“Uwe Hodari Tu na Ushujaa Mwingi”
“Ni lazima ninyi wanaume msiwaogope wao, kwa maana Yehova Mungu wenu ni Yeye ambaye anapigana kwa ajili yenu.”—KUMBUKUMBU 3:22, NW.
1. (a) Hali ilikuwaje katika Israeli mwishoni mwa safari yao ya jangwani? (b) Musa alitoa kitia-moyo gani?
WAKATI ulikuwa umefika wa matukio ya maana sana katika historia ya Israeli. Taifa takatifu la Mungu lazima lijitayarishe sasa kuingia katika Nchi ya Ahadi! Kwa miaka 40, Musa alikuwa amewaongoza Waisraeli kupita jangwa kubwa na lenye kutisha. Lakini sasa, katika mkoa wa Yordani katika nchi ya Moabu, aliwahutubia watu wa Mungu mara ya mwisho. Akiwa mwenye umri wa miaka 120, “jicho lake halikupofuka, wala nguvu za mwili wake hazikupunguka,” wala nguvu za sauti yake hazikupunguka. Yoshua, ambaye alikuwa karibu kumfuata, na wana wa Israeli wote lazima walisisimuka kusikia maelezo yenye nguvu ya Musa kuhusu sheria ya Yehova na kitia-moyo chake chenye kani nyingi cha kuwa hodari waliposonga kuingia wakaitwae nchi.—Kumbukumbu 1:1-5, 19, 21, 29, 30; 3:22; 31:6, 7, 23; 34:7.
2. Tunajuaje kwamba maandishi ya mambo hayo ni kwa kutufundisha sisi leo?
2 Je! matukio haya ya zamani sana zilizopita ni historia tu? Sivyo kabisa! Mtume Paulo anatuambia: “Kwa kuwa yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Warumi 15:4) Maandishi hayo yana ulinganifu wa kisasa. Yanaweza kututia nguvu leo kwa vita ya kiroho. Pia, yanatumika kuwa “onyo kwetu sisi ambao juu yao miisho ya mifumo ya mambo imefika,” yakitusaidia tuepuke mitego ya Shetani.—1 Wakorintho 10:11, NW; 1 Petro 4:7.
Nguvu za Yoshua—Kutoka Chanzo Kipi?
3, 4. (a) Kwa nini tunahitaji kukuza hali ya kutoogopa? (b) Tunaweza kufanyaje hivyo?
3 Karibuni sana sasa, watu wa Mungu wataingia katika mfumo mpya wa mambo wa Yehova. Kwa sababu ya matukio yanayoonekana duniani, tunahitaji kukuza hali ya kutoogopa. Tunaweza kufanyaje hivyo? Yoshua alipojitayarisha kuingia katika Nchi ya Ahadi, Mungu alimshauri hivi: “Uwe hodari tu na ushujaa mwingi, uangalie kutenda sawasawa na sheria yote aliyokuamuru Musa mtumishi wangu; usiiache, kwenda mkono wa kuume au wa kushoto, upate kufanikiwa sana kila uendako. Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo [utatenda kwa hekima, NW].”—Yoshua 1:7, 8.
4 Aa, hiyo ndiyo siri! Isome Biblia kila siku. Ina sheria ya Mungu kwa ajili ya sisi. Itafakari. Tii vikumbusho vyayo. Usijiruhusu ugeuzwe kwenye ulimwengu ulio karibu yako wenye kupenda vitu vya kimwili na wenye kukosa adili. Katika hali yo yote unayojikuta, tenda kwa hekima. Tumia kwa kufaa maarifa sahihi na ufahamu wa kiroho ambao umepata kupitia funzo la Neno la Mungu. Zungumza na wengine juu yayo. Kwa kufanya hivyo na kwa kumtegemea Yehova, unaweza kuwa ‘hodari na ushujaa mwingi, na kuifanikisha njia yako,’ kweli kweli.—Linganisha Zaburi 1:1-3; 93:5; 119:165-168.
5. (a) Kama Yoshua, wahudumu vijana wanaweza kupataje nguvu? (b) Ni mradi gani bora ambao vijana Mashahidi wanaweza kuwa nao leo?
5 Yoshua alikuwa “mtumishi wa Musa tangu ujana wake”na kuendelea. (Hesabu 11:28) Bila shaka ushirika huo wa karibu sana ulimsaidia apate nguvu za kiroho. Vivyo hivyo, wahudumu vijana leo wanaweza kupata nguvu kwa kufanya kazi pamoja na wazazi waliojitoa, mapainia, Mashahidi wa muda mrefu, na watumishi wengine washikamanifu wa Yehova. Kushiriki kutoa ushuhuda nyumba kwa nyumba pamoja na wenye bidii hivyo linaweza kuwa jambo la kufurahisha na linaweza kusaidia kujenga ukomavu na tamaa ya kusonga mbele katika huduma kwa vijana wetu. (Matendo 20:20, 21; Isaya 40:28-31) Kuna mradi gani ulio bora sana ambao Mashahidi vijana wangeweza kuwa nao kuliko utumishi wa wakati wote kwa ajili ya Ufalme wa Yehova!—Zaburi 35:18; 145:10-12.
6. Yoshua alikuwaje mfano kwetu kuhusiana na kampeni dhidi ya Waamaleki?
6 Musa alipomwagiza Yoshua apigane na Waamaleki, “Yoshua akafanya kama Musa alivyomwambia.” Alitii; hivyo, akapata ushindi. Sisi, pia, tutashiriki katika utetezi wa Yehova ikiwa tutasikiliza kwa makini maagizo ya vita ambayo tunapokea kupitia tengenezo lake. Yehova alimwambia Musa akumbuke ushindi Wake juu ya Amaleki kwa kuandika katika kitabu na kuufafanua masikioni mwa Yoshua. Bila shaka Yoshua akatukuza ushindi wa Yehova zaidi kwa kuzungumza na wengine kuuhusu. Kwa njia iyo hiyo, sisi leo tunaweza kujulisha watu matendo makuu ya Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova na kutangaza “siku ya kisasi” yake inayokaribia sana juu ya waovu.—Kutoka 17:10, 13, 14; Isaya 61:1, 2; Zaburi 145:1-4.
7, 8. (a) Ni uhakika gani ambao Yoshua na Kalebu walionyesha waliporudi kutoka Kanaani? (b) Ni onyo na kitia-moyo kipi tunachopata kutokana na jinsi Yehova alivyoshughulika na mambo wakati huo?
7 Musa alipowatuma wakuu 12 wakapeleleze Nchi ya Ahadi, alimtia Yoshua katika hesabu yao. Waliporudi, kumi kati ya wapelelezi hao walionyesha woga mkuu kwa wakaaji wa nchi wa Kanaani na kuwashawishi watu wafanye kampeni ya kurudi Misri. Lakini Yoshua na Kalebu walitangaza hivi kwa ushujaa: “Ikiwa [Yehova] anatufurahia, atatuingiza katika nchi hii atupe iwe yetu, nayo ni nchi yenye wingi wa maziwa na asali. Lakini msimwasi [Yehova], wala msiwaogope wale wenyeji wa nchi, maana wao ni chakula kwetu; uvuli uliokuwa juu yao umeondolewa, naye [Yehova] yu pamoja nasi; msiwaogope.”—Hesabu 13:1–14:38.
8 Walakini, kusanyiko la Waisraeli liliendelea kunung’unika, hivi kwamba Yehova akachukua hatua na kuwahukumia Waisraeli hao wenye woga miaka 40 ya kutanga-tanga jangwani. Wanaume wao wote wa vita walikufa bila kuiona Nchi ya Ahadi, isipokuwa Kalebu na Yoshua. Lo! ni onyo kwetu leo kama nini! Tusinung’unikie kamwe mipango ya Yehova. Hata tukiwa katika maeneo ambayo ni magumu sana kutoa ushuhuda, na tuwe na ushujaa na wenye nguvu katika kwenda kwenye nyumba za watu tukiwa na ujumbe wa Ufalme wenye kuokoa uhai. Tusiwe kama waasi-imani wa kisasa ambao, badala ya kutoa ushuhuda peupe, wanapendelea kusingizia ndugu zao na kurudi katika njia za ulimwengu—Misri iliyofananishwa.—Hesabu 14:1-4, 26-30; Luka 12:45, 46; linganisha Matendo 5:27-29, 41, 42.
Jina la Yehova Latangulizwa!
9. Yoshua aliishije kulingana na jina lake jipya?
9 Orodha ya Biblia ya wapelelezi 12 inamtaja Yoshua kuwa Hoshea, kumaanisha “Wokovu.” Lakini kufikia hapa maandishi yanasema: “Musa aliendelea kumwita Hoshea mwana wa Nuni Yehoshua [likimaanisha ‘Yehova Ni Wokovu’].” Kwa nini Musa alitilia mkazo jina la Yehova? Ni kwa sababu Yoshua alitumikia hasa kwa ajili ya utetezi wa jina hilo! Yoshua akawa mfano ulio hai wa utii kwa amri ambayo Musa angetilia mkazo baadaye kwa Israeli: “Nawe mpende [Yehova], Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa [nafsi] yako yote, na kwa nguvu zako zote.” Katika kufanya hivyo, alipendelewa kuonyesha kwamba ‘Yehova ni wokovu.’—Hesabu 13:8, 16, NW; Kumbukumbu 6:4.
