Kutoa Watoto Wawe Dhabihu—Kwa Sababu Gani Kulichukizwa Sana?
“Nao wamepajenga mahali palipoinuka pa Tofethi, palipo katika bonde la mwana wa Hinomu, ili kuwateketeza wana wao na binti zao motoni; jambo ambalo mimi sikuliagiza, wala halikuingia moyoni mwangu.”—Yeremia 7:31.
KATIKA siku za wafalme Wayudea Ahazi na Manase, taifa la Israeli lilitumbukia katika mtego wa ibada iliyopotoshwa ya mataifa jirani. Hiyo ilitia ndani kutoa watoto wao wawe dhabihu kwa Moleki. (2 Mambo ya Nyakati 28:3; 33:6, 9) Ingawa baadaye Mfalme Yosia aliondolea mbali mengi ya mazoea yale ‘ya kuchukiza,’ “[Yehova] hakuuacha ukali wa ghadhabu yake nyingi, ambayo kwayo hasira yake iliwaka juu ya Yuda, kwa sababu ya machukizo yote ambayo Manase amemchukiza.” (2 Wafalme 23:10, 26) Kwa sababu gani? Ni jambo gani lililofanya kosa hilo liwe la ‘kuchukiza’ sana hata lisiweze kusamehewa?
“Kutoa watoto wawe dhabihu kulikuwa sehemu kubwa ya ibada ya Malik-Baali-Kronos wa Foinike,” kinasema kichapo Funk & Wagnalls Jewish Encyclopedia. Hapo kwanza Wafoinike walikaa katika majimbo ya pwani ya kaskazini ya Kaanani. Kwa maana wao walikuwa mabaharia, walianzisha makao katika sehemu za kigeni za eneo lote la Bahari ya Kati, na ko kote walikokwenda wakaipeleka ile desturi yao ya ibada yenye kuchukiza kutoa watoto kama dhabihu. Kitu fulani kilichochimbuliwa katika ardhi mahali ulipokuwa mji wa kale wa Carthage wa Wafoinike (ambapo sasa pana kiunga cha Tunis katika Tunisia, Afrika ya Kaskazini) kimetoa mwangaza fulani juu ya kadiri ambavyo zoea hilo lilikuwa limepotoka.
Mahali hapo paligunduliwa mara ya kwanza mwaka 1921. Lakini kuanza na miaka ya 1970 uchimbuzi mwingi ulifanywa kwa sababu ya kupanuka kwa ule mji wa kisasa kuelekea eneo hilo. Mahali hapo palipochimbuliwa pakaonekana kuwa palikuwa eneo kubwa sana ambapo mabaki ya watoto walioteketezwa kwa moto kwa kutolewa dhabihu yalizikwa. Jarida linaloitwa Biblical Archaeology Review linaripoti hivi:
“Mahali hapa akina mama na baba wa Carthage walizika mifupa ya watoto wao walioteketezwa kwa moto kutolewa dhabihu kwa mungu Ba’al Hammon na kwa mungu-mke Tanit, kuanzia karne ya nane B.C. mpaka karne ya pili B.C. ilipofika karne ya nne B.C. eneo hilo la Tophet [jina ambalo limetokana na lile la Kibiblia, Tofethi] huenda likawa lilikuwa na ukubwa wa meta za mraba 6,000, likiwa na sakafu tisa za maziko.”
Maeneo yanayofanana na hilo yamegunduliwa katika Sicily, katika Sardinia, na mahali penginepo katika Tunisia. Wakati mmoja, maeneo yote hayo yalikuwa yamekaliwa na Wafoinike waliotoka kwao. Katika eneo la maziko la Carthage, wachunguzi walikuta alama nyingi sana za mawe za kutambulisha sehemu hizo, zikiwa zimechorwa mambo ya mungu-mke Tanit, ambaye ametambulishwa kuwa mungu-mke wa Kaanani aliyeitwa Ashtorethi, au Astarte, mke wa Baali. Chini ya mawe hayo palipatikana mitungi ya udongo, mingine ikiwa imepambwa kwa rangi zenye uangavu. Mifupa iliyoteketezwa ya waliotolewa wawe dhabihu ilikuwa ndani ya mitungi hiyo.
Ili kuonyesha ni kwa kadiri gani zoea hilo lilifanywa, ripoti hiyo ilisema: “Kwa kutegemea wingi wa mitungi iliyopatikana katika eneo tulilochimbua iwe kiwango cha kukadiriwa, sisi tunaona kwamba huenda mitungi 20,000 ikawa iliwekwa humo kati ya mwaka 400 na 200 B.C.” Hesabu hiyo kubwa sana inaonekana kuwa ya kushangaza zaidi wakati mtu anapozingatia kwamba katika siku zile ambazo mji wa Carthage ulipokuwa ungali mashuhuri, idadi ya watu ilikuwa karibu 250,000 tu kulingana na kichapo hicho.
Mambo yaliyoandikwa katika mawe hayo ya kupatambulisha mahali penyewe yanaonyesha kwamba watoto walitolewa dhabihu ili kutimiza nadhiri ambazo wazazi wao walimtolea Baali au Tanit ili yeye naye awafanyie mambo fulani. Majina ya vyeo na madaraja ya ukubwa yaliyoandikwa katika mawe hayo yanaonyesha kwamba zoea hilo lilifanywa sana hasa na watu wenye maisha ya juu zaidi, inaonekana kusudi lao ni kuomba miungu hiyo ibariki jitihada zao za kujipatia na kudumisha utajiri na umashuhuri wao. Nyingine ya mitungi hiyo ilipatikana ikiwa na mabaki ya watoto wawili au watoto hivi. Kwa kuamua kulingana na tofauti za umri wao, inawezakana kwamba watatu hao walikuwa wa jamaa ile ile moja.
Ikiwa zoea la Wafoinike hao ni la kushtua, basi kumbuka kwamba ‘Manase aliwakosesha Yuda na wenyeji wa Yerusalemu, hata wakazidi kufanya mabaya kuliko mataifa, aliyowaharibu [Yehova] mbele ya wana wa Israeli.’ (2 Mambo ya Nyakati 33:9) Yehova hakuwa akitia chumvi aliposema: “Nao wamepajaza mahali hapa damu ya wasio na hatia.” (Yeremia 19:4) Kwa kufaa, makala ya kichapo hicho Review inasema hivi: “Ushuhuda unaozidi kuongezeka wa vitu vilivyochimbuliwa na wa michoro iliyopatikana, ambao ulitolewa na watu wa Carthage wenyewe, unadokeza sana kwamba waandikaji wa vitabu vya kihistoria na wa Kibiblia walijua mambo waliokuwa wakisema.”
Hivyo, kama vile Yehova ‘alivyoangamiza’ yale “mataifa” ya Wakaanani wenye kuabudu sanamu, ndivyo pia yeye hakuwaachilia Waisraeli wasio waaminifu. Wao walipokea kile walichokistahili kwa haki mikononi mwa Wababuloni katika mwaka 607 K.W.K. Vivyo hivyo, yeye atataka sababu kwa wale ambao leo wanashiriki moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja katika kumwaga damu ya mamilioni mengi kupitia mazoea yenye kuchukiza sana kama vita, uuaji, na utoaji mimba.—Ufunuo 19:11-15.