Kupiga Moyo Konde Kulinisaidia Nifanikiwe
Kama ilivyosimuliwa na Joseph A. Oakley
ILIKUWA furaha kama nini katika 1950 kuwa miongoni mwa 123,707 waliohudhuria mkusanyiko wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova kwenye Yankee Stadium ya Jiji la New York katika United States! Tena lilikuwa pendeleo kama nini baada ya hapo kuhudhuria darasa la 16 la shule ya umisionari ya Gileadi katika mkoa wa juu wa New York!
Baada ya kuhitimu nilipewa mgawo, pamoja na kikundi cha Waaustralia wenzangu, kwenye kazi ya umisionari katika nchi ya mbali ya Pakistani. Tulifika kule katika kiangazi cha 1951. Mwaka wa kwanza hasa ulileta majaribu makali.
Moja la hayo lilikuwa joto la hewa isiyo na unyevunyevu, yenye mavumbi, iliyo tofauti kabisa na ubaridi wa Victoria ya kusini ya Australia na Tasmania ambako nilikuwa nimeishi. Halafu kulikuwa na homa ya matumboni, kufura ini, na magonjwa mengine ya muda mrefu yaliyopata walio wengi kati ya sisi tuliofika karibuni. Mmoja wa wanadarasa wenzetu kijana alikufa mwaka huo wa kwanza.
Jaribu jingine lilikuwa umaskini na hali za maisha zilizo tofauti. Muda mfupi baada ya kufika nilipewa mgawo niwe mhudumu mwenye kusafiri, ambao ulitaka nifunge safari ndefu zenye upweke katika magari-moshi na nyakati nyingine safari hizo zilihusu kulala katika majukwaa ya vituo vya magari-moshi.
Hata hivyo jaribu jingine lilikuwa ukosefu wa itikio kwa ujumbe wetu wa Ufalme miongoni mwa wakaaji ambao kwa wingi walikuwa ni Waislamu. Lilikuwa pia jambo lenye kujaribu kweli kweli kueleza ujumbe huo katika lugha ngumu, iliyo mpya, ya Kiurdu.
Lingalikuwa jambo rahisi kuchoshwa na mambo hayo na kujiendea nyumbani. Ili kubaki kule kupiga moyo konde kulihitajiwa, tena sana. Mimi nafurahi kwamba mambo yaliyonipata kule mbeleni yalinisaidia nielekeane na majaribu hayo kwa mafanikio.
Mambo Yaliyofinyanga Maisha Yangu
Mimi nililelewa katika shamba moja karibu kilometa 18 nje ya Geelong, ambao ni mji wa pwani katika mkoa wa Victoria wa Australia. Siku moja ya Aprili katika 1935, nilipokuwa nikizuru mjini, Binti Hudson mmoja alianzisha maongezi nami na akanihimiza nihudhurie hotuba ya Biblia. Nilikuwa na wasiwasi juma lote kwa sababu nilikuwa nimemwahidi mama huyo mzee mpendwa na mnyofu, ambaye kwa wazi alikuwa mwenye bidii sana, kwamba ningehudhuria. Kwa kweli sikutaka kwenda, lakini sikuwa na ushujaa wa kumkatisha tamaa.
Kwa hiyo wakati ulipofika, nikiwa na mashaka-mashaka ya kutotaka kwenda nilitimiza ahadi yangu nikaenda. Ajabu ni kwamba nilifurahia mkutano ule sana hata nikaanza kuhudhuria kwa ukawaida. Mambo niliyojifunza yalinisadikisha kwamba nilikuwa nimeupata ukweli, nami nikabatizwa kwenye kusanyiko moja lililofanywa katika Geelong mwaka ule ule.
Miezi michache baadaye wasichana wawili mapainia wenye bidii walitembea mwendo wa zaidi ya kilometa 1.6 katika shamba lililolimwa ili wafikie shamba letu. Kilichonivutia juu yao ni imani na bidii waliyokuwa nayo. Nakumbuka nikiwauliza wangelala wapi usiku huo, kwa maana walitaja kwamba walikuwa katika safari ya kwenda kwenye mgawo wa eneo jipya katika mji mdogo wa Bacchus Marsh, karibu kilometa 56 kutoka hapo.
“Bado hatujajua, lakini tutatafuta mahali fulani kabla usiku haujaingia,” wao wakajibu. “Ikiwa sivyo, tutapiga hema yetu.” Ilikuwa tayari imepita saa 10 jioni, na michana ilikuwa mifupi na yenye baridi. Mimi nikafikiri hivi mwenyewe: ‘Hakika huku ndiko kupainia!’ Jambo hilo pia lilinifanya nianze kufikiri hivi mwenyewe: ‘Mimi nafanya nini hapa shambani, nikiwa nimejikunjia maili nyingi kutoka waliko watu? Ni nini kinachonizuia nisiwe mhudumu painia kama wanawake hawa vijana? Mimi ni kijana na mwenye afya pia. Ikiwa wao wanaweza kufanya hivyo, mbona mimi nisiweze?’ Nikapiga moyo konde papo hapo kwamba kabla ya muda mwingi kupita mimi pia ningekuwa painia.
Nikapiga Moyo Konde Kuendelea na Uamuzi Wangu
Baba alipinga sana wazo la mimi kuondoka nyumbani na kuanza kazi ya kuhubiri wakati wote pamoja na Mashahidi wa Yehova. Yeye alikuwa amekuwa mwelekezaji wa shule ya Jumapili kwa karibu miaka 30 na alikuwa na maoni mabaya yasiyo na msingi dhidi ya Mashahidi. Ijapokuwa hivyo, mimi nilikuwa nimeanza umri wa miaka 21, na mama hakuwa na kipingamizi cho chote kikubwa nilipomweleza wazi mipango yangu. Kwa hiyo, mwishowe, tarehe ya Juni 30, 1936, ikawekwa kuwa ndiyo siku ambayo ningeondoka nyumbani.
Baba yangu aliwaomba wafanya biashara kadha mashuhuri waseme nami ili nikubali kuacha hiyo “shughuli ya kuchukiza sana” kama yeye alivyoiita. Wanaume hao walijaribu sana kunibembeleza nibaki nyumbani, wakitumia hoja za namna zote, kama vile: ‘Wewe utaleta aibu juu ya dini ya jamaa yenu.’ ‘Wewe unajiunga na kikundi kisichojulikana na kisichopendwa hata kidogo na watu,’ na ‘Ni jambo gani linalokuthibitishia kabisa kwamba utapata usaidizi wa kipesa?’
Ubembelezi huo uliojaribiwa—ambao unawezekana ulifanywa kwa nia nzuri sana—uliendelea kwa majuma mengi. Ijapokuwa hivyo, jambo la kushangaza ni kwamba walivyozidi kujaribu kunisihi nisiende, ndivyo mimi nilivyozidi kupiga moyo konde nijiunge na hesabu za mapainia.
Juni 30 ikafika, siku yenye baridi na dhoruba! Mimi nikafunga virago vyangu vyote katika pikipiki yangu nikaondoka kuelekea Melbourne, karibu kilometa 64 kutoka hapo. Nilikuwa nimealikwa nikafanye kazi kule pamoja na kikundi fulani cha mapainia. Sasa maisha mapya kabisa yenye kusudi yakafunguka mbele yangu, lakini kulikuwa na majaribu mengi.
Kuelekeana na Upinzani kwa Kupiga Moyo Konde
Katika siku hizo njia kuu ya kuenezea ujumbe wa Ufalme ilikuwa kwa kutumia magari yenye vikuza sauti ili kutangaza hotuba za Biblia zilizorekodiwa za msimamizi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, J. F. Rutherford. Kwa karibu miaka mitano, mimi niliendesha moja la “magari” hayo, ile niliyoendesha ikiwa ni vani yenye pambo laini sana katika mabapa na yenye vifaa vya kutosha. Ilijulikana kila mahali kuwa lile “Ogopesho Jekundu.”
Sauti aali na yenye kina ya Ndugu Rutherford ilipotokea katika kipaaza sauti cha muundo wa pembe ilikuwa “tamu” kwa watafutaji wachache wa ukweli, lakini kwa wapinzani wa ukweli ilikuwa kama sumu. (Linganisha 2 Wakorintho 2:14-16.) Pindi kwa pindi, nilikuwa nikirushiwa maji kupitia bomba la kunyunyizia maua ya bustani, au vani ilikuwa ikipigwa kwa mawe.
Hotuba za Ndugu Rutherford zenye kufunua wazi uwongo wa kidini, kwa upande ule mwingine, zilivuta kweli kweli watu wengine. Kwa mfano, bwana mmoja wa hali ya juu aliomba nakala ya kila moja ya hotuba zilizorekodiwa za Rutherford na kila kitabu ambacho alikuwa ameandika. Sisi tulipotembelea nyumba kubwa ya bwana huyo, rekodi hizo na vitabu zilikuwa nzito sana hata nikazipeleka kwake kwa shida. Mwanamume huyo alifurahi sana kuzipata, akaandika hundi ya pauni 15 (ambazo wakati huo zilikuwa dola 70) pale pale. Hilo lilikuwa ndilo angusho langu lililo kubwa zaidi!
Katika 1938 Ndugu Rutherford aliorodheshwa kutembelea Australia na kutoa hotuba ya Biblia katika Jumba Kuu la Mji, katika Sydney, New South Wales. Mimi nilikuwa miongoni mwa wale waliopaswa kuzunguka barabara zote za Sydney wakiwa na gari la kupaaza sauti, tukitoa matangazo ya pale pale juu ya ziara iliyokuwa ikija. Lile “Ogopesho Jekundu” lilikuwa limetayarishwa kwa njia ya pekee kwa ajili ya programu hiyo ya majuma sita likiwa na tangazo kubwa pande zote mbili za vani yenyewe. “Mbumburusho” huo ulitokeza upinzani mwingi sana.
Kwa sababu ya mkazo mwingi wa kidini, mpango uliokuwapo wa kutumia Jumba Kuu la Mji la Sydney ulifutwa. Sasa mgawo wangu ukawa kutumia gari la kupaaza sauti ili watu watie sahihi zao katika maombi ya kuteta. Tulitembelea vikundi vikubwa vya wafanya kazi wakati wa mapumziko ya chakula na, ijapokuwa mahali pengi palikuwa na upinzani, tukafanikiwa kupata mamia ya sahihi zenye kupendelea uhuru wa kusema. Kwa ujumla makumi ya maelfu ya sahihi zilipatikana katika sehemu zote za nchi. Lakini ijapokuwa tulipelekea wawakilishi wa baraza la mji wa Sydney ombi hilo lenye sahihi nyingi, bado tulikatazwa tusitumie Jumba Kuu la Mji.
Hata hivyo, kama inavyokuwa mara nyingi sana, jambo hilo liligeuka likawa lenye faida kwa watu wa Yehova. Kwa maana Nyanja za Michezo za Sydney zilikodiwa, na kwa sababu ya watu wengi sana kujua habari hizo kwa sababu ya upinzani uliotokea, hudhurio kwenye hotuba ya Ndugu Rutherford lilifurika likawa la watu wapatao 12,000, kulingana na makadirio ya polisi. Kwa kuwa Jumba Kuu la Mji lingeweza kuwa na viti karibu 5,000 tu, upinzani ulileta matokeo ya kuwezesha watu walio zaidi ya mara mbili ya hesabu hiyo waisikie hotuba!
Kupiga Moyo Konde Wakati wa Marufuku
Ilipotokea Vita ya Ulimwengu ya Pili katika 1939, upinzani uliongezeka. Ndipo, katika Januari 1941, kazi ya Mashahidi wa Yehova ikapigwa marufuku katika sehemu zote za Australia. Mimi nilikuwa nikipainia katika Melbourne wakati huo na nikiishi kwenye bohari la kuwekea vitabu vya Sosaiti.
Siku moja polisi sita wa Jumuiya ya Madola wenye vifua vipana walifika pale na kumkabili mtumishi wa bohari Jack Jones na mimi. Mimi nilipewa dakika tano tu za kuondoka katika chumba changu cha ghorofani. Je! wewe umepata kujaribu kufunga virago vyako vyote kwa dakika tano? Sikuwa nimekaribia hata kumaliza kufanya hivyo wakati polisi hao walipoingia chumbani kwa fujo na kurusha-rusha nje dirishani nguo zangu zote na vifaa nilivyokuwa sijafunga.
Ijapokuwa hivyo, marufuku haikukomesha utendaji wetu. Tukitumia Biblia, tuliendelea kuhubiri nyumba kwa nyumba na kufanya mikutano ya ukawaida katika Melbourne. Wakati wa 1942, mwaka wa pili wa marufuku, mimi niliitwa niende Sydney tena, safari hii kusaidia katika kuitengeneza kazi katika makundi saba ya Mashahidi wa Yehova kule.
Makao ya Betheli katika Sydney yalikuwa wakati huo yanakaliwa na maafisa wa kiserikali wa Jumuiya ya Madola. Tukiwa katika makao makubwa yenye ghorofa mbili mwendo mdogo tu kutoka hapo, tulipanga utendaji wote wa kitengenezo. Mgawo wangu ulikuwa kutembelea kila moja la makundi ya Sydney na, kwa kutumia pikipiki yenye kigari kilichofunganishwa nayo, nipelekee makundi muhtasari ya mikutano na vitu vingine vilivyohitajiwa ili yaendelee na mipango ya kitengenezo na kusonga mbele.
Kutumikia Katika Tasmania
Marufuku ilipoondolewa Juni 1943, nilipewa mgawo wa kusaidia katika kusimamisha tena bohari la vitabu katika Melbourne. Ndipo, katika 1946, niliwekwa rasmi nitumikie nikiwa “Mtumishi kwa akina Ndugu” mwenye kusafiri (ambaye sasa ni mwangalizi wa mzunguko) katika mkoa wa kisiwa cha Australia cha Tasmania. Kijiografia, Tasmania ni kisiwa kizuri kimazingira, chenye vilima-vilima vilivyo na vilele vingi vyenye kufunikwa na theluji muda mwingi wa mwaka.
Nilipotumikia nikiwa mwangalizi mwenye kusafiri, kulikuwa na makundi saba tu na vikundi kadha vilivyo peke yavyo katika kisiwa kizima. Kati ya ziara na ziara za kutembelea makundi, nilipainia kwenye mji mdogo unaoitwa Mole Creek. Upinzani wenye jeuri kuelekea Mashahidi ulikuwa umetokea kwa ghafula kule wakati wa vita. Lakini kufikia wakati huu ulikuwa umefifia, na hesabu fulani ya watu nilioangushia vichapo wakawa Mashahidi walio wakfu hatimaye.
Ni wakati nilipokuwa ningali Tasmania, katika 1950, kwamba nilipokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la 16 la Gileadi. Baada ya kuhitimu, kama ilivyosimuliwa mwanzoni-mwanzoni, nilipewa mgawo kwenda Pakistani.
Ndoa na Jamaa
Nilipokuwa nimekuwa Pakistani miaka sita, nilioa Edna Marsh, aliyekuwa amekuwa akitumikia akiwa mmisionari katika Japani. Edna alijiunga nami, nasi tukafungua makao mapya ya wamisionari katika Quetta, mji ulio katika jimbo la miinuko ya Pakistani. Tulitumia miaka miwili katika Quetta, lakini kwa sababu mtoto wetu wa kwanza alikuwa akielekea kupatikana tukaamua turudi Australia. Sasa ni mambo gani yaliyokuwa mbele yetu?
Hatukuwa tumepata kamwe kuwa na shaka juu ya mahali pa kutulia na kukuza jamaa yetu. Mimi nilikuwa nimeahidi kwamba kama ingekuja kutokea kwamba nirudi kutoka utumishi wa nchi ya kigeni ningerudi Tasmania. Ijapokuwa hivyo, tulikuwa ni kama tumeishiwa kabisa na mapeni, na kwa mtu mwenye umri wa miaka 45 kama mimi ilikuwa shida kupata kazi. Hata hivyo tuliazimia tusiache kazi ya kimwili ituzuie kwenda kwenye mikutano ya kundi na utumishi wa shambani.
Kwa msaada wenye fadhili wa ndugu za kiroho, mimi niliweza kuanzisha kibiashara changu mwenyewe cha kusafisha madirisha ya nyumba. Kwa muda wa zaidi ya miaka 20 sikukosa mkutano hata mmoja wala utumishi wa shambani kwa sababu ya kujitia katika kazi ya kimwili, ingawa nyakati nyingine ilinihitaji kupiga moyo konde ndipo niweze kukataa matoleo ya kikazi na pesa za ziada zilizopatikana kwa njia hiyo. Hivyo sisi tuliweza kulea watoto wetu wawili katika njia ya ukweli na kuwa na ushirika wa kawaida katika utendaji wote wa Ufalme.
Sasa watoto wetu wamekua na hawatutegemei sisi tena. Wote wawili wako imara katika ukweli, binti yetu akiwa amefurahia miaka kadha ya kupainia kabla ya kuolewa. Mwana wetu na mke wake sasa wako karibu kutumikia mahali ambako uhitaji ni mkubwa zaidi katika utumishi wa painia.
Maisha Yenye Kuthawabisha
Hivi majuzi tulipokea ziara kutoka kwa rafiki wa zamani aliyekuwa mtu wa kwanza kuchukua msimamo wake upande wa ukweli katika mji wa Quetta katika Pakistani. Baada ya mkutano mmoja kwenye Kundi la Launceston letu hapa katika Tasmania, rafiki huyo wa kike alieleza kundi jinsi yeye alivyoagiza mtumishi wake mara mbili aniambie kwamba yeye hakuwa nyumbani nilipotembelea kule. Ijapokuwa hivyo, baadaye nilipomkuta katika bustani naye akawa hawezi ‘kuponyoka,’ alianza kuuliza maulizo, na mwishowe akakubali funzo la Biblia. Yeye alisimulia anavyoshukuru kwamba mimi nilipiga moyo konde kwa kudumu katika mgawo huo mgumu wa nchi ya kigeni ya Pakistani.
Miaka michache kabla ya hapo, kwenye mkusanyiko mmoja katika Sydney, mwanamke mmoja kijana alipiga mbio kunielekea akanikumbatia kwa bidii yenye joto jingi. Kwa kushangaa, nikamdokezea kwamba alikuwa anakosea. “Hapana,” yeye akajibu, “kwani wewe si Joe Oakley? Wewe na Alex Miller mlijifunza na jamaa yetu katika Lahore, Pakistani, na sasa mama na dada yangu na mimi tumo katika ukweli na tunaishi katika Sydney.”
Mambo yaliyoonwa kama hayo yamechanga kweli kweli kuniletea uradhi wa kuwa nilishiriki kwa ukamili katika utangazaji wa Ufalme. Ni jambo zuri kama nini kuona baraka ya Mungu juu ya kazi hiyo! Nilipotumikia mara ya kwanza hapa katika Tasmania katika 1946, walikuwapo wahubiri wa Ufalme tisa katika mji wote wa Launceston. Sasa yapo makundi matatu, kila moja likiwa na wahubiri zaidi ya 90!
Kwa kweli, kutokana na mambo yaliyoonwa yanayoridhisha ya miaka yangu zaidi ya 50 ya utumishi wa Kikristo, mimi naweza kusema bila kusita-sita hata kidogo kwamba kupiga moyo konde kumenisaidia nifanikishe utumishi huo.
[Picha katika ukurasa wa 24]
Gari la kupaaza sauti lililotumiwa kutangaza ujumbe wa Ufalme katika Sydney
[Picha katika ukurasa wa 25]
Joe Oakley pamoja na kundi dogo katika Quetta, Pakistani, wakati Jumba la Ufalme jipya lilipofunguliwa Desemba 15, 1955