Biblia—Ina Mafaa Kwako
“EE MWANADAMU, yeye amekuonyesha yaliyo mema,” ndivyo akaandika mtu wa Mungu miaka zaidi ya 2,700 iliyopita. (Mika 6:8) Lakini je, hayo yangali ni “mema” au yenye mafaa kwetu sisi katika siku zetu za kisasa?
“Biblia iliandikwa muda mrefu kabla mtu ye yote hajajua lo lote juu ya saikolojia ya kisasa na ukuzi wa maoni ya akilini kati ya watu wa jinsia tofauti,” anasema Dakt. Chesen. “Hata ikiwa makusudi ya waandikaji wayo yalikuwa mazuri kabisa, haiwezi kuwa waliyafikiria mambo hayo ya maana. Na hata hivyo Biblia na wafasiri wayo wanasema mengi juu ya maadili na/au amri.”
Wazo hilo lingalikuwa sawa kama Biblia ingekuwa zao la fikira za mwanadamu. Lakini kama ilivyoonyeshwa katika toleo letu la Aprili 1, 1986, Biblia si neno la mwanadamu bali la Mungu. Jambo hilo la maana haliwezi kusahauliwa mbali. Kwa sababu gani? Kwa sababu maarifa ya Mungu hayawekewi mipaka na wakati wala hali, kama inavyokuwa kwa maarifa ya mwanadamu, wala hayabadilikani. Akiwa ndiye Muumba wa wanadamu, Mungu anajua kabisa kabisa jinsi tulivyoumbika na yale yanayotufaa zaidi sisi. Kwa hiyo kwa kufaa mtume anasema: “Andiko lote liliongozwa na Mungu na ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu apate kuwa na uwezo wa kutosha, aliye tayari kabisa kwa kila kazi njema.”—2 Timoteo 3:16, 17, NW.
Basi, namna gani yale mabadiliko makubwa sana ambayo yametukia katika nyakati zetu za kisasa? Je! maoni yaliyoko si kwamba sisi tunaishi katika kizazi chenye uhuru na mwangaza mwingi zaidi wa maarifa? Je! nyingi za zile pingu za kimapokeo hazikutupiliwa mbali na jamii ya watu kwa ujumla? Ni kweli, lakini kujapokuwa na maarifa yaliyoongezeka na “uhuru” unaosemekana umepatikana karibuni, mahitaji ya msingi ya mwanadamu na umbo lake havijabadilika bado. Kwa ndani, sisi tungali jinsi ile ile. Tungali tuna tamaa za kula, kunywa, kulala, kuzaana, na kuabudu, kama walivyokuwa babu zetu. Tungali tuna uhitaji wa kupendwa na kuonyeshwa shauku, na tunataka kuwa wenye furaha. Tungali tunahitaji kuishi maisha zenye kusudi.
Kanuni za Biblia zinashughulikia mahitaji hayo. Zaidi ya hilo, mafundisho ya Biblia ni kwa faida yetu, hata katika siku hizi za kisasa. Isitoshe, matokeo yanayopatikana kwa kufuata mashauri ya Biblia ni bora kuliko yo yote yanayopatikana kwa njia nyinginezo. Acheni tuchunguze kwa ufupi jinsi hilo lilivyo kweli katika mambo ya adili, mipango ya kiuchumi, na afya.
Biblia na Maadili
Moja la mabadiliko yaliyo makubwa zaidi katika nyakati zetu za kisasa limekuwa kuhusiana na maoni juu ya adili. Mazoea ambayo hapo kwanza yalionwa kuwa ya kuchukiza sana yamekubalika. Wanawake wanaozaa watoto bila ndoa hawaepwi na jamii ya watu kama hapo kwanza. Watu wa jinsia moja wenye kulalana wanatetea waziwazi “haki” zao. Maoni yanayoshikiliwa mahali pengi ni kwamba hakuna mtu aliye na haki kulalamika wala kuingilia mazoea yo yote yanayofanyika kati ya watu wazima waliokubaliana. Na viwango vya Biblia vinakataliwa kuwa vyenye kufuata mtindo wa siku za Malkia Viktoria.
Lakini viwango vya Biblia viliwekwa na Mungu muda mrefu kabla ya karne ya 19, kile kizazi cha Malkia Viktoria wa Uingereza. Navyo vinaendelea kuthibitika kuwa vyema kwa wanadamu. Hakika hilo linaweza kuonwa wakati mtu anapofikiria kwamba ile “adili mpya” imetokeza hesabu yenye kuongezeka sana ya talaka, utoaji mwingi wa mimba, kipuku cha mimba za vijana matineja, na namna nyingi sana za magonjwa yanayoambukizwa kwa kufanya ngono. Hayo ni matatizo yenye gharama kubwa, yenye kudhoofisha, na hata kuleta kifo. Je haingefaa zaidi kufuata shauri la Biblia kuhusu ngono, usafi wa adili, na uaminifu katika ndoa? —Mithali 5:3-11, 15-20; Malaki 2:13-16; Waebrania 13:4; 1 Wakorintho 6:9, 10.
Angalia hasa jinsi jambo hilo lilivyo kweli kuhusiana na ugonjwa mmoja tu, kama ulivyoonyeshwa katika ripoti kutokana na gazeti The New York Times: “ ‘UKIMWI unaendelea kuenea haraka sana kati ya wale walio katika vikundi vyenye kuelekea kupatwa nao, lakini si nje ya vikundi hivyo,’ akasema Dakt. David J. Sencer, Kamishna wa Afya Mjini New York. “Wale wanaoelekea kupatwa na ugonjwa huu ni kutia ndani watu wanaolalana na wale wa jinsia yao, na wanaume wa jinsia ya kiume na ya kike pia; wenye kutumia dawa za kulevya kwa kuziingiza mishipani; . . . wale wanaopokea damu kutokana na watoaji walioambukiwa na ugonjwa, na wenzi wa ngono au watoto wa wale walio na ugonjwa wa UKIMWI.”
Kwa kweli, ni jambo jipi la akili zaidi —dakika chache za raha haramu, mara nyingi zikiambatana na woga na wasiwasi, au dhamiri safi na hali ya kujiheshimu? Ni jambo jipi linaloleta furaha na uradhi wa kudumu—ngono ya muda mfupi ikiwa na uwezekano wa kupatwa na matokeo yenye msiba, au kujifunga katika wajibu thabiti wa kuwa na ndoa safi ambayo Biblia inafundisha?
Biblia na Matatizo ya Kijamii
Si watu wengi wanaiona Biblia kuwa yenye utatuzi kwa matatizo ya kiuchumi. Hata hivyo, kufuata viwango vyayo kunaweza kukuongezea chakula chako. Kwa jinsi gani?
Mara nyingi, kiasi kingi cha mapato ya mtu kinatumiwa ovyo-ovyo. Kufuata sana mashauri ya Biblia kutahifadhi pesa hizo zitumiwe kwa makusudi yenye mafaa. Kwa mfano, zoea moja ambalo mara nyingi linaongoza kwenye umaskini ni lile la kunywa kupindukia. Mamilioni ya watu wakiisha kutia mishahara yao mikononi, wanaelekea kwenye nyumba za pombe au vileo. Katika visa vingi, wanaondoka huko bila pesa za kutosha kulipia gharama mbalimbali au kutolea jamaa zao chakula cha kutosha. Nyakati nyingine wanalazimika kukopa pesa ili wapate riziki. Kwa hekima, Biblia inakataza unywaji wa kupita kiasi; inatetea hali ya kuwa na kiasi.—Mithali 23:20, 21, 29, 30; 1 Timotheo 3:2, 3, 8.
Ndivyo ilivyo kwa wale wanaoifuata ile tabia ya kuvuta sigareti au kutumia vibaya dawa za kulevya. Lo, tabia hizo zinagharimu kama nini! Na jinsi ilivyo vigumu kuziacha! Mfano mzuri ni barua hii aliyoandikiwa msaikolojia Joyce Brothers, kama ilivyochapishwa katika gazeti New York Post: “Mimi nilianza kutumia kasumba kwa sababu niliona raha na wengi wa rafiki zangu walikuwa wakiivuta puani wakati wa miisho ya juma. Basi, hiyo inanizuia mambo yote mema maishani mwangu nami naona vigumu sana kuiacha. Mimi ni mama mwenye watoto wawili na ninaogopa sana kwamba nisipoweza kuiacha karibuni, wao wataumia. Ninaitumia mara mbili kila siku. Nimelemewa na madeni mengi, maskini mimi.”
Mtumiaji mwingine wa dawa za kulevya aliandika hivi: “Sisi wawili, mume wangu na mimi, ni watu ambao tumefaulu katika kazi zetu za maisha na tumekuwa tukitumia kasumba kwa miaka mitatu. Hapo kwanza ilitufurahisha sana lakini sasa imekuwa zaidi na zaidi jambo la kutushughulisha sisi. Kwa kweli, imeanza kuchukua muda mwingi wa maisha zetu. Sasa sisi tuna madeni kwa sababu tabia zetu zinatuletea hasara. Sisi wote wawili tunalevywa nayo kweli kweli. Siku nyingine nyingine ndoto tunazotiwa nayo hazikomi kamwe.”
Wavutaji tumbaku pia wanaumizwa kiuchumi na tabia yao, ingawa labda si kwa kadiri moja na dawa za kulevya. Ripoti ya sasa katika gazeti Modern Office Technology inasema: “Watu wasio wavutaji tumbaku ambao wanatafuta kazi wataelekea zaidi kuajiriwa kuliko wale waliohitimu kama wao wanaovuta tumbaku, kulingana na matokeo ya uchunguzi yaliyojulishwa hivi karibuni katika taifa zima Uchunguzi huo, uliotegemea mahoji yaliyofanywa pamoja na manaibu wasimamizi na wakurugenzi wa wafanya kazi wa mashirika makubwa zaidi Amerika . . . ulifunua kwamba waajiri wa siku hizi wanapendelea sana sana watafutaji kazi ambao hawavuti tumbaku.” Kwa sababu gani? Kwa sababu, kama ilivyoonyeshwa katika uchunguzi wa baraza fulani kuvuta tumbaku kunaongeza gharama za kiafya za taifa, kutia ndani gharama za kitiba na kukosesha matokeo katika kazi, karibu dola bilioni 65 kwa mwaka—zinazolingana na dola 2.17 kwa kila kifurushi cha tumbaku kinachouzwa!
Ndiyo, mtu anasaidika kiuchumi kwa kufuata tu shauri hili la Biblia: “Na tujitakase nafsi zetu na uchafu wote wa mwili na roho.” (2 Wakorintho 7:1) Na ndivyo ilivyo kwa wale ambao, kwa kufuata kanuni za Biblia, wanajiepusha na namna zote za kucheza kamari. (Isaya 65:11, 12; Luka 12:15) Zaidi ya hilo, wale wanaofuata sana kanuni za Biblia wanathawabishwa sana na waajiri kazi kwa sababu ya unyofu wao, ukamilifu, na bidii yao, na wanaelekea kuwa ndio wa kwanza kuajiriwa na wa mwisho kufutwa kazi.— Wakolosai 3:22, 23; Waefeso 4:28.
Biblia na Afya
Kwa kuwa leo sisi tumeendelea sana kitiba, je! shauri la Biblia limepitwa na maendeleo hayo? Uhakika ambao umestaajabisha wachunguzi ni jinsi Biblia ilivyo sahihi na yenye kulingana na maarifa ya kisasa kuhusiana na mambo ya tiba na afya, ingawa iliandikwa katika wakati ambao ushirikina ulikuwa tele na ujuzi ulikuwa haba juu ya matibabu ya kisasa, au hata juu ya viini vya magonjwa.
Bila shaka, matatizo ya kiafya ni mengi kujapokuwa na sayansi ya kisasa ya tiba. Hata hivyo, mashauri ya Biblia yanaendeleza afya iliyo bora zaidi. Kama ilivyokwisha kusemwa, kufuata kanuni za Biblia kunatulinda na mazoea na magonjwa yanayoharibu sana afya yetu. Pia, mashauri hayo yanasaidia kuleta nafuu katika afya yetu ya akili. Biblia inayatambua matokeo ambayo mielekeo ya akilini na maoni ya moyoni yanatokeza katika mwili. (Mithali 14:30) Kwa hiyo inatuelekeza tuache kuwa na mielekeo na maoni ya moyoni yenye kudhuru, na kutusaidia tuibadilishe na sifa zenye mielekeo mizuri, zenye kujenga.
Angalia shauri lililotolewa kwenye Waefeso 4:31, 32: “Uchungu wote na ghadhabu na hasira na kelele na matukano yaondoke kwenu, pamoja na kila namna ya ubaya; tena iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane.” Ndiyo, Biblia inakazia badiliko la kuacha utu wenye uharibifu na madhara ili kuwa na utu mpya wa Kikristo wenye afya. (Waefeso 4:20-24; Wakolosai 3:5-14) Inatusaidia tuonyeshe wazi tunda la roho ya Mungu: “upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujiweza.” (Wagalatia 5:22, 23) Biblia inaandaa chakula chenye afya ambacho akili na moyo vinaweza kula na kuwa na amani.—Mithali 3:7, 8; 4:20-22; Wafilipi 4:6-8).
Tena, wale wanaoishi kwa kufuata maagizo ya Biblia hawajihusishi katika uhalifu, ghasia, fujo za kuasi, wala mambo mengine yanayoleta madhara ya kimwili. Wao wana dhamiri njema, ambayo inasaidia sana kudumisha nia yenye furaha na afya nzuri ya kimwili. (1 Petro 3:16-18) Zaidi ya hilo, wale wanaotumia mashauri ya Biblia wanafurahia maisha ya kinyumbani yaliyo machangamfu, yenye kuthawabisha, yenye furaha pamoja na uhusiano wenye amani na wengine.
Ndiyo, hakika Biblia ina mafaa kwa siku zetu. Jambo hilo linaonekana wazi katika maisha za mamilioni ya watu leo wanaozitumia kweli kweli kanuni zayo. Nayo inaweza kukusaidia wewe. Unaalikwa uyajaribu mafundisho yayo kwa kuyatumia katika maisha yako. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukuonyesha njia.