Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Je! mabaki ya wapakwa mafuta wa Bwana walio duniani ni sehemu ya tengenezo la Yehova la kimbingu, lililo mfano wa mke, “Yerusalemu wa juu”?
Wapakwa mafuta walio duniani wanaweza kusemwa kuwa ndio sehemu inayoonekana ya tengenezo la Mungu, jamaa yake ya ulimwengu mzima ya viumbe wenye akili.
Wakiwa watu mmoja mmoja ‘wanaozaliwa mara ya pili,’ wanakuwa wana wa kiroho wa Yehova. (Yohana 3:3,5; Warumi 8:15-17) Yehova ndiye Baba yao. Hata hivyo wana “mama” pia, kwa maana mtume Paulo aliandika kwamba “Yerusalemu wa juu . . . ndiye mama yetu sisi.” Lazima huo uwe ni mtajo unaomaanisha tengenezo la kimbingu la roho washikamanifu ambao Yehova anawaona kuwa “mke” wa mfano. (Wagalatia 4:26) Wakristo wapakwa mafuta wanapopokea thawabu yao ya kimbingu, kwa kweli wanachukua mahali pao katika hilo tengenezo la kimbingu.—Ufunuo 4:4:14:1-5.
Bado mabaki wapakwa mafuta walio duniani hawajawa kwa uhalisi sehemu ya “Yerusalemu wa juu.” Lakini kwa sababu ya cheo chao kisicho na kifani cha kuwa wana wa kiroho wenye taraja la uzima wa kimbingu, na kwa sababu wao wanawakilisha “mke” wa kimbingu wa Mungu, nyakati nyingine Yehova kwa njia ya kuwagusia tu anawahusisha ndani maamrisho yanayotolewa, unabii mbalimbali, ahadi mbalimbali, na maneno ya faraja yanayoelekezwa kwa tengenezo lake lililo mfano wa mke katika mbingu.
Tunaweza kutoa mfano wa jambo hilo katika maneno yanayohusu Israeli wa kale. Kupitia Isaya, Yehova alieleza habari za mwanamke aliye katika minyororo, katika mavumbi, anayehitaji kuamka na kuangaza nuru. (Isaya 51:9, 14; 52:1,2; 60:1, NW) Hali hizo hazijawa kati ya wana wa Yehova wa kiroho walio washikamanifu ambao ndio wanaojumlika kuwa “mwanamke” wake wa kimbingu. Lakini, zilikuwa katika taifa la Israeli. Waisraeli walipofunguliwa kutoka utumwa wa Babuloni mwaka 537 K.W.K., waliamka, wakasimama kutoka mavumbini, kisha hata wao wakaanza kuangaza nuru ya Yehova waliyokuwa wameangaziwa naye. Yerusalemu uliojengwa upya (uliolisimamia taifa) ulikuwa kama mke aliyekuwa ameachwa lakini ambaye sasa alikuwa amedaiwa arudi na akawa akizaa watoto, Wayahudi waliokuwa katika taifa lililorudishwa. (Isaya 54:1-8, 60:1-22; 66:7-14, NW) Kwa hiyo maneno yaliyo katika Isaya juu ya hali ya “mwanamke” (ambaye ‘mwenyewe aliye mume’ wake alikuwa Yehova) yalitukia katika taifa la kidunia lenye kuwakilisha mwanamke huyo.
Sasa na tuondoe fikira huko zielekee kwenye taifa la kiroho ambalo Mungu angelikubali yeye (na “mwanamke” wake wa kimbingu) akiisha kuacha kutumia Israeli wa kimwili. (Wagalatia 6:16) Baada ya kuwa “tasa” kwa karne nyingi, “Yerusalemu wa juu” ulianza kuzaa wana wa kiroho. Yesu ndiye aliyekuwa wa kwanza kuzaliwa, mwaka 29 W.K., kisha akafuatwa na wengine 144,000, kuanza na mitume na kuja kufikia wakati wetu. (Wagalatia 4:21-31) Mwanzoni-mwanzoni mwa karne hii, kwa kipindi kifupi mabaki ya Waisraeli wa kiroho walijiacha washindwe na mikazo kisha wakaingia katika hali iliyo kama utumwa. Halafu, mwaka 1919, walitolewa katika utumwa wa Kibabuloni wakiwa kama taifa jipya lililozaliwa katika nchi ya kiroho. Hivyo, tunaweza kuona kwamba maneno ya Isaya ya kiunabii kuhusu Yerusalemu wa kale yana ulinganifu katika Israeli wa kiroho duniani.
Fikiria, pia, Ufunuo 12:1-17. Mwishoni mwa majira ya Mataifa mwaka 1914 W.K., “mwanamke” wa kimbingu wa Mungu aliizaa serikali ya Ufalme ikiwa “mtoto mwanamume.” Shetani aliyeshushwa “akamkasirikia yule mwanamke.” Lakini hakuelekeza shambulio lake moja kwa moja mbinguni kwenye tengenezo la Mungu lililo mfano wa mke, ambalo hakuwa tena na ruhusa ya kuliingia. Bali, Shetani alifanya vita na “wazao wake waliosalia” wanaowakilisha mwanamke huyo hapa duniani.
Hivyo, kama vile ilivyokuwa zamani kwa Israeli wa kidunia, ndivyo ilivyo kwa Israeli wa kiroho. Hali iliyo katika “Yerusalemu wa juu” inaonekana kwa jinsi mambo yalivyo kati ya watoto wake duniani. Katika maana ya kuhusika moja kwa moja, zile amri, masahihisho, faraja, na ahadi zinazoelekezwa kwa mwanamke wa kimbingu wa Yehova, zinawagusa hasa wale walio duniani wenye kuwakilisha mwanamke huyo, ambao wana taraja la kuwa sehemu ya tengenezo la kimbingu la Mungu.
■ Je! wale wa “Mkutano mkubwa” wanakuwa sehemu ya tengenezo la Yehova la ulimwengu mzima?
Sasa, kabla ya ile “dhiki kubwa,” Mashahidi wa Yehova wote wanamtumikia Mungu kwa furaha katika umoja. Hawawi na mgawanyiko kwa sababu ya jambo la kwamba hesabu ndogo ni wapakwa mafuta kwa roho na wanatazamia kwenda mbinguni, hali walio wengi wana tumaini la kupata uzima katika paradiso ya kidunia. Kama Yesu alivyoonyesha, wale “kondoo” na wale “kondoo wengine” wanaungana na kuwa “kundi moja.” (Yohana 10:11, 16) Hivyo, tengenezo la Yehova la watumishi lililopo sasa limejumlishwa kuwa hivyo na vikundi vyote viwili, vyenye matumaini mawili yaliyo mbalimbali.
Yehova alitangulia kuona kwamba mwanamke wake angefurahia ufanisi huo. Alionyesha kwamba watu wa kutoka mataifa yote, wale wasio Waisraeli wa kiroho, wangekusanywa kwa wingi. (Isaya 60:1-22; 61:5-9) Kitabu cha Ufunuo kinaeleza juu ya “mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha, wamesimama mbele ya kile kiti cha enzi, na mbele za Mwana-Kondoo.” Hao ni watu wenye matumaini ya kidunia, si wale wa lile taifa la kiroho la wapakwa mafuta ambao hasa ndio wanaowakilisha tengenezo la Yehova la ulimwengu mzima leo. Hata hivyo, ule “mkutano mkubwa” unasimama mbele ya kiti cha enzi cha Mungu na Mwana-Kondoo wakiwa na kanzu zilizofanywa nyeupe kwa kuoshwa ndani ya damu ya Mwana-Kondoo. Hata sasa wana msimamo mzuri kama nini!—Ufunuo 7:9-17.
Hawa wa “mkutano mkubwa” wanajaribiwa pia juu ya ukamilifu wao. Wakiendeleza uaminifu sasa mpaka mwisho wa Utawala wa Miaka Elfu na jaribu la mwisho, Yehova atawatangaza kuwa waadilifu wakiwa wanadamu waliokamilika, pamoja na wafufuliwa watakaokuwa sehemu ya “kondoo wengine” wa Yesu. Kwa ‘kuwekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu’ kwa njia hiyo, wataufurahia “uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.” (Warumi 8:21) Kama vile Adamu na Hawa walivyokuwa hapo mwanzo, wakati huo wao watakuwa sehemu inayoonekana ya tengenezo la Yehova la ulimwengu mzima. Watakuwa ndio wazao wakamilifu na wenye akili wa Yehova na tengenezo lake lililo katika mbingu ambalo ni mfano wa mke.