Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Ni nini linalomaanishwa kwenye 2 Samweli 18:8, andiko linalosema hivi: “Msitu ukala watu wengi kuliko wale walioliwa na upanga”?
Absalomu mwana wa Mfalme Daudi mwenye umbo zuri alinyakua kiti cha kifalme na akalazimisha baba yake aukimbie Yerusalemu. Baada ya hapo, katika msitu wa Efraimu (labda mashariki mwa Mto Yordani) pigano lilitukia kati ya majeshi ya Absalomu na watu wale waliokuwa washikamanifu kwa mfalme mpakwa mafuta wa Yehova, Daudi. Usimulizi kwenye 2 Samweli 18:6, 7 unaripoti kwamba katika pigano hilo kali wanaume wa Daudi walichinga waasi 20,000. Kwa sehemu, mstari unaofuata unaongezea hivi: “Na siku ile huo msitu ukala watu wengi kuliko wale walioliwa na upanga.”
Wengine wamedokeza kwamba maneno hayo yanarejeza kwenye askari waasi wakimezwa na wanyama-mwitu wenye kukaa katika msitu. (1 Samweli 17:36:2 Wafalme 2:24) Lakini kuliwa halisi hivyo na wanyama hakuhitaji kuwa ndiko kunakomaanishwa, kama vile isivyohitaji kumaanishwa kihalisi kwamba “upanga” ndio uliowala waliochingwa katika pigano. Kwa kweli, pigano hilo ‘lilienea huko juu ya uso wote wa nchi [ambayo ilikuwa ikionekana].’ Kwa hiyo elezo linaloelekea zaidi kuwa ndilo linalofaa ni kwamba wanaume wa Absalomu waliokimbizwa, waliokuwa wakikimbia kwa woga wa ghafula kupitia msitu huo wenye miamba-miamba, labda walitumbukia katika mashimo na mabonde yaliyofichika, na wakanaswa katika vichaka vya chini vilivyosongamana sana. Jambo la kupendeza ni kwamba, usimulizi unaendelea kueleza kwamba Absalomu mwenyewe akawa jeruhi wa msitu huo. Inaonekana kwamba kwa sababu ya nywele zake nyingi, kichwa chake kilinaswa katika mti mkubwa, jambo hilo likimwacha wazi bila msaada katika hatari ya kupata ushambulizi wenye kuleta kifo wa Yoabu na wanaume wake. Mzoga wa Absalomu ‘ulitupwa katika shimo kubwa msituni, wakaweka juu yake chungu kubwa sana la mawe.’ —2 Samweli 18:9-17.