Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 11/15 kur. 26-30
  • Je! Wewe Unatafuta Mwenzi wa Maisha?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wewe Unatafuta Mwenzi wa Maisha?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Waoe au Waolewe Katika Bwana Tu’
  • Wengi Wanatazama Kwingine
  • Moyo Wetu Mdanganyifu
  • ‘Unavuna Unachopanda’
  • Mngojee Yehova
  • Ndoa​—Zawadi Kutoka kwa Mungu
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
  • Ndoa—Zawadi Kutoka kwa Mungu Mwenye Upendo
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Mwongozo wa Mungu Katika Kuchagua Mwenzi wa Ndoa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Kuwekea Nyumba Yako Msingi Mzuri
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 11/15 kur. 26-30

Je! Wewe Unatafuta Mwenzi wa Maisha?

“HAKUNA uhusiano, ushirika au uenzi ulio wa kupendeza, wenye urafiki na haiba kuliko ndoa nzuri.” Hivyo ndivyo imesemwa. Kwa hiyo, si ajabu kwamba mamilioni ya waseja wangependa kuwa na mwenzi wa maisha.

Wengine wanategemea kompyuta iwasaidie kujua ni nani atakayekuwa mwenzi wao wa ndoa, na wengine wanategemea nyota. Lakini ni afadhali zaidi kama nini kumtegemea Muumba wetu, Mwanzishi wa ndoa! (Mwanzo 2:18-24) Kupendezwa kwa Mungu nasi na hekima aliyo nayo ni msingi imara wa tumaini wa mashauri na kanuni zake zinazotusaidia tujue mambo tunayopaswa kutazamia katika mwenzi wa ndoa. (Zaburi 19:7) Neno lake linaagiza Wakristo:

‘Waoe au Waolewe Katika Bwana Tu’

Kwa sababu gani? Ni kwa sababu Yehova Mungu anajali masilahi yetu ya milele. Shauri la mtume Paulo la ‘kuoa katika Bwana tu’ linapatana na zoea la watumishi wa kwanza wa Yehova waliochagua wenzi wa ndoa waliokuwa waabudu wa kweli kama wao. (1 Wakorintho 7:39; Kumbukumbu la Torati 7:3, 4) Faida za kufanya hivyo ni nyingi sana na zinapasa kuzingatiwa.

Kwa mfano, mwenzi wa ndoa anayetii Mungu anaweza kusaidia mwenzake waendeleze uaminifu kwa Baba yetu mwenye upendo wa kimbingu. (Linganisha Mhubiri 4:9-12.) Wenzi wa ndoa walio Wakristo wanaweza kutiana moyo na kupata mafanikio ya kukabiliana wakiwa pamoja na majaribu mbalimbali. Wanaweza kwa umoja kuipinga mikazo inayodhoofisha vifungo vya ndoa. Kwa kuwa wote wanamtegemea Yehova na kutumia mashauri yake yaliyo mazuri sana, wanaweza kwa urahisi mkubwa zaidi kuyapita magumu yanayotatiza na kushirikiana kwa upatano badala ya kuwa washindani. Jitihada zao za moyo mweupe za kutumikia Yehova na kufinyanga maisha zao zilingane na maisha zake zitasaidia kuwapa ndoa yenye mafanikio inayoheshimu Muumba wetu.

Miaka kadha iliyopita, mwanamke mmoja jina lake Gloria alikuwa na ushirika wa karibu pamoja na mwanamume kijana aliyekuwa akihudhuria mikutano ya Kikristo na hata alikuwa akitoa maelezo kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi. Mwanamke huyo alipokea onyo la upole asiendelee kushirikiana kikaribu na mtu huyo asiyebatizwa lakini yeye akawa amependana sana naye hivi kwamba hakutumia shauri hilo. Hata hivyo, yeye alijua shauri hilo lilikuwa zuri. Kwa hiyo siku moja alimpelekea Yehova sala kwa bidii, akamwomba sana msaada wake katika jambo lile. Muda mfupi baada ya hapo, iligunduliwa kwamba mwanamume huyu kijana alikuwa akitenda mambo yasiyo ya adili, na basi Gloria akaukata urafiki ule pale pale. Mwishowe yeye aliolewa na Mkristo kijana aliye mzuri sana. Leo, kijana huyo ni mzee aliyewekwa rasmi, na watoto wao wawili ni watendaji katika ukweli. Mwanamke huyu anapotazama nyuma, anasema hivi: “Shukrani zimwendee Yehova, nimeepuka matatizo mengi. Kwa sababu ya mwelekezo Wake, mimi nimepokea mashauri yaliyo bora kabisa, yakaniruhusu niishi maisha yenye furaha pamoja na mume mwenye upendo.”

Wengi Wanatazama Kwingine

Basi, ni kwa sababu gani mtu aliye wakfu angetazama kwingine anapotafuta mwenzi wa ndoa? Je! Mkristo huyo hasadiki kwamba Yehova anajua na anatamani kilicho bora zaidi sana kwa ajili yetu? (Mithali 3:1-7; Zaburi 145:16) Namna gani wewe? Je! wewe unaamini kwamba Yehova ndiye “Mungu wa kweli” (Zaburi 31:5) Ikiwa ndivyo, basi kwa uhakika wewe unatambua kwamba sikuzote yeye anatoa mashauri yanayofaa na yenye faida ambayo yanastahili kutumainiwa. (Isaya 48:17, 18) Kwa kweli Baba yetu mwenye upendo wa kimbingu anatoa mashauri kwa kufikiria masilahi yetu ya milele, lakini huenda sisi bila kutazama mbali tukafanya mipango yetu ihusu wakati ujao wa karibu tu. Ingawa hivyo, wakati wa kutafuta mwenzi wa maisha, je! haitupasi tupangie wakati wa mbele zaidi wala si ule wa hapa karibu tu?​—Zaburi 37:11, 29.

Je! wewe unaamini kweli kweli kwamba Ufalme wa Mungu uko karibu na baada ya muda mfupi utachukua hatua ya kusafisha dunia? Na je! wewe unajiona mwenyewe ukiwa katika Paradiso ya duniani pote iliyotabiriwa? Au unatamani kufurahia mfumo wa mambo wa sasa kwa ukamili? Je! wewe unatafuta mwenzi aliye na uwezo wa kukutolea wewe mtindo fulani mzuri wa maisha? Au unatafuta mtu anayeendelea kutanguliza ibada ya kweli? (Mathayo 6:33) Kwa kweli, ni jambo gani unalotanguliza maishani mwako? Ni hekima tuchunguze mawazo na makusudio yetu ya ndani kabisa. Halafu, ikihitajiwa kabisa, tunaweza kufanya marekebisho na hivyo tuepuke mwendo unaoweza kuchukiza Yehova.​—Linganisha Zaburi 78:40, 41.

Moyo Wetu Mdanganyifu

Yeremia 17:9 linaonya kwamba “moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote.” Kwa hiyo tunahitaji tuendelee kuulinda. Ni vizuri pia kukumbuka kwamba mara nyingi wale wanaopuuza onyo la upole la Biblia lenye uongozi wa Mungu na vikumbusho vinavyotolewa kwa upendo na wazee wa kundi na wengineo wanatiririsha machozi mengi na kupatwa na mambo yanayowaumiza moyoni.

‘Lakini mnawezaje kusema hivyo?’ huenda mtu fulani akauliza. ‘Mimi najua ndugu mmoja ambaye hakuoa mwabudu mwenzake, na sasa wote wawili wanatumikia Yehova.’ Ni kweli, katika visa vichache mambo yamekuwa hivyo, nasi tunafurahi kwamba wenzi wote wawili sasa ‘wanatembea katika ukweli.’ (3 Yohana 4, NW) Hata hivyo, yule ndugu aliyeoa mtu asiyebatizwa hakuwa mtiifu. Je! inaweza kuwa kwamba roho hiyo ya kujitegemea itatokea wazi kwa mara nyingine tena? Je! ingeweza kuwa atashawishwa afikiri anajua mambo vizuri zaidi ya Mungu na hivyo apuuze mashauri ya Biblia na kutumaini hekima yake mwenyewe katika hali nyingine? Tunatiwa moyo ‘tumtumaini Yehova kwa moyo wetu wote. (Mithali 3:5) Hiyo inamaanisha kujipatanisha kwa utii na mapenzi ya kimungu katika mambo yote. Kwa hiyo inatupasa tutake kusitawisha moyo wenye utii, mmoja unaolishinda jaribu la utii hata katika mambo madogo. (Luka 16:10) Tukikosa kutii Mungu, ni kielelezo cha aina gani tunachositawisha? Ndugu yule ambaye ‘hakuoa katika Bwana’ labda anatambua kosa lake la kufanya mambo kivyake na ametafuta msamaha wa Yehova. Lakini je! hivyo ndivyo wewe unavyotaka kuanza ndoa yako?

‘Lakini mvulana rafiki yangu ameanza kujifunza Biblia na anahudhuria mikutano ya Kikristo,’ huenda mtu mwingine akasema. Ndiyo, lakini ni kwa sababu gani yeye anajifunza? Je! sababu ni ili aweze kumpata mtu fulani awe mwenzi wake wa ndoa au sababu yake ni kujifunza juu ya Yehova Mungu na kumtumikia? Huenda muda wote wa uchumba makusudio ya mwanamume yule yakawa ya kutiliwa mashaka. Wewe utagundua nini baada ya ile siku ya arusi? Bila shaka, huenda ukangoja mpaka mvulana rafiki yako awe amebatizwa lakini muda mfupi tu baada ya hapo uipange tarehe ya arusi. Tukisema jinsi mambo yalivyo hasa, kwa kufanya hivyo ‘unaoa katika Bwana.’ Lakini je! unatenda kupatana na roho ya shauri hilo?

Je! wewe umeona inavyokuwa wakati ndugu anapopendekezwa kwa ajili ya mapendeleo fulani ya utumishi? Je! inatosha kwamba yeye amebatizwa? La, bali ndugu huyo ‘anajaribiwa juu ya kufaa kwanza.’ (1 Timotheo 3:10, NW) Je! tunaweza kujifunza somo fulani kutokana na jambo hilo? Ndiyo. Tua, tazama, na usikilize. Tua ufikirie uzito wa ndoa. Tazama mtu huyo, si kwa macho yaliyo kiwi-kiwi cha kulewa mahaba, bali kwa kumwona jinsi alivyo hasa. Sikiliza pia. Je! yeye (awe ni mwanamume au ni mwanamke) anasema mambo yanayotoka moyoni akiwa na maneno yenye upendo ya kumsifu Mungu? Je! yeye ameonyesha kwa kipindi kinachotosha ushuhuda wa kwamba ana ukuzi wa Kikristo? Baada ya yeye kuonyesha uaminifu wake na sifa za kiroho, hapo wakati wa kutosha umekuwa umepita ili kumfikiria kama anaweza kuwa mwenzi wa maisha. Mshairi mmoja mwenye akili nyingi alisema hivi:

“Wasichana! kisa cha masimulizi yangu

Somo hili lakutolea​—

Usichague mwenzi wa ndoa afaaye tu,

Bali wakati ufaao kuolewa pia.”

Ni jambo gani linaloweza kutukia moyo wetu ukitufanya tutupe kando mashauri mema na sababu halisi? Matokeo yanaweza kuwa yenye msiba. Kumbuka, Biblia inasema kwamba:

‘Unavuna Unachopanda’

Fikiria lililompata Jakilini. Mzee mmoja alimshauri juu ya urafiki aliokuwa akianzisha na kijana mmoja mwanamume nje ya kundi la Kikristo. Lakini kwa sababu yeye alihisi kwamba akina ndugu walikuwa wakiweka vizuizi vingi mno, aligeuza sikio lake asisikie mapendekezo yaliyotolewa kwa kutegemea Biblia. Kwa kufikiria mwelekeo wake mwenyewe hapo kwanza, baadaye yeye alikiri kwamba, “Mtu anaona yale tu anayotaka kuona tu bali si yale ambayo Yehova anaona na kusema.” Kijana huyo mwanamume alianza kujifunza Biblia na mwishowe akabatizwa. Katika muda wa miezi mitatu tu, walifunga ndoa.

Matatizo yalitokea upesi sana. Kwa kweli matatizo hayo yalianza wakati wa fungate! Vitabia visivyotamanika ambavyo Jakilini hakuwa ameviona au alivyokuwa ameviona lakini akavichukua kuwa si vya maana sana, sasa vilionekana wazi. Yeye alikuwa ametazamia sana kuwa na ndoa yenye furaha na umoja, lakini akajuta kwa sababu mambo yalienda kinyume. Mume wake alitengwa na ushirika akamwacha yeye akiwa na watoto wao wawili wachanga. Sasa, si mikazo tu ya kiuchumi ya mfumo huu unaoendelea kuzorota anayolazimika kukabiliana nayo, bali pia ugumu mkubwa wa kulea watoto wawili wadogo, akitunza mahitaji yao ya kimwili na ya kimoyo. Jakilini amejifunza nini kutokana na machungu hayo yaliyompata? “Utii,” yeye anasema. “Ingawa huenda mashauri yakaonekana kana kwamba ni ya ukatili au huenda yasionekane kuwa ndiyo yanayokufaa wewe zaidi, imekupasa uyaone ni kama yanatoka kwa Yehova na imekupasa uyatii kikamili.”​—Wagalatia 6:7; Zaburi 86:11.

Fikiria mfano mwingine. Maritza alimkuta kazini mtu ambaye alikuja kuwa mume wake. Yeye alimwonyesha vitu katika ulimwengu ambavyo Maritza hakuwa amevijua​—navyo havikuonekana vikiwa vibaya sana kwake. Mwanamume huyu alikuwa na elimu nyingi, alikuwa na adabu njema, na aliweza kusema mambo ya kiakili juu ya habari za namna nyingi. Ingawa Maritza alipewa maonyo mengi ya Maandiko, hayakumwingia kamwe. Walikuwa ‘wamependana’ sana.

Baada ya muda mfupi mikutano ya Kikristo ikaonekana na Maritza kuwa yenye kawaida ile ile isiyo na ladha, isiyovutia sana kama jioni zile za kusisimua alizotumia akiwa na mshirika wake mwenye kumtumbuiza. Kabla ya ndoa yao, mwanamume huyo aliahidi kwamba yeye hangevuruga mipango ya Maritza ya kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na ndivyo ilivyokuwa. Lakini, kidogo kidogo Maritza alijikuta akiwa mwenye shughuli nyingi za mambo mengine hata akaachilia utendaji wake wa kiroho uchukue nafasi ya pili, naye akawa si mtendaji.

Namna gani yale maongezi yenye kutumbuiza? Yalikoma pole kwa pole, mwishowe mume wake akampa talaka, akimwacha na watoto wanne wa kuanzia miaka minne mpaka tisa. Mshtuko wa tukio hili ulimduwaza, na ni baada ya miaka mitatu kumalizika alipoweza kutulia kiasi cha kutosha ili achanganue lililokuwa limetukia na angefanya nini na maisha yake. Yeye aliendelea kujiambia hivi: “Kuishi ni kutaabika.” Lakini jambo hilo halikumridhisha kwa sababu aliweza bado kuikumbuka miaka alipokuwa mwenye furaha, alipofurahia hata kupigwa na upepo baridi usoni akiwa katika huduma ya shambani, akishiriki na wengine habari njema za Ufalme.

“Jamani, ningaliweza kuepuka maumivu mengi na kisirani jinsi gani kama tu ningalisikiliza!” Maritza akasema kwa mshangao. Kupitia wanashule wenzi wa watoto wake, alipata tena njia ya kuonana na Mashahidi wa Yehova. Kupendezwa kwake na ukweli na upendo wake kwa Yehova ukaamshwa tena, na sasa yeye na watoto wake ni watendaji katika utumishi wake. Sasa Maritza anapendekeza hivi kwa moyo wote: “Jifunze kujitiisha kwa mwongozo ambao Yehova anatutolea na utambue kwamba watu ambao hungewafikiria sana ndio Yehova anatumia kutujulisha mapenzi yake.” Ni kama vile Yesu Kristo alivyosema: “Jiangalieni basi jinsi msikiavyo.” (Luka 8:18) Ndiyo, tua, tazama, na usikilize!

Wakati wa mkutano ule mwingine tazama huku na huku kwenye Jumba la Ufalme. Bila shaka utaona Wakristo wengi wenye furaha waliofunga ndoa na utaona kwamba wanafurahi sana kutumia wakati wao wakishirikiana na kuelezana mambo yaliyoonwa. Kwa upande ule mwingine, huenda ukaona wengine walio pale peke yao kwa sababu wenzi wao wa ndoa si waamini. Loo! Wao wanaona ni laiti waume au wake zao wangalikuwa pamoja nao! Mara nyingi wao wanalazamika kufanya haraka ya kwenda nyumbani mara tu baada ya mkutano na kuyakosa maongezi yenye kujenga na ushirika pamoja na waamini wenzao. Je! wewe una nia kujasiria ile hatari ya kujikuta bure tu ukiwa katika hali kama hizo kwa sababu ya kupuuza onyo la upole la ‘kuoa au kuolewa katika Bwana tu’? Badala ya kuwa hivyo, lingekuwa jambo la hekima kama nini kufuata maagizo ya Yehova na hivyo kuepuka matokeo yenye kusikitisha!—Zaburi 119:9; Mithali 28:26.

Mngojee Yehova

‘Lakini,’ huenda wewe ukasema, ‘Mimi nashindwa kabisa kupata mtu ye yote ndani ya kundi. Humo mna watu wachache sana wa umri wangu.’ Huenda hiyo ikawa kweli. Lakini je! wewe umesadiki kwamba Yehova anakutaka wewe uwe mwenye furaha? ‘Yeye anakujali wewe.’ (1 Petro 5:6, 7, NW) Je! wewe unakumbuka mithali ile inayosema: “Mke mwenye busara, mtu hupewa na [Yehova]”? (Mithali 19:14) Basi, je! kwa sababu gani usiifikirie habari hiyo ya ndoa katika sala?​—Wafilipi 4:6, 7.

Je! wewe unamkumbuka Hana na tamaa yake ya kupata mtoto? Alifanya nini? Aliyamimina yaliyokuwa moyoni mwake katika kumsihi sana Yehova, akimtumaini kabisa. Halafu akamwachia mambo mikononi mwake. Katika wakati unaofaa, alipokea jibu zuri sana kwa sala yake​—kuzaliwa kwa mwana.​—1 Samweli 1:9-11, 18-20; Zaburi 62:8.

Ingawa huenda watu wa umri wako wakawa ni wachache katika kundi la kwenu, namna gani juu ya makusanyiko ya mizunguko na mikusanyiko ya wilaya? Sisi tunahudhuria makusanyiko hayo kwa sababu za kiroho. Lakini wale wanaojitolea utumishi wao nyakati kama hizo wanapata uradhi wa kutumikia wengine na kukutana na ndugu na dada wanaotumikia Yehova kwa nafsi yote. Na katika pindi hizo kuna uwezekano wa kwamba utakutana na yule atakayekuwa mwenzi wako wa maisha.

Lakini hata ikiwa huwezi sasa kupata Mkristo anayefaa kuwa mwenzi wa ndoa, mtegemee Yehova kwa sala akusaidie ufuatie maisha safi ukiwa mseja. Na ukiwa bado hujafunga ndoa, sitawisha sifa na uwezo utakaokuwezesha uwe mume na baba mwema au mke na mama mwema. (Wagalatia 5:22, 23) Wengi wamesaidiwa wafanye hivyo kabisa kwa kuichukua huduma ya wakati wote wakiwa mapainia. Lo, ni njia bora kama nini kutumia wakati na nishati zako!

Basi, ikiwa wewe unatafuta mwenzi wa maisha utaanzia wapi? Na iwe kwamba unamtafuta kati ya waabudu wenzako wa Yehova walio watendaji, wale wanaoshiriki miradi yako maishani na walio na tamaa kubwa ya kumtumikia milele. (2 Timotheo 2:22) Na Yehova akikubariki uwe na mwenzi wa maisha anayeogopa Mungu, ndoa yako na iwe ife inayoheshimu Mungu wetu mwenye upendo.

[Blabu katika ukurasa wa 29]

“Jamani, ningaliweza kuepuka maumivu mengi na kisirani jinsi gani kama tu ningalisikiliza!”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki