Mwandiko Ukutani—Je! Unauona?
“Kwa mkono wake mwenyewe atangulia kuona anguko lake, . . .
Ni kama mwandiko ukutani.”
KWA maneno hayo, Jonathan Swift mwandikaji Mwailandi wa karne ya 18 alieleza hali ya mfanya kazi ya benki. Kwa kuzingirwa na wateja wenye kutaka warudishiwe pesa zao, yeye akahisi kwamba mwisho wake ulikuwa karibu. Kwa karne nyingi, yale maneno ‘mwandiko ukutani’ yamemaanisha kwamba hatari iko karibu sana.
Lakini ‘mwandiko ukutani’ wa awali ulitokea miaka zaidi ya 2,500 iliyopita. Na kutimizwa haraka sana kwa mwandiko huo kulibadili mwendo wa historia. Ili tuzidi kuchunguza asili ya maneno ‘mwandiko ukutani’ ni lazima twende kwenye kitabu cha Biblia cha Danieli. Kufanya hivyo kutatusaidia tuone ubora wa maonyo yaliyo katika Maandiko na kunapasa kutuongoze tutii onyo lenye umaana mkubwa sana katika siku zetu.
Kutoka Cheo cha Juu cha Mamlaka
Ni jioni ya Oktoba 5, 539 K.W.K. Wakaaji wa Babuloni wanakunywa na kucheza dansi. Ingawa maadui Wamedi na Waajemi wako kwenye malango, mji wenyewe unaonekana ni kama uko salama. Kuta zao hazipitiki, kwa hiyo kila mtu na ajifurahishe mwenyewe. Kwani, sauti za karamu zinaweza kuwaonyesha wazingira mji kwamba mji huo unaweza kukinza kwa muda mrefu!
Katika lile jumba kuu la makao yake ya kifalme, na bila shaka akiwa na kiburi kingi, Mfalme Belshaza anawakagua watu mashuhuri ambao amewaita wawe pamoja kwa ajili ya pindi hiyo. Ameagiza watumishi wake walete vyombo vya dhahabu na fedha ambavyo babu yake, Mfalme Nebukadreza, alichukua kutoka hekalu la Yehova katika Yerusalemu makumi ya miaka iliyotangulia. ‘Kwa kutumia vyombo hivi acheni tunywe divai tuisifu miungu yetu” huenda Belshaza akawa hata anapaaza sauti akisema hivyo.—Danieli 5:1-4.
Mpaka Angamizo Kamili
Kwa ghafula, uso wa Belshaza unageuka rangi kwa woga mwingi. Pale, mbele ya kinara cha taa kilicho karibu na ukuta, mkono unatokea na kuandika maneno rahisi manne lakini chemsha bongo. Basi, ule muziki na kule kucheza dansi kunakoma. Mfalme ameingiwa na woga mkuu na magoti yake yanagongana. Ishara mbaya hii inamaanisha nini? Waiteni wenye hekima na wanajimu! Mtu ye yote atakayeweza kufasiri mwandiko huu atapewa heshima nyingi.—Danieli 5:5-7.
Kila mtu anatetemeka anapongojea wenye hekima waseme jambo fulani. Lakini wao wanafadhaika. Ni nini ile maana ya kifumbo ya huo ‘mwandiko ukutani’? Hakuna mtu anayethubutu kutoa elezo, naye mfalme anaingiwa na woga mwingi hata zaidi wanaposhindwa.—Danieli 5:8, 9.
Anaposikia mambo yanayoendelea, malkia anaingia ndani ya jumba lile. Anamkumbusha Belshaza kwamba katika ufalme kuna mwanamume mmoja wa kigeni mwenye hekima ambaye amekwisha kuthibitisha uwezo wake. Kwa hiyo, Danieli anaitwa. Kwa ushujaa, yeye anamkumbusha mfalme jambo lililompata Nebukadreza miaka mingi iliyotangulia. Halafu, Danieli anamwambia Belshaza jambo litakalompata, akisema:
“Huu ndio mwandiko uliochorwa: MENE, MENE, TEKEL na PARSIN.
“Hii ndiyo fasiri ya neno hilo: MENE, Mungu amehesabu siku za ufalme wako na ameumaliza.
“TEKEL, wewe umepimwa katika mizani na umepatikana kuwa umepungukiwa.
“PERES, ufalme wako umegawanywa na kupewa kwa Wamedi na Waajemi.”—Danieli 5:7-9. NW.
Utimizo wa Haraka Sana
Je! Belshaza atalazimika kungojea muda mrefu aone kama maneno ya Danieli ni sahihi? Acheni tuone ni jambo gani linalofuata kutukia kisha tufikirie matukio ambayo yana umaana usio wa kihistoria tu.
Majeshi ya Wamedi na Waajemi yamekuwa yakichimba mifereji ili kuupotosha Mto Eufrati unaotiririka kupitia mji wa Babuloni. Mfalme Koreshi amengojea jioni hiyo ili atekeleze mpango wake, akitumaini Wababuloni watalegeza ulinzi wao kwa sababu ya ile karamu. Sasa, ile mifereji inafunguliwa. Maji ya mto huu uliopotoshwa yanapokwisha kushuka vya kutosha, askari wanafuatana wakiteremka katika kingo za mto huo kuingia bonde la mto.
Usiku huu, yale malango ya mji yanayoishia mtoni yameachwa wazi, labda kwa sababu ya kujitumaini kupita kiasi. Lile jeshi la Wamedi na Waajemi linaupenya mji, likitia hofu nyingi katika watu linapopita. Kikosi kimoja kinafanikiwa kuingia katika makao ya kifalme, na Belshaza anauawa. Ile milki kuu ya Kibabuloni imeanguka.—Danieli 5:30.
Uharibifu Ambao Pia ni wa Ghafula
Usahihi wa fasiri ya Danieli unaonyesha uzito wa maonyo ya Biblia. Maneno ya baadaye yaliyoandikwa na mtume Paulo yanaonyesha kwamba kuna matukio mengine ya ghafula na ya maana ambayo bado yanakuja. Katika barua yake ya kwanza kwa Wakristo Wathesalonike ambayo iliongozwa na Mungu, yeye anaandika hivi: “Wakati wo wote wanaposema: ‘Amani na usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafula [kutoka kwa Mungu] utakapokuwa juu yao papo kwa hapo sawasawa na umivu ghafula la taabu juu ya mwanamke mwenye mimba; nao hawataokoka kwa vyo vyote.”—1 Wathesalonike 5:3, NW.
Lakini sawa na vile Danieli na Wayahudi walivyookolewa wakati Babuloni ulipoanguka, kwa njia iyo hiyo inawezekana kuokoka uharibufu huo utakaoletwa na Mungu. Jinsi gani? Kwa kuendelea kuwa macho kiroho na hivyo kufurahia ulinzi wa Yehova. “Lakini ninyi, ndugu,” akasema Paulo “ninyi hamko katika giza, hata siku hiyo iwapate ninyi kama ambavyo ingepata wevi.”—1 Wathesalonike 5:4, NW.
Paulo alikuwa akielekeza kwenye “siku ya Yehova,” wakati utakaokuwa wa Mungu kujiingiza katika mambo ya kibinadamu kupitia Ufalme Wake wa Kimasihi. (1 Wathesalonike 5:2, NW) Ni wakati gani tunapopaswa kutazamia huo ‘mwandiko ukutani’—vile vionyesho vya kutangulia kutuonya juu ya kujiingiza huko katika mambo ya kibinadamu? Unabii wa mapema zaidi, ulioandikwa katika Danieli sura 2, unajibu ulizo letu.