Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 12/1 kur. 4-7
  • Uadilifu Mbele za Mungu—Jinsi Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uadilifu Mbele za Mungu—Jinsi Gani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Sababu Inayofanya Tuhitaji Kupatanishwa na Mungu
  • Maoni ya Wakatoliki Juu ya “Kuhesabiwa Haki”
  • Maoni ya Waprotestanti
  • Wala Maoni ya Wakatoliki Wala ya Waprotestanti Juu ya ‘Kuhesabiwa Haki’ Si Sawa
  • Biblia Inafundisha Nini?
  • Wanatangazwa Kuwa Waadilifu “Ili Wapate Uzima”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Je! Wewe Una Msimamo Unaofaa na Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Je! Historia ya Kidini Ina Manufaa Yo Yote Kwako Wewe?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Yale Mapinduzi Makubwa ya Kidini
    Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 12/1 kur. 4-7

Uadilifu Mbele za Mungu​—Jinsi Gani?

“GOD ‘e say ‘im alrite.” (Mungu an‘sema ‘ye iko sawa). Inaonekana hivyo ndivyo maneno “kuhesabiwa haki” yameandikwa katika tafsiri “Agano Jipya” iliyofanywa majuzi kwa Kiingereza cha kuvunjia cha kule New Guinea. Ijapokuwa maneno ya lugha hiyo yanasikika kuwa na ladha ya kigeni, yanaeleza wazo la msingi linaloambatana na neno linalotafsiriwa katika Biblia “kuhesabiwa haki,” au “tangazo la kuwa mwenye uadilifu,” kama linavyosemwa katika Warumi 5:16, NW.

Kwa upande mwingine, watu wengine wanasema: ‘Mimi naishi maisha yenye tabia njema. Nafanyia wengine mema niwezapo. Mimi niko tayari kumlaki Muumba wangu.’ Ni wazi wanaelewa kuhesabiwa haki kuwa na maana ya kujihesabia haki. Kulingana na Biblia, fundisho la “kuhesabiwa haki” linahusiana na jinsi Mungu anavyotuona sisi na jinsi yeye anavyoshughulika nasi. Yehova ndiye “Muumba.” (Isaya 40:28) Yeye ndiye “Mhukumu ulimwengu wote.” (Mwanzo 18:25) Basi, hakuna jambo lingeweza kuwa la maana kuliko jinsi yeye anavyotufikiria.

Sababu Inayofanya Tuhitaji Kupatanishwa na Mungu

Biblia inasema hivi juu ya Yehova: “Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Yeye ndiye kiwiliwili cha uadilifu. Akiwa ndiye Muumba na Mpaji-Uzima, yeye ana haki ya kuweka kiwango, au kawaida, ya kuamulia yanayofaa na yasiyofaa. Mambo yanayopatana na kiwango cha Mungu ni maadilifu.

Hivyo, Mungu ndiye anayewekea viumbe wake wenye akili shabaha wanayopaswa kufikia ikiwa wanataka kuishi kupatana na Muumba wao. Kuikosa shabaha, au kiwango hicho, ndiko kunakoitwa dhambi na lugha zile zilizotumiwa kwanza kabisa kuiandikia Biblia. Basi, dhambi ni ukosefu wa uadilifu. Ni kushindwa kufuata maelezo ya Mungu juu ya mambo yanayofaa na yasiyofaa. Kwa hiyo, dhambi ni namna fulani pia ya ukosefu wa utaratibu, namna fulani ya kutokutii sheria.​—1 Yohana 5:17; 3:4.

Yehova “Mungu si Mungu wa machafuko, bali wa amani.” (1 Wakorintho 14:33) Hapo kwanza viumbe wake wote katika mbingu na dunia walikuwa wakamilifu. Walipewa uhuru wa kuchagua. (2 Wakorintho 3:17) Walifurahia “uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.” (Warumi 8:21) Kwa muda ambao viwango vyake vya uadilifu viliheshimiwa, amani na utengemano vilidumu katika sehemu zote za ulimwengu mzima. Machafuko yalipenya ndani ya ulimwengu huo wakati, kule mbinguni kwanza, na baadaye duniani, viumbe fulani walipopata kuwa wasiomtii Mungu, wakaikataa haki aliyo nayo ya kuwatawala. Wakaondoka kwenye kiwango cha Mungu cha yale yanayofaa na yasiyofaa. Wakaikosa shabaha na hivyo wakajifanya kuwa watenda dhambi.

Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa. (Mwanzo 3:1-6) “Kwa hiyo . . . dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.” (Warumi 5:12) Tangu wakati wa uasi wao, dhambi ‘imetawala kama mfalme pamoja na kifo,’ kwa sababu wazao wote wa Adamu “wote wamefanya dhambi na hupungukiwa” na kiwango cha uadilifu cha Mungu. (Warumi 5:21; 3:23, NW) Ndiyo sababu tunahitaji kupatanishwa na Mungu.

Maoni ya Wakatoliki Juu ya “Kuhesabiwa Haki”

Uhitaji huo wa kupatanishwa na Mungu unatambuliwa na makanisa yote yanayodai kuwa ni ya Kikristo. Lakini, ufahamu wa jinsi upatanisho huo unavyopatikana na wa msimamo wa Mkristo mbele za Mungu unatofautiana katika mafundisho ya Wakatoliki na Waprotestanti.

Kwa habari ya imani rasmi za Wakatoliki, kichapo The Catholic Encyclopedia kinasema: “Kuhesabiwa haki kunamaanisha badiliko au geuzo la umbo linalotokea katika nafsi ambalo kwalo mwanadamu anahamishwa kwenye ile hali ya kuwa na dhambi ya asili, alimozaliwa akiwa mtoto wa Adamu, kisha analetwa kwenye neema na kuwa mwana wa Mungu kupitia Yesu Kristo, yule Adamu wa pili.” Kamusi inayoitwa A Catholic Dictionary inatoa maelezo haya mengine: “Hapa sisi tunazungumza tu namna watu wazima wanavyoinuliwa katika hali ya kifo na dhambi na kuletwa kwenye upendeleo na urafiki wa Mungu; kwa maana kwa habari ya vitoto vichanga Kanisa linafundisha kwamba wakati vinapobatizwa vinahesabiwa haki bila ya vyenyewe kujifanyia kitendo cho chote.”

Kwa ufupi, Kanisa Katoliki linafundisha kwamba “kuhesabiwa haki” ni kitendo kinachotendwa na Mungu kisha mtu anayebatizwa katika imani ya Kikatoliki anafanywa mwadilifu na kutakaswa kweli kweli na ile karama ya “neema” ya kimungu. Pia linadai kwamba kuhesabiwa haki kunaweza (1) kuongezwa na ustahili wa mtu mwenyewe, au matendo mema; (2) kupotezwa na dhambi yenye kuleta kifo na kwa kutokuamini; (3) kupatikana tena kwa sakramenti ya kitubio. (4) Ndani ya mpango huo, ni lazima Mkatoliki aliyehesabiwa haki aungamie padri dhambi zake ili apate ondoleo la dhambi. (5) “Adhabu [yo yote] ya muda”a ambayo bado mtu anaistahili hata baada ya kupata ondoleo la dhambi inaweza kufidiwa kwa matendo mema au kusamehewa kwa “rehema ya dhambi.”

Maoni ya Waprotestanti

Kuuzia watu rehema za dhambi mwanzoni mwa karne ya 16 ndiko kulikoanzisha yale Marekebisho ya Kiprotestanti ya kujitenga na Ukatoliki. Mtawa Mkatoliki, Martin Lutheri, alilishambulia zoea hilo katika hoja 95 alizobandika katika mlango wa kanisa-ngome katika Wittenberg, Ujeremani, mwaka 1517. Lakini, kwa kweli, Lutheri alichukua hatua nyingine iliyo kubwa zaidi ili akatae imani rasmi ya Kikatoliki. Alilikataa pia fundisho lote la kanisa juu ya kuhesabiwa haki. Ikithibitisha jambo hilo, kamusi A Catholic Dictionary inasema: “Utofautiano wa imani juu ya njia inayotumiwa ili watenda dhambi wahesabiwe haki mbele za Mungu ndio ukawa habari kubwa ya magombano kati ya Wakatoliki na Waprotestanti wakati wa yale Marekebisho ya Kiprotestanti ya kujitenga na Ukatoliki. ‘Fundisho hilo’ (yaani, fundisho la kuhesabiwa haki kwa sababu ya imani tu) ‘lisipokubaliwa,’ anasema Lutheri katika kichapo chake Table Talk, ‘basi mambo yetu sisi yataishia hapo.’”

Lutheri alimaanisha nini hasa kwa kusema ‘kuhesabiwa haki kwa sababu ya imani tu’? Akiwa Mkatoliki, Lutheri alikuwa amejifunza kwamba ili mtu ahesabiwe haki ubatizo unahusika, ustahili wa mtu binafsi, na matendo mema, na pia sakramenti ya kitubio yenye kutolewa na padri, ambaye anasikia ungamo la mtu, halafu anampa ondoleo la dhambi, kisha anamwekea mtu huyo matendo anayopaswa kufanya kwa kusudi la kujiadhibu mwenyewe ili alipie makosa yake.

Katika jitihada zake za kupata amani na Mungu, Lutheri alikuwa amekwisha kuzitumia njia zote zilizohitajiwa na imani rasmi ya Kiroma juu ya kuhesabiwa haki, kutia na kufunga kula, kusali, na kujiadhibu, lakini hayo yakawa kazi bure. Kwa sababu dhamiri yake haikutulizwa na matendo hayo, alisoma tena na tena Zaburi na barua za Paulo, na mwishowe akapata amani ya akili kwa kukata shauri kwamba Mungu anahesabu wanadmau kuwa wenye haki, si kwa sababu ya ustahili wao, matendo yao mema, wala kujiadhibu kwao wenyewe, bali kwa sababu ya imani yao tu. Alisisimukia sana wazo hilo la “kuhesabiwa haki kwa sababu ya imani tu” mpaka akaliongeza neno “tu” mwishoni mwa neno “imani” katika tafsiri ya Kijeremani aliyofanya juu ya Warumi 3:28!b

Makanisa yaliyo mengi ya Kiprotestanti yalifuata maoni ya Lutheri juu ya “kuhesabiwa haki kwa neema kupitia imani.” Kwa kweli jambo hilo lilikuwa limekwisha kusemwa na Jacques Lefevre d’Etaples, Mfaransa aliyetaka marekebisho kabla hayajatokea. Ikitoa muhtasari ya tofauti iliyopo kati ya maoni ya Wakatoliki na Waprotestanti juu ya kuhesabiwa haki, kamusi A Catholic Dictionary inasema hivi: “Wakatoliki wana maoni ya kwamba kuhesabiwa haki ni tendo ambalo kupitia hilo mwanadamu anafanywa kuwa mwenye haki kweli kweli; Waprotestanti nao wana maoni ya kwamba ni tendo ambalo katika hilo mwanadamu anatangazwa na kujulikana tu kuwa mwenye haki, nayo matendo mema ya mtu mwingine, yaani ya Kristo, ndiyo yanayotumiwa kumfanya awe katika hali hiyo.”

Wala Maoni ya Wakatoliki Wala ya Waprotestanti Juu ya ‘Kuhesabiwa Haki’ Si Sawa

Imani rasmi ya Wakatoliki inaruka mipaka ya mambo ambayo Biblia inafundisha wakati inapodai kwamba “mwanadamu anafanywa kuwa mwenye haki kweli kweli,” au kuwa mwadilifu, kwa karama ya neema ya kimungu anayopewa anapobatizwa. Si ubatizo unaosafisha dhambi ya awali, bali ni damu ya Kristo iliyomwagwa. (Warumi 5:8, 9) Pana tofauti kubwa kati ya Mungu kumfanya mtu kweli kweli awe mwadilifu na kuhesabiwa, au kufikiriwa kuwa mwadilifu. (Warumi 4:7, 8) Mkatoliki ye yote aliye mnyofu, anayejitahidi sana kupambana na dhambi, anajua kwamba yeye hajafanywa kweli kweli kuwa mwadilifu. (Warumi 7:14-19) Kama angekuwa ni mwadilifu kweli kweli, hangekuwa na dhambi za kuungamia padri.

Tena, kama imani rasmi ya Wakatoliki ingekuwa ikifuata Biblia, Mkatoliki mwenye kujua kwamba yeye ni mtenda dhambi angeungamia Mungu dhambi zake, amwombe msamaha kupitia Yesu Kristo. (1 Yohana 1:9—2:2) Maombezi ya padri wa kibinadamu katika hatua yo yote ya mtu ya “kuhesabiwa haki” hayana msingi katika Biblia, sawa na vile mtu kujifanyia matendo mengi ya ustahili ili apate rehema ya dhambi kusivyo na msingi wa Biblia.​—Waebrania 7:26-28.

Bila shaka wazo la Waprotestanti la kwamba Mkristo anahesabiwa haki anapotangazwa kuwa mwadilifu kwa kutegemea ustahili wa dhabihu ya Kristo linakaribiana zaidi na linalofundishwa na Biblia. Hata hivyo, makanisa fulani ya Kiprotestanti yanafundisha “kuhesabiwa haki kwa sababu ya imani tu” na, kama tutakavyoona baadaye, kwa kufanya hivyo yanakosa kufikiria sababu za waziwazi zilizotokezwa na mtume Paulo na Yakobo. Mwelekeo wa makanisa hayo wa kujikinai kiroho unasemwa kwa ufupi katika kifungu hiki cha maneno, “ukiisha okolewa, umeokolewa daima.” Waprotestanti fulani wanaamini kwamba kumwamini Yesu kunatosha ili kuokolewa na, kwa hiyo, kuhesabiwa haki kunautangulia ubatizo.

Tena, ijapokuwa makanisa mengine ya Kiprotestanti yanafundisha kwamba mtu anahesabiwa haki kwa imani yanamfuata John Calvin Mfaransa aliyetaka marekebisho ya kidini, nayo yanafundisha kwamba kila mtu ameandikiwa yatakayompata. Hivyo yanalikataa fundisho la Biblia kwamba mtu ana uhuru wa kuchagua atakalofanya. (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Basi, inaweza kusemwa kwamba wala mawazo ya Wakatoliki wala Waprotestanti kuhusu kuhesabiwa haki, hayapatani kabisa na Biblia.

Biblia Inafundisha Nini?

Hata hivyo ni hakika kwamba Biblia inafundisha fundisho la “kuhesabiwa haki,” au njia ambayo mwanadamu anaweza kupewa msimamo wa uadilifu mbele za Mungu. Tumetangulia kuona sababu inayofanya tuhitaji tupatanishwe na Mungu, kwa kuwa sisi sote tumezaliwa tukiwa, si watoto wa Mungu, bali “watoto wa hasira.” (Waefeso 2:1-3) Kubaki au kutobaki kwa hasira ya Mungu juu yetu kunategemea kama tutakubali au tutakataa uandalizi wake wenye rehema wa kupatanishwa na huyo aliye Mungu mtakatifu na mwadilifu. (Yohana 3:36) Uandalizi huo wenye upendo ndio “ukombozi uliolipwa na Kristo Yesu.”​—Warumi 3:23, 24, NW.

Mtume Paulo alionyesha kwamba dhabihu ya ukombozi ya Kristo inayafungulia njia matumaini mawili, moja “duniani” na lile jingine “katika mbingu.” Aliandika hivi: “Mungu aliona vema ujazi wote ukae katika yeye [Kristo], na kupitia kwake apatanishe tena kwake mwenyewe vitu vingine vyote kwa kufanya amani kupitia damu ambayo alimwaga juu ya mti wa mateso, si kitu kama ndivyo vitu vilivyo duniani ama vitu vilivyo katika mbingu.”​—Wakolosai 1:19, 20, NW.

Ili mtu ashiriki moja la matumaini mawili hayo, anahitajiwa kabisa awe na msimamo wa uadilifu mbele za Mungu, na hiyo inatia ndani mambo mengi kuliko “kumwamini Yesu” tu. Mambo yanayohusika hasa kwa Wakristo walio na tumaini la kimbingu na wale walio na tumaini la kuishi milele katika dunia-paradiso yatafikiriwa katika makala mbili zinazofuata. Tafadhali endelea kusoma, nawe usisite-site kumwomba Shahidi wa Yehova aliyekupa gazeti hili azungumze nawe juu ya makala hizi kwa kuitumia Biblia.

[Maelezo ya Chini]

a Kulingana na imani rasmi ya Kikatoliki, dhambi inahusu hatia na aina mbili za adhabu​—ya milele na ya muda. Hatia na adhabu ya milele inafanyiwa malipo kupitia sakramenti ya kitubio. Ni lazima adhabu ya muda ifanyiwe fidia katika maisha ya sasa kwa kutenda mambo mema na kufanya mazoea ya kujiadhibu, au katika maisha yanayofuata katika moto wa purgatori. Rehema ya dhambi ni ondoleo nusu au kamili la adhabu ya muda, nalo linafanywa kwa kuutumia ustahili wa Kristo, Mariamu, na “watakatifu.” Ustahili huo unakuwa umewekwa akibani katika “Sanduku la Hazina ya Kanisa.” “Matendo mema” yanayopasa kufanywa ili mtu apate rehema ya dhambi yanaweza kuwa ni pamoja na kutembelea mahali patakatifu au kuchanga pesa za kusudi fulani lililo “jema.” Kwa njia hiyo, nyakati zilizopita pesa zilikuwa zikichangwa kwa ajili ya vile Vita Vitakatifu na kwa ajili ya kujenga makathedro, makanisa, na hospitali.

b Lutheri alitokeza shaka pia juu ya kama barua ya Yakobo ni sehemu ya Maandiko Matakatifu, akiwa na fikira ya kwamba njia inayotumiwa na Yakobo kueleza mambo katika sura ya 2, yaani, imani isiyo na matendo imekufa, inapingana na maelezo ya mtume Paulo juu ya kuhesabiwa haki “pasipo matendo.” (Warumi 4:6) Alishindwa kutambua kwamba Paulo alikuwa akisema juu ya matendo ya Torati ya Kiyahudi.​—Warumi 3:19, 20, 28.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

KANISA KATOLIKI linafundisha kwamba kuhesabiwa haki kunafanya mwanadamu awe mwadilifu kweli kweli, lakini kwamba hali ya kuhesabiwa haki inaweza kupotezwa kwa kutenda dhambi ya kifo au inaweza kuzidishwa kwa ustahili wa mtu binafsi

[Blabu katika ukurasa wa 6]

WAPROTESTANTI WENGI wanaamini mtu anahesabiwa haki, au kutangazwa kuwa mwadilifu, kwa sababu ya imani tu, na kwamba kumwamini Yesu kunawekea mtu bima ya wokovu. Wengine wanaamini kwamba, kabla ya kuanza kuishi, mtu anakuwa amekwisha kuandikiwa kwamba atahesabiwa kuwa mwenye haki

[Blabu katika ukurasa wa 7]

BIBLIA inafundisha kwamba mwanadamu ana uhuru wa kuchagua atakalofanya na kwamba dhabihu ya ukombozi ya Kristo inafungua njia ya matumaini mawili, moja la kimbingu na lile jingine la kidunia. Matumaini yote mawili yanahusu kupokea msimamo wa uadilifu mbele za Mungu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki