Wewe Ungechaguaje Kitabu kwa Ajili ya Wanadamu Wote?
KAMA ungeweza kusoma kitabu kimoja kwa juma ujapokuwa na shughuli zile zote za kila siku zinazokupasa kufanya, ungeweza kusoma mabuku zaidi ya 3,000 katika muda wa maisha yako. Ingawa huenda hesabu hiyo ikaelekea kuwa ya kushangaza, hiyo ni kitone kidogo tu katika ndoo unapofikiria kwamba kila mwaka vitabu ambavyo ni zaidi ya mara 10 za hivyo vinachapishwa kila mwaka katika United States peke yake. Na hiyo hata haitii ndani maelfu ya vitabu vya masomo bora ambavyo kila mtu mwenye elimu anapaswa kuwa amekwisha kuvisoma.
Ni wazi kwamba vitabu vinapohusika, maoni yaliyotolewa karibu miaka 3,000 iliyopita yanafaa leo kuliko wakati mwingine wo wote: “Hakuna mwisho wo wote wa kutunga vitabu vingi; na kusoma sana huuchosha mwili.”—Mhubiri 12:12.
Lakini kati ya mvuvumko huo wa vitabu, je, kuna kimoja chenye thamani na maana sana hivi kwamba kinatokeza kati ya vingine vyote kuwa kitabu ambacho kila mtu anapaswa kusoma? Je, kuna kimoja kinachovipita vizuizi vya kitaifa, kitamaduni, na kilugha kisha kinastahili kuwa kitabu kwa ajili ya wanadamu wote?
Kusudi la kuchagua tunayosoma halipasi kuwa kujipatia elimu fulani tu kwa sababu mwishowe mambo tunayosoma yanaelekeza mawazo yetu, maadili, na uamuzi wetu kwa njia fulani. Walimu, wazazi, na watu wengine wameshughulisha fikira zao wakichagua mambo yanayopasa kusomwa, zamani na hata sasa. Uchunguzi mwingi na mahoji yamefanywa kutaka kujua ni mambo gani yanayohitajiwa kabisa kusomwa, na matokeo yameonyesha mambo mengi.
Uchaguzi wa Wataalamu
Mwaka 1890 mchapishaji wa kitabu fulani alizungumza habari hiyo na waandikaji wengi mashuhuri wa siku zake. Akawaomba wavitaje vitabu walivyoona ni vya maana zaidi. Matokeo yakawa nini? “Biblia, maandishi ya Shakespeare na ya Homer ndiyo yaliyopendelewa zaidi na watu wenye kisomo katika karne ya kumi na tisa,” ndivyo kinavyoripoti kitabu kimoja cha marejezo. “Tena,” kinaongezea, “mfuatano wa vitabu hivyo kulingana na ubora wavyo ungebaki hivyo hivyo usibadilike hata leo.”
Uchunguzi wa karibuni zaidi umekubaliana na jambo hilo. Kwa mfano, katika Septemba 1982, gazeti Time lilichapisha jibu la wataalamu, wanahistoria, na wanamaktaba wanane mashuhuri kwa ulizo hili, “Ni vitabu gani vitano ambavyo kila mtu mwenye elimu anapaswa kuwa amekwisha kuvisoma? ” Ingawa wataalamu hao hawakukubaliana na mambo yote, watano kati ya hao wanane—kwa wazi wakiwa ndio wengi zaidi—waliitia Biblia ndani ya mapendekezo yao. Kwa habari ya uchunguzi mwingine wa namna iyo hiyo, kichapo Psychology Today kinaripoti kwamba “kati ya vitabu 165 ambavyo vilitajwa, Biblia ilipata kura nyingi zaidi: 15. Hakuna kitabu kinginecho kilichoikaribia.”
Yenye kupendeza hasa ni mambo yaliyoonekana katika uchunguzi wa maoni ya watu ulioendeshwa na gazeti The Korea Times ili kujua jinsi watu wasio Wakristo wa taifa hilo wanavyoyaona makanisa ya Kikristo. “Uchunguzi wa maoni ulionyesha kwamba Wakristo, wakilinganishwa na wasio Wakristo, wanajiona zaidi, wanajinyakulia pesa kwa pupa zaidi na kutokudhamiria wajibu wao,” likasema gazeti hilo. Lakini, ripoti hiyo inaendelea kusema: “Kwa habari ya ukosefu wao wa imani, asilimia 70 ya wenye kutoa maoni wanaihesabu Biblia kuwa yenye ubora mkuu.”
Uchaguzi wa Mwisho
Uchunguzi mwingi wa namna hiyo unaweza kutajwa kuonyesha kwamba, tena na tena, Biblia imetajwa kuwa ndicho kitabu kinachopita vinginevyo vyote. Kwa sababu mbalimbali, imekuwa ndio uchaguzi wa mwisho kati ya vitabu vinginevyo, zamani na hata sasa, katika nchi za mashariki na hata za magharibi.
Ingawa hivyo, jambo la maana zaidi ni kwamba, maoni yako binafsi ni nini? Je! unaiona Biblia kuwa ya kizamani na isiyo na thamani kubwa katika kutatua matatizo ya leo katika ulimwengu wetu wa kisasa ulio wa kisayansi? Je! unaiona kuwa kitabu cha Wazungu ambacho si cha maana sana kwako? Au Biblia ina ujumbe ambao watu wote leo wanahitaji kuujua? Je! inahusiana vizuri na matatizo yanayokabili watu kila mahali leo? Je! kweli Biblia ni kitabu kwa ajili ya wanadamu wote?