa katika makundi ya Mashahidi wa Yehova mwaka wa 1943. Kuhusu kusudi kuu la shule hiyo, kitabu cha kwanza cha kuongozea shule hiyo kilisema: “Mtaala huu haukuandaliwa ili kuchukua wakati unaotumia katika utumishi wa shambani, bali umepangwa ili kukufanya uutumie kwa ufundi zaidi. Kwa kusema kwa njia ya moja kwa moja zaidi, kusudi la huu ‘Mtaala katika Huduma ya Kitheokrasi’ ni kutayarisha ‘wanaume waaminifu’, wale ambao wamesikia Neno la Mungu na kuthibitisha imani yao katika huo, ‘kuweza kufundisha wengine’ kwa kwenda mlango kwa mlango, kwa kufanya marudio [ziara za kurudia], kwa kuongoza mafunzo ya kielelezo na mafunzo ya kitabu, na, kwa ufupi, kwa kushiriki katika kila sehemu ya utumishi wa Ufalme. Ni kwa ajili ya kusudi moja la kumfanya kila mmoja awe mhudumu wa Kitheokrasi mwenye matokeo iwe kwa utukufu wa jina la Bwana; ili awe tayari zaidi kutangaza peupe tumaini lililomo ndani yake; ili ‘afae kufundisha, awe mwenye subira, akiagiza kwa upole’. (2 Tim. 2:24, 25) Mtu ye yote asiache kuona kusudi hilo la kwanza la mtaala huu.” (Course in Theocratic Ministry, ukurasa 4) Hilo lingali ndilo kusudi kuu la Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Je! wewe umekuwa ukifuata habari nzuri juu ya kufundisha, kusoma, kusema mbele ya watu hadharani, na nyingine kama hizo, zilizomo katika vitabu vya shule hiyo?a Je! wewe umejiandikisha? Je! wewe unakubali kwa shukrani na kutimiza migawo yako kwenye programu ya shule? Uandalizi huo wa Yehova kupitia tengenezo lake unaweza kusaidia kukufanya uwe mhudumu stadi mwenye bidii.

Mazoezi kwa Ajili ya Kufundisha kwa Bidii

17. Ni maandalizi gani ya kiroho ambayo Yehova amewafanyia wale wanaofundisha wengine ukweli wake mtakatifu?

17 Yehova anatoa maandalizi mengi ya kiroho kwa ajili ya wale waliopendelewa kufundisha wengine ukweli wake mtakatifu. Kati ya mambo mengine, anatoa vitabu vya Biblia, mikutano ya kila juma, na makusanyiko makubwa zaidi. Maandalizi hayo yanawezesha Mashahidi wake walio wakfu wawe walimu stadi na wenye bidii.

18. Kwa kufuata mifano ya Yesu na Paulo, wazee wanaweza kufanya mipango gani waendeleze mbele huduma ya shambani leo?

18 Lakini namna gani ikiwa sisi ni wazee waliowekwa rasmi au ni mashahidi wa Yehova wenye ujuzi zaidi? Basi upendo kwa ajili ya wengine wapasa kutusukuma tusaidie wapya na Wakristo wasio na ujuzi sana ili wawe walimu stadi zaidi na wenye juhudi zaidi. Hakika hilo linafaa, kwa maana Yesu aliwatuma wanafunzi 70 baada tu ya kuwapa maagizo ya huduma yao. (Luka 10:1-24) Paulo aliwafundisha waangalizi wa Efeso “waziwazi, na nyumba kwa nyumba,” na kufanya hivyo kungetia kuwazoeza watoe ushuhuda kwa watu wasioamini walipokuwa wakienda mlango kwa mlango katika huduma ya shambani. (Matendo 20:20, 21) Hali moja na hiyo, wazee, mapainia, na wengine wanaweza kwa furaha kuzoeza Mashahidi wenzao katika huduma ya shambani leo. Je! wewe unaona uhitaji wa mazoezi hayo? Basi kwa vyo vyote yatafute na uyakubali. Je! wewe ni mzee? Basi fanya mipango ya kuzoeza wengine katika huduma huku wewe mwenyewe ukiongoza kwa bidii katika utumishi wa shambani.

Endelea Kusitawisha Ustadi

19. Ni kwa sababu gani tunapaswa kusali juu ya huduma yetu?

19 Madaktari wa upasuaji, maseremala, na wengine wanaweza kuwa stadi zaidi kwa kuendelea kujifunza na kufuata maarifa waliyokwisha kutwaa. Ni hali moja na wahudumu Wakristo. Basi, ni jambo la maana kama nini kwamba kila shahidi wa Yehova aliye wakfu ajitahidi sana kuongeza ustadi wake akiwa mwalimu wa habari njema! Na kwa kuwa hii ni kazi ya Yehova, yapasa kuwa habari ya kuzungumzwa kwa bidii katika sala zetu. Tukitafuta msaada na uongozi wa Mungu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba atabariki huduma yetu ya bidii. Kama mtume Yohana alivyosema: “Lo lote tuombalo, twalipokea kwake [Yehova Mungu], kwa kuwa twazishika amri zake, na kuyatenda yapendezayo machoni pake.”​—1 Yohana 3:22.

20. Mfumo huu unapokaribia mwisho wake, azimio letu sisi Mashahidi wa Yehova lapasa kuwa nini?

20 Mfumo wa mambo mbovu wa sasa unapokaribia mwisho wake, basi, na tujikaze kwa bidii katika huduma. Na ‘tujiangalie wenyewe na mafundisho yetu,’ tupate wokovu sisi wenyewe na wale wanaotii ujumbe wa Ufalme. Ndiyo, na tufanye kila jitihada kufundisha kwa ustadi na bidii.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa mfano, tafadhali ona Kiongozi cha Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Qualified to Be Ministers (Chapa Iliyosahihishwa), vilivyochapishwa na Sosaiti yetu.

Wewe Ungesemaje?

◻ Licha ya kuhubiri, kazi ya kufanya wanafunzi inataka nini?

◻ Ni kwa sababu gani ni jambo la maana sana ‘kuangalia mafundisho yako’?

◻ Baadhi gani ya njia za kuongeza ustadi wa kufundisha?

◻ Mikutano ya Kikristo inaweza kutusaidiaje tuwe walimu stadi na wenye bidii wa Neno la Mungu?

◻ Wazee na Mashahidi wengine wenye ujuzi wanaweza kufanya nini kuhusu huduma ya shambani?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kupiga picha akilini juu ya matukio ya Biblia kunaweza kukusaidia uwe mwalimu bora zaidi

[Picha katika ukurasa wa 17]

Mwalimu wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi anasaidia wanafunzi wawe wastadi katika huduma wa Ufalme

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki