Ripoti ya Watangazaji wa Ufalme
Kuwakusanya “Kondoo Wengine” wa Bwana katika Australia
“NITAYATIKISA mataifa, na vitu vinavyotamanika vya mataifa yote lazima vitaingia,” ndivyo alivyoandika nabii Hagai miaka zaidi ya 2,500 iliyopita. (Hagai 2:7, NW) Leo, watu hao wanaotamanika wamemiminika kweli kweli kwenye nyumba ya Yehova ya ibada. Ingawa hivyo, nyakati nyingine huenda wasionekane kuwa wenye kutamanika sana kwa nje, kama inavyoonyeshwa na hili jambo lililoonwa kutoka Australia:
◻ Jumapili moja ndugu mwenye kusafiri katika gari lake akahudhurie mkutano alifanya jambo asilopata kamwe kulifanya: Alisimama ambebe mwomba-kubebwa mmoja. Ndugu hakujua ni kwa sababu gani alisimama ambebe mwanamume huyo kijana, kwa maana alikuwa na nywele na ndevu chafu-chafu na mavazi yake yalikuwa yamechakaa-chakaa, tena hata hakuinua kidole gumba kuonyesha anataka kubebwa. Ndugu alipata hisia ya ghafula kwamba inampasa asimame na kumchukua mtu huyo. Mwanamume huyo kijana alipoingia ndani ya gari, alisema: “Wewe unaenda kanisani, sivyo?” Ndugu alishangaa, akajibu: “Eh, ndiyo, naenda kwenye Jumba la Ufalme” “Mimi nitaenda na wewe,” akasema mwanamume huyo kijana.
Ndugu alijaribu kumsadikisha asiende naye kwa sababu ya sura yake. Lakini mwanamume huyo kijana akasisitiza ataenda kisha akasimulia hadithi hii: Yeye alikuwa ameondoka nyumbani akiwa na umri wa miaka 16, na tangu wakati huo alikuwa amejihusisha sana na dawa za kulevya na ukosefu wa adili. Alikuwa akiishi chini ya karatasi fulani ya plastiki nyuma ya miinuko yenye mchanga mkavu karibu na ufuo wa bahari. Alipokuwa huko alianza kufikiri kwa uzito juu ya maana ya maisha. Hakufurahia hali alimokuwa ameingia, kwa hiyo akapelekea Mungu sala kuomba msaada. Alisema kwamba alikuwa amemwambia Mungu angeenda barabarani na kumwomba kwamba Yeye aelekeze mtu fulani aje kumbeba na kumpeleka kwenye kanisa la kweli. Ni mara chache magari yanapopitia barabara hiyo iliyo pekee. Ni magari matatu tu yaliyopita hapo kwa muda wa saa kadha, na hakuna hata moja lililosimama. Alikuwa karibu kufa moyo wakati ndugu yetu alipokuja na kumchukua.
Alihudhuria mikutano yote juma hilo na kuanza kujisafisha. Hata aliuondoa msalaba aliokuwa ameuvaa shingoni. Akaamua kurudi nyumbani katika Tasmania, ambako alitumia mwezi mmoja akiisoma Biblia na kusali. Kwa kutambua kwamba alihitaji msaada wa kibinafsi ili azidi kufanya maendeleo, alienda kwenye afisi ya tawi ya Australia ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi. Mapainia fulani walitumwa wakajifunze naye, akafanya maendeleo ya haraka sana. Ukweli kutoka katika Biblia uliyapa maisha yake kusudi na tumaini kwa wakati ujao. (Mithali 10:28) Katika muda wa miezi saba akabatizwa na kufanya upainia msaidizi, na sasa anatumikia akiwa painia wa kawaida katika Sydney.
◻ Tunaweza ‘kuyapamba mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu’ kwa kushika sana kanuni za Biblia katika mwenendo wetu. (Tito 2:10) Jambo hilo lilionyeshwa katika kisa cha ndugu mmoja aliyeajiriwa kazi katika shirika ambako ugomvi wa viwandani ulitokea juu ya kusafirisha nje kondoo na ng’ombe. Kila mfanya kazi aliombwa achange dola moja ili asaidie kuutetea ugomvi huo. Ndugu alipokataa, afisa wa chama cha wafanyi kazi alimtisha kwamba angepoteza kazi yake. Ndugu akaeleza kwamba kulingana na dhamiri, yeye hangeweza kuunga mkono fujo zilizokuwa zikipangwa. Afisa wa chama akampa saa moja ya kufikiria jambo hilo.
Sasa ndugu akaanza kufanywa dhihaka na wafanya kazi wenzake. Akawaeleza kwamba jambo kubwa halikuwa ile dola, bali kwamba yeye angekuwa na hatia ya damu akiwaunga mkono halafu mtu fulani aumizwe au auawa kwa sababu wengine wa wenye kuhusika katika ugomvi huo walikuwa na bunduki na marungu. Mfanya kazi mmoja akasema hajapata kusikia maoni ya namna hiyo, naye akataka kujua mengi zaidi. Baada ya muda fulani ndugu aliweza kuanza funzo la Biblia pamoja naye, na ijapokuwa mfanya kazi huyo alipingwa na mkeye, mwanamume huyo alianza kuhudhuria mikutano baada ya muda mfupi. Leo yeye ni mmoja wa ndugu zetu walio wakfu. Kwa habari ya yule afisa wa chama hakurudi kuja kumuuliza-uliza.
Kwa kweli wale wanaopenda Mungu na uadilifu wataletewa ukweli wauone wazi kwa njia moja au nyingine, nao watautambua. Yesu alisema: “Kondo wengine ninao . . . Imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia.” (Yohana 10:16) Zaidi ya 42,000 wa “kondoo wengine” hapa katika Australia wamekwisha kuisikiliza sauti ya Mchungaji Mwema, na kila siku wengine zaidi wanakusanywa kwenye mkono wa kuume wa upendeleo wa Yesu.—Mathayo 25:31-34.
[Blabu katika ukurasa wa 22]
Tunaweza ‘kuyapamba mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu,’ kwa mwenendo wetu mwema