Je! Wewe Unaweza Kupanua Eneo Lako Ukiwa Painia?
YESU KRISTO alisema hivi safari moja: “Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia; maana kwa sababu hiyo nalitumwa.” (Luka 4:43) Bila shaka, Yesu alikuwa ndiye mtangaza Ufalme mkubwa mwenye kuwatangulia wote, painia wa kweli katika utumishi mtakatifu wa Yehova.
Kama Yesu, mtume Paulo alikuwa mhudumu wa wakati wote aliyependezwa sana sana na kazi ya kueneza evanjeli. Kwa kweli, yeye alikuwa na tamaa nyingi ya kupanua eneo la huduma yake.—Linganisha Warumi 15:23, 24; 2 Wakorintho 10:15, 16, NW.
Wakiwa na roho inayofanana na hiyo, wengi wa mashahidi wa kisasa wa Yehova wamejifanya kuwa tayari wakatumikie wakiwa wamisionari katika nchi za kigeni. Wahudumu wengine Wakristo wanatumikia mahali ambako uhitaji ni mkubwa zaidi. Na wengi zaidi wameona inawezekana kuwa mapainia, wahubiri wa wakati wote wa habari njema.
Lakini namna gani wewe? Ikiwa wewe hutumikii sasa ukiwa painia, je! unaweza kupanua eneo lako, kwa usemi wa mfano, uwe mtangaza Ufalme wa wakati wote?
Faida za Utumishi wa Painia
Mapainia wenye bidii na wenye matokeo hawasukumwi na kupendezwa na faida za kibinafsi bali na upendo kwa Mungu na tamaa ya kusaidia wengine. Wahudumu wa wakati wote walio namna hivyo wanajisikia sana wakiwa na uhitaji wa kutumia Neno la Mungu katika maisha zao na wanafurahi sana kwamba wanaweza kuutafutia nafasi utumishi wa wakati wote. Nako kufanya hiyo kunaleta faida.
‘Kutangaza kila siku habari njema za wokovu unaoletwa na Yehova’ ni faida moja ya utumishi wa painia. (Zaburi 96:2, NW) Kwa kweli, kusema kwa ukawaida juu ya Mungu na makusudi yake kunaridhisha, hasa kwa sababu kufanya hivyo kunasaidia wengine waingie katika njia inayoongoza kwenye uzima. “Hakuna furaha inayozidi ile ya kujifunza Biblia pamoja na mtu na kumwona akiwa mwabudu wa Yehova,” akasema dada mmoja ambaye amekuwa katika utumishi wa painia kwa miaka 46.
Ustadi mkubwa zaidi katika kuutumia ‘upanga wa roho, neno la Mungu,’ ni faida inayotokana na matumizi ya ukawaida ya Biblia katika huduma ya painia. (Waefeso 6:17) Maneno haya ni mfano tu wa maneno ambayo yamesemwa na mapainia wengi: “Zaidi ya kuongeza ushujaa wangu, mimi nilipata kuzoelea sana maandiko mengi ya Biblia niliyoyaweka katika kumbukumbu la akili zangu, tayari kuyatumia.”
Uvutano mzuri wa utumishi wa painia unaweza kuhisiwa pia kundini. Kuhusu jambo hilo mzee mmoja aliandika hivi: “Ulitokeza tofauti kubwa sana! Mwendo wa kundi ulibadilika. Maelekeo sasa ni kuongeza ushiriki wetu zaidi na zaidi katika utumishi wa Yehova.” Ndiyo; huenda wengine wakasisimuliwa sana na mfano wa bidii wa wahudumu mapainia.
Mtu anaweza kuwa mwenye uhakika mkubwa zaidi katika Yehova kwa kushiriki katika huduma ya painia. Bila shaka, wahudumu wa wakati wote wanalazimika kushinda matatizo. Mume na mke mapainia walionyesha uhakika wao kwa maneno haya: “Shukrani ni kwa Yehova, sisi hatujapungukiwa na cho chote. Tukiwa mapainia tumekuwa wenye kumtegemea Yehova na tumeona namna anavyotoa msaada tunapouhitaji zaidi.”—Zaburi 34:10; 37:25.
Baraka kwa Sababu ya Kujitahidi Kuufikia
‘Nijaribuni, tafadhali, mwone kama sitafungua malango ya mafuriko ya mbingu na kuwamwagia kabisa baraka,’ akasema Yehova karne nyingi zilizopita. (Malaki 3:10, NW) Wakati wa mwaka wa utumishi wa 1984, wastani wa ulimwenguni pote wa mapainia ulikuwa 258,936. Na lo, Yehova amewabariki kama nini wahudumu hao wa wakati wote!
Kwa mfano, fikiria baraka zilizofurahiwa na mapainia katika jimbo la Amazon huko Brazili. Kwa ujumla, mashua zinatumiwa kufika kwenye vijiji vilivyotawanyika sana kando kando ya mto. Makao ya watu fulani yako kwenye kingo za mto, na nyumba zao za mbao zimejengwa kwa kuinuliwa na maboriti ili ziwe juu ya maji wakati wa majira ya mafuriko. Nyumba hizo zimeunganishwa na njia zilizotengenezwa kwa miti isiyonyooka vizuri, ambayo nyakati nyingine ni hatari sana, hasa kwa watu wazito-wazito. Maji yanapokuwa yamepungua, ni vigumu kufikia nyumba hizo lakini inawezekana kwa kupita katika mimea iliyo huko chini au kando kando ya ukingo wa mto wenye matope. Kusafiri kwa mitumbwi myepesi kunaweza kuwa jambo la kujasiria sana, kwa maana nyakati nyingine inapinduka. Zaidi ya mambo hayo, kuna matatizo yanayoletwa na maleria, homa ya matumbo, minyoo, joto kali sana, na kuvamiwa na wadudu. Lakini, kujapokuwa na magumu hayo roho ya Yehova inasaidia ndugu zetu wafanikiwe kuzitangaza habari njema katika maeneo ya namna hiyo.—Zekaria 4:6.
Dada mmoja painia anayetumikia katika jimbo la Amazon alisema hivi: “Kazi yetu ilikuwa ya kuridhisha sana.” Akitaja jambo zuri lililoonwa, alieleza juu ya ziara ya kurudia mwanamume fulani aliyekuwa amekubali baadhi ya vitabu vyetu. Dada huyo alilazimika kusafiri muda wa saa mbili kwa mashua, lakini alipofika akamkuta mwanamume huyo akikaanga unga wa muhogo katika joko kubwa. Kama mwanamume huyo angekatiza kazi yake kungekuwa na hatari ya kuunguza unga huo. Basi dada angeweza kufanya nini? Dada huyo painia akamwomba mwenzake aendelee kukoroga-koroga unga huo kwa ule mwiko mkubwa. Hivyo mwanamume huyo akapata nafasi ya kusikiliza kwa makini huku painia akimwonyesha namna ya kujifunza kichapo alichokuwa amejipatia.
Mara nyingi sana, ndugu zetu wanaofanya kazi katika jimbo hilo wanaamka kabla ya mapambazuko ili wafikie nyumba za watu kungali asubuhi. Ndipo mapainia wanapoendelea kutoa ushuhuda mchana kutwa. Naye Yehova anawabariki sana!—Mithali 10:22.
Mahali penginepo, pia, katika Brazili mapainia wanafurahia baraka nyingi katika utumishi wa Yehova. Kwa mfano, wazia furaha ya painia mmoja aliyeweza kusaidia mfungwa mmoja ajifunze ukweli. Mwanamume huyo, ambaye wakati mmoja aliogopwa kwa sababu ya hasira yake yenye kutokeza jeuri, alikuwa akitumikia kifungo cha muda mrefu gerezani. Lakini, alipousadiki ukweli utu wake uligeuzwa sana hata wakuu wa gereza wakavutiwa kisha wakampa ruhusa ya kuhubiri humo gerezani. Mwanamume huyo ambaye sasa amebatizwa amepewa kifungo cha nje na anaongoza mafunzo kadha ya nyumbani ya Biblia.
Painia huyo ameweza pia kusaidia wengine katika gereza ilo hilo. Kuhusu kazi hiyo anaeleza hivi: “Ni sababu ya kunipa furaha nyingi sana, kwa sababu mbegu niliyoweza kupanda imekwisha kuchipuka na kuzaa matunda.” Sasa wanaume wasiopungua wanne ambao wamefunguliwa gerezani wanahudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. Wengine wanne wanauchukua ukweli kwa uzito, na mmoja wao anajitayarishia ubatizo.
Eneo Ni Kubwa
Ongezeko linaloendelea kutokea katika hesabu ya waabudu wa Yehova ni ushuhuda wa wazi kwamba bado Mungu ana watu wengi wa kukusanya katika eneo la ulimwenguni pote. (Linganisha Matendo 18:9, 10.) Je! wewe unaweza kuwa na ushiriki mkubwa zaidi katika kazi hii ya kufanya wanafunzi?
Ikiwa wewe hujaanza kupainia, mbona usiongee na wale wanaopata mafanikio katika utumishi wa wakati wote? Wewe, pia, unaweza kufanikiwa ukiwa painia. Baada ya kuchunguza hali zako katika sala, huenda ukaweza kupanua eneo lako ukiwa painia.
[Picha katika ukurasa wa 22]
Mapainia katika jimbo la Amazon wanatumia njia iliyo ya kawaida Zaidi ya kusafiri katika mitumbwi na mashua kubwa zinzoendeshwa kwa kupiga makasia