Kujua Yaliyo Katika Habari
Je! Ni Jina “Lenye Kuudhi”?
Kutolisema jina la Mungu, kuliandika kutokana na lugha ya awali kuwa YHWH bila kuongeza mambo mengine zaidi ya herufi hizo, na kulitamka kuwa “Bwana,” ni pendekezo linalopasa kukubaliwa, kinasema kichapo cha pindi kwa pindi cha Kikatoliki kinachoitwa Comnuovi tempi. Huo ndio mwitikio uliofanywa kwa ombi lililotokezwa na “Shirika kwa Ajili ya Urafiki wa Wayahudi na Wakristo” la Roma, na ombi hilo lilitiwa sahihi na wanatheolojia na wanachuo mashuhuri wa Kikatoliki na Kiyahudi wote pamoja. Ombi hilo lilitaka kwamba “mashirika ya uchapishaji na wahariri wa magazeti ya kila siku na ya pindi kwa pindi” waache kulitumia jina “Yahweh” kwa sababu ni “lenye kuudhi Wayahudi, ambao wanalifikiria jina la Mungu kuwa lisilotamkika.” Shirika lile linasema kwamba ombi lao la kusihi linategemea “pokeo la muda mrefu la Kiyahudi” ambalo “limedumishwa bila kukatizwa” mpaka leo.
Lakini je! inawapasa Wakristo waongozwe na mapokeo ya Kiyahudi? Je! ingekuwa sawa kwao kuweka jina la Mungu kando na kuepuka kulitamka? Biblia inaonyesha kwamba Mungu anataka watu wote wajue kwamba yeye, ‘aitwaye jina lake Yehova,’ ndiye Aliye Juu Zaidi Sana. (Zaburi 83:18; Ezekieli 38:23; Malaki 3:16) Yesu aliweka mfano katika jambo hili. Badala ya kufuata mapokeo ya Kiyahudi ‘yaliyotangua neno la Mungu,’ yeye alifundisha wafuasi wake kusali hivi: “Acha jina lako litakaswe.” (Mathayo 6:9, NW; 15:6) Na saa chache tu kabla ya kifo chake cha dhabihu, yeye alisema katika sala hivi: “Nami naliwajulisha [wanafunzi] jina lako, tena nitawajulisha hilo.”—Yohana 17:26.
Uchumba: Je! Ni Mkataba?
Mwanamke kijana Mbrazili na mwanamume mchumba wake walikuwa ndiyo sasa tu wamemaliza kuitia fanicha nyumba yao mpya. Mialiko ilikuwa imekwisha kupelekwa, na kila jambo lilionekana kuwa tayari kwa ajili ya arusi yao, iliyokuwa imebakiza siku tatu tu. Kwa kutazamia maisha mapya yake, bibi-arusi alikuwa ameacha kazi yake. Ndipo, bila taarifa yo yote, bwana-arusi akavunja uchumba huo. Kwa kuduwazwa na kukata tamaa, bibi-arusi aliyekataliwa akatafuta msaada wa kisheria. Mwanasheria mwenye kumtetea alitoa hoja ya kwamba ‘uchumba ni mkataba wa hatua ya kwanza, na ukivunjwa bila sababu inayofaa, yule mtu asiye na hatia anapasa kulipwa ridhaa kwa hasara yo yote iliyompata.’ Mahakama ilikubali na kuagiza mwanamume yule ampe mwanamke ambaye alikuwa amechumbia ‘mahari inayolingana na mshahara uliotangulia kuwekwa na sheria kisha alipe gharama za mahakama na malipo ya wanasheria.’ Akitoa maelezo juu ya uamuzi huo, mwanasheria Nereu Mello, aliandika hivi katika gazeti la kila siku la Sao Paulo linaloitwa Jomal da Lapa: “Uchumba ni mkataba mzito sana na kuuvunja hakupuuzwi mbele ya Sheria.”
Wazo hilo la uzito wa uchumba si jipya. Chini ya Sheria ya Musa mwanamke aliyechumbiwa ambaye alitenda uasherati alipokea adhabu iliyo sawa na ya mwanamke mzinzi aliyeolewa. Hivyo yeye alitendwa kwa njia tofauti na mwanamke mseja aliyefanya uasherati. (Kumbukumbu 22:23, 24, 28, 29) Wakati huo wa nyuma uchumba ilionwa kuwa kifungo cha kudumu—kama kwamba watu wale wawili walikuwa tayari wamekwisha kufunga ndoa. (Mathayo 1:19) Wakristo leo pia wanautambua uchumba kuwa hatua nzito. Wao hawauoni kuwa jambo la kuchukuliwa kwa urahisi tu.—Linganisha Mathayo 5:37.
Imerekebishwa Ilingane na Ufundi wa Kisasa
Baada ya Martin Lutheri kulaumu vikali uuzaji masamaha (ondoleo la namna fulani za adhabu ya kutenda dhambi), Kanisa Katoliki la Roma lilifanya zoea hilo liwe haramu katika 1562. Lakini afisa wa Vatikani Pedro Albellan alikazia hivi majuzi kwamba lile fundisho la kuwapa watu masamaha lingali “haliwezi kukanwa na haliwezi kubadilishwa. Kitabu kimoja cha maelezo cha Katoliki ya Roma kinachohusu masamaha kinaonyesha kwamba Vatikani imerekebisha imani hiyo ya kale ilingane na ufundi wa kisasa. Kulingana na gazeti The Times la London, sasa maaskofu wanaweza “kuwapa waaminifu wao samaha kamili kwa kutumia redio au televisheni mara tatu kwa mwaka wakati wao wanapotoa baraka kwa jina la Papa.” Ijapokuwa hivyo, kuna kizuizi kimoja. “Ni lazima hilo lifanywe kupitia utanganzaji ulio hai,” anasema Luigi de Magistris wa Makao Matakatifu ya Kimitume ya Vitubio na Masamaha Katika Vatikani, ambayo ni afisi inayoshughulika na masamaha. “Kutazama kurudiwa kwa kipindi kilichorekodiwa hakutoshi.”
Lakini yawe yanauzwa au mtu anapewa mwenyewe au kupitia televisheni, je! masamaha ya kupewa na padri na kulipiwa yanapatana na Maandiko? Ingawa nyakati nyingine Yesu alisamehe dhambi bure, yeye hakusema lo lote juu ya uhitaji wa masamaha ya kupewa na padri. Wala mitume hawakufanya hivyo. “Damu yake Yesu, Mwana wake [Mungu], yatusafisha dhambi yote,” akaandika mtume Yohana. “Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, atusafishe na udhalimu wote.” (1 Yohana 1:7, 9) Ikiwa dhambi zote zinasamehewa hivyo, ni kitu gani kingine kilichobaki kulipiwa na adhabu au kufunikwa kwa kupewa masamaha ya padri?—Yohana 3:36, Warumi 5:10.