Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 11/15 kur. 22-25
  • Watu Wasiojiweza Ambao Ni Wahubiri Wenye Uwezo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Watu Wasiojiweza Ambao Ni Wahubiri Wenye Uwezo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mwenye Kupooza Aliye na Maisha Kamili
  • Mwanamke Huyu Anatafuta Sikio Lenye Kusikia
  • Ndugu Watatu Wanaoshiriki
  • Ni Wasiojiweza Lakini Wameazimia
  • Baraka za Huduma ya Painia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Kutembea kwa Nafsi Yote katika Njia ya Uzima
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Yehova Ategemeza Jeshi Lake la Watumishi wa Wakati Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Mapainia Hutoa na Kupokea Baraka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 11/15 kur. 22-25

Watu Wasiojiweza Ambao Ni Wahubiri Wenye Uwezo

YULE kijana mwanamume mwenye sura nzuri aliye na viegemeza-miguu amepooza nusu ya mwili wake. Mwanamke huyu mwenye macho yenye furaha ni kiziwi na bubu. Wale waungwana watatu wanaotabasamu wamepatwa na ugonjwa wa kudhoofika minofu. Wote wana nini kwa ujumla? Je! ni hali za kutokujiweza? Labda. Je! ni uwezo wao? Hakika ndivyo ilivyo! Wote ni wahubiri wenye uwezo​—wahudumu mapainia wa wakati wote.

Watu hao wanasema kwamba mambo matatu ndiyo yamewafanya wafanikiwe wakiwe wahudumu mapainia: (1) mwelekezo hakika kutoka kwa Yehova Mungu kupitia tengenezo lake lenye upendo; (2) msaada usioyumba-yumba kutoka kwa jamaa zao na washiriki wa kundi la Kikristo; na (3) tamaa ya moyoni ya kutaka kupanua mapendeleo yao ya utumishi. Acheni tuone ni kwa sababu gani na jinsi gani watu hao wasiojiweza wanajithibitisha kuwa wahubiri wanaojiweza.

Mwenye Kupooza Aliye na Maisha Kamili

Hata ingawa hatumii miguu yake, Masashi Tokitsu mwenye umri wa miaka 35 amekuwa painia wa kawaida kwa miaka mitano. Yeye alikua akiwa na ndoto za kuwa mwalimu wa michezo ya kuzoeza mwili. Lakini ndoto hizo zilivunjiliwa mbali akiwa na umri wa miaka 15 alipoanguka kutoka chuma lala. Alipopatwa na tukio hilo chungu, alihisi kwamba taa za maisha yake zilikuwa zimezimwa. Lakini zilianza kurudi alipokuwa akijifunza Biblia. Ila, wakati huu zilikuwa ni taa za ukweli. (Linganisha Yohana 1:5.) Katika muda wa miezi kumi, Masashi alibatizwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Sikiliza anapotueleza ni kwa sababu gani na jinsi gani yeye akawa painia.

“Karibu kuanzia pale pale mwanzoni, mimi nilihisi kwamba kusudi la kujifunza kwangu Biblia lilikuwa lile la kuhubiria wengine. Kwa hiyo nilishika nafasi hiyo niseme na mtu ye yote aliyekuja nyumbani. Mimi niliwaonea mapainia wivu mwingi zaidi. Nilitamani kama nini niwe kule nje nikiwahubiria watu kila siku! Watu waliopooza wanaelekea kupatwa na vidonda vinavyotokana na kulala sana kitandani, mimi nilipatwa na kimoja kibaya sana kiunoni ambacho kilikuwa kikitoa usaha, umajimaji na damu. Kule tu kubadili-badili vitambaa vya kufungia vidonda mara nyingi kwa siku kulimaliza wakati mwingi sana! Kwa kufikiri kwamba singeweza kuwa painia katika huu mfumo wa mambo, niliguswa moyoni nikatiririsha machozi niliposoma katika vichapo vya Sosaiti yetu yale maneno yenye fadhili na uchangamfu yaliyoelekezwa kwa wale wasioweza kupainia.

“Kwa sababu ya kuwa na vidonda katika pande zote mbili za kiuno, nilipatwa na homa yenye kuteremsha joto la mwili wangu. Ajabu ni kwamba ilikuwa ikimalizika nilipoenda kwenye mikutano ya Kikristo. Halafu nilipopewa dokezo lenye utambuzi na ndugu mmoja aliye tabibu, nilipasuliwa vidonda hivyo. Upasuaji wa pili ulifanikiwa kabisa, hivi kwamba baada ya miezi mitano ya kupata nafuu nikaanza kutumikia nikiwa painia msaidizi. Lakini, wakati huo niliwaza kwamba ili nitunze vizuri daraka langu nikiwa mzee wa kundi, huenda upainia wa kawaida ukanilemea mno. Kundi lilikuwa ndipo sasa tu litoke kuundwa, na ni mimi pekee niliyekuwa mzee.

“Wakati ule ule, nilipendezwa na dada mmoja nikitaka kumwoa, lakini yeye hakupendezwa nimwoe. Jambo hilo liliniumiza sana, nikawaza kwamba lazima tokeo hilo liwe ni mapenzi ya Yehova, na hakukuwa na nafasi ya kujiachilia niongozwe na maoni ya moyoni yangu binafsi hali kulikuwa na kazi nyingi sana ya kufanywa ndani ya kundi. Nikahisi kwamba dawa iliyo bora zaidi kwangu ni kujihusisha hata zaidi katika kazi ya kitheokrasi. Miezi miwili baadaye, nilijiandikisha kuwa painia wa kawaida. Ili kupainia mtu akiwa amepooza, marekebisho ya kiutu ni ya maana zaidi sana kuliko ya kimwili. Unahitaji msaada mwingi sana kutoka kwa wengine ili utimize mambo unayotaka kufanya. Kwa hiyo ni lazima ujifunze njia inayopendeza ya kupata ushirikiano huo kutoka kwa wengine. Kwa kuwa mimi naweza kuendesha gari katika utumishi wa shambani, wakati wo wote inapowezekana ninalisimamisha karibu na mwingilio wa nyumba za watu. Sikuzote nafanya kazi pamoja na mhubiri mwingine wa Ufalme anayeketi katika kiti cha nyuma. Msaidiaji wangu ananichukulia mkoba wangu na hukumbuka ni kitu gani ninachohitaji kutoka mle, na ninakihitaji kwa mfuatano gani.

“Kwa kuwa tunasafiri katika barabara nyembamba-nyembamba, nyakati nyingine ninasimama pale tu penye mlango wa ua na kupaaza sauti katika njia ya kuingilia ili mwenye nyumba asikie. Ikiwa kuna ngazi, msaidiaji wangu anaenda mlangoni kuonyesha mwenye nyumba Biblia huku nikiwa ndimi ninayesema kutoka pale chini. Kunapokuwa na nyumba zilizo rahisi kufikiwa zikiwa zimefuatana katika mstari, au ghorofa ya chini iliyo na watu katika jengo lenye vyumba vingi, akina ndugu wananifadhili kwa kuniachia nyumba hizo zilizo rahisi kufikiwa. Kwa ajili ya kazi ya magazeti, mimi nampunguzia furushi msaidiaji wangu kwa kumwacha anichukulie kifuko kidogo tu chenye magazeti na broshua.

“Kwa kuwa mimi ni mwangalizi wa utumishi, ninapenda kuketi nisikilize wakati mafunzo ya nyumbani ya Biblia yanapoongozwa. Kwa hiyo tunafanya mafunzo hayo katika nyumba fulani ya mhubiri wa Ufalme ambayo ni rahisi mimi kufikia, au wao wanakuja nyumbani kwangu. Kwa hiyo unaweza kuona kwamba mimi nahitaji msaada kutoka kwa akina ndugu. Ni jambo la maana akina ndugu waelewe si jinsi tu ya kunisaidia bali pia kwamba mimi najua jinsi ya kukubali msaada wao kwa njia inayoonyesha ninaufurahia.

“Nilipoanza upainia mara ya kwanza, nilitoa ushuhuda mwingi kupitia uandikaji barua. Lakini, kwa kuwa sasa naweza kuvaa viegemeza-miguu mchana kutwa bila matokeo yo yote mabaya, karibu kazi yangu yote ya kuhubiri inafanywa nikiwa pamoja na mapainia na wahubiri wale wengine. Faida moja inayokuja upesi kutokana na kufanya utumishi mchana kutwa ni kupata usinginzi mzito ulio mtamu usiku kucha. Kutumia Biblia kila siku kunaongeza kina cha usadiki wangu mwenyewe kwamba nina ukweli. Kushiriki sehemu moja kwa moja katika matukio ya maisha ya kila siku na kuona jinsi watu wanavyouhitaji ukweli kunaongeza kina cha upendo wangu kwao. Kufanya kazi sikuzote na mtu fulani kunanipa pia nafasi za kufanya kazi ya uchungaji na kunanisaidia nipate kulijua kundi vizuri hata zaidi.

“Bila shaka, nautazamia mfumo mpya wa mambo na kuweza kumtolea Yehova utumishi nikiwa na mwili wenye afya. Lakini si lazima ningoje mpaka wakati huo. Kumtumikia yeye sasa, nikiwa na hali za kupungukiwa au bila hizo, ndiyo nafasi nzuri zaidi iliyopo kwa vijana na wazee pia.”

Mwanamke Huyu Anatafuta Sikio Lenye Kusikia

“Miaka yangu ya ukuzi ilijawa na kulia,” anasema Katsuko Yamamoto. Baada ya kupatwa na homa iliyopandisha sana joto la mwili wake pamoja na surua, Katsuko alibaki akiwa kiziwi alipokuwa na miaka miwili. Mwanamke huyo anakumbuka yale maumivu makali ya kwenda shuleni na kuvumilia dhihaka kali zisizo na fadhili za watoto wengine. Katsuko ni mwenye furaha akiwa painia tangu mwaka 1981, naye anaeleza jinsi anavyofanya upainia.

“Kwa sababu mimi siwezi kupashana habari na watu kwa kutumia mdomo, kwa ajili ya huduma ya shambani natumia maandishi na kumwonyesha mwenye nyumba. Mara nyingi namwomba dada anayesikia aende pamoja nami ili kuhakikisha kwamba watu wanaelewa ninavyosema. Nyakati nyingine mimi mwenyewe ninajifanyia ziara ya kurudia ya kwanza kisha naomba dada mwenye kusikia aende pamoja nami katika ziara ile ya pili. Nimeweza kuongoza mafunzo ya Biblia kwa njia hiyo. Ninapoonyesha uthamini kwa fadhili za Yehova kwa njia hiyo ninafurahi sana.”

Siku za “kulia” za Katsuko zimepita sasa. Leo, mwanamke huyo Mkristo mwenye kupendeza anapata furaha ya kweli katika maisha yake yenye shughuli akiwa mhudumu painia.

Ndugu Watatu Wanaoshiriki

Wale akina Tanizono watatu ambao ni ndugu wamoja wana umri wa miaka 40 na kitu na wana ule ugonjwa wa kudhoofika minofu ya mikono na miguu yote pamoja na kiuno. Kabla ya kujifunza ukweli, wao walitegemeza maisha zao juu ya kazi ya kimwili, wakitumainia kazi hiyo ingewasahaulisha jinsi ugonjwa huo unavyoharibu mwili pole kwa pole mpaka mtu anapatwa na kifo cha mapema. Kila mmoja wao alianza funzo la Biblia akiwa mbali na wale wengine na wote wakapata maarifa ya kuujua ukweli. Ili waonyeshe uthamini wao kwa Yehova, wangeweza kufanya nini wapanue utumishi wao? Yule ndugu mdogo zaidi, Toshimi, anatuambia hivi:

“Mimi niliishi pamoja na ndugu yangu mkubwa zaidi Akimi, na mke wake mpaka 1979. Kwa sababu sikuweza tena kujitunza mwenyewe, ndipo nilipojiunga na ndugu yangu Yoshito katika makao ya kutunzia wagonjwa. Nikiwa kule nikaanza kutumikia nikiwa painia msaidizi na katika muda wa miaka mitano iliyofuata nikajifunza Biblia pamoja na watoto zaidi ya 12 katika wadi. Mmoja wa watoto hao alilazimika kuacha kujifunza alipopingwa na wazazi wake lakini wao wakapunguza upinzani wao alipowaomba sana wamwache ajifunze tena. Alikufa akiwa na miaka 16 na tumaini hakika la kupata ufufuo. Karibu mwaka mmoja baadaye, mimi nilipokea simu kutoka kwa wale wazazi waliokuwa wapinzani hapo kwanza. Wao walikuwa wakiletewa matatizo fulani na binti yao mdogo zaidi na wakaona kwamba funzo lingemsaidia.

“Ndugu yangu Yoshito na mimi tulitaka kuwa mapainia wa kawaida. Lakini je! tungeweza kutimiza ule mradi unaotakwa kila mwaka wa saa 1,000? Ni kweli kwamba jambo tu tulilohitaji ni kuongeza wakati tuliotumia katika huduma kwa saa 30 tu zaidi kila mwezi. Lakini je! miili yetu ingeweza kustahimili? Halafu tena, tukawaza, ‘Tusipofanya hivyo sasa, tutafikia hatua ambayo hatutaweza.’ Tuliendelea kutaja-taja maneno ya Paulo katika 1 Wakorintho 9:16 katika mazungumzo yetu. ‘Tena ole wangu nisipoihuburi Injili!’ Kwa uhakika, sisi tuna wajibu wa kuhubiri habari njema tuwe au tusiwe tuna afya njema. Kwa hiyo tulipeleka maombi yetu na tukaanza upainia wa kawaida Septemba 1, 1984.”

Yoshito anaongeza hivi: “Nilipokuwa nimeujaribu upainia ‘wa muda’ katika Januari 1976, niliharibu afya yangu na nikalazimika kubaki kitandani bila kutoka-toka kwa miezi miwili. Woga wangu ulio mwingi zaidi ulikuwa kwamba upainia wa ukawaida ungenifanya niwe mgonjwa na kunilazimisha nikose mikutano. Jambo la kufurahisha ni kwamba kufikia Agosti 1985 niliweza kufikia mradi wangu katika saa nami sikuwa nimekosa hata mkutano mmoja kwa sababu ya kupainia!”

Toshimi anaeleza hivi: “Njia yetu kubwa ya kutimiza huduma yetu ni kupitia uandikaji barua. Tunaandikia watu ambao hawakupatikana nyumbani, marafiki, watu wa ukoo, washiriki wa jamaa wasioamini wa wale walio kundini, na wakaaji wa maeneo ya mlimani yanayohubiriwa katika huduma ya nyumba kwa nyumba mara mbili tu kwa mwaka. Tunahubiri vivi hivi kwa madaktari, wauguzi, wafanya kazi ambao ni wanafunzi, na wagonjwa wengine. Kufikia sasa, wagonjwa sita wamejifunza ukweli. Watatu kati yao walikuwa wahubiri wa Ufalme na walikuwa wakingojea ubatizo walipokufa. Sisi tumefurahia faida za kimwili kwa kuendelea kujishughulisha, tunapata uradhi wa kiakili kwa kujua tunaifanya kazi ya kuhubiri, na tunapata furaha ya moyoni kwa kuwatia wengine moyo.”

Yoshito anaongeza hivi: “Kwa kuwa sisi ni wazee wa kundi, sote wawili tunaweza kusema kutokana na yale tuliyojionea wenyewe tunapoongea na wale wanaojitahidi kufikia utumishi wa painia. Tulipopeleka maombi ya kuwa mapainia, dada wawili wenye umri mkubwa katika kundi letu walisukumwa na moyo pia wajiunge na mapainia. Mimi nafurahi hasa kusema kwamba kupatana na roho ya Zaburi 119:71, njia yangu ya zamani ya kuwa na fikira zenye mwelekeo mbaya imebadilika ikawa ile ya Yehova. Ndiyo, ‘Ilikuwa vema kwangu kuwa naliteswa, nipate kujifunza amri zako.’”

Sasa, ni zamu ya ndugu yule mkubwa kuongea: “Akimi anasema: “Ni kupitia fadhili za akina ndugu na mke wangu mwenye upendo na anayeniunga mkono, kwamba mimi naweza kufanya yale ninayofanya kwa njia ya kitheokrasi. Mimi siwezi kutembea hata hatua moja. Kwa miaka 14 sasa, akina ndugu wamenisaidia bila kuchoka nifike kwenye kila mkutano na kusanyiko. Tangu wakati nilipoanza kujifunza, mambo yaliyoonwa katika upainia ndiyo yaliyoongewa zaidi wakati vijana walipokusanyika pamoja kwa ajili ya ushirika. Kama ilivyodokezwa katika Huduma ya Ufalme Yetu, mimi niliamua kujaribu kupainia kwa mwaka mmoja. Nikiwa na mashaka fulani-fulani juu ya hali yangu ya kimwili, katika sala nilimtolea Yehova ahadi ya kufanya hivyo, nami nimeifanya upya ahadi kila mwaka kwa muda wa miaka mitano. Katika utumishi wa shambani, ninatumia baiskeli yenye magurudumu matatu iliyotengenezwa kwa ajili ya watu wasiojiweza. Nikiwa nayo naweza kufika karibu na mahali pa kuingilia pa nyumba nyingi. Mara nyingi ninaketi katika maeneo yenye wapitaji wengi. Ikiwa ni wachache tu wanaopita pale, ninatoa sala papo hapo nipate mtu wa kutolea ushuhuda, halafu anakuja mtu mwenye sikio la kusikia. Wanafunzi wa Biblia wanakuja nyumbani kwangu kujifunza, nami nimeweza kusaidia watu wanane wasonge mbele kufikia ubatizo.

“Kwa kuwa mimi ndimi mwangalizi-msimamizi na mwangalizi wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ninafika mikutanoni mapema ili niweze kuwasalimu akina ndugu. Kwa sababu siwezi kuwafikia kwa urahisi kwenye nyumba zao, kutumia kwa kufaa wakati kabla na baada ya mikutano ni kwa maana sana. Pia ninatumia mara nyingi simu kwa ajili ya kazi ya uchungaji.

“Katika muda wa miaka minne au mitano hivi iliyopita, nguvu za minofu yangu zimepungua sana. Ufikapo usiku, ninakuwa siwezi kabisa kusongeza mnofu wo wote wa mwili, na mkazo huo umeongezeka kufikia kadiri ya kwamba ninahisi kana kwamba ninafinywa sana kitandani. Mke wangu anapindua-pindua mikono na miguu yangu ili niweze kupata kitulizo fulani. Ni katika nyakati kama hizo kwamba maneno yenye uchangamfu na ya upendo kutoka kwa akina ndugu yanaponisaidia niendelee kuonyesha tabasamu ya uso ambayo natumaini inaonyesha hali iliyo katika moyo wangu wala si katika mwili wangu.”

Kwa sasa ugonjwa huo hauwezi kuzuiwa usiendelee kusonga mbele. Lakini wale ndugu akina Tanizono wanaona kwamba kuendelea kushughulisha miili yao katika utumishi wa shambani, kuijua hali ya mwenye nyumba na mahitaji yake, kufanya kazi kwa ukaribu pamoja na waamini wenzao, na kuhisi wakipata ujazi kutokana na kutumikia Mungu wakiwa mapainia kumewasaidia wazidi kupunguza mwendo wa ugonjwa huo. Wao wanamshukuru Yehova kama nini!

Ni Wasiojiweza Lakini Wameazimia

Hali za kutokujiweza kimwili hazikupunguza upendo na bidii ambayo wahubiri hawa wenye uwezo wanayo kwa huduma ya wakati wote. Azimio lao ni kama lile la mtume Paulo, aliyeandika hivi: “Hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa; lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku.”​—2 Wakorintho 4:16.

Bila shaka, si watangazaji Ufalme wote wasiojiweza kimwili wanaoweza kuwa wahubiri wa wakati wote. Hali zinatofautiana mtu na mtu. Lakini lo lote ambalo watu hao wanaweza kufanya ili wamsifu Aliye Juu Zaidi na kusaidia wengine kiroho litawaletea furaha kubwa, uradhi wa kibinafsi, na baraka ya Mungu wetu mwenye upendo, Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Masashi Tokitsu

Katsuko Yamamoto

Akimi Tanizono

Toshimi Tanizono

Yoshito Tanizono

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki