“Masuala ya Kisheria Katika Tiba ya Kutia Damu Mishipani”
UGONJWA ulio wa karibuni zaidi na hatari zaidi wa karne ya ishirini, UKIMWI.” Hivyo ndivyo Dakt. L. A. Lasky (Mwanasayansi Mkuu, wa Shirika la Genentech) alivyoeleza tatizo lililofanya kuwe na mkutano Septemba 19-20, 1985, katika Washington, D.C., U.S.A.
Inaelekea unajua kwamba UKIMWI (Ukosefu wa Kinga Mwilini, au AIDS) umesemwa kuwa unaweza kutokana na dawa zilizotengenezwa kwa kutumia damu au kwa kutiwa damu mishipani. Programu iliyochapishwa ilieleza hivi:
“Hakuna tatizo la kiafya tunaloweza kukumbuka kuwa limetokeza mazungumzo mengi na woga mwingi kati ya watu kama hili. Visa vya UKIMWI huenda vikawa maradufu muda wa mwaka mmoja unaokuja, na kufikia Waamerika milioni moja [na wengine zaidi wasiohesabika katika nchi nyinginezo] huenda wakaambukiwa. Basi, hatia ya kuweza kushtakiwa kisheria kwa sababu ya UKIMWI ni kubwa.”
Jumla ya madaktari, wasomi wa sheria, na wafanya kazi wa benki ya damu karibu 200 walikusanyika kwa ajili ya mkutano unaohusu “Masuala ya Kisheria Katika Tiba ya Kutia Damu Mishipani.” Kazi za wengi wao zilihusu kutia damu mishipani. Lakini pia hesabu fulani ya Mashahidi wa Yehova walihudhuria. Acheni tuwaeleze visehemu fulani vya mambo yaliyofunuliwa na wasemaji.
Mambo makubwa yaliyohangaikiwa ni hatari ya kueneza UKIMWI kupitia damu na hatari za kisheria kwa watu wa namna yao wanaokusanya, kutayarisha, au kuuza damu. Hangaikio hilo la pili lilionekana wazi katika hotuba ya kwanza, iliyohusu ‘tengenezo, mipango ya kiuchumi na usimamizi wa hifadhi ya damu.’ Dakt. P. J. Schmidt alisema usimamizi huo ni wa tangu miaka ya 1600. Denis tabibu Mfaransa alihusika “katika kesi ya kwanza ya kutia damu mishipani kwa njia isiyofaa” katika historia, kwa sababu ya “kumpa damu,ya mwana-kondoo kijana mmoja mwanamume, akafa.” Je! usimamizi wa matumizi ya damu ungali unahitajiwa? Schmidt aliungama hivi: “Mimi nafikiri kuna mengi yanayofanyika bila kujulikana. Hata hivyo tendo lenyewe la kutia damu mishipani ni tatizo kubwa sana la kila siku. Katika nchi hii damu inatiwa mishipani mara nyingi sana sana kwa kusudi la kuchunguza viini vya magonjwa katika damu na kujua jinsi yanavyoweza kuzuiwa yasienee, na mara nyingi uchunguzi huo unafanywa bila kufuata kanuni ya kisheria.”
Baadaye, Dakt. Paul Ness (wa Hospitali ya Johns Hopkins) alihutubu juu ya “Hitilafu Zinazoweza Kutokea kwa Kutia Damu Mishipani.” Yeye aliona kwamba “ni vigumu sana katika muda wa nusu saa [tu] kueleza hitilafu zote zinazoweza kutokea kwa kutia damu mishipani.” Kwa kweli yeye alikusudia kuonyesha slaidi yenye kutoa onyo ambalo lingekuwa ni kama kisingizio tu chenye kusema “Onyo, hitilafu zifuatazo zinaweza kuja kwa kutiwa damu mishipani,” akiorodhesha “karibu mambo 50 mbalimbali . . . [Lakini nilijua kwamba orodha hiyo haingekuwa kamili kwa vyo vyote.”
Dakt. Johanna Pindyck (wa Programu Kuu Inayohusiana na Damu New York) alisema kwamba ‘ugonjwa wa kufura ini usio wa aina ya A wala B ndiyo maradhi yenye kusumbua zaidi yanayoambukia kwa kutiwa damu mishipani.’ Aina hiyo ya ugonjwa wa kufura ini “inawaziwa kuwa inasababishwa na viini visivyopungua viwili, lakini umbo lavyo halijatambuliwa vizuri. Uchunguzi umekuwa ukifanywa muda wa miaka mingi—kufikia miaka 10 mpaka 15 hivi—lakini bado hatujakigundua kisababishi.” Kwa habari ya njia bora zaidi inayopatikana ya kuchunguza damu ionekane kama ina ugonjwa wa aina hiyo, mwanamke huyo alieleza hivi: “Mimi ningesema, labda asilimia 10 ya damu iliyopo ndiyo inayochunguzwa kwa sasa, au labda kiasi kichache kuliko hicho.”
Walipokuwa wakiuzungumza UKIMWI Dakt. Pindyck na wengine walitoa maoni yenye tumaini la kwamba uchunguzi wa kupima damu ambao umekuwa ukifanywa nyakati za sasa unawezesha benki za damu zikaribie kukomesha “utiaji damu mishipani kuwa chanzo cha ambukizo la UKIMWI.” Je, zinaweza? Baadaye Dakt. Laskey alisema kwamba uchunguzi wa sasa ‘unagharimu sana, ni hatari kufanywa, na hauwi sahihi kabisa.’ Namna gani ikitumiwa njia fulani mpya anayoona ni bora? Yeye alieleza juu ya majaribio yaliyofanywa katika wagonjwa wenye UKIMWI au maradhi yenye kutatiza sana yanayohusiana na UKIMWI. Katika hesabu fulani kati yao, uchunguzi uliofanywa ulishindwa kuugundua UKIMWI katika maradhi hayo. ‘Hakuna mtu [yaani, hakuna wo wote wa uchunguzi uliofanywa ungaliupata’ [au kuugundua] UKIMWI, akasema.
Basi unaweza kuelewa ni kwa nini watu wengi wanafikiria kuhifadhi akiba ya damu yao wenyewe au kukubali damu ya rafiki tu au mtu wa ukoo. Lakini Dakt. Joseph Bove (wa Hospitali ya Yale-New Haven) alipinga jambo hilo, akishikilia kwamba lingegharimu sana na kuleta upungufu mwingi. Aliongeza hivi: “Kimoja cha visababishi vikubwa vya vifo vinavyotokea kwa sababu ya kutia damu mishipani ni usimamizi mbaya—kuingiza damu isiyofaa ndani ya mtu. Naona haya . . . [kusema] kwamba mwaka 1985 tunashindwa kumtia mgonjwa painti ya damu inayomfaa yeye mwenyewe, ingawa tuna elimu nyingi ya ufundi, tuna makompyuta na vitu vinginevyo. Lakini ukweli ni kwamba hatuwatii damu inayowafaa, na hivyo ndivyo tunavyoua watu.”
Basi, waliokuwapo mkutanoni waliongea sana juu ya masuala ya kisheria. Benki ya damu inaweza kujilindaje isifanyiwe kesi za matumizi mabaya ya damu? Kwa kuwa sasa njia za kuchunguza damu zinapatikana, ikiwa uchunguzi wa damu ya mchangaji unaonyesha wazi kwamba damu yake ina viini vya UKIMWI, je, benki ya damu inapasa kuwajulisha habari hizo wale waliopokea damu yake miaka michache iliyopita? Dakt. Schmidt (mkurugenzi wa benki moja ya damu) alisema: “Kwa sasa mimi sipendelei kwamba watu wajulishwe. Sisi tunafanya yale yatupasayo, si zaidi ya hayo.” Je, mahakama zinapasa kuombwa zitoe amri kulazimisha kwamba damu itiwe ndani ya wenye kuikataa, kama Mashahidi wa Yehova wenye kuikataa kwa sababu za kidini?
Kwa kweli, Mashahidi wa Yehova walifikiriwa katika hotuba ya Dakt. William Dornette yenye kusema, “Masuala ya Kutokujali Wajibu na Kulaumika.” Alieleza kwamba msingi mmoja unaofanya Mashahidi wakatae damu “ni sura hii ya kitabu cha Mwanzo [9:3, 4]. Nayo inasema wazi kwamba ‘nawapeni hivi vyote. Bali nyama pamoja na uhai, yaani, damu yake, msile.’ ” Ni kwa kadiri gani msimamo huo ulivyo wa akili, na Mashahidi wana haki gani ya kisheria kukataa damu?
Dornette, daktari wa tiba na sheria pia, alishauri hivi: “Kwa miaka mingi sana washiriki wa imani ya Mashahidi wa Yehova wameonwa kuwa ni washamba wasiojua wanalofanya, kwa sababu madaktari wamekuwa wakijiona sana kuwa wamesomea kazi yao na wanajua kila kitu. Jambo la kwanza tunalopaswa kutambua ni kwamba [Mashahidi] wanafuata dini kwa ndani. Pili, wao ni raia wa Amerika . . . Tatu, wao wana haki ya kufuata dini, na wanapendezwa na kupata nafuu . . . Wanaamini utibabu. Nami nafikiri ni lazima tuheshimu haki ambazo kila mmoja wao anazo kufuata dini akiwa na uhuru.” Aliongeza hivi: “Kushindwa kuomba idhini ni kosa kama la kushambulia na kujeruhi mtu. Kushindwa kuomba idhini ya kutia mtu damu ni kosa kama la kushambulia na kujeruhi mtu. . . . Ukiomba mgonjwa atoe taarifa ya kwamba amekataa, umejiondolea mwenyewe uwezekano wa kulaumika katika mahakama.”
Msemaji mwingine, msomi wa sheria Susan Lentz, alikazia jambo hilo, akisema: “Ni jambo la maana kuelewa kwamba idhini yenye ushahidi inakuwa ya maana ikiwa tu unatambua kwamba jambo linalohusika si haki ya kutoa tu idhini, bali haki ya kukataa pia kutoa idhini.” Mwanamke huyo aliongeza kwamba “katika mwaka huu huu kumekuwa na maamuzi matatu au manne [ya mahakama] kudhubutisha kwamba wagonjwa walio Mashahidi wa Yehova wana haki za kukataa kutiwa damu.” Alimalizia hivi: “Wakati mambo ambayo mmekuwa mkisikia siku moja na nusu zilizopita kuhusu UKIMWI na matatizo yanayohusiana nao yanapozidi kuwa tatizo kubwa, angalau katika akili za watu kwa ujumla, matatizo yanayohusiana na kukataa huenda pia yakaongezeka.”
Utapata habari zaidi zenye mafaa juu ya UKIMWI katika Awake! la Aprili 22, 1986.
[Sanduku katika ukurasa wa 26]
Je, wagonjwa wanaweza kutumaini kwamba benki ya damu itaweza kugundua damu iliyochafuliwa na viini vya UKIMWI? Dakt. Myron Essex, mwenyekiti wa idara ya bayolojia ya kansa kwenye Shule ya Harvard ya Afya kwa Watu Wote, alisema majuzi hivi: “Inaelekea kabisa kuwa kwamba uchunguzi unaofanywa haugundui kiasi kinachozidi asilimia 90, nami ningekisia kwamba unagundua kiasi cha asilimia 75 mpaka 80 hivi, wala si zaidi. Ningestaajabu sana kama si zaidi ya hapo.”—The New York Times, Oktoba 4,1985.
[Sanduku katika ukurasa wa 27]
“Uchunguzi mpya wa kupima damu, uliokubaliwa mwezi Aprili uliopita na ambao unatumiwa na benki zote za damu, unagundua kiini kile tu kinachohitilafiana na kiini cha UKIMWI, HTLV-III. jambo la kusikitisha ni kwamba hauwagundui watu ambao wana kiini chenye ambukizo la UKIMWI ndani ya damu yao lakini ambao damu yao bado haijatokeza kiini cha kuhitilafiana na kile cha UKIMWI. . . . Basi, hesabu ndogo lakini inayofaa sana kufikirwa ya watu karibu milioni moja walio na kiini cha UKIMWI ndani ya damu yao hawataonekana wakiwa na viini vinavyohitilafiana na hicho cha ugonjwa huo watakapokuwa wakipimwa kama kawaida kwenye benki za damu.”—Sanford F. Kuvin, M.D., Jerusalem, Novemba 17,1985.