10. (a) Jina la Yehova linamaanisha nini kwako? (b) Tunaweza kupata nguvu gani kutokana na maneno zaidi ya Yehova kwa Yoshua?
10 Je! sisi nasi hatujaliona jina la Yehova kuwa lenye thamani sana na linalostahili sifa yote? Jina lake tukufu linamaanisha “Yeye Anafanya Iwe” kuhusiana na kutimiza ahadi zake. Ahadi zake za Ufalme ni zenye kufurahisha moyo jinsi gani! Tukiwa na bidii kama ile ya Yoshua, lazima tutake kulitukuza jina la Yehova na makusudi yake mbele ya wote ambao huenda wakakubali tumaini la mfumo mpya wake ulio safi na wenye uadilifu. Katika nyakati hizi zenye majaribu, tunaweza kupata nguvu kutokana na maneno zaidi ya Yehova kwa Yoshua: “Je! si mimi niliyekuamuru? Uwe hodari na moyo wa ushujaa; usiogope wala usifadhaike; kwa kuwa [Yehova], Mungu wako, yu pamoja nawe kila uendako.”—Yoshua 1:9.a
11. (a) Maana ya jina la Yesu ilikaziwaje alipopanda kuingia Yerusalemu? (b) Yesu alilionaje jina la Yehova, na ni jambo gani linaloonyesha hivyo?
11 Jina la Kigiriki linalolingana na Yoshua, au Yehoshua, ni Yesu, ambalo pia linamaanisha “Yehova Ni Wokovu.” Ni kupitia kwa Yesu Kristo Yehova anaandaa wokovu kwa wanadamu. Katika mwaka 33 W.K. wakati Yesu alipoingia Yerusalemu akiwa amempanda mwana-punda, watu wengi waliendelea kupaza sauti wakisema: “Mbarikiwa ajaye kwa jina la [Yehova].” (Marko 11:9 Zekaria 9:9) Yoshua alikuwa mfano halisi wa Yesu, ambaye ‘alituachia kielelezo, tufuate nyayo zake.’ (1 Petro 2:21) Kama Yoshua, Yesu aliliona jina la Yehova kuwa lenye thamani kubwa, naye alitukuza jina hilo. Mara mbili katika sala yake ya mwisho pamoja na wanafunzi wake, yeye alitilia mkazo jina la Mungu akisema: “Jina lako nimewadhihirishia watu wale ulionipa katika ulimwengu. . . . Nami naliwajulisha jina lako, tena nitawajulisha hilo; ili pendo lile ulilonipenda mimi liwe ndani yao, nami [katika muungano pamoja nao].” (Yohana 17:6, 26) Tunapendelewa jinsi gani kuwajulisha wengine jina hilo!
12. Ni matendo yapi yenye nguvu tunayongojea leo, na kwa sababu gani?
12 Tunaposoma maandishi ya Biblia kuhusu uongozi mshikamanifu wa Yoshua, tunaweza kujua kwamba Yoshua Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo, anawaongoza watu wa Mungu leo. “Siku ya [Yehova]” ya utetezi sana imekaribia. Jinsi tunavyongojea kwa hamu sana utimizo wa ahadi yake ya mfumo mpya wa uadilifu utakaofuata siku hiyo! (2 Petro 3:10-13, 17, 18) Kwa uhakika basi, tunatazama mbele kwenye matendo zaidi yenye nguvu ya Yehova, hata ya nguvu zaidi kupita yale aliyofanya kupitia Yoshua.
Mwujiza wa Yehova Kwenye Yordani
13. (a) Ni hali gani iliyowapata Waisraeli upande wa mashariki wa Yordani iliyoonekana kana kwamba haingewezekana? (b) Utii wa Waisraeli ulithawabishwaje?
13 Ulikuwa wakati wa mavuno mwaka 1473 K.W.K., na Yordani ulikuwa umefurika. Nafsi milioni kadha, wazee na vijana, wanaume, wanawake, na watoto, wangewezaje kuvuka maji hayo mengi yenye mkondo mkubwa? Hata hivyo Yehova alikuwa amemwamuru Yoshua hivi: “Haya basi, ondoka, vuka mto huu wa Yordani; wewe na watu hawa wote.” Na watu nao wakamjibu Yoshua wakisema: “Hayo yote uliyotuamuru tutayafanya.” Israeli wakavunja kambi. Makuhani wakatangulia, wakiwa wamelibeba sanduku la agano, ambalo lilikuwa limefunikwa kwa uangalifu na lililoonyesha kuwapo kwa Yehova pamoja nao. Ndipo Yehova akaanza kufanya ‘mambo ya ajabu kati yao,’ kwa kuwa “hao waliolichukua hilo sanduku walipofika Yordani, na nyayo za makuhani waliolichukua sanduku zilipotiwa katika maji ya ukingoni . . . maji yaliyoshuka kutoka juu yakasimama”! Maji yaliyokuwa chini ‘yakatindikwa,’ ili yatiririke kwenye Bahari ya Chumvi, na “watu wakavuka.” (Yoshua 1:2, 16; 3:5-16) Lo! mwujiza wa ajabu kweli kweli!
14. Jambo hili lina ulinganifu gani leo, na matokeo ya ushuhuda yamekuwa nini?
14 Yordani wenye msukosuko unapata ulinganifu katika mfuriko wa jamii ya wanadamu wote ambao sasa unajisongeza mbele kuelekea uharibifu wa Har–Magedoni. (Linganisha Isaya 57:20; Ufunuo 17:15.) Leo, Yehova anakawiza mwisho huo wenye uharibifu huku akiwaimarisha, watu wake, ambao sasa wamepita hesabu ya 3,000,000—hesabu inayolinganishwa na ile ya watu wa Mungu walioenda pamoja na Yoshua.—Linganisha Habakuki 2:3.
15. (a) Ni jambo gani katika nyakati za kisasa linalofananishwa na ushujaa ulioonyeshwa na makuhani huko nyuma? (b) “Mkutano mkubwa” unafananishwaje katika habari hii?
15 Mamilioni ya Waisraeli walipokuwa wakivuka bonde la mto, “hao makuhani waliolichukuwa sanduku la agano la [Yehova] wakasimama imara mahali pakavu katikati ya Yordani,” kufananisha Yehova Mungu akikatiza mambo. (Yoshua 3:17) Ilikuwa katika 1919 wakati kikundi kidogo cha Mashahidi wapakwa-mafuta kilipokanyaga kwa ushujaa mbele ya “maji” ya wanadamu. Katika 1922 walijibu kwa ujasiri mwito wa ‘mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni Mfalme na Ufalme wake,’ kama wakisema: “Mimi hapa, nitume mimi.” Yehova anawahakikishia hivi: “Upitapo katika maji mengi nitakuwa pamoja nawe; na katika mito, haitakugharikisha.” Katika 1931, aliwastahi kwa kuwapa jina Mashahidi wa Yehova. (Isaya 6:8; 43:2, 12) Kati ya wale waliovuka Yordani wangekuwako Waisraeli wasio Walawi na wazao wa watu wasio Waisraeli “kundi kubwa la watu waliochangamana nao” lililokuwa limeondoka Misri pamoja na Musa. Katika maana ile ile, “mkutano mkubwa” leo unashiriki kuvuka kwenda kwenye mfumo mpya wa Mungu, huku mabaki ya kikundi cha ukuhani cha kiroho wakisimama wakiwa ‘wameimarika, bila kutikisika,’ wakiwa mfano bora katika imani yao.—Kutoka 12:38; Ufunuo 7:9; 1 Wakorintho 15:58.
Kufanya Ukumbusho wa Mwujiza Huo
16. (a) Mwujiza wa Yordani ulifanyiwaje ukumbusho? (b) Jambo hili linadokeza nini kuhusu matendo yenye nguvu ya Yehova leo?
16 Yehova aliendelea kufanya ukumbusho wa mwujiza huo wa Yordani, akiamuru kwamba wanaume 12, wenye kuwakilisha makabila ya Israeli, wayachukue mawe 12 kutoka katika bonde la mto na kuyaweka magharibi mwa ufuo kwenye Gilgali. Mawe hayo yangesimama huko yakiwa ukumbusho wenye kudumu kwa jina la Yehova na matendo yake yenye nguvu. Wana wajao wa Israeli wangeambiwa kwamba ukumbusho huo ulifanywa ili “watu wote wa duniani wapate kujua mkono wa [Yehova], ya kuwa ni mkono wenye uweza, ili wamche [Yehova], Mungu wenu, milele.” (Yoshua 4:1-8, 20-24) Katika nyakati za kisasa, matendo ya ajabu ya Yehova ya kuwahifadhi watu wake, ijapokuwa mashambulizi mabaya sana ya viongozi wa kisiasa na kidini, yanasimama kuwa ukumbusho wa kwamba Yehova yu pamoja na watu wake. Bila shaka kazi kuu zake za kisasa katika kutetea jina lake zitakumbukwa daima katika mfumo wake mpya wa mambo.—Ufunuo 12:15, 16; Zaburi 135:6, 13.
17. (a) Ni ukumbusho upi zaidi ambao Yoshua alifanya? (b) Wanadamu wameshindwaje kuepa ushuhuda kama huo leo?
17 Ukumbusho zaidi ulifanywa: “Kisha Yoshua akapanga mawe kumi na mawili katikati ya Yordani, mahali pale miguu ya hao makuhani waliolichukua hilo sanduku la agano iliposimama; nayo yapo pale pale hata hivi leo.” Makuhani walipotoka katika bonde la mto na Yehova akayaachilia mafuriko ya maji yaliyozuiwa, maji hayo yakaja yakiyazunguka kwa mvumo mkubwa mawe kumi na mawili ya ushuhuda. (Yoshua 4:9) Kuanzia wakati huo na kuendelea, mafuriko hayo hayangeepuka kuwapo kwa mawe yale. Vivyo hivyo leo, wanadamu wanazidi kujisongeza haraka zaidi kuelekea “Bahari ya Chumvi” (Bahari ya Kifo) ya Har–Magedoni. Lakini hawawezi kuepuka ushuhuda ambao Mashahidi wa Yehova wamerundika ulimwenguni kote huku wakiwa ‘wamesimama imara katika roho moja, kwa nafsi moja wakishindania Injili.’ (Wafilipi 1:27, 28) Maandishi yanayopatikana yanaonyesha kwamba, wakati wa miaka 67 mpaka wakati huu wa mwaka 1986, Mashahidi wameangusha katika nyumba za watu duniani pote, katika lugha zaidi ya 200, vitabu zaidi ya 570,000,000 na nakala za magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! zaidi ya 6,400,000,000, na pia mamilioni ya maandikisho ya magazeti—ushuhuda mkubwa wenye kukumbukwa kweli kweli!
18. (a) Ni sifa zipi ambazo jamii ya ukuhani imeonyesha leo? (b) Watu wote wa Mungu wamechochewaje?
18 Tunaweza kuwa wenye furaha kwamba Mashahidi wameendelea mpaka mwaka huu wa 1986. Kufanya mapenzi ya Mungu kumekuwa kazi ngumu, kama wakati ambapo kila mmoja wa wale wanaume 12 alipobeba jiwe lake la ukumbusho mpaka Gilgali. Lakini roho nzuri ya upainia imewaunganisha watu wa kisasa wa Mungu, ikiwachochea ‘wawe hodari na moyo wa ushujaa.’—Zaburi 27:14; 31:24; Sefania 3:9.
19. Katika kurudia matukio zaidi ya siku za Yoshua, tunaweza kuwa na uhakika gani?
19 Matukio mengine katika siku za Yoshua lazima yatutie moyo tusonge mbele, tukiwa na uhakika wa kwamba Yehova atafanya miujiza zaidi kwa ajili ya watu wake. Makala yetu inayofuata itarudia baadhi ya hayo.
[Maelezo ya Chini]
a Asher Goldenberg anaandika hivi katika kichapo Metre and Its Significance in the Bible (Kiebrania) kwamba katika kipindi cha Hekalu la Kwanza, kwa ujumla majina maalum yalipewa umbo mrefu zaidi, yakiunganisha sehemu ya Tetragramatoni, kuonyesha ushikamanifu kwa Yehova. Yeye anatoa maelezo kwamba “katika vitabu vitano vya Musa, Musa analibadili jina la Hoshe ben-Nun liwe ‘Yehoshua’ anapomtuma aende kupeleleza; hivyo alitangulia kuona kwamba [Yoshua] hangemsaliti [Yehova].”
Kuyatafakari Matukio Katika Siku za Yoshua—
◻ Kwa sababu gani ni lazima hayo yaonwe kuwa zaidi ya historia tu?
◻ Tunawezaje kukuza ushujaa na nguvu za kiroho?
◻ Ni kielelezo kipi bora alichotuachia Yoshua?
◻ Ni katika njia zipi Yoshua alimfananisha Yesu?
◻ Ni matukio yapi leo yanayolingana na yale ya Yordani?