Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 10/15 kur. 4-7
  • Amani na Usalama—Kupitia Ufalme wa Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Amani na Usalama—Kupitia Ufalme wa Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kinachohitajiwa Ni Zaidi ya Hekima ya Kibinadamu
  • Kuwaondoa Adui Wenye Nguvu Zinazozidi za Kibinadamu
  • “Mtoto” wa Mungu
  • Kuileta Ile “Dunia Mpya “
  • ‘Kufua Panga Ziwe Majembe’
  • Amani na Usalama Kutoka Chanzo Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Amani na Usalama wa Kweli Ni Karibu!
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Amani Ile ya Uhalisi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Amani Duniani—Itapatikanaje?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 10/15 kur. 4-7

Amani na Usalama​—Kupitia Ufalme wa Mungu

“MAKUSUDI ya Umoja wa Mataifa ni haya: 1. Kudumisha amani na usalama wa mataifa yote.”​—Charter of the United Nations.

Hili ni wazo lenye kusifika. Lakini kama vile tumeona, matokeo ya miaka 40 iliyopita yanaonyesha wazi kwamba Umoja wa Mataifa haukufaulu “kudumisha amani na usalama wa mataifa yote.” Wala hautafanyiza tofauti yo yote kwa kuutangaza mwaka 1986 kuwa “Mwaka wa Amani ya Kimataifa.”a

Kuna njia moja tu ambayo kupitia hiyo amani na usalama wenye kudumu italetwa penye dunia hii​—hiyo ni Ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Yesu Kristo. Hiyo ndiyo serikali ile halisi mbinguni ambayo Yesu alifundisha wafuasi wake kusali wapewe. (Mathayo 6:9, 10) Lakini ni kwa sababu gani hiyo itaweza na hali Umoja wa Mataifa umeshindwa? Jibu rahisi ni kwamba: Ufalme wa Mungu utaweza kwa sababu zile zile ambazo zimefanya Umoja wa Mataifa usiweze.

Kinachohitajiwa Ni Zaidi ya Hekima ya Kibinadamu

Katika toleo letu lililotangulia, tuliona kwamba sababu moja ya kuwa Umoja wa Mataifa ulilaaniwa kushindwa hata ufanyeje ni kwamba Mungu hakumpa mwanadamu hekima au haki ya kujisimamia mwenyewe. (Yeremia 10:23) Hivyo, hakuna tengenezo la kibinadamu, hata liwe na makusudi mazuri namna gani, linaloweza kuleta amani na usalama.

Tofauti na hivyo, Yesu Kristo, Mfalme aliyewekwa wa Ufalme wa Mungu, ameonyesha sikuzote hekima inayozidi ile ya kibinadamu. (Mathayo 13:54) Mfano mmoja bora ni Mahubiri ya Mlimani yake yanayojulikana sana. (Mathayo, sura 5 mpaka 7) Katika hayo alieleza jinsi ya kupata furaha ya kweli, jinsi ya kutuliza magombano, jinsi ya kuepuka ngono zisizo za adili, na jinsi ya kuwa na wakati salama ujao. Je! si jambo la akili nzuri kutazamiwa kwamba mtawala mwenye hekima nyingi hivyo na mwenye kuifahamu hali ya kibinadamu angejua jinsi ya kuleta amani na usalama?

Zaidi ya hilo, utambuzi mwingi wa Yesu uliongezwa na uwezo wake wa kimuujiza wa kuona ndani ya mioyo ya wanadamu na kujua ni kusudi gani hasa linalowafanya watende mambo na pia mawazo yao ya kindani. (Mathayo 9:4; Marko 2:8) Fikiria maana ya jambo hilo: Pingamizi moja kubwa linalozuia amani na usalama leo ni kutokuaminiana. Kwa sababu ya kutokujua kila mmoja ana fikira na makusudi gani, mara nyingi wanadamu na mataifa wanakuwa wasioaminiana. Kutokuaminiana huko kunakuwa kizuizi cha amani. Lakini hilo si tatizo kwa mtawala yule anayeweza “kusoma mioyo ya wanadamu.”​—Yohana 2:25, tafsiri ya Biblia ya Knox.

Kuwaondoa Adui Wenye Nguvu Zinazozidi za Kibinadamu

Sababu kubwa nyingine iliyofanya jitihada za Umoja wa Mataifa za kuleta amani kuwa zililaaniwa kushindwa tu ni yale mavutano ya “mtawala wa ulimwengu huu,” Shetani Ibilisi. (Yohana 12:31, NW) Yeye na magenge yake ya kishetani wanajua kwamba wana ‘kipindi kifupi tu cha wakati’ kabla hawajaondolewa. Wakiwa wameazimia wafanyize “ole kwa dunia,” wamezuia amani kwa kugawanya wanadamu kisiasa na kitaifa.​—Ufunuo 12:9-12, NW.

Ni nani angeweza kuondoa wachochezi hao wa vita walio na nguvu zinazozidi za kibinadamu? Biblia inajibu kwamba ni Yesu Kristo, yule anayetajwa kuwa Mikaeli, ambaye, akiwa pamoja na malaika zake, aliwatupa Shetani na mashetani wake nje ya mbingu. Hivyo tunasoma: “Kisha nikaona malaika [Yesu] akishuka kutoka mbinguni, mwenye ufunguo wa [Hadesi], na mnyororo mkubwa mkononi mwake. Akamshika yule joka, yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani . . . akamtupa katika [Hadesi], akamfunga, akatia muhuri juu yake.” (Ufunuo 20:1-3) Kwa hiyo Shetani ataondoshwa. Hapo tu ndipo itakapowezekana kufurahia uzima katika amani na usalama wa kweli.

“Mtoto” wa Mungu

Toleo letu lililotangulia lilitaja sababu ya tatu inayofanya Umoja wa Mataifa usiweze kamwe kuleta amani na usalama: Huo ni mtoto wa ulimwengu huu na ukiwa hivyo unarithi udhaifu mbalimbali, maovu, na ufisadi unaoonyesha jinsi zilivyo tabia za mataifa yaliyo wanachama wake.

Tofauti yenye kuburudisha ni kwamba Ufalme utakaoleta amani na usalama unafananishwa katika Ufunuo 12:5 kuwa “mtoto” wa Mungu. Mtawala mwenye kuuongoza anaonyesha tabia za Mungu. Angalia nyingine za sifa za kuvutia zinazodhihirishwa na Yesu Kristo, mtawala wake: upendo wa kujinyima (Yohana 15:12, 13); uchangamfu na kujisikia (Mathayo 9:10-13; Luka 7:36-48); unyenyekevu (Yohana 13:3-5, 12-17); huruma (Marko 6:30-34); kusikitikia watu (Waebrania 2:17, 18; 4:15); imara ya kushikilia uadilifu (Isaya 11:4, 5). Je! wewe hungefurahia kujinyenyekeza chini ya Mtawala wa namna hiyo?

Kuileta Ile “Dunia Mpya “

Sababu ya mwisho inayofanya Umoja wa Mataifa usiweze kamwe kuleta amani ilionyeshwa na maneno ya Dag Hammarskjold aliyekuwa Katibu Mkuu, ambaye huko nyuma mwaka 1953 alisema: “Tumaini letu lililo kubwa zaidi ni kwamba sisi turuhusiwe kuiokoa dunia hii ya kale.” Ikiwa alikuwa akifikiria kudumisha mfumo wa mambo ya sasa wa ulimwenguni pote, basi jitihada hizo za kuiokoa “dunia hii ya kale” ni lazima zitashindwa tu. Kwa sababu gani?

Kwanza, sehemu ya “dunia hii ya kale” ni serikali za kibinadamu. Serikali moja moja zinaendeleza utukuzo wa taifa, ambao unagawanya wanadamu; utukuzo wa taifa unakazia faida za taifa moja badala ya kutafuta masilahi ya ujumla ya mataifa yote. Kupendezwa hivyo na mambo ya kibinafsi kunabomoa jitihada zo zote za Umoja wa Mataifa za kuleta amani. Ni kama vile makala ya mhariri katika gazeti The Guardian la Uingereza ilivyosema: “Kwa kuwa hakuna lo lote la mataifa yaliyo wanachama lililo tayari kujinyima faida zalo lenyewe kwa faida ya wote, mataraja ya kubadili mambo yawe mazuri ni madogo sana. Kazi moja tu iliyo halisi ya Baraza [Kuu la Umoja wa Mataifa] ni kutumikia likiwa kiwango cha kupimia maoni ya watu duniani pote. Ajenda zalo zimejaa masuala ambayo yamefanyiwa majadiliano muda wa miaka mingi bila ya maendeleo yo yote makubwa ya kuelekea kwenye utatuzi.”

Lakini kuna sababu nyingine yenye mkazo zaidi juu ya kinachofanya jitihada za Umoja wa Mataifa za kuiokoa “dunia hii ya kale” ziwe za bure tu: Unapingana na makusudi ya Mungu. Jinsi gani? Katika macho ya Mungu ile ‘dunia ya kale’ haiwezi kubadilishwa iwe nzuri. Wakati unakaribia ambapo kusudi la Mungu lililosemwa litatimizwa. Ni kama vile mtume Yohana alivyoeleza jambo hilo: “Nikaona mbingu mpya na dunia mpya; kwa maana mbingu za kwanza na dunia ya kwanza zimekwisha kupita.” (Ufunuo 21:1, ZSB) Katika kuondoa serikali za kibinadamu, Ufalme wa Mungu utaondolea mbali utukuzo wa taifa wenye kuleta migawanyiko. Badala ya huo “dunia mpya,” yaani, jamii ya kibinadamu yenye maelekeo ya uadilifu, itasitawi chini ya serikali moja ya kimbingu, Ufalme wa Mungu. Ni hapo tu ndipo wanadamu watakapoweza kufurahia amani na usalama wa kweli ulimwenguni pote.

‘Kufua Panga Ziwe Majembe’

Kwamba hilo ni tumaini linalostahili kuwa nalo inahakikishwa na maneno ya unabii wa Biblia yaliyoandikwa kwenye ukuta mmoja unaoelekeana na Umoja wa Mataifa. Hapo unasema: “Watafua panga zao ziwe majembe. Na mikuki yao iwe miundu: taifa halitainua upanga juu ya taifa jingine. Wala hawatajifunza vita tena kamwe.”​—Maneno hayo yamenakiliwa kutoka Isaya 2:4.

Hapana, Umoja wa Mataifa haukuweza kuzuia mataifa ‘yasiinuliane upanga.’ Hata hivyo, kuna watu wanaotoa ushuhuda ulio hai kwamba ‘wamefua panga zao zikawa majembe.’ Wameonyesha umoja unaovipita vizuizi vya kikabila na kitaifa. Hata wapatwe na mkazo wa namna gani, Wakristo hao wasiokuwamo hawawezi ‘kuinua upanga’ juu ya mwanadamu mwenzao. Wao ni akina nani? Ni Mashahidi wa Yehova.

Mfano wa namna wao wanavyotenda wanapokazwa washiriki katika vita vya mataifa ni jambo lililopata Shahidi mmoja katika nchi moja ya Kiafrika yenye matendo mengi ya uvamizi wa kisiasa.

Ili kuongeza watu wapya katika jeshi lao la uvamizi, kikundi kimoja cha wavamizi katika nchi hiyo kinatorosha wanaume kisha kinawatolea uchaguzi: Watumikie katika jeshi la wavamizi au wapigwe risasi. Siku moja walitorosha mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Viongozi wa watu hao, waliokuwa wamekuwa wakinywa pombe, wakamwambia achague analotaka. Waliweka chupa mbili za pombe, wakaelekeza kidole kwenye moja ya chupa hizo na kusema kwamba inasimamia serikali, ile nyingine inasimamia kikundi chao cha uvamizi. ‘Wewe uko upande wa chupa ipi?’ wakamuuliza. Shahidi akafikiri kidogo, kisha alipoona chupa nyingine za pombe karibu, akachukua moja na kuiweka katikati ya zile mbili, akisema: ‘Hapa ndipo nilipo.’ Akaongezea: ‘Mimi ni mtu asiyekuwamo, kwa kuwa niko upande wa Ufalme wa Mungu.’ Baada ya hapo, akapigwa mara kadha. Halafu akalazimishwa kufanya kazi ya kiutumwa katika kambi ya wavamizi, asijue kama wangempiga risasi au hapana. Baada ya miezi minane, alitoroka wakati vikosi vya serikali viliposhambulia kambi hiyo.

Mashahidi wa Yehova wamekubali kufungwa gerezani, hata kupatwa na kifo, badala ya kushiriki katika vita vya mataifa. Hivyo, katika Ujeremani ya Nazi maelfu yao waliingizwa katika kambi za mateso kwa sababu walikataa kuunga mkono utawala wa Nazi wenye kutumia maogofyo. Mamia ya Mashahidi waliuawa au wakafa katika kambi za mateso. Hata hivyo, kwa kuwa sasa serikali katili sana ya Nazi imekwisha kumalizika zamani, Mashahidi wa Yehova ni tele katika Ujeremani na pande zote za dunia.

Lakini ni kwa sababu gani wao wanaweza ‘kufua panga ziwe majembe’? Jibu linaweza kupatikana katika utangulizi wa Katiba ya shirika la UNESCO, inayosema: “Kwa kuwa vita vinaanza katika akili za wanadamu, kinga za amani zinapasa kujengwa katika akili za wanadamu.”

Kupatana na jambo hilo, kwa habari ya wale ‘wanaofua panga ziwe majembe,’ unabii wa Isaya unasema, “wala hawatajifunza vita tena kamwe.” Kwa kujifunza Maandiko na kuyatumia katika maisha yao, ‘wanajifunza njia zake na kwenda katika mapito yake.’ (Isaya 2:3, 4) Kwa msaada wa roho takatifu, ‘wanafanya upya nia zao,’ nao wanakuwa wenye kuamanika.​—Warumi 12:2, 18.

Ushuhuda ulio wazi kwamba Mashahidi wa Yehova ‘wamefua panga zao zikawa majembe’ unahakikisha kwamba inawezekana kuishi katika amani na usalama. Njia ya maisha wanayofuata sasa inaonyesha kwa kadiri ndogo yale ambayo Ufalme wa Mungu kupitia Kristo utatimiza duniani pote karibuni.

Je! taraja hilo linakuvutia wewe? Mashahidi wa Yehova watafurahia kukueleza ushuhuda unaoonyesha kwamba karibuni Ufalme wa Mungu utaleta amani na usalama wenye kudumu. Mbona usiende kuwaona hapo walipo katika eneo lenu au uandikie wachapishaji wa gazeti hili? Jifunze mengi zaidi juu ya jinsi unavyoweza ‘kufua panga ziwe majembe’ sasa, ukiwa na taraja la kufurahia hivi karibuni uzima katika ulimwengu mzima usio na vita.

[Maelezo ya Chini]

a Ili upate mazungumzo marefu zaidi juu ya sababu ambayo imefanya Umoja wa Mataifa ushindwe, tafadhali ona Mnara wa Mlinzi wa Oktoba 1, 1985.

[Sanduku katika ukurasa wa 5]

Sababu Zilizofanya Umoja wa Mataifa Ushindwe:

◻ Hekima ya kibinadamu ni kidogo mno (Yeremia 10:23)

◻ Mavutano ya Shetani yanaharibu jitihada zao (Ufunuo 12:12)

◻ Huo ni mtoto wa ulimwengu huu na unarithi udhaifu wake mbalimbali (1 Yohana 5:19)

◻ Huo unajaribu kuiokoa “dunia hii ya kale,” na hali jambo hilo linapinga makusudi ya Mungu (1 Yohana 2:17)

Sababu Zitakzofanya Ufalme wa Mungu Ushinde

◻ Mtawala wao ana hekima inayozidi ile ya kibinadamu na anaweza kusoma mioyo ya wanadamu (Yohana 2:25)

◻ Utawaondoa wachochezi wa kishetani wa vita (Ufunuo 20:1-3)

◻ Huo ni “mtoto” wa Mungu na mtawala wao anaonyesha sifa za Mungu (Ufunuo 12:5)

◻ Utasimamisha “dunia mpya” yenye uadilifu chini ya serikali moja tu ya kimbingu (Ufunuo 21:1)

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ufalme wa Mungu utasimamisha “dunia mpya,” jamii ya kibinadamu yenye uadilifu, ambayo itasitawi chini ya serikali moja ya kimbingu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki