‘Sijapata Kusoma Cho Chote Kinachofanana Nacho’
KITABU Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation kimesaidia wengi waelewe waziwazi zaidi jinsi uhai ulivyofika hapa duniani na unakoelekea. Mtu mmoja aliandika hivi: “Mimi nina umri wa miaka 78 na nimekuwa nikisoma tangu nilipokuwa na miaka miwili. Lakini sijapata kusoma cho chote kinachofanana na kitabu Life—How Did lt Get Here? Ni cha kustaajabisha kweli kweli. Habari zilizomo zinaiduwaza akili.”
Kutoka New Zealand mwanamume mmoja aliandika kwamba kitabu hicho “bila shaka ni kimoja cha vitabu vya kutokeza zaidi katika historia ya uchapishaji wa kisasa.” Mwingine katika Italia alitangaza hivi: “Kitabu hicho ni bora zaidi ya vyote! Mimi nimekisoma bila kuacha na bila kuchoka, kama inavyofaa kufanya kuhusu vitabu vyenye uzuri usio wa kawaida.”
Mfanya biashara mmoja katika Uingereza alichukua nakala 25 kwa ajili ya washirika wake wa kikazi. Upesi akaishiwa na nakala alizozichukua kisha akachukua nyingine 25. Na mwalimu mmoja wa kidini katika United States aliagiza nakala za ziada 24 azitumie katika vipindi vyake vya kufundisha.
“Sayansi Sahihi”
Mwanafunzi mmoja katika Kanada alisema: “Mimi nakiita kitabu changu cha masomo ya sayansi nami naweza kuwaambia ninyi kikweli kwamba nimejifunza sayansi iliyo sahihi zaidi kutokana na kitabu hiki kuliko ile niliyojifunza sikuzote nilizokuwa nikienda shuleni.”
Kwa habari hiyo, mwanamume aliandika hivi: “Nilipokuwa nimejiandikisha katika programu ya chuo kikuu yenye kutolea watu cheti, nililipa mamia mengi ya dola kwa ajili ya masomo mbalimbali ambayo hayakuwa na habari za kukizidi kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? Masomo hayo yalikuwa ya hesabu, bayolojia, somo la tabia za urithi, somo la kemia inayohusu vitu visivyo hai na vilivyo hai, na somo la asili na ukuzi wa wanadamu. Sasa nimetambua kwamba ningaliweza kuokoa pesa nyingi kwa kununua kitabu chenu kwa dola 2.50. Wakati ule ule, ninyi mmeyaondoa mambo yasiyohitajiwa ili yale ya maana yaonekane wazi.”
Mwanamke mmoja anayefundisha chuoni somo linalohusu maisha ya wanyama alieleza uthamini wake kwa kusema: “Hii ndiyo namna ya kitabu cha marejezo nimekuwa nikitaka hasa niwe nacho. Uchunguzi wote ambao mara nyingi mimi nimesema ni laiti ningalikuwa na wakati au hamu ya kuufanya umekwisha tayari kufanywa kwa ajili yangu!” Vivyo hivyo, mtu mwingine aliandika hivi: “Mimi nathamini kweli kweli uchunguzi wote mrefu ambao bila shaka ulihitaji kufanywa kuhusiana na kitabu hiki. Kwa sababu gani? Lazima iwe ilichukua miezi mingi kuchunguza kwa ukamili kila kichwa cha mazungumzo!”
Kusitawisha Uthamini kwa Muumba
Wakati mwanamume mmoja alipoandika barua ya kuonyesha jinsi ‘alivyovutiwa sana’ na kitabu hiki, yeye aliongeza hivi: “Si kwamba tu kitabu hiki kinasadikisha bali pia kinaamsha mawazo ya moyoni!” Na hilo ndilo kusudi la kitabu chenyewe—kuamsha uhakika wa mtu katika Muumba mwenye upendo aliye na kusudi zuri sana kwa wanadamu.
Hivyo, mwanamume mmoja mwenye jamaa aliandika kwamba ‘kimeongeza uthamini wetu kwa Baba yetu aliye mzuri sana nacho kinaelewesha wazi, kwa njia haijapata kufanywa na kichapo kinginecho chote cha kibinadamu, akili nyingi za Mbuni wetu.’ Vivyo hivyo, mwanamke mmoja alisema kwamba kati ya vitabu vyote ambavyo amepata kusoma, “hiki ndicho kimefaidi zaidi urafiki wangu na Yehova. Yeye ni Mungu wa kuogopesha kama nini!” Na mwanamke mmoja Mkanada aliandika hivi: “Nashindwa kueleza vizuri kabisa jinsi nivavyojisikia moyoni. Hii ndiyo mara ya kwanza nimekaribia zaidi ya nyakati zote kuelewa upendo mkubwa sana wa Yehova. Viungo vyangu vya ndani vinanifanya nitoe machozi kwa kuona jinsi kitabu hiki kilivyo na nguvu za kuvuta watu.”
Kwa watu wenye mioyo myeupe ambao wamekuwa na mashaka juu ya kuwako kwa Muumba, barua inayofuata inataja vizuri matokeo ya kitabu hicho: “Asanteni! Kwa miaka mingi niliona ikiwa vigumu kuamini kuna Muumba kwa sababu niliamini kwamba wanadamu walitokea kwa kugeuka-geuka. Lakini ndipo niliponunua kitabu chenu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? Mimi najisikia kama kipofu ambaye amewezeshwa kuona kwa mara ya kwanza. Mimi nimetafuta msingi unaofaa, na sababu zinazofaa, kueleza asili ya uhai duniani na mwishowe nimezipata katika kitabu chenu. Hicho kimenipa majibu yote ambayo nimekuwa nikitafuta miaka yote hii. Sina maneno ya kuwashukuru vya kutosha! Endeleeni na kazi yenu nzuri!”
Kwa kweli kitabu hicho kimeamsha sana shauku ya watu wengi. Bila shaka kitaendelea kuelekeza wengine kwenye Muumba, Yehova Mungu, ili waweze kufaidika sasa na mpaka milele katika mfumo wake mpya wa mambo duniani.—2 Petro 3:13.