Amani na Usalama Ndilo Tumaini
“Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilitangaza bila kura yo yote ya kupinga mwaka 1986 kuwa Mwaka wa Amani ya Kimataifa. Mwaka huo utatangazwa rasmi tarehe 24 Oktoba 1985, hiyo ikiwa ndiyo sikukuu ya 40 tangu Umoja wa Mataifa uanzishwe.”
WEWE unayaonaje maneno hayo rasmi yaliyosemwa na tengenezo la Umoja wa Mataifa? Je! yanakufanya ujisikie ukiwa na uhakika zaidi juu ya wakati ujao? Watu wengi wangesema kwamba inafaa kujaribia jambo lo lote linaloahidi watu hata uwezekano ulio mdogo kabisa wa kuleta amani. Basi kuna ubaya gani wa kujaribia “Mwaka wa Amani ya Kimataifa”?
Hakika, “Mwaka wa Amani” ulio namna hiyo ungepatana na miradi ya waanzilishi wa tengenezo la Umoja wa Mataifa. Huko nyuma mwaka 1944, rais wa United States alitamka hivi: “Sisi tumekaza nia . . . ili tuyatengeneze mataifa yanayopenda amani kwa njia ambayo kupitia umoja wa tamaa, umoja wa nia, na umoja wa nguvu yatakuwa katika hali ya kuweza kuhakikisha kwamba hakuna mchokozi wala mshindaji mwingine atapata hata nafasi yenyewe tu ya kujitokeza. Ndiyo sababu tangu pale pale mwanzoni mwa vita, na katika wakati ule ule tunapoendesha mipango yetu ya kijeshi, tumeanza kuweka misingi ya kuwa na tengenezo kuu la kudumisha amani na usalama.”
Watu wengi walikuwa na mawazo hayo. “Ili Umoja wa Mataifa uje kutokea, kulihitajiwa kabisa kuwe na baraza kubwa la watu wenye kuamini mwanadamu ana uwezo wa kufanya mema, na kujisikia kwamba matumaini yao yanaweza kuonyeshwa kuwa yanafaa,” kinasema kitabu Defeat of an Ideal cha Shirley Hazzard, ambaye alifanya kazi kwa muda wa miaka kumi akiwa mmoja wa makarani wa Umoja wa Mataifa.
Mkataba wa kuanzishwa kwa Tengenezo hilo lililokuwa limezaliwa karibuni ulitaja matumaini ya waanzilishi walo: “Makusudi ya Umoja wa Mataifa ni: 1. Kudumisha amani na usalama wa mataifa yote . . . 2. Kusitawisha mahusiano ya kirafiki kati ya mataifa kwa kuheshimu kanuni ya haki zenye usawa na kwa mataifa kujifanyia maamuzi yao . . . 3. Kufikia ushirikiano wa mataifa yote katika kutatua matatizo ya mataifa yote . . . ” Je! ingeweza kuwa miradi hiyo ina kasoro fulani?
Kusema kweli, Umoja wa Mataifa ulianza kwa njia ya kuvutia. Masuala mazito-mazito ya ulimwengu yalizungumzwa. Mwaka 1948, Tangazo la Ulimwengu Mzima Juu ya Haki za Kibinadamu lilipitishwa. Kazi yenye mafaa ya kutendea wanadamu mambo ya fadhili ilianzishwa ili kupunguza umaskini, njaa, magonjwa, na tatizo la wakimbizi. Viwango vya mataifa yote viliwekwa, kwa mfano viwango vya kuhakikisha usalama wa meli na ndege, vyeti vya afya kwa ajili ya wenye kusafiri kwenye majimbo fulani, bei zinazolingana za kusafirisha bidhaa kwa njia ya posta, na kugawana haki za hewani za mawasiliano ya matangazo ya redio.
Umoja wa Mataifa ulihusika sana katika jitihada za kufanya amani katika lile pigano la miaka 1947-49 kati ya India na Pakistan. Hata ulitumia nguvu za kijeshi wakati askari wenye kuongozwa na bendera ya shirika hilo walipoingia Korea mwaka 1950 na Kongo (ambayo sasa ni Zaire) mwaka 1960. Kungali kuna vikosi vya kutunza amani vya Umoja wa Mataifa katika Saiprasi na Mashariki ya Kati. Ndiyo, katika muda wa miaka 40 iliyopita Umoja wa Mataifa umejithibitisha. Nchi zaidi ya 150 zimeonyesha kwamba zinatambua hivyo kwa kupeleka wajumbe kwenye makao makuu yake maarufu katika Mji wa New York, kwenye kingo za Mto East.
Lakini ni kwa kadiri gani Umoja wa Mataifa umetimiza agizo lake la msingi la ‘kudumisha amani na usalama wa mataifa yote’? Na ule “Mwaka wa Amani ya Kimataifa” uliotangazwa utakuwa na matokeo gani?