Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w87 3/1 kur. 10-15
  • ‘Juu ya Mnara wa Ulinzi Mimi Ninasimama’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Juu ya Mnara wa Ulinzi Mimi Ninasimama’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wakristo wa Kwanza-kwanza: Wateteaji wa Neno la Mungu
  • Magazeti Yaliyo na Maoni Yenye Kufika Mbali
  • Mnara wa Mlinzi na Amkeni!: Vipiganiaji vya Ukweli
  • “Ee Mlinzi Habari Gani za Usiku?”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Kutumikia Pamoja na Mlinzi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Kukua Katika Ujuzi Sahihi Juu ya Kweli
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Mnara wa Mlinzi na Amkeni!—Majarida ya Wakati Ufaao Yenye Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
w87 3/1 kur. 10-15

‘Juu ya Mnara wa Ulinzi Mimi Ninasimama’

“Na yeye akaendelea kuita kwa sauti kuu kama simba: ‘Juu ya mnara wa ulinzi, O Yehova, mimi ninasimama daima mchana, na kwenye kituo changu cha kutunzia zamu mimi ninakuwa huko mausiku yote.’”​—ISAYA 21:8, NW.

1, 2. (a) Ni mradi gani aliokuwa nao C. T. Russell? (b) Vitabu vya Kibiblia vingesaidiaje kutimiza mradi wake?

MWANAMUME mcha-Mungu mwenye umri wa miaka 21 anayeishi kaskazini-mashariki mwa United States alikuwa na utume. Ulikuwa mradi wake kuyafunua mafundisho ya uwongo ya kidini ya siku zake, hasa mafundisho ya mateso ya milele na watu kuandikiwa mambo yatakayowapata maishani. Pia, yeye alitaka kuutetea ukweli juu ya ukombozi na kusudi na jinsi ya kuja kwa Kristo. Yeye angefanyaje yote hayo? Ni kwa kuangaza nuru ya Neno la Mungu, Biblia Takatifu, juu ya imani za kidini.—Zaburi 43:3; 119:105.

2 Charles T. Russell, msimamizi wa Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi, ndiye aliyekuwa mwanamume huyo, naye aliamua katika 1873 kuchapisha vitabu vya kidini viwe njia ya kuangaza ukweli wa Biblia kama upasavyo. Kwa wasomaji wenye mioyo myeupe, vichapo hivyo vingefunua nyufa zilizo katika mafundisho yanayoshikiliwa sana na Jumuiya ya Wakristo. Kasoro zo zote za kimafundisho zilizofichwa hazingeepuka kumulikwa na nuru yenye nguvu ya Biblia? (Waefeso 5:13) Wakati ule ule, vitabu hivyo vingekaza fikira juu ya ‘fundisho lenye afya’ ili kujenga imani ya wasomaji. (Tito 1:9; 2:11, NW; 2 Timotheo 1:13) Je! juhudi kwa ajili ya ukweli wa Biblia iliyomsukuma Russell katika utafutaji wake ilikuwa na kanuni ya mwongozo?—Linganisha 2 Wafalme 19:31.

Wakristo wa Kwanza-kwanza: Wateteaji wa Neno la Mungu

3. Kristo Yesu aliuwekaje mwendo wa kuupigania ukweli?

3 Wakristo wa karne ya kwanza walitetea matumizi ya Neno la Mungu miongoni mwa Wayahudi na watu wa Mataifa. Walisimama kama kwamba walikuwa juu ya mnara wa mlinzi, wakiwatangazia ukweli wote ambao wangetaka kusikia. (Mathayo 10:27) Kiongozi wao, Yesu Kristo, ndiye aliyewawekea mwendo. Yeye alisema: “Mimi nimezaliwa kwa ajili ya haya, na kwa ajili ya haya mimi nalikuja ulimwenguni, ili niishuhudie kweli.” (Yohana 18:37) Ingawa alikuwa mkamilifu, yeye alikataa kutegemea hekima yake mwenyewe au maoni yake binafsi. Bali, mafundisho yake yalitokana na Mwalimu Mkuu Zaidi wake, Yehova Mungu. “Sifanyi neno kwa nafsi yangu,” yeye akaambia kikundi cha Wayahudi. “Ila kama Baba alivyonifundisha ndivyo ninenavyo.” (Yohana 8:28; ona pia Yohana 7:14-18.) Kulingana na masimulizi ya Injili ya huduma yake ya kidunia, yeye alijulikana kuwa alitaja-taja au akanena fikira zenye ulinganifu na vifungu vilivyotokana na karibu nusu ya vitabu vya Maandiko ya Kiebrania.—Luka 4:18, 19; Isaya 61:1, 2, (Zaburi 31:5), Luka 23:46.

4. Toa mifano ya jinsi Yesu alitumia Neno la Mungu kufundisha ukweli.

4 Hata baada ya kufa na kufufuliwa kwake, bado Kristo alikuwa akitumia Neno la Mungu kufundisha ukweli. Kwa mfano, wakati Kleopa na mwandamani wake walipokuwa wakisafiri kutoka Yerusalemu kwenda Emau, Yesu alisaidia wanafunzi hao kufikiri kwa kuziona sababu za Maandiko. Usimulizi unasema hivi: “Akaanza kutoka Musa na manabii wote, akawaeleza katika maandiko yote mambo yaliyomhusu yeye mwenyewe.” (Luka 24:25-27) Baadaye siku iyo hiyo, Yesu aliwatokea mitume 11 na wengine wa wanafunzi wake ili kujenga imani yao. Jinsi gani? Kwa matumizi ya ustadi ya Maandiko. Luka anaandika: “Ndipo [Yesu] akawafunulia akili zao wapate kuelewa na maandiko. Akawaambia, Ndivyo ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya tatu.”—Luka 24:45, 46.

5. Kwenye Pentekoste 33 W.K., Petro alifuataje mfano wa Kristo katika kuyatumia Maandiko?

5 Kwa kufuata Mweka-mfano walo, katika mwaka 33 W.K. kundi la Kikristo lilianza huduma ya peupe kwa matumizi ya Maandiko. Mazingira ni eneo la waziwazi nje ya nyumba moja katika Yerusalemu. Baada ya kusikia uvumi wa “upepo wa nguvu ukienda kasi” kutoka nyumba hiyo, kutano la maelfu ya Wayahudi wa Yerusalemu na wasafiri Wayahudi wanavutiwa kwenye mahali hapo na kukusanyika. Petro anapiga hatua kwenda mbele—mitume wale wengine 11 wamemzunguka—na kwa sauti yenye nguvu nyingi yeye anaanza kunena hivi: “Watu wa Yudea na ninyi nyote wakaaji wa Yerusalemu, acheni jambo hili lijulikane kwenu na mtege sikio kwenye semi zangu.” Ndipo akionyesha “mambo yaliyosemwa na nabii Yoeli” na yale ambayo “Daudi anasema,” Petro anaeleza maana ya miujiza ambayo kutano hilo la watu limetoka kushuhudia sasa hivi na kwamba “Mungu alimfanya yeye kuwa Bwana na Kristo pia, Yesu huyo ambaye ninyi mlitundika mtini.”—Matendo 2:2, 14, 16, 25, 36.

6. (a) Eleza jambo lililotukia kwenye mkutano mmoja wa baraza lenye kuongoza la karne ya kwanza. (b) Makundi yalipashwaje habari juu ya uamuzi wa baraza lenye kuongoza, na kulikuwa na manufaa gani?

6 Wakati Wakristo wa kwanza-kwanza walipohitaji habari za kuwaelewesha wazi juu ya imani na mwenendo, baraza lenye kuongoza la karne ya kwanza lilifanya pia matumizi mazuri ya Maandiko. Kwa mfano, kwenye mkutano wa baraza lenye kuongoza katika mwaka 49 W.K., mwanafunzi Yakobo, akitenda kama mwenyekiti, anakaza fikira zao juu ya andiko linalofaana sana na habari hiyo linalopatikana kwenye Amosi 9:11, 12. “Ndugu zangu, nisikilizeni,” yeye anasema. “Simeoni ametueleza jinsi Mungu hapo kwanza alivyowaangalia Mataifa ili achague watu katika hao kwa ajili ya jina lake. Na maneno ya manabii yapatana na hayo, kama ilivyoandikwa.” (Matendo 15:13-17) Baraza zima lilikubaliana na pendekezo hilo la Yakobo na ndipo wakaandika uamuzi wao wenye kutegemea Maandiko ili kwamba uweze kupelekwa kwenye makundi yote na kusomwa nayo. Matokeo yalikuwa nini? Wakristo hao “walifurahia sana kitia-moyo hicho,” na “makundi yakaendelea kuthibitika kweli kweli katika imani na kuongezeka katika hesabu siku kwa siku.” (Matendo 15:22-31; 16:4, 5, NW) Hivyo, kundi la kwanza-kwanza la Kikristo likawa “nguzo na tegemezo la ukweli.” Lakini namna gani historia ya kisasa? Je! C. T. Russell na wanafunzi wa Biblia wenzake wangeiga mfano huo mzuri sana wa karne ya kwanza? Wao wangeupiganiaje ukweli?—1 Timotheo 3:15, NW.

Magazeti Yaliyo na Maoni Yenye Kufika Mbali

7. (a) Kusudi la Mnara wa Mlinzi wa Sayuni lilikuwa nini? (b) Lilitegemea nani kwa msaada?

7 Julai 1879 uliona kuzaliwa kwa kisafarishaji kikuu cha Russell cha nuru ya elimu ya Biblia—Mnara wa Mlinzi wa Sayuni na Mtangaza Habari za Kuwapo kwa Kristo (katika Kiingereza). Toleo la kwanza lilionyesha wazi kusudi bora la gazeti hilo: “Kama vile jina lalo linavyoonyesha, gazeti hili lina shabaha ya kuwa ndilo mahali pa kuchungulia mambo ambapo habari za upendezi na faida zinaweza kutangazwa kwa ‘kundi dogo,’ na kuwatolea ‘nyama katika majira yapasayo’ wale ‘watu wa nyumba ya imani,’ “likiwa ndilo Mtangaza Habari za Kuwapo kwa Kristo.’ Msingi wa gazeti hilo ulikuwa kuweka tumaini katika Mungu Mwenye Nguvu Zote. Toleo lalo la pili lilisema: “Tunaamini ‘Mnara wa Mlinzi wa Sayuni’ linaungwa mkono na YEHOVA, na maadamu ndivyo ilivyo halitaomba kamwe wala kusihi wanadamu walisaidie. Wakati Yeye anayesema: ‘Dhahabu yote na fedha ya milimani ni vyangu,’ atakapokosa kutoa pesa zilizo za lazima, tutafahamu ni wakati wa kuacha kulichapa.”

8. Eleza ukuzi wa Mnara wa Mlinzi kulingana na Isaya 60:22 na Zekaria 4:10.

8 Mnara wa Mlinzi wa Sayuni, ambalo sasa ni Mnara wa Mlinzi, limeendelea kuchapishwa kwa miaka zaidi ya 107 sasa. Limekua likaacha kuwa gazeti la kila mwezi lenye nakala 6,000 lenye kupigwa chapa katika lugha moja likawa gazeti la mara mbili kwa mwezi lenye nakala 12,315,000 linalopatikana katika lugha 103.—Linganisha Isaya 60:22; Zekaria 4:10.

9. Kichwa Mnara wa Mlinzi kilikuwaje chenye kufaa?

9 Kichwa hicho, Mnara wa Mlinzi wa Sayuni, kilikuwa uchaguzi unaofaa uliofanywa na Russell. Neno linalotumiwa kwa kawaida katika Maandiko ya Kiebrania kwa “mnara wa ulinzi” linamaanisha “mahali pa kuchungulia mambo” au “kituo cha kutazamia,” ambapo kutoka hapo mtunza-zamu angeweza kuona adui kwa urahisi akiwa mbali na kutoa onyo la mapema juu ya kukaribia kwa hatari. Basi, kwa miaka 59 ya kwanza ya kuchapishwa kwa gazeti hilo ilifaa kwamba ukurasa wenye kichwa ukawa na mtajo huu wenye mwito wa ushindani kutokana na Isaya 21:11, 12, Biblia ya King James Version: “Mlinzi, Usiku Una Nini?” “Asubuhi Yaja.”

10. Leo ni nani aliye mlinzi wa Isaya 21:11, naye anatangaza ujumbe gani?

10 Mlinzi wa unabii wa Isaya aliyewekwa mahali pa kuchungulia alikuwa anakaribia kupiga hatua kuja mbele. Kati ya hali mbovu ya giza la dunia iliyokuwako, Russell alikuwa ametangaza kwa furaha habari njema za “asubuhi” iliyokuwa ikija. Utawala wa Mileani wa Yesu Kristo wa amani ndicho kichwa cha taarifa hiyo ya habari inayofurahisha. Lakini kabla “asubuhi” haijafika, jamii inayotumika kama mlinzi—mabaki ya Israeli wa kiroho leo—inaonya kwa ujasiri juu ya kuendelea kwa “usiku,” ambako kutafikia hatua iliyo na giza jingi zaidi katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har–Magedoni.—Ufunuo 16:14-16.

11, 12. (a) Maneno ya Isaya 21:8 yanaonyeshaje kwamba jamii ya mlinzi ina uaminifu na iko chonjo? (b) Ripoti ya leo inakuja kupitia chombo gani, na sana-sana inaenezwaje?

11 Mapema kidogo, katika Isaya 21:8, NW, tunapewa utangulizi kuhusu mlinzi huyo mwaminifu kwa maneno haya: “Na yeye akaendelea kuita kwa sauti kuu kama simba; ‘Juu ya mnara wa ulinzi, O Yehova, mimi ninasimama daima mchana, kwenye kituo changu cha kutunzia zamu mimi ninakuwa huko mausiku yote.’”

12 Piga picha katika akili yako uone mlinzi akiwa katika mnara ulioinuka juu, akiwa ameegemea mbele, akitazama sana kwenye upeo wa macho wakati wa nuru ya mchana, akikaza sana macho yake yalipenye giza wakati wa usiku—sikuzote akiwa chonjo. Sasa umepata wazo kuu linalotolewa na Neno la Kiebrania kwa “mnara wa ulinzi” (mits·peh’) kama lilivyotumiwa katika Isaya 21:8 (NW). Kwa kuwa mlinzi huyo anakesha sana, ni nani mwenye akili nzuri ambaye angetilia shaka ripoti yake yenye kutangazwa wazi sana? Vilevile leo, jamii ya mlinzi imejitahidi sana kwa kuyachunguza-chunguza Maandiko waone mambo ambayo Yehova ameuwekea huu mfumo wa mambo. (Yakobo 1:25) Ndipo mlinzi huyo anapopaaza sauti kutangaza ujumbe huu bila woga, sana-sana kupitia kurasa za Mnara wa Mlinzi. (Linganisha Amosi 3:4, 8.) Gazeti hili halitajikunyata kamwe kwa kuogopa kuupigania ukweli!—Isaya 43:9, 10.

13. Ni jarida gani jenzi lililotokea katika 1919, nalo lina kusudi gani kama lile jingine?

13 Oktoba 1, 1919, gazeti jipya lilitokea katika jukwaa la ulimwengu: The Golden Age.a Jamii ya mlinzi ingetumia chombo hicho kama jarida jenzi la Mnara wa Mlinzi. Ingawa makala zalo hazingepekua ndani ya habari za Biblia kwa kina kirefu kama zile zilizo katika Mnara wa Mlinzi, hilo pia lingewafanya wanadamu wawe chonjo kuona mafundisho ya dini ya uwongo, uharibifu unaokuja wa mfumo wa mambo maovu ya sasa, na dunia mpya inayokuja ya uadilifu. Ndiyo, hilo pia lingeupigania ukweli!

14. Shabaha ya gazeti Consolation, na baadaye Amkeni!, ilikuwa nini?

14 Miaka kumi na minane baadaye lile jina The Golden Age lilibadilishwa likawa Consolation. “Jina jipya hilo linasimamia ukweli,” likasema toleo la Oktoba 6, 1937. Consolation likawa Amkeni! kuanzia toleo la Agosti 22, 1946 (katika Kiingereza). Katika toleo hilo, gazeti hilo lilitoa ahadi hii hakika: “Shabaha kubwa zaidi ya gazeti hili itakuwa kushika ukamilifu wa kusema ukweli.” Mpaka leo, halijashindwa kutimiza ahadi hiyo. Kwa njia isiyo na kifani, magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yanauinua ukweli juu ili watu wote wauone. Kwa kufanya hivyo magazeti hayo yanakifuata kijia kilichotayarishwa na kundi la Kikristo la kwanza-kwanza.—3 Yohana 3, 4, 8.

Mnara wa Mlinzi na Amkeni!: Vipiganiaji vya Ukweli

15. (a) Ni njia gani ya kutolea chakula cha kiroho leo inayofanana na ile iliyokuwa katika kundi la Kikristo la kwanza-kwanza? (b) Zaidi ya kunakili maneno ya vifungo vya Biblia, ni jambo gani jingine linalohitajiwa? Toa mifano.

15 Jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” yule “mlinzi,” inatumia leo gazeti Mnara wa Mlinzi chini ya mwelekezo wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova liwe kipitio chao kikuu cha kutolea “chakula [cha kiroho] kwa wakati wake.” (Mathayo 24:45) Jambo hilo linafuata kielelezo cha kundi la karne ya kwanza, ambalo lilizitia habari za kuelewesha mambo ya fundisho na maadili kwa namna ya maandishi ili “ndugu wote wasomewe.” (1 Wathesalonike 5:27) Tangu pale pale mwanzoni mwalo, Mnara wa Mlinzi limekuwa gazeti lenye kutumia Biblia na kufundisha Biblia. Kwa mfano, toleo la kwanza la Mnara wa Mlinzi wa Sayuni lilinakili maneno au kutaja bila maneno maandiko zaidi ya 200 kutokana na angalau vitabu mbalimbali vya Biblia 30. Lakini mengi yanahitajiwa zaidi ya kunakili tu maneno ya mistari ya Biblia. Watu wanahitaji msaada ili wayafahamu. Sikuzote gazeti Mnara wa Mlinzi limeongezea watu uwezo wa kufahamu Biblia. Kuanzia 1892 mpaka 1927 kila toleo lilichapa habari za Biblia za kusoma kila juma na mazungumzo ya kifungu kikuu kutokana na kila usomaji. Ili upate mifano mingine, ona chati yenye kichwa Makala za Mnara wa Mlinzi Zenye Kufanyiza Historia Yetu, Mwongo kwa Mwongo.”

16, 17. Mhariri wa kwanza wa Mnara wa Mlinzi alifanya nini kuhakikisha kwamba sikuzote gazeti hilo lingepigania ukweli wa Biblia?

16 Gazeti Mnara wa Mlinzi lingedumishaje usafi wa ujumbe wenye kuchapwa nalo? Mhariri wa kwanza wa gazeti hilo, C. T. Russell alianzisha njia za ulinzi ili kuhakikisha kwamba mambo yenye kuchapwa katika Mnara wa Mlinzi yalikuwa ndiyo ukweli kama ulivyofahamiwa wakati huo. Moja ya njia hizo za kuzuia makosa inatambulishwa katika wasia wake uliofanywa Juni 27, 1907. (Russell alikufa Oktoba 31, 1916.) Wasia wake unasema:

“Mimi naelekeza kwamba kabidhi yote ya uhariri wa MNARA WA MLINZI WA SAYUNI itakuwa mikononi mwa halmashauri ya ndugu watano, ambao mimi nawasihi wawe na uangalifu mkuu na uaminifu kwa ukweli. Makala zote zenye kutokea katika safu za MNARA WA MLINZI WA SAYUNI zitakuwa na kibali kamili cha angalau watatu wa halmashauri hiyo ya watano, nami nahimiza kwamba jambo lo lote linalokubaliwa na watatu hao likijulikana au lionwe kuwa tofauti na maoni ya mmoja au wote wawili wa wale washiriki wengine wa halmashauri, makala hizo zitangojezwa ili kwanza zifikiriwe, sala itolewe na mazungumzo yafanywe kwa miezi mitatu kabla hazijachapishwa—ili kwa kadiri inayowezekana umoja wa imani na vifungo vya amani vidumishwe katika usimamizi wa uhariri wa jarida hilo.”

17 Kila mshiriki wa Halmashauri ya Uhariri, kulingana na wasia wa Russell alipaswa kuwa “mshikamanifu kabisa kwa mafundisho ya Maandiko,” nao walipaswa kuonyesha vitabia vikuu vya “usafi wa maisha, ufahamu usio na makosa katika ukweli, juhudi kwa Mungu, upendo kwa akina ndugu na uaminifu kwa Mkombozi.” Pia, Russell aliweka sharti la kwamba “haitaonyeshwa kwa namna yo yote ni nani ameziandika makala mbalimbali zenye kutokea katika jarida hilo . . . ili kwamba ukweli upate kutambuliwa na kuthaminiwa kulingana na ustahili ulio nao wenyewe, na ili Bwana hasa ndiye apate kutambuliwa kuwa Kichwa cha kanisa na chemchemi ya ukweli.”

18. Kwa sababu gani sisi tunaweza kuyasoma magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa uhakika?

18 Kufikia leo Baraza Linaloongoza linafuata miongozo kama iyo hiyo. Kila makala katika magazeti yote mawili, Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, na kila ukurasa, kutia na ile michoro iliyomo, inachunguzwa kwa makini sana na washiriki waliochaguliwa wa Baraza Linaloongoza kabla haijachapwa. Zaidi ya hilo, wale wanaosaidia kuandika makala kwa ajili ya Mnara wa Mlinzi ni wazee Wakristo wanaothamini uzito wa mgawo wao. (Linganisha 2 Nyakati 19:7.) Wao wanatumia saa nyingi katika kupekua-pekua Biblia na vifaa vingine vyenye marejezo ili kuhakikisha kwamba yanayoandikwa ndiyo ukweli na kwamba yanafuata Maandiko kwa uaminifu. (Mhubiri 12:9, 10; 2 Timotheo 1:13) Si jambo lisilo la kawaida makala moja ya gazeti—ambayo huenda wewe ukaisoma kwa dakika 15—kuchukua kuanzia majuma mawili mpaka zaidi ya mwezi mmoja ikitayarishwa.

19. Wewe unaweza kufanya nini uupiganie ukweli wa Biblia?

19 Basi, wewe unaweza kuyasoma magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa uhakika. Lakini unaweza kufanya zaidi ya hilo. Unaweza kuwatolea wengine magazeti hayo kwa shauku ili wao pia waweze kujifunza ukweli na kupata manufaa kutokana na kusikia ujumbe mbalimbali wa yule ‘mlinzi anayesimama juu ya mnara wa ulinzi.’ (Isaya 21:8, NW) Ndiyo, ukiwa pamoja na mlinzi huyo wa kisasa, wewe pia unaweza kupigania ukweli wa Biblia.

[Maelezo ya Chini]

a Jambo la kupendeza ni kwamba, wasomaji fulani walikatishwa tamaa hapo kwanza na muundo wa jalada la The Golden Age. Kwao ulionekana kuwa wa kikawaida mno. Kwa kujibu, ripoti ya kila mwaka ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi ilisema: “Kuhusiana na jambo hilo sisi tungedokeza kwamba wakati ule ule kulipoanza kuchapishwa kwa The Golden Age kulikuwa na mgomo wa wachapaji katika Greater New York. Siku chache tu kabla ya hapo, mkataba ulikuwa umefanywa wa kuchapisha The Golden Age na watu wale waliokuwa wakiziendesha mashine za uchapaji zinazotumia aina ya karatasi na jalada lililotumiwa katika gazeti hilo hawakufanya mgomo. Hivyo ilielekea kuwa kwamba hali ya jalada na karatasi ilikuwa imechaguliwa kwa uongozi wa kimungu, kwa sababu kama karatasi na jalada la aina nyingine lingalikuwa limechaguliwa haingaliwezekana hata kidogo kuanza kulichapa gazeti hilo. Hivyo Bwana alielekea kuwa alipendelea kichapo hicho kichanga sana.”

Je! Wewe Unakumbuka?

◻ Kwa sababu gani C. T. Russell akaanza kuchapisha vitabu vya Kibiblia?

◻ Wakristo wa kwanza-kwanza waliupiganiaje ukweli?

◻ Kwa sababu gani neno“Mnara wa Mlinzi” limo katika kichwa cha gazeti hili?

◻ Ni nani “mlinzi” wa kisasa, na ni chombo gani hasa anachotumia ili kukuza sauti yake?

◻ Magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yanapiganiaje ukweli wa Biblia?

[Chati katika ukurasa wa 13]

Makala za Mnara wa Mlinzi Zenye Kufanyiza Historia, Mwongo kwa Mwongo

1879 “Mungu Ni Upendo”—ilipigania dhabihu ya ukombozi ya Yesu kuwa ndiyo msingi wa kukombolewa kwa wanadamu

1879 “Kwa Nini Uovu Uliruhusiwa”—ilieleza sababu kuwapo kwa Yesu Kristo kusingeonekana

1880 “Mwili Mmoja, Roho Moja, Tumaini Moja”—ililenga kabisa 1914 kuwa mwisho wa Nyakati za Mataifa

1882 “Mshahara wa Dhambi Ni Mauti”—ilifunua fundisho la mateso ya milele kuwa ni kukana upendo wa Mungu

1885 “Mageuzi na Kipindi cha Ubongo”—ilifunua nadharia ya mageuzi kuwa si ya kweli

1897 “Maandiko Yanasema Nini Juu ya Upashanaji Habari na Ulimwengu wa Roho?“—ilitoa uthibitisho wa kwamba mashetani ndio chanzo cha upashanaji habari na roho waovu

1902 “Mungu Kwanza—Kuweka Rasmi Kwake”—ilikazia kutii sheria ya Mungu katika jamaa na katika shughuli za kibiashara

1919 “Wabarikiwa Ni Wasioogopa”—ilileta uhai mpya kwenye tengenezo lenye kuamka la waabudu wasioogopa

1925 “Kuzaliwa kwa Lile Taifa”—ilielewesha wazi mambo ya unabii yenye kuonyesha kwamba Ufalme wa Mungu ulizaliwa katika 1914

1931 “Jina Jipya”—kuanzia hapa na kuendelea jina Mashahidi wa Yehova lingetofautisha Wakristo wa kweli na Jumuiya ya Wakristo yenye kuasi imani

1935 “Ule Umati Mkubwa”—ilionyesha kwamba kukusanywa kwa wale ambao wangeishi milele duniani kulikuwa kukiendelea

1938 “Tengenezo”—ilitoa utangulizi wa mpango wa kitheokrasi kweli kweli miongoni mwa Mashahidi wa Yehova

1939 “Kutokuwamo”—iliimarisha Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wavumilie mikazo ya Vita ya Ulimwengu ya Pili

1942 “lle Nuru Pekee”—ilitangaza kiishara cha ‘kusonga mbele na’ kazi ya ushujaa ya kutoa ushahidi

1945 “Wasioondoleka kwa Ajili ya Ibada Inayofaa”—ilionyesha kwamba ni lazima Wakristo wajiepushe na kutiwa damu mishipani

1952 “Kuliweka Tengenezo Likiwa Safi”—ilionyesha kwamba hatua ya makundi ya kutenga watu na ushirika ni ya Kimaandiko

1962 “Kujitiisha Chini ya ‘Mamlaka Zilizo Kuu’—Kwa Sababu Gani?”—ilitoa sababu za kujitiisha kwa kiasi chini ya mamlaka za kibinadamu

1973 “Kuliendeleza Kundi la Mungu Likiwa Safi Katika ‘Wakati wa Hukumu Yake’”—ilihimiza kuepuka kabisa matumizi ya tumbaku

1979 “Juhudi kwa Nyumba ya Yehova”—ilirudia kwamba kuhubiri nyumba kwa nyumba kunafuata kielelezo cha kimitume

1982 “Wapendwa Jiendelezeni Mkiwa Katika Upendo wa Mungu”—iliwaweka Wakristo chonjo kuona njia ya utendaji wa waasi-imani

1983 “Kutembea Pamoja na Mungu Katika Ulimwengu Wenye Jeuri”—ilithibitisha kwamba ni lazima Wakristo wasihusike kamwe na jeuri

1984 “Zizi la Karibuni kwa Ajili ya “Kondoo Wengine”—ilieleza wazi jinsi jamii hii ya kidunia imeletwa katika umoja pamoja na wale walio katika “zizi” la agano jipya

1987 “Yubile ya Kikristo Yafikia Upeo Katika Mileani” —ilionyesha jinsi Wakristo wote washikamanifu wanavyopata uhuru na uzima

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki