Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w87 4/15 kur. 15-20
  • Ongeza Amani Yako Kupitia Maarifa Sahihi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ongeza Amani Yako Kupitia Maarifa Sahihi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Maarifa Sahihi ya Mungu”
  • Maarifa Sahihi ya Kristo
  • Uhitaji wa Kuchukia Uovu
  • Kukabiliana na Balaa Zenye Kuharibu Amani
  • Maarifa ya Kibinafsi Hutoa Amani
  • Na Tulikweze Jina la Yehova Pamoja
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Kwa Nini Sisi Twahitaji Maarifa Sahihi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Zawadi Inayotoka kwa Yehova Mwenyewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Sikuzote Umtwike Yehova Mzigo Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
w87 4/15 kur. 15-20

Ongeza Amani Yako Kupitia Maarifa Sahihi

“Na mwongezewe fadhili zisizostahilika na amani kupitia maarifa sahihi ya Mungu na ya Yesu Bwana yetu.”​—2 PETRO 12, NW.

1, 2. (a) Ni kwa sababu gani uhusiano wenye amani pamoja na Mungu unaweza kulinganishwa na ndoa? (b) Sisi tunaweza kutiaje nguvu amani yetu pamoja na Mungu?

ULE uhusiano wenye amani ulioanzishwa pamoja na Mungu wakati wa ubatizo wako, katika njia fulani, ni kama ndoa. Ingawa siku ya arusi ni yenye kufurahisha, huo ni mwanzo tu wa uhusiano wenye thamani kubwa. Kwa jitihada, wakati, na ujuzi, uhusiano wa ndoa utakua uwe wenye thamani hata zaidi, upate kuwa mahali pa kupumzikia wakati wa taabu. Hivyo, pia, kwa bidii na msaada wa Yehova, wewe unaweza kuongeza amani yako pamoja naye.

2 Mtume Petro alieleza jinsi wale waliokuwa ‘wamepata imani’ wangeweza kutia nguvu amani yao pamoja na Mungu. Yeye aliandika: “Na mwongezewe fadhili zisizostahilika na amani kupitia maarifa sahihi ya Mungu na ya Yesu Bwana yetu.”—2 Petro 1:1, 2, NW.

“Maarifa Sahihi ya Mungu”

3. Kuwa na maarifa sahihi ya Yehova na Yesu kunamaanisha nini?

3 Neno la Kigiriki kwa “maarifa sahihi” (e·piʹgno·sis) lililotumiwa katika habari hii lamaanisha maarifa yenye kina kirefu zaidi, ya ndani zaidi. Namna ya kitenzi inaweza kuelekeza kwa maarifa yaliyopatikana kwa mambo ambayo mtu binafsi anajionea na inafasiriwa “jua kikamili” kwenye Luka 1:4, NW. Mwanachuo Mgiriki Culverwel anaeleza kwamba kwake yeye neno hilo linadokeza ‘kufahamu vizuri zaidi jambo nililojua hapo kwanza; kuona kitu kwa uhalisi zaidi ambacho nilikuwa nimeona hapo kwanza kikiwa mbali.’ Kupata “maarifa sahihi” kama hayo kunatia ndani kupata kumjua Yehova na Yesu Kristo kwa ukaribu zaidi wakiwa watu, kupata kufahamu vizuri zaidi sifa zao.

4. Sisi tunaweza kuongezaje maarifa yetu ya kumjua Mungu, na ni kwa sababu gani jambo hilo linaendeleza amani yetu pamoja naye?

4 Njia mbili za kupata maarifa hayo ni kupitia mazoea mazuri ya funzo la kibinafsi na kuhudhuria kwa ukawaida mikutano ya watu wa Mungu. Katika njia hizo utajifunza kwa njia iliyo wazi zaidi jinsi Mungu anavyojiendesha mwenyewe na analofikiria. Utafanyiza akilini mfano wa utu wake ulio wazi zaidi. Lakini kumjua Mungu kwa ukaribu kunamaanisha kuiga na kuonyesha mfano huo. Kwa mfano, Yehova alieleza mtu aliyeonyesha kutokuwa na ubinafsi kwa kimungu, kisha Yeye akasema: “Je! huku siko kunijua’”? (Yeremia 22:15, 16; Waefeso 5:1) Kumwiga Mungu kwa ukaribu zaidi kunaongeza amani yako pamoja naye kwa sababu wewe unafanya maendeleo katika kuvaa utu mpya, “ambao kupitia maarifa sahihi unafanywa mpya kulingana na mfano wa Yeye aliyeuumba.” Unakuwa mwenye kumpendeza Mungu zaidi.—Wakolosai 3:10, NW.

5. (a) Maarifa sahihi yalimsaidiaje mwanamke mmoja Mkristo? (b) Ni katika njia zipi tunaweza kumwiga Yehova kwa ukaribu zaidi?

5 Mwanamke mmoja Mkristo anayeitwa Lynn aliliona kuwa jambo gumu kusamehe kwa sababu ya kufahamiana vibaya na Mkristo mwenzake. Lakini funzo la kibinafsi la uangalifu la Lynn lilimfanya achunguze mwelekeo wake. “Mimi nilikumbuka Yehova ni Mungu wa namna gani, jinsi yeye haweki kinyongo,” akakubali. “Mimi nilifikiria yale mambo yote madogo madogo tunayomfanyia Yehova kila siku, lakini yeye haweki hesabu yayo. Jambo hili kati yangu na dada yangu Mkristo lilikuwa dogo sana kwa kulinganisha. Kwa hiyo kila nilipomwona, nilijiambia, ‘Yehova anampenda kama vile anavyonipenda mimi.’ Hilo lilinisaidia kushinda tatizo hilo.” Je! wewe unaona sehemu ambazo katika hizo wewe pia unahitaji kumwiga Yehova kwa ukaribu zaidi?—Zaburi 18:35:103:8, 9; Luka 6:36; Matendo 10:34, 35; 1 Petro 1:15, 16.

Maarifa Sahihi ya Kristo

6. Yesu Kristo alionyeshaje kwamba ile kazi ya kuhubiri ilikuwa ndiyo ya maana zaidi kwake?

6 Kuwa na maarifa sahihi ya Yesu kunataka kuwa na “akili ya Kristo” na kumwiga. (1 Wakorintho 2:16, NW) Yesu alikuwa mtangazaji wa ukweli mwenye shauku. (Yohana 18:37) Roho yake yenye bidii nyingi ya kueneza evanjeli haikuzuiwa na chuki za kijamii zisizo na msingi. Ingawa Wayahudi wengine walichukia Wasamaria, yeye alimtolea ushuhuda mwanamke Msamaria kando ya kisima. Kwani, hata kuzungumza kwa muda mrefu na mwanamke ye yote hadharani huenda kulikunjiwa uso!a Lakini Yesu hakuruhusu hisia za kijamii zimzuie kutoa ushuhuda. Kazi ya Mungu ilikuwa yenye kuburudisha. Yeye alisema: “Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake.” Furaha ya kuona itikio la watu, kama yule mwanamke Msamaria na watu wengi wa mji wake, kulimtegemeza Yesu kama chakula. —Yohana 4:4-42; 8:48.

7. (a) Maarifa ya kumjua Kristo yapaswa yatusukume sisi tufanye nini? (b) Je! Mungu anatazamia watumishi wake wote wafanye kiasi kile kile cha kuhubiri? Eleza.

7 Je! wewe unahisi kama alivyohisi Yesu? Inakubalika, kuanzisha mazungumzo juu ya Biblia na mtu usiyemjua ni jambo gumu kwa wengi, na mara nyingi linakunjiwa uso na wengine katika ujamii. Lakini. ili kuwa na mwelekeo wa akili kama ule wa Yesu, hatuwezi kuepuka uhakika huu: Lazima tutoe ushuhuda. Bila shaka si wote wanaoweza kufanya kiasi kile kile cha kuhubiri. Hicho kinatofautiana kulingana na uwezo na hali zetu mbali mbali. Hivyo usihisi kwamba Mungu hatosheki kamwe na utumishi mtakatifu wako. Hata hivyo, maarifa yetu ya kumjua Yesu, yanapasa yanatusukume tufanye yote tuwezayo. Yesu alisifu utumishi wa nafsi yote.—Mathayo 13:18-23; 22:37.

Uhitaji wa Kuchukia Uovu

8, 9. Ni baadhi ya mambo gani ambayo Mungu anachukia, nasi tunaweza kuonyeshaje chuki iyo hiyo?

8 Maarifa sahihi pia hutusaidia kuthamini ni mambo gani yanayochukiwa na Yesu na Yehova. (Waebrania 1:9; Isaya 61:8) “Kuna vitu sita’ anavyovichukia [Yehova]; naam, viko saba vilivyo chukizo kwake. Macho ya kiburi, ulimi wa uongo, na mikono imwagayo damu isiyo na hatia; moyo uwazao mawazo mabaya; miguu iliyo myepesi kukimbilia maovu; shahidi wa uongo asemaye uongo; naye apandaye mbegu za fitina kati ya ndugu.” (Mithali 6:16-19) Mielekeo na namna hizo za mwenendo ni “chukizo kwake.” Neno la Kiebrania linalotafsiriwa hapa “chukizo” linatokana na neno linalomaanisha “kukirihi, kutapisha,” “kutopenda kabisa, kama vile kile kinachoudhi milango yote ya fahamu; kuchukia, kuchukia kwa hasira.” Kwa hiyo, ili tuwe na amani pamoja na Mungu ni lazima tukuze hali kama hiyo ya kutopenda kabisa.

9 Kwa mfano, epuka “macho ya kiburi na wonyesho wo wote wa kiburi.” Baada ya ubatizo wengine wamehisi ya kwamba hawahitaji tena msaada wa ukawaida wa wale waliowafundisha. Lakini Wakristo wapya wanapaswa wakubali kwa unyenyekevu msaada wanapoendelea kuimarika vizuri katika ukweli. (Wagalatia 6:6) Pia epuka kupiga porojo, jambo ambalo kwa urahisi linaweza kutokeza “fitina kati ya ndugu.” Kwa kueneza maneno uliyosikia tu kwa wengine yasiyo ya fadhili, uchambuzi usioweza kuthibitishwa, au uwongo, huenda tusiwe ‘tukimwaga’ damu isiyo na hatia, lakini kwa kweli tunaweza kuharibu sifa nzuri ya mwingine. Sisi hatuwezi kuwa na amani pamoja na Mungu ikiwa hatuna amani pamoja na ndugu zetu (Mithali 17:9) Mathayo 5:23. 24) Mungu anasema pia katika Neno lake kwamba “yeye amechukia kutaliki.” (Malaki 2:14, 16. NW) Ikiwa umeoa au kuolewa, je! wewe unajitahidi kuendeleza ndoa yako iwe yenye nguvu? Je! kuchezacheza kwa mahaba na kuchezacheza isivyofaa na mwenzi wa ndoa wa mwingine ni jambo linalokuchukiza sana wewe? Je! wewe, kama Yehova, unachukia sana ngono zisizo za adili? (Kumbukumbu 23:17, 18) Kuchukia mazoea kama hayo si rahisi, kwa kuwa hayo yanaweza kuuvutia mwili wetu wenye dhambi, nayo yanakubaliwa na ulimwengu.

10. Sisi tunaweza kusitawishaje hali ya kuchukia uovu?

10 Kama msaada wa kusitawisha chuki juu ya uovu, kutumbuizwa na mawonyesho ya sinema, vipindi vya televisheni, au vichapo vinavyozungumzia kuwasiliana na roho waovu, mambo yasiyo ya adili, au jeuri. (Kumbukumbu 18:10-12; Zaburi 11:5) Kwa kufanya kutenda mabaya kuonekane kuwa ‘si jambo baya sana’ au hata ni kwenye kuchekesha, utumbuizo huo unapunguza jitihada za kusitawisha chuki ya kimungu juu ya mambo hayo. Kwa upande mwingine, sala ya bidii itasaidia, kwa kuwa Yesu alisema: “Salini kwa kuendelea, kwamba ninyi msiweze kuingia katika kishawishi. Roho, bila shaka, ina shauku, bali mwili ni dhaifu.” (Mathayo 26:41, NW) Kwa habari ya kuelekeana na tamaa ya kimwili yenye nguvu, Mkristo mmoja alisema: “Mimi najilazimisha kusali. Nyakati nyingine najihisi kuwa nisiyestahili kumkaribia Yehova, lakini kwa kujilazimisha kulifanya, kwa kumsihi, ninapata ile nguvu ninayohitaji.” Utafahamu vizuri zaidi ni kwa sababu gani Yehova anachukia kutenda mabaya ikiwa utajikumbusha akilini mwako matokeo yenye uchungu ya kufanya hivyo.​—2 Petro 2:12, 13.

11. Ni mambo gani yanayoweza kutusumbua sisi nyakati nyingine?

11 Hata ingawa una amani pamoja na Mungu, nyakati nyingine utasumbuliwa na mikazo ya kila siku na vishawishi na hata na udhaifu wako mwenyewe. Kumbuka, umejifanya mwenyewe kuwa shabaha ya pekee ya Shetani. Yeye anapiga vita dhidi ya wale wanaozishika amri za Mungu na ni Mashahidi wa Yehova! (Ufunuo 12:17) Hivyo, basi, amani yako ya ndani inaweza kudumishwaje?

Kukabiliana na Balaa Zenye Kuharibu Amani

12. (a) Ni nini yaliyo mazingira ya Zaburi 34? (b) Maandiko yanaelezaje hisia za Daudi wakati wa kupatwa na jambo hilo?

12 “Ni nyingi balaa za mwadilifu,” akaandika Daudi kwenye Zaburi 34:19, NW. Kulingana na andiko la juu la Zaburi hii, Daudi aliandika kufuatia kutano la karibu na kifo. Akimkimbia Mfalme Sauli. Daudi alitafuta kimbilio kwa Akishi, mfalme Mfilisti wa Gathi. Watumishi wa mfalme huyo walimtambua Daudi na, wakikumbuka matendo yake ya kivita ya wakati uliopita kwa ajili ya Israeli, walimlalamikia Akishi. Wakati Daudi alipoyasikia mazungumzo yao Daudi akayatia maneno hayo moyoni mwake, akamwogopa sana Akishi, mfalme wa Gathi.” (1 Samweli 21:10-12) Hata hivi, huu ulikuwa mji wa nyumbani wa Goliathi, na Daudi alikuwa ameua shujaa wao—na hata alikuwa akibeba upanga wa jitu hilo! Je! wao sasa wangetumia upanga huo mkubwa kukata kichwa chake? Daudi angefanyaje?​—1 Samweli 17:4; 21:9.

13. Daudi alifanya nini wakati wa balaa hiyo, na sisi tunaweza kufuataje mfano wake?

13 Daudi alimtolea Mungu sala ya kusihi pamoja na vilio vya bidii nyingi apate msaada. “Huyo mwenye kusumbuliwa aliita, na Yehova mwenyewe akasikia. Na kutoka taabu zake zote Yeye alimwokoa,” akasema Daudi. Pia yeye alisema: “Kutoka hofu zangu zote yeye alimkomboa.” (Zaburi 34:4, 6, 15, 17, NW) Je! wewe pia umejifunza kumtolea Yehova sala ya kusihi, ukimwaga moyo wako kwake katika nyakati za masumbuko? (Waefeso 6:18; Zaburi 62:8) Ingawa huenda taabu yako hasa isiwe yenye kutazamisha kama ya Daudi, bado wewe utaona kwamba Mungu atakupa msaada katika wakati unaofaa. (Waebrania 4:16) Lakini Daudi alifanya mengi zaidi ya kusali.

14. Daudi alitumiaje “uwezo wa kufikiri,” naye Mungu ameandaa nini kutusaidia sisi tufanye vivyo hivyo?

14 “[Daudi] akaubadilisha mwenendo wake mbele yao, akajifanya mwenye wazimu mikononi mwao. . . . Ndipo huyo Akishi akawaambia watumishi wake, Angalieni, mwaona ya kuwa mtu huyu ana wazimu; basi, maana yake nini kumleta kwangu?” (1 Samweli 21:13-15) Daudi alifikiria mbinu ambayo kupitia hiyo alitoroka. Yehova alizibariki jitihada zake. Vivyo hivyo, tunapokabiliwa na matatizo yenye magumu, Yehova anatazamia sisi tutumie uwezo wetu wa akili wala si kumtazamia tu atufanyie kila kitu. Yeye ametupatia Neno lake lililoongozwa kwa roho, ambalo ‘litampa asiye na ujuzi werevu, . . maarifa na uwezo wa kufikiri.’ (Mithali 1:4, NW; 2 Timotheo 3:16, 17) Mungu pia ameandaa wazee wa kundi, wanaoweza kutusaidia sisi tujue jinsi ya kudumisha viwango vya Yehova. (