Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 10/1 kur. 30-31
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Habari Zinazolingana
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
  • Kupambana na Ufisadi kwa Kutumia Upanga wa Roho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Utii wa Kikristo kwa Sheria
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 10/1 kur. 30-31

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

■ Mkristo anaweza kutofautishaje kati ya hongo (au kutoa rushwa, kunakokatazwa katika Biblia) na kutoa “bahashishi” au “zawadi” kwa ajili ya utumishi uliotolewa?

Tunahitaji kufahamu kwamba mazoea yanatofautiana eneo moja na jingine. Njia zinazokubaliwa katika nchi fulani zingekuwa zenye kuudhi au zisizofaa mahali penginepo. Kwa mfano, huenda watu katika nchi moja wakainama mbele ya afisa fulani, lakini katika nchi nyingine lionwe kuwa ibada ya sanamu.a Vivyo hivyo, zoea la “kutoa bahashishi” linalokubaliwa katika nchi moja linaweza kuwa la kushtua au lililo haramu kisheria katika nchi nyingine. Wanapokumbuka tofauti hizo, Wakristo wote wanapaswa kutumia shauri la Mungu linalokataza hongo.

Hongo ni nini, na Biblia inasema nini juu ya jambo hilo? Kichapo The World Book Encyclopedia kinaeleza hivi: “Kutoa hongo kunamaanisha kumpa au kumtolea mtu mwenye cheo cha madaraka kitu fulani chenye thamani, halafu naye anavunja wajibu wa kazi yake au sheria ili amfaidi yule aliyempa kitu kile.” Kwa hiyo kumpa hakimu pesa (au zawadi) ili abadili uamuzi wake na kupotosha haki ni kumhonga. Kutolea mtu pesa ili atumie sheria kwa udanganyifu, kama vile kuomba mkaguzi wa majengo au magari apuuze uvunjaji fulani wa sheria, ni kuhonga pia.

Mungu anakataza kuhonga, akiambia mahakimu Waisraeli: “Msipotoe maamuzi; wala usipendelee uso wa mtu; wala usitwae rushwa [hongo]; kwa kuwa rushwa hupofusha macho ya wenye akili, na kugeuza dawa ya wenye haki.” (Kumbukumbu la Torati 16:19; linganisha Mithali 17:23; Isaya 1:23; 5:23; 1 Samweli 8:3-5.) Yehova mwenyewe anakiweka kiwango, kwa maana kwake “hakuna udhalimu wala upendeleo wala kuchukua rushwa.” (2 Mambo ya Nyakati 19:7, NW; Kumbukumbu la Torati 10:17) Wakristo wanaotamani kibali cha Mungu wanakataa kutumia hongo (rushwa).​—Linganisha Matendo 24:26.

Ingawa watu ulimwenguni pote wanalaumu kutoa hongo na wana sheria za kupinga jambo hilo, wengi wanakabili tatizo linaloonyeshwa katika ulizo lililo juu. Wao wanajua kwamba “zawadi” au “bahashishi” inahitajiwa ndipo maafisa wadogo katika nchi yao waweze kukubali kuwafanyia shughuli yao au kuifanya vizuri. Kwa mfano, kichapo The Wall Street Journal kilisema hivi juu ya nchi moja yenye kujawa na infuleshoni: “Ili kupata pesa za ziada zilizohitajiwa ili kuishi, wafanya kazi wa serikali wanaanza ufisadi mdogo-mdogo. ‘Inakuwa lazima uwape malipo ili wao wakupe karatasi ya kujaza ya aina yo yote,’ anasema mkuu wa shirika moja la serikali. Wakati ule ule, maafisa wanaoshughulika na uhamiaji wanasumbua-sumbua watalii wa kigeni wasiojua la kufanya kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa kwa kutaka dola 20 ndipo wawapigie muhuri vyeti vyao vya usafiri wasije wakaachwa na ndege zao.”

Hivi majuzi, kichapo U.S.News & World Report kilieleza juu ya watu kukawizwa katika shughuli za kiafisi, kisha wanalipa pesa kama ilivyo kawaida sana katika sehemu zote za ulimwengu. Kwa mfano, kichapo hicho kilisema hivi: “Siku hizi ni lazima Mhindi ampe afisa pesa kwa siri ili mtoto wake akubaliwe kuandikishwa shuleni, kuruhusiwa kulala hospitali, hata kupata nafasi ya kusafiri katika gari-moshi. Mifano mingine ya jambo hilo ni kutia ndani hii:

—Mfanya biashara anahitaji cheti kabla hajaweza kufanya kazi. Yeye anamlipa afisa malipo ya cheti hicho kwenye afisi ya serikali, lakini kila mtu anajua kwamba bila ya yeye kutoa “zawadi” karatasi zake zitawekwa chini ya karatasi zile nyingine zote. Yeye akitoa ile “bahashishi” iliyo kawaida kutolewa, ingawa kwa kufanya hivyo haombi atangulizwe mbele ya wengine, karatasi yake itashughulikiwa vizuri.

—Katika nchi fulani, watu wanajua kwamba maafisa wanaotunza sheria za barabarani wanalipwa mshahara mdogo na wanatazamiwa wauongezee kwa kuomba “chai.” Afisa anasimamisha dereva na kusema kwamba sheria fulani imevunjwa, kwa hiyo ni lazima mtu huyo alipe faini. Dereva anapokataa akisema kwamba hakuvunja sheria, afisa yule anamwonya kwamba jambo hilo likifikishwa mahakamani, yeye atamshtaki mtu huyo kwamba alionyesha jeuri pia kuelekea afisa. Hivyo, watu wengi wanaona afadhali walipe ile “faini” wakiwa na maoni ya kwamba wanatoa kodi isiyoamriwa rasmi. Wengine wanakataa, wakiwa na nia ya kutendwa lo lote lile.

—Baraza la mji ndilo linalopaswa kufanya uandalizi wa kuja kuchukua-takataka. Lakini ni jambo la kawaida wenye nyumba kuwapa “zawadi” wanaochukua-takataka. Mtu asipofanya hivyo, takataka yake “inasahauliwa,” naye anaweza kupigwa faini kwa sababu ya kuwa na mazingira yenye uchafu.

Matatizo hayo yanaonyesha kwamba watu wengi wenye mamlaka wanatumia cheo chao cha kiserikali kujipatia faida ya udhalimu. (Mhubiri 8:9) Wakristo wanatamani sana mfumo mpya wa Mungu wenye uadilifu, lakini kabla haujaja ni lazima wakabiliane na mfumo uliopo. (2 Petro 3:13) Huenda hiyo ikamaanisha kuzikubali hali za kwao ambamo watumishi wa serikali wanatazamia kupewa zawadi ili wafanyie watu shughuli zao. Hata katika nchi ambako jambo hilo ni la kawaida, wengi wa Mashahidi wa Yehova wanaoshughulika na wakaguzi na maafisa wa forodhani wamekataa kutoa “bahashishi” ili kupata vitu ambavyo sheria inawastahilisha kuvipata. Kwa sababu wao wanajulikana kwa msimamo huo, wanatendewa mambo ambayo watu walio wengi hawaweza kufanyiwa bila kutoa malipo. (Mithali 10:9) Lakini, ni lazima kila Mkristo aongozwe na dhamiri yake iliyoelemishwa na Biblia kulingana na hali ya kwao.

Upendo kwa jirani ni jambo linalopasa kufikiriwa. (Mathayo 22:39) Lingekuwa jambo lisilo la upendo kwa kutumia “zawadi” ili mtu atendewe jambo fulani analopendelea, kama vile kusogezwa mbele ya watu wengine katika mstari, huku akiwapita wale waliokuwa wakingoja. Yesu alitushauri tutendee wengine kama vile sisi tunavyotaka tutendewe. (Mathayo 7:12) Wakristo wengine wanaweza wakaonelea kwamba, zamu yao katika mstari huo ifikapo, wanaweza kufuata lile zoea la nchi yao la kutoa “zawadi” ili afisa awafanyie shughuli inayompasa. Bila shaka, katika nchi ambazo si desturi kutoa “zawadi” ya namna hiyo au ambako kuzitoa kunashtua watu kuwa ni jambo lisilofaa Mkristo mwenye upendo atatenda kwa njia isiyokwaza wengine.​—1 Wakorintho 10:31-33.

Jambo jingine la kufikiriwa ni utii kwa sheria. Yesu alihimiza: “Mpeni Kaisari yaliyo ya Kaisari, na yaliyo ya Mungu mpeni Mungu.”b (Marko 12:17; ona pia Mathayo 17:24-27.) Ni jambo la namna yake ikiwa Mkristo ambaye hakuvunja sheria anatazamiwa ampe “bahashishi” mfanya kazi wa serikali au afisa mwingine. Lakini namna gani ikiwa kwa kweli Mkristo alikuwa ameivunja sheria? Inapokuwa hivyo, yeye angewezaje kwa dhamiri nzuri kutoa hongo (rushwa) ili amshawishi afisa apuuze tendo hilo la kuvunja sheria? Mtume Paulo aliandika kwamba inatupasa tuogope mamlaka zilizo kuu za kiserikali, ambazo zimepewa uwezo wa “kuonyesha ghadhabu juu ya yule anayezoea lililo baya.” (Warumi 13:3, 4, NW) Msimamo wa Paulo mwenyewe ulikuwa: Ikiwa alifanya kosa, yeye angekubali adhabu inayofaa. (Matendo 25:10, 11) Hivyo, inaweza kuwa lazima Mkristo aliyevunja sheria fulani ya barabarani alipe faini au malipo fulani, kama inavyoelekezwa na afisa au hakimu.

Paulo alisema pia kwamba serikali ni ‘wahudumu kwenu kwa faida yenu.’ Ijapokuwa maafisa fulani ni wenye pupa, serikali zinatoa utumishi mbalimbali kwa faida ya watu wote. Kwa mfano, maafisa wanakagua magari waone kama yanafaa kuwa barabarani au sivyo, na wanachunguza kama majengo yamejengwa kupatana na sheria za kujikinga na moto. Basi, ikiwa Mkristo anaona kwamba angeweza kumpa bahashishi afisa anayetazamia kupewa “malipo ya utumishi,” bila ya Mkristo huyo kuruka mipaka ya sheria, ni wazi kwamba kufanya hivyo ni tofauti sana na kuhonga (kumpa rushwa) mkaguzi ili apuuze vitendo vya kuvunja sheria.

Hata wawe wanaishi katika nchi gani, inawapasa Wakristo wajizoeze hekima yenye mafaa wanaposhughulika na hali za kwao. Watumishi wa Mungu wanapasa wakumbuke kwamba watu watakaokuwa ‘wageni katika hema lake na kukaa katika mlima mtakatifu wake’ hawawezi kutumia njia ya kuhonga (kutoa rushwa). (Zaburi 15:1, 5, NW) Kwa habari ya kutoa“bahashishi” ili kupokea utumishi ambao kwa haki wanaustahili au ili kuepuka kutendwa na maafisa isivyofaa, ni lazima Mkristo aamue ni jambo gani linaloruhusiwa na dhamiri yake kisha akubali kuchukua daraka la matata yo yote yanayoweza kutokana na jambo hilo. Hakika inampasa yeye afuatie mwendo utakaomwacha akiwa na dhamiri nzuri yeye binafsi na ambao hautii doa katika sifa nzuri za Ukristo wala kukwaza watazamaji.​—2 Wakorintho 6:3.

[Maelezo ya Chini]

a “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” gazeti Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Juni 1,1968.

b Wazee katika kundi la Kikristo wana daraka la kushughulikia vitendo vya kuvunja sheria ya Kimungu, kama vile wivi, uuaji, na ukosefu wa adili. Lakini Mungu hakuwawekea wazee wa kundi takwa la kufikiliza sheria na amri za Kaisari. Kwa hiyo, Paulo hakujiona akiwa na lazima ya kumpeleka Onesimu mikononi mwa wakuu Waroma. Onesimu alikuwa mtoro chini ya sheria ya Kiroma. (Filemoni 10, 15) Bila shaka, mtu akivunja vibaya sana sheria ya serikali, awe na sifa ya kuwa mvunjaji sheria, yeye hangekuwa mfano mwema na anaweza hata kutengwa na ushirika. (1 Timotheo 3:2, 7, 10) Ikiwa uvunjaji sheria wake ulihusika katika kusababisha kifo cha wengine, anaweza kuwa na hatia ya damu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki