Je! Wewe Una Msimamo Unaofaa na Mungu?
HUENDA watu wengi wasione maana ya kuuliza hivyo. Kwa maoni yao, kujiona kwa mtu mwenyewe kuwa yuko sawa ndilo jambo la maana zaidi. ‘Fanya ujitakialo’ ni msemo unaotumiwa na watu wengi sana siku hizi. Msemo mwingine unasema ‘Usijione mwenye hatia.’
Hayo si maoni ya vijana wachache tu waliojawa na falsafa ya maisha ya ubinafsi. Kwa mfano, katika Ufaransa, ambako asilimia 82 ya idadi ya watu ni Wakatoliki waliobatizwa, uchunguzi uliofanywa mwaka 1983 ulifunua kwamba ni asilimia 4 tu ya watu wanaolikubali wazo la kwamba kuna dhambi. Kwa habari ya United States, miaka kadha iliyopita Dakt. Karl Menninger, anayesemwa kuwa “baba wa udaktari wa magonjwa ya akili katika Amerika,” alisukumwa na moyo kuandika kitabu kizima juu ya kichwa Whatever Became of Sin? Ndani yacho aliandika hivi: “Tukiwa taifa zima, tuliacha rasmi ‘kutenda dhambi’ karibu miaka ishirini iliyopita.” Jalada la kitabu hicho lilisema: “Neno ‘dhambi’ limekaribia kumalizika katika msamiati wa maneno tunayotumia.”
Kweli, wazo la kwamba kuna dhambi limefichika sana leo hivi kwamba watu wengi, hata wale wanaodai kuwa Wakristo, wangetatizika wakiambiwa waeleze dhambi ni nini hasa.
Mashaka ya Kisasa
Hata hivyo, ijapokuwa wazo la kwamba kuna dhambi limepungua, mambo kadha ambayo yametukia ulimwenguni hivi majuzi yamefanya watu waanze kufikiri. Jambo moja ni hesabu kubwa ya mimba zinazotolewa katika nchi nyingi zilizositawi zaidi ulimwenguni. Nyingine zazo, ingawa sana-sana ni “za Kikristo,” zina sheria zisizokataza sana utoaji mimba. Pupa hiyo ya kuua-ua vijusu imekuwa na matokeo fulani hivi kwamba watu wanaokataa wazo la kwamba kuna dhambi wanalazimika kuona ugumu wa kueleza.
Kwa mfano, ni kwa sababu gani wanawake ambao falsafa yao ya maisha inawaruhusu watoe mimba wanajisikia wakiwa wenye hatia baadaye, na hata wanapatwa na magonjwa yenye kusababishwa na wasiwasi wa akili? “Hata hivyo uchunguzi mwingi unaonyesha kiasi kikubwa cha wenye kutoa mimba kuwa wenye kasoro-kasoro,” hata katika nchi ya Yugoslavia iliyo ya Kikomunisti. (Kichapo The New Encyclopcedia Britannica) Profesa Henri Baruk, aliye mshiriki wa Chuo cha Kifaransa cha Mambo ya Tiba, anaeleza kituko hicho kuwa kinasababishwa na uvunjaji wa “kanuni fulani ya msingi iliyoandikwa katika moyo wa watu wote.” Ikaandikwa na nani?
Kituko kingine cha hivi majuzi ambacho kimefanya watu waanze kufikiri ni mweneo wa ulimwenguni pote wa magonjwa ambayo watu wanaambukizwa kwa kufanya ngono. AIDS (yaani EDSI, au ugonjwa unaomaliza nguvu za mwili za kujikinga na maradhi), ambao unaua watu wengi, umetokeza mashaka na huzuni kuu kati ya watu wengi wanaodhani ngono za ovyoovyo zimewapa uhuru wa vizuizi vya kizamani. Hasara kubwa inayowajia watu wengi kwa sababu ya “uhuru” wao wa kufanya ngono inafanya wengine wao wawaze kwamba labda wanaadhibiwa. Wanaadhibiwa na nani?
Vikumbusho hivyo vya kisasa vya kwamba mwanadamu hawezi kukosa kuadhibiwa akidharau kanuni za adili vinafanya watu wengi wenye kufikiri warudie kukadiria maoni yao juu ya dhambi na wajibu walio nao wa kumjibu Mungu kwa matendo yao.
Msimamo wa Makanisa Kuhusiana na Dhambi
“Dhambi ya karne hii ni upotevu wa hisia yote ya dhambi.” Papa Pius wa 12 alisema maneno hayo yenye mkazo huko nyuma sana mwaka 1946. Kwa wazi, hali ya mambo imeharibika zaidi tangu wakati huo. Katika hati yake ya hivi majuzi kuhusu dhambi na ungamo, inayoitwa “Upatanisho na Kitubio,” Papa John Paul wa 2 aliyataja maneno hayo ya mtangulizi wake kisha akaonyesha masikitiko mengi juu ya kile alichokiita kufunikwa kwa wazo la dhambi katika jamii ya leo inayofuata malimwengu.
Papa aliwakumbusha pia mapadri Wakatoliki, na Wakatoliki kwa ujumla, kwamba si vizuri sana kufuata ile desturi iliyo katika makanisa mengi ya Kikatoliki leo ya kukusanya watu ili wawe pamoja wanapofanya ungamo na kupata maondoleo ya dhambi zao. Alisema kwamba ungamo la watu mmoja mmoja ndiyo “njia pekee ya kawaida na inayofaa” ya kuishika ile sakramenti ya kitubio. Katika imani rasmi za Kikatoliki, kitubio kinahusiana na matendo mema ya kupatanisha mtenda dhambi na Mungu.
Makanisa ya Kiprotestanti yaliyo mengi yanakanusha uhitaji wa kuungamia padri. Yanashikilia kwamba kuungamia Mungu kunatosha ili kusamehewa dhambi, lakini mengine yanapendelea watu kwa ujumla waungame na kupata ondoleo la dhambi zao wakiwa pamoja kwenye “ibada ya Ushirika.” Waprotestanti wengi wanaamini kwamba imani ndiyo tu inayohitajiwa ili kuhesabiwa kuwa mwenye haki mbele za Mungu.
Watu wengi wanabaki wakiwa wametatizwa kwa sababu ya mafundisho hayo yenye kupingana yaliyo ndani ya yale yanayoitwa makanisa ya Kikristo juu ya ungamo, kitubio na kuhesabiwa haki, au jinsi ya kupata msimamo unaofaa mbele za Mungu. Wanajisikia kwamba inawapasa wawe wanafanya jambo fulani ili wawe na msimamo unaofaa na Mungu, lakini hawajui hatua za kuchukua.
Makala inayofuata itaeleza ni kwa sababu gani tunahitaji tupatanishwe na Mungu, kisha iyachunguze maoni ya Wakatoliki na Waprotestanti juu ya “kuhesabiwa haki.” Makala nyingine mbili zitaeleza yanayofundishwa na Biblia juu ya habari ya kujipatia msimamo wenye uadilifu mbele za Mungu, na jinsi jambo hilo linavyokuhusu wewe.