Maisha na Huduma ya Yesu
Yohana Anapungua, Yesu Anazidi
BAADA ya sikukuu ya Kupitwa katika masika ya mwaka 30 W.K., Yesu na wanafunzi wake wanaondoka Yerusalemu. Lakini, hawarudi makwao katika Galilaya bali wanaingia nchi ya Yudea ambako wanabatiza watu. Yohana Mbatizaji amekuwa akifanya kazi iyo hiyo kwa muda wa mwaka mmoja sasa, na bado ana wanafunzi wanaoshirikiana naye.
Kwa kweli, Yesu mwenyewe habatizi watu, bali wanafunzi wake ndio wanaofanya hivyo kwa mwelekezo wake. Ubatizo wanaofanya una maana moja na ule uliofanywa na Yohana, kwa kuwa ni mfano wa toba ya Myahudi juu ya dhambi alizotenda juu ya agano la Torati ya Mungu. Lakini, baada ya ufufuo wake, Yesu anawaagiza wanafunzi wake wafanye ubatizaji ulio na maana tofauti. Ubatizo wa Kikristo ni mfano unaoonyesha mtu amejiweka wakfu atumikie Yehova Mungu.
Lakini, hapa mwanzoni-mwanzoni, ingawa Yohana na Yesu wanafanya kazi zao wakiwa mbali mbali, wote wawili wanafundisha na kubatiza wenye kutubu. Lakini wanafunzi wa Yohana wanaona wivu na kumpelekea malalamiko juu ya Yesu: “Rabi . . . tazama, huyo anabatiza na watu wote wanamwendea.”
Badala ya kuwa mwenye wivu, Yohana anafurahia sana mafanikio ya Yesu na pia anataka wanafunzi wake wafurahi sana. Anawakumbusha hivi: “Ninyi wenyewe mwanishuhudia ya kwamba nalisema, Mimi siye Kristo, bali nimetumwa mbele yake.” Halafu anatumia mfano mzuri sana: “Yeye aliye naye bibi arusi ndiye bwana arusi; lakini rafiki yake bwana arusi, yeye anayesimama na kumsikia, aifurahia sana sauti yake bwana arusi. Basi hii furaha yangu imetimia.”
Yohana, akiwa ndiye rafiki ya Bwana-arusi, alifurahi sana karibu miezi sita kabla ya hapo wakati alipojulisha wanafunzi wake kwa Yesu. Wengine wao wakawa wenye kutazamiwa kuwa washiriki wa jamii ya bibi-arusi wa kimbingu wa Kristo ambayo sehemu yake ni Wakristo waliopakwa mafuta kwa roho. Yohana anawataka wanafunzi wake wa sasa pia wamfuate Yesu, kwa kuwa kusudi lake ni kutayarisha njia ili huduma ya Kristo ipate mafanikio. Ni kama vile Yohana anavyoeleza: “Yeye hana budi kuzidi, bali mimi kupungua.”
Muda mfupi baada ya hapo, Yohana anakamatwa na Mfalme Herode. Herode amemchukua Herodia, mke wa Filipo ndugu yake, awe kama mkeye mwenyewe, na wakati Yohana anapofunua wazi mbele ya watu wote kwamba vitendo vyake havifai, Herode anaagiza afungwe gerezani. Yesu anapopata habari za kukamatwa kwa Yohana, anaondoka Yudea akiwa pamoja na wanafunzi wake kwenda Galilaya. Yohana 3:22–4:3; Matendo 19:4; Mathayo 28:19; 2 Wakorintho 11:2; Marko 1:14; 6:17-20.
◆ Ni nini maana ya mabatizo yaliyofanywa kwa mwelekezo wa Yesu kabla ya ufufuo wake? Na baada ya kufufuliwa kwake?
◆ Yohana anaonyeshaje kwamba lalamiko la wanafunzi wake halifai?
◆ Kwa sababu gani Yohana anafungwa gerezani?