Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 7/1 kur. 26-29
  • Peke Yangu Lakini Sijaachwa Kamwe

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Peke Yangu Lakini Sijaachwa Kamwe
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kujua Kweli kwa Mara ya Kwanza
  • Sasa Nikiwa Peke Yangu Sana
  • Uwasiliano na Tengenezo
  • Mkusanyiko na, Hatimaye, Ubatizo
  • Kurudi Mount Gambier
  • Migawo Mipya
  • Utumishi wa Wakati Wote Wenye Kuendelea
  • 1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Kupiga Moyo Konde Kulinisaidia Nifanikiwe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • “Endelea na Kazi Mpaka Imalizike”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • “Kutafuta Kwanza Ufalme”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 7/1 kur. 26-29

Peke Yangu Lakini Sijaachwa Kamwe

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA ADA LEWIS

Sikuzote nimekuwa na mwelekeo wa kukaa peke yangu. Pia mimi ni mwenye kuazimia sana—nyakati nyingine wengine huita tabia hiyo utundu—katika kila kitu ninachofanya. Najua vilevile jinsi ilivyo rahisi kuwa mwenye kusema mambo waziwazi, na tabia hii imenisababishia matatizo katika miaka hiyo yote.

NA BADO, nashukuru kwamba Yehova Mungu hajanikataa kwa sababu ya matatizo ya utu wangu. Kwa kujifunza Neno lake, nimeweza kurekebisha utu wangu na hivyo nimetumikia masilahi ya Ufalme wake kwa miaka ipatayo 60. Tangu utotoni, nimekuwa mpenda-farasi sana, na msaada wa Mungu katika kudhibiti utundu wangu mara nyingi umenikumbusha jinsi hatamu inavyoweza kutumiwa kudhibiti farasi.

Nilizaliwa karibu na ziwa maridadi lenye rangi ya buluu katika Mount Gambier katika Australia Kusini mwaka wa 1908. Wazazi wangu walikuwa na shamba la ng’ombe wa maziwa, nami nilikuwa binti mkubwa zaidi kati ya watoto wanane. Baba yetu alikufa sote tulipokuwa tungali wachanga sana. Hilo liliniachia daraka kubwa la kusimamia hilo shamba, kwa kuwa ndugu zangu wawili wakubwa zaidi walihitaji kufanya kazi nje ili kuletea familia mapato. Maisha katika shamba yalikuwa kazi ngumu yenye kudai mno.

Kujua Kweli kwa Mara ya Kwanza

Familia yetu ilikuwa ikihudhuria Kanisa Presbiteri, nasi tulikuwa washiriki wa kawaida wenye kufuata kanisa. Nilikuja kuwa mwalimu wa shule ya Jumapili na kuchukua kwa uzito lile jukumu la kufundisha watoto kile nilichoamini kuwa sawa kiroho na kiadili.

Katika 1931 babu yangu alikufa, na miongoni mwa vitu vyake vilikuwa vitabu kadhaa vilivyoandikwa na msimamizi wa wakati huo wa Watch Tower Society, J. F. Rutherford. Nilianza kusoma The Harp of God na Creation, na kadiri nilivyovisoma, ndivyo nilivyostaajabu zaidi kujua kwamba mambo mengi ambayo niliamini na nilikuwa nikifundisha watoto hayakuungwa mkono na Biblia.

Nilishtuka kujua kwamba nafsi ya binadamu si kitu kisichoweza kufa kamwe, kwamba watu walio wengi hawataenda mbinguni wafapo, na kwamba hakuna mateso ya milele katika moto wa helo kwa waovu. Pia nilifadhaika kugundua kwamba kushika sabato ya Jumapili kila juma si takwa la Kikristo. Kwa hiyo nilikabili maamuzi mazito: kushikamana na mafundisho ya kawaida ya Jumuiya ya Wakristo au kuanza kufundisha kweli ya Biblia. Haikunichukua muda mrefu kuamua kuacha kushirikiana na Kanisa Presbiteri.

Sasa Nikiwa Peke Yangu Sana

Familia yetu, marafiki, na watu niliokuwa nimewajua katika kanisa langu la zamani hawakufurahi hata kidogo nilipotangaza kusudi langu la kuacha kanisa na kuacha kufundisha shule ya Jumapili. Na walipogundua kwamba nilikuwa nikihusika na wale waitwao watu wa Judge Rutherford, hilo liliongezea tu porojo hiyo moto. Sikuondoshwa hasa katika kanisa, lakini wengi wa familia yetu na wale waliokuwa marafiki wangu wa zamani walikuwa baridi kunielekea, kwa kusema machache.

Kadiri nilivyojifunza na kuthibitisha maandiko yaliyoorodheshwa katika vitabu nilivyokuwa nikisoma, ndivyo nilivyoanza kuona uhitaji wa kuhubiri peupe. Nilijifunza kwamba Mashahidi wa Yehova huenda nyumba kwa nyumba, hiyo ikiwa sehemu ya huduma yao ya peupe. Lakini wakati huo hakukuwa na Mashahidi katika wilaya yetu. Kwa hiyo, hakuna mtu aliyenitia moyo au kunionyesha jinsi ya kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Nilijihisi nikiwa peke yangu sana.

Hata hivyo, amri ya Biblia ya kuhubiria wengine ilikuwa ikinirudia-rudia akilini, nikaamua ni lazima nianze kuhubiri kwa njia fulani. Baada ya kusali sana, niliamua kuanza kuzuru nyumba za jirani kuwaeleza tu yale niliyokuwa nimejifunza katika mafunzo yangu na kujaribu kuwaonyesha mambo haya katika Biblia zao wenyewe. Nyumba niliyozuru kwanza ilikuwa ile ya msimamizi wa shule ya Jumapili niliyofundisha awali. Itikio lake baridi na maelezo yake hasi kuhusu kuacha kwangu kanisa hakika hayakuwa mwanzo wenye kunitia moyo. Lakini nilihisi uchangamfu fulani na nguvu fulani ya kindani nilipokuwa nikitoka kwake na kuendelea kuzuru nyumba nyinginezo.

Hakukuwa na upinzani wa moja kwa moja hasa, lakini nilishangazwa na ubaridi wa ujumla wa washiriki wangu wa zamani wa kanisa nilipowatembelea. Kwa mshangao wangu na mtamauko, nilipata upinzani mkubwa zaidi kutoka kwa ndugu yangu mkubwa zaidi, ukinikumbusha maneno ya Yesu: “Mtasalitiwa na wazazi wenu, na ndugu zenu, na jamaa zenu, na rafiki zenu, . . . Nanyi mtachukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu.”—Luka 21:16, 17.

Nilikuwa nimekuwa mwendesha-farasi mwenye uzoefu nikiwa ningali na umri mchanga, kwa hiyo niliamua kwamba njia ya haraka zaidi ya kufikia nyumba za watu ingekuwa kupanda farasi. Hilo liliniwezesha kwenda mbali katika eneo la mashambani lililokuwa karibu. Lakini, alasiri moja farasi wangu alijikwaa na kuanguka kwenye barabara yenye kuteleza, nami nikavunjika vibaya fuvu. Kwa muda fulani, kulikuwa na wasiwasi kwamba singeokoka. Baada ya anguko hilo, barabara zilipokuwa na majimaji au yenye kuteleza, nilisafiri kwa farasi na kigari chepesi kikokotwacho na farasi chenye magurudumu mawili badala ya kupanda farasi.

Uwasiliano na Tengenezo

Muda fulani baada ya aksidenti yangu, kikundi cha wahubiri wa wakati wote, wanaoitwa mapainia sasa, walizuru wilaya ya Mount Gambier. Hivyo, kwa mara ya kwanza, niliweza kuongea ana kwa ana na waamini wenzangu. Kabla ya kuondoka, walinitia moyo kuandikia ofisi ya tawi ya Watch Tower Society na kuuliza jinsi ninavyoweza kushiriki katika kazi ya kuhubiri peupe kwa njia iliyopangwa kitengenezo zaidi.

Baada ya kuandikia Sosaiti, nilipokea vitabu, vijitabu, na kadi ya kutoa ushuhuda iliyokuwa imechapishwa ya kutumia kujijulisha milangoni. Nilihisi nikiwa karibu zaidi na ndugu na dada zangu wa kiroho kwa sababu ya mawasiliano kwa barua kutoka ofisi ya tawi. Lakini kikundi hicho cha mapainia kilipoondoka na kwenda mji mwingine, nilihisi nikiwa peke yangu sana kuliko wakati mwingine wowote.

Kwa sababu ya kuzunguka kwa kawaida nikitoa ushahidi kila siku—hasa kwa farasi na kwa kigari—nilikuja kujulikana sana katika wilaya. Na wakati uo huo, niliweza kushughulikia kazi zangu za shamba. Kufikia wakati huo familia yetu ilikuwa imeacha kupinga hali hii na haikufanya jitihada yoyote ya kuingilia mambo yangu. Kwa miaka minne nilitumika kwa njia hii nikiwa mtangazaji aliye peke yake, asiyebatizwa wa habari njema.

Mkusanyiko na, Hatimaye, Ubatizo

Katika Aprili 1938, Ndugu Rutherford alizuru Australia. Upinzani mkali wa makasisi ulifanya kandarasi ya kutumia Sydney Town Hall ifutwe. Hata hivyo, katika dakika ya mwisho, ruhusa ya kutumia Sports Grounds ilipatikana. Mipango iliyolazimika kubadilishwa hata ikathibitika kuwa yenye manufaa, kwa kuwa maelfu mengi zaidi ya watu yangeweza kutoshea katika Sports Grounds iliyokuwa kubwa zaidi. Wapatao 12,000 walikuja, upendezi wa wengi yaonekana ukiamshwa na upinzani wenye kuchochewa na makasisi kwa mkutano wetu.

Kuhusu ziara ya Ndugu Rutherford, mkusanyiko wa siku kadhaa ulifanywa pia katika kiunga kimoja cha Sydney kilichokuwa karibu. Ni huko ambako hatimaye nilifananisha wakfu wangu kwa Yehova Mungu kwa ubatizo wa maji. Je, waweza kuwazia shangwe niliyopata ya kukusanyika hatimaye pamoja na mamia ya ndugu na dada kutoka kotekote katika bara kubwa la Australia?

Kurudi Mount Gambier

Niliporudi nyumbani, nilijihisi kuwa peke yangu sana, lakini niliazimia kuliko wakati mwingine wowote kufanya niwezayo katika kazi ya Ufalme. Muda mfupi baadaye nilikuja kujua familia ya akina Agnew—Hugh, mke wake, na watoto wao wanne. Waliishi katika mji wa Millicent, kilometa 50 tu kutoka Mount Gambier, nami nilikuwa nikisafiri kilometa 50 kwenda, na kilometa 50 kurudi kwa farasi na kigari ili kuongoza funzo la kawaida la Biblia nao. Walipokubali kweli, upweke wangu ulipunguka.

Upesi, tulifanyizwa katika kikundi cha kutoa ushahidi kwa njia iliyopangwa kitengenezo. Kisha, kwa furaha, mama yangu akaanza kupendezwa akajiunga nami katika safari ya kwenda na kurudi ya kilometa 100 kujifunza na kikundi hiki kipya kilichotoka kufanyizwa. Tangu wakati huo, sikuzote mama alikuwa mwenye kutia moyo na mwenye msaada, ingawa ilikuwa ni miaka kadhaa kabla ya yeye kubatizwa. Sikuwa mpweke tena!

Kikundi chetu kidogo kilitokeza mapainia wanne, wasichana watatu wa akina Agnew—Crystal, Estelle, na Betty—na mimi. Baadaye, katika miaka ya mapema ya 1950, hao wasichana wote watatu walihudhuria Watchtower Bible School of Gilead. Walipewa migawo wakiwa wamishonari katika India na Sri Lanka, ambako wangali wanatumika kwa uaminifu.

Katika Januari 1941 utendaji wa Mashahidi wa Yehova ulipigwa marufuku katika Australia, kwa hiyo upesi tukachukua hatua. Tuliweka kila kitu tulichotumia katika huduma—fasihi, vinanda vyenye kubebeka, mahubiri ya Biblia yaliyorekodiwa, na kadhalika—katika sanduku kubwa. Kisha tukaweka sanduku hilo katika kibanda na kuleta nyasi kwa vigari kadhaa na kulizika sanduku ndani yazo.

Licha ya marufuku, tuliendelea kuhubiri nyumba kwa nyumba, lakini kwa tahadhari, tukitumia Biblia pekee kuzungumza na wenye nyumba. Nilikuwa nikificha magazeti na vijitabu chini ya tandiko la farasi na kuvitoa tu wakati upendezi wa kweli kwa ujumbe wa Ufalme ulipopatikana. Hatimaye, katika Juni 1943, marufuku iliondolewa, na kwa mara nyingine tena tuliweza kutoa fasihi peupe.

Migawo Mipya

Katika 1943, nilijitoa kuwa painia, na mwaka uliofuata nilitoka Mount Gambier kwenda kwenye mgawo mwingine. Kwanza, nilialikwa kutumika kwa muda mfupi kwenye ofisi ya tawi ya Sosaiti katika Strathfield. Baada ya mgawo huo, nilipokea kwa mfululizo migawo katika majiji madogo kusini mwa New South Wales na magharibi mwa Victoria. Hata hivyo, mmojapo migawo yangu yenye kuthawabisha kiroho zaidi ulikuwa katika kutaniko moja kubwa katika jiji la Melbourne. Nikiwa nimetoka mji mdogo wa mashambani, nilijifunza mambo mengi sana nikitumikia huko.

Katika mgawo wangu katika eneo la chini la wilaya ya Gippsland ya Victoria, mwandamani wangu wa upainia, Helen Crawford, nami tuliongoza mafunzo mengi ya Biblia na, kwa muda mfupi, kuanzisha kutaniko. Wilaya hiyo ilikuwa na eneo kubwa la mashambani, na kwa usafiri tulikuwa na gari moja zee ambalo halikutegemeka. Nyakati nyingine tuliliendesha, lakini mara nyingi tulilisukuma. Nilitamani farasi kama nini! Nyakati nyingine ningeweza kusema kwa ukweli: “Ningetoa kitu chochote (ila Ufalme) nipate farasi!” Katika miji mingi ya wilaya hiyo leo, kuna makutaniko yenye nguvu na Majumba ya Ufalme yaliyo mazuri.

Katika 1969, nilipokea mgawo wa kwenda Canberra, jiji kuu la Australia. Hapa palikuwa mahali pagumu na penye upendezi pa kutoa ushahidi, kwa kuwa mara nyingi tulikutana na wafanyakazi wa ubalozi mbalimbali wa kigeni. Ningali natumika hapa, lakini katika miaka ya majuzi nimekazia akili ushahidi wangu katika eneo la viwanda vya jiji hili.

Katika 1973 nilikuwa na pendeleo la kuhudhuria mikusanyiko mikubwa Marekani. Jambo jingine kuu la maisha yangu lilikuwa kuwa mjumbe wa mkusanyiko katika 1979 na kutalii Israeli na Jordan. Kuzuru mahali-mahali panapotajwa katika Biblia na kutafakari juu ya matukio yaliyotukia hapo kulikuwa ono lenye kugusa moyo kwelikweli. Niliweza kujionea jinsi mtu anavyohisi kuelea katika Bahari ya Chumvi, ikiwa na maji yayo mazito yenye chumvi, na katika ziara yetu ya Petra katika Jordan, nilipata fursa nyingine tena ya kupanda farasi. Jambo hilo lilinikumbusha zile siku za awali farasi waliponisaidia kufikia maeneo mbalimbali na ya mashambani nikiwa na ujumbe wa Ufalme.

Utumishi wa Wakati Wote Wenye Kuendelea

Tamaa yangu ya kuendelea na utumishi wa wakati wote licha ya kuzeeka imeendelezwa na maandalizi ya kipekee kama vile Shule ya Utumishi wa Painia na mikutano ya mapainia ambayo hufanywa wakati wa makusanyiko ya mzunguko, na vilevile kitia-moyo chenye kuendelea ambacho mimi hupokea kutoka kwa waangalizi wasafirio. Naweza kusema kwa kweli kwamba Yehova amehakikisha kwa fadhili kwamba siku zangu za kuwa peke yangu ni jambo lililopita.

Sasa nina umri wa miaka 87, na baada ya miaka ipatayo 60 ya kumtumikia Yehova, nina jambo la kutia moyo kwa wengine ambao huenda pia ni wasema-mambo waziwazi na wenye kujitegemea sana: Sikuzote nyenyekea kwa mwongozo wa Yehova. Yehova na atusaidie kudhibiti kusema kwetu waziwazi, na aendelee kutukumbusha daima kwamba ingawa twaweza kujihisi tukiwa peke yetu, hatatuacha kamwe.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki