Amani na Usalama Kutoka Chanzo Gani?
INGAWA Umoja wa Mataifa umefanya utumishi wenye mafaa katika pande fulani, mtu ye yote anayejua sana habari atalazimika kukubali kwamba kufikia sasa huo umeshindwa kuleta amani na usalama. Jambo hilo linakubaliwa wazi na wale wanaolitetea kwa bidii zaidi tengenezo hilo.
Hivyo, huko nyuma mwaka 1953, miaka minane tu baada ya kuzaliwa kwalo, Dag Hammarskjöld, aliyekuwa Katibu-Mkuu wakati huo, alikiri hivi: “Ingawa watangulizi wetu walikuwa wakiwazia-wazia mawazo ya mbingu mpya, tumaini letu lililo kubwa zaidi ni kwamba sisi turuhusiwe kuiokoa dunia hii ya kale.” Miaka 26 baadaye, C. William Maynes, msaidizi wa katibu wa serikali, alilazimika kukiri hivi: “Lile kusudi kuu la Baraza la Usalama na Baraza Kuu lilikuwa kudumisha amani na usalama wa kimataifa. . . . Kuna ushuhuda wa kwamba tengenezo hilo limeshindwa kutimiza kusudi lake lililo kuu.”
Unafaa Cho Chote?
Ukweli ni kwamba, kwa kiasi kikubwa mengi ya maamuzi yaliyo ya maana zaidi kuhusiana na amani na usalama muda wa miaka 40 iliyopita yamefanywa nje ya Umoja wa Mataifa. Mwaka 1982, Katibu Mkuu Javier Perez de Cuellar alisikitishwa na uhakika wa kwamba “mwaka huu, tumeona Tengenezo hili likisukumizwa kando au likijibiwa vikali tena na tena, kwa sababu hii au hii, katika hali ambazo lingalipaswa, na lingaliweza, kuwa limetimiza jambo la maana na lenye kujenga.” Sababu ni nini?
Wengine wanasema sababu ya mambo kuwa hivyo ni ongezeko kubwa sana la mataifa yaliyo washirika wa tengenezo hilo. Hesabu ya washirika 51 wa kwanza imeongezeka ikawa zaidi ya 150, na kila moja la mataifa hayo lina kura yenye nguvu zinazolingana katika lile Baraza Kuu. Hata hivyo mengine ya mataifa hayo ni madogo sana. Hivyo, taifa la visiwa Mtakatifu Christopher na Nevis, ambalo ndilo taifa la 158 kujiunga na tengenezo hilo, lina idadi ya watu wanaopungua 50,000, na hata hivyo lina kura yenye nguvu zinazolingana na za taifa la China, ambalo lina idadi ya watu wanaokaribia kuwa bilioni moja. Ni kweli kwamba mpango huo unayapa mataifa yale madogo nafasi ya kusikiwa; lakini hausaidii sana kufanya mataifa yale makubwa zaidi yawe na moyo wa kuyachukua kwa uzito maamuzi ya tengenezo hilo.
Tatizo la pili linagusiwa na Shirley Hazzard: “Mamlaka ya kulazimisha haikukabidhiwa kwa Tengenezo la Umoja wa Mataifa, bali wenye mamlaka hiyo ni washiriki wale wale ambao ndio wanaoelekea zaidi kuhitaji kulazimishwa.” Ndiyo kusema, tengenezo hilo linaweza kufanya maamuzi, lakini kwa sehemu kubwa haliwezi kuyatekeleza. Matatizo mazito ya ulimwengu yanazungumzwa kirefu kwa ukawaida. Maazimio yanapitishwa rasmi—halafu yanasahauliwa. Mwaka 1982, katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa alisikitishwa sana na “ukosefu wa kuheshimiwa kwa maamuzi yalo na wale ambao yamefanywa kwa ajili yao.”
Hayo ni matatizo ya kitengenezo—na kuna mengine yanayotajwa na wachanganuzi. Lakini kuna sababu nyingine za ndani na nzito zaidi zilizofanya Umoja wa Mataifa ushindwe.
Yale Matatizo Yenye Kina Kirefu
“Wakati huo lilielekea kuwa jambo linalowezekana kuthibitisha, kwanza kabisa, mfumo wa kudumishia amani na usalama wa mataifa yote chini ya maandalizi ya Mkataba wake,” akasema Javier Perez de Cuellar, akikumbuka wazo lile walilokuwa nalo waanzilishi wa tengenezo hilo. “Njozi hiyo tukufu imepatwa na nini? Baada ya muda mfupi ilizimishwa na tofauti zilizo kati ya yale Mataifa makubwa zaidi. . . . Tena, ulimwengu ukawa mahali penye kutatanisha zaidi, penye machafuko kuliko vile ilivyokuwa imetumainiwa itakuwa.”
Kwa kweli, hakukuwa kamwe na uwezekano wa kwamba Umoja wa Mataifa ungeleta amani na usalama. Jukumu la kufanya hivyo lilikuwa gumu mno. Maelezo ya katibu mkuu huyo yanatukumbusha maneno ya nabii Yeremia: “Kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Wanadamu, wakiwa na hekima na uwezo wao wa kadiri tu, hawataweza kamwe kutatua tatizo la kuletea watu wote amani na usalama.
Katibu mkuu huyo alisema waanzilishi wa Umoja wa Mataifa walikuta kwamba ulimwengu ni ‘wenye kutatanisha zaidi’ ya vile walivyokuwa wametumainia. Kuna sababu kubwa ya hali kuwa hivyo, na ni wazi hawakuijua. Lakini mtume Yohana anaieleza kwa njia hii: “Ulimwengu mzima uko katika uwezo wa yule mwovu.” (1 Yohana 5:19, NW) Biblia inatuambia kwamba leo “yule mwovu,” Shetani, anasababisha “ole wa nchi,” akiwa “mwenye ghadhabu nyingi.” (Ufunuo 12:12) Uhakika wenye kuhuzunisha wa kwamba kuna Shetani na mavutano yake ulikuwa umekwisha kuziangamiza jitihada za Umoja wa Mataifa za kuleta amani kabla hata hazijaanzwa.
Kumbuka, pia, kwamba tengenezo la Umoja wa Mataifa ni mtoto wa ulimwengu huu na hivyo limerithi tabia zao. Hali mbalimbali za udhaifu, maovu, na ukosefu wa adili ulio katika taifa moja moja pasipo kuepukika zimo pia katika Umoja wa Mataifa. Alexander Solzhenitsyn alitajwa kuwa akisema hivi mwaka 1972: “Robo karne iliyopita, Tengenezo la Umoja wa Mataifa lilizaliwa huku wanadamu wote wakiwa na matumaini makubwa. Lakini kwa huzuni, kwa sababu ya kuwa katika ulimwengu mfisadi, hata huo ukawa mfisadi.” Biblia inaonya hivi: “Hapana amani kwa wabaya, asema [Yehova].” (Isaya 48:22) Tengenezo ‘lenye ufisadi’ haliwezi kamwe kuleta amani na usalama.
Namna Gani Amani na Usalama?
Kwa hiyo, je! kutangazwa kwa mwaka 1986 kuwa “Mwaka wa Amani ya Kimataifa” kutafanyiza tofauti yo yote? Inaelekea sana kwamba haitakuwa hivyo, kwa maana matatizo yaliyotangulia kutajwa hayawezi kabisa kutatuliwa na wanadamu. Huo “Mwaka wa Amani” utaelekea kushindwa kuleta wanadamu karibu zaidi na amani na usalama sawasawa tu na vile ule “Mwaka wa Watoto” wa 1979 ulivyoshindwa kufanya hali ya watoto wa mataifa yote iwe nafuu, au sawasawa na vile “Mwaka wa Wanawake wa Kimataifa” wa 1975 ulivyoshindwa kuufanya ulimwengu uwe mahali pazuri zaidi pa wanawake kuishi.
Lakini, ni wazi kwamba mtu fulani anapaswa kuchukua hatua ya kuleta amani na usalama ndipo wanadamu waweze kuendelea kuwa hai. Leo, mataifa yaliyo na silaha za nyukilia yana uwezo wa kuangamiza sehemu kubwa ya viumbe vilivyo hai duniani. Silaha za ufundi mwingi zinazotumiwa kote kote zinaua watu wengi sana kila mwaka. Sasa amani ya kweli inaelekea kuwa imesonga mbali zaidi ya wakati mwinginewo! Ikiwa Umoja wa Mataifa umeshindwa kutatua matatizo hayo, anayeweza ni nani?
Matukio ya huko nyuma yanadokeza jibu lenye tumaini. Karibu miaka 3,000 iliyopita, Mfalme Daudi, aliyekuwa mfalme-shujaa wa kivita, aliandika habari za mtawala wa wakati ujao ambaye hakika angefaulu kuleta amani ya mataifa yote. Katika sala ya kuombea mtawala huyo, Daudi alisema: “Milima itawazalia watu amani, na vilima navyo kwa haki. Siku zake yeye, mtu mwenye haki atasitawi, na wingi wa amani hata mwezi utakapokoma.”—Zaburi 72:3, 7.
Ni mtawala gani ambaye angeweza kuleta amani hiyo ya kudumu? Daudi hakuwa akielekeza kwa tengenezo la kibinadamu, bali kwa Mungu wake, Yehova, kuwa ndiye ambaye jambo hilo lingetukia kwa mamlaka yake. Je! alikuwa akiwazia-wazia mambo yasiyowezekana? Hapana. Sulemani, mwana wa Daudi, alimtegemea Mungu uyo huyo, na wakati wa utawala wake Yehova alionyesha uwezo Wake kwa njia yenye kufananisha ya baadaye, akauletea amani Ufalme wa Sulemani, uliokuwa katika moja la majimbo yenye kupiganwa vita nyingi zaidi duniani. Sulemani hakuwa mfalme-shujaa wa kivita, hata hivyo wakati wa utawala wake, ‘Yuda na Israeli walikaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, tokea Dani [upande wa kaskazini] mpaka Beersheba [upande wa kusini], siku zote za Sulemani.”—1 Wafalme 4:25.
Ni kweli kwamba amani hiyo haikudumu. Waisraeli waliangukia njia za ulimwengu usio na adili wakapoteza usalama waliokuwa wamepewa na Mungu. Hata hivyo, zaidi ya karne mbili baadaye, wakati Waashuri wakatili walipofanya shughuli ya kuleta amani kwa kutisha watu, nabii Isaya alitabiri kuja kwa Mfalme aliyekuwa amefananishwa na Sulemani. Aliandika hivi: “Jina lake ataitwa Mshauri wa Ajabu . . . Mwana-Mfalme wa Amani. Kwa wingi wa utawala huo wa mwana-mfalme na kwa amani hakutakuwako mwisho.”—Isaya 9:6, 7, NW.
Huyo “Mwana-Mfalme wa Amani” ni nani? Miaka zaidi ya 700 baada ya siku za Isaya, wakati mamlaka ya ulimwengu ya Roma ilipokuwa ikijaribu kutekeleza namna yake ya kuleta amani na usalama wa mataifa yote, Mfalme huyo alitokea katika nchi ya Daudi—Yudea—akiwa ndiye Yesu Kristo. Aliambia wananchi wenzake habari za Ufalme wa Mungu, ambao yeye angekuwa ndiye Mfalme wao. Ufalme huo ungekuwa wa kimbingu, hivyo uweze kutatua matatizo yaliyoletwa na mavutano ya Shetani na ukosefu ambao mwanadamu alizaliwa nao wa kutokuweza kujitawala mwenyewe. Kwa wazi wananchi wenzi wa Yesu waliupendelea utawala wa Kiroma kisha wakafanya Yesu auawe kisheria. Hata hivyo, kama vile historia inavyoshuhudia waziwazi, yeye alifufuliwa kwa wafu akapaa mbinguni, huku akingojea wakati wa Mungu ili aanze kutawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu.
Kwa kweli, utimizo wa unabii unatia alama siku zetu kuwa ndio wakati wa tukio kubwa hilo. Kuzaliwa kwa Ufalme wa Mungu mbinguni kisha kutupwa kwa Shetani duniani ndiko kulikotokeza “ghadhabu nyingi” ya Shetani na kumfanya alete “ole wa nchi.” (Ufunuo 12:7-12) Matokeo yamekuwa nini? Vita na taabu nyingine za kibinadamu, kama ilivyotabiriwa na Yesu mwenyewe. Dunia imekuwa mahali pa “huzuni kuu ya mataifa, wasijue njia ya kutokea.”—Luka 21:25, 26, NW; Mathayo 24:3-13.
Njia ya Mwanadamu au Njia ya Mungu?
Unabii mbalimbali wa Yesu, unaotufikia sisi tangu karibu miaka 2,000 iliyopita, umetoa maelezo sahihi juu ya hali za ulimwengu kuliko yale maneno ya kutazamia mema yaliyosemwa wakati wa kuzaliwa kwa Umoja wa Mataifa miaka 40 iliyopita. Kushindwa kwa tengenezo hilo kupata “njia ya kutokea” kunaongeza mkazo tu kwamba matabiri ya Biblia ni sahihi. Kwa kweli, kulingana na maneno ya Isaya, wale wale walio “wajumbe wa amani wanalia kwa uchungu” wakiwa wamevurugwa na kushindwa kwao.—Isaya 33:7.
Jambo hilo linakazia sababu ya mwisho inayofanya Umoja wa Mataifa usiweze kamwe kuleta amani duniani. Huo unajaribu kuileta kwa njia inayopingana kabisa na njia ya Mungu. Kulingana na makusudi ya Yehova ambayo amesema, amani haitakuja kwa kuyaunganisha mataifa ya ulimwengu huu, bali ni kwa kuyaondoa kabisa kisha badala ya hayo Ufalme wa Mungu uwepo. (Danieli 2:44) Dag Hammarskjöld alisema alikuwa akijitahidi “kuiokoa dunia hii ya kale.” Ikiwa kwa kusema hivyo alimaanisha mfumo wa ulimwengu uliofanyizwa kwa mataifa ya kisiasa yanayojitegemea, basi matumaini yake yangekosa kutimia tangu hapo hapo mwanzoni. Ukweli ni kwamba, “dunia hii ya kale” lazima iondokee mfumo mpya. “Ulimwengu unapita.” (1 Yohana 2:17, NW) Hakuna cha kuuokoa, hata tengenezo la Umoja wa Mataifa haliwezi.
Kwa kuwa mataifa yana uchoyo wa uzalendo, kuna njia moja tu halisi ya kuletea amani na usalama. Ufalme wa Mungu tu ndio unaoweza kuleta amani ya namna ambayo mwanadamu ametamani sana tangu alipofukuzwa katika bustani ya Edeni. Hili ni moja la maelezo ya usalama utakaoletwa na utendaji wa Ufalme huo: “[Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:4.
Je! ahadi hiyo inasikika kuwa isiyoweza kutimia? Kusema ukweli, hilo tu ndilo tumaini letu, na toleo linalofuata la Mnara wa Mlinzi litaizungumza sababu kwa urefu zaidi. Kwa sasa, tungependa kuvuta fikira zako kwenye jambo la maana: Kwamba historia ya Umoja wa Mataifa haijamalizika bado. Tengenezo hilo litashiriki sehemu ya maana katika matukio ya wakati ujao. Tunakutia moyo usome makala mbili zinazofuata. Zinazouzungumza wakati ujao wa tengenezo la Umoja wa Mataifa kupatana na unabii wa Biblia.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Jukumu la kuleta Amani ni gumu mno kwa Umoja wa Mataifa
[Hisani]
U.S. Army photo
[Picha katika ukurasa wa 6]
“Ulimwengu mzima uko katika uwezo wa yule mwovu.” Hiyo ni kutia ndani Umoja wa Mataifa
[Picha katika ukurasa wa 7]
Umoja wa Mataifa hautafuata maadili kamwe, sawa tu na vile taifa moja moja yenye kuufanyiza yasivyofuata maadili