Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Je! Mkristo aliye na matumaini ya kidunia anaweza kusemwa kuwa ni sehemu ya “mkutano mkubwa” sasa, kwa sababu yeye hajaokoka bado ile ‘dhiki kubwa’?—Ufunuo 7:9, 14.
Ndiyo, inafaa kumsema hivyo kwa sababu ya mataraja aliyo nayo.
Ufunuo sura ya 7 unataja vikundi viwili. Cha kwanza ni wale 144,000 “waliotiwa muhuri katika kila kabila ya Waisraeli.” (Ufunuo 7:4) Kulinganisha Ufunuo 14:1-5 kunaonyesha kwamba wale 144,000 ‘wananunuliwa katika nchi,’ ili wawe “malimbuko kwa Mungu.” Basi, hao ndio watakaotawala mbinguni pamoja na Kristo. (Wagalatia 6:16; 2 Timotheo 4:18) Kikundi kile cha pili ni “mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu,” ambao ‘unatoka katika dhiki ile iliyo kuu.’
Katika habari zinazozunguka, Ufunuo 7:9-17 unaonyesha waokokaji wa kidunia wa dhiki inayokuja. Kwa hiyo mtu mwenye kutaka kudai mambo kupita kiasi angeweza kusema kwamba maneno “mkutano mkubwa” yanawahusu tu watu watakaokuwa wameokoka dhiki hiyo. Lakini je! kuna uhitaji mkubwa wa kusema ni hao tu? Hatuamini hivyo. Kwa wazi, wale watakaookoka watakuwa walilazimika kuwa wamekwisha kukusanywa kabla ya ile ‘dhiki kubwa’ ili waweze kustahili kuokoka. Hivyo, sisi tumeyatumia maneno “mkutano mkubwa” kwa Wakristo washikamanifu ambao wakati huu wanatumikia Yehova Mungu wakiwa na taraja la kuokoka na la ‘kuongozwa kwao kwenye chemchemi za maji yenye uhai duniani. (Ufunuo 7:17) Mmoja wa “mkutano mkubwa” akifa sasa, kabla tu ya ile ‘dhiki kubwa,’ kuna kila sababu ya kutazamia afufuliwe kwenye uzima duniani.
Mambo kama hayo yanaweza kusemwa juu ya maneno “kondoo wengine.” Katika Yohana 10:7-16, Yesu alisema kwanza juu ya “kondoo” wake, tunaowaelewa kuwa ni “kundi dogo” lililokusudiwa uzima wa kimbingu. Ndipo Yesu aliposema: “Kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili [la kimbingu], na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja.” Mara nyingi sisi tumetoa ushuhuda wa Kimaandiko kutambulisha kwamba “kondoo wengine” ni wale ambao taraja lao ni uzima wa kidunia.—Luka 12:32.
Huenda mtu akawaza hivi: Yesu alikuwa akielekeza kwenye mkusanyo wa wakati ujao wa “kondoo wengine,” kwa hiyo maneno hayo yanatumika kwa wale tu ambao, baada ya Yesu kusema hivyo, wangelikubali tumaini la Kibiblia la uzima wa milele duniani. Lakini, inaonekana kuwa si lazima kuyafanya maneno hayo yatumike hivyo tu, kama kwamba Yesu alikuwa akifafanua mambo kulingana na vile yanavyofuatana kulingana na tarehe au mfululizo. Tunaamini kwamba yeye alikuwa akikazia kwamba ndiye mchungaji wa kondoo waliounganishwa kwa umoja. Watu fulani wenye mfano wa kondoo wanaingia katika zizi ili waende mbinguni. Kuna kondoo wengine pia watakaomkubali yeye kuwa mchungaji; wao watakuwa katika umoja pamoja na wale waliotajwa kwanza. Kwa kuwa na maoni hayo, maneno “kondoo wengine” yanatia ndani wanaume wenye imani waliokufa kabla Yesu hajafungua njia ya kwenda mbinguni, watu kama Noa, Abrahamu, Ayubu, Daudi, na Yohana Mbatizaji. (Mathayo 11:11; Matendo 2:29; Waebrania 10:19, 20) Wakati hao watakapofufuliwa katika mfumo mpya wa mambo, wataweza kumkubali yule Mchungaji Mwema wawe na taraja la uzima wa kidunia usio na mwisho wakiwa pamoja na wale wengine wa “kondoo wengine” wa Yesu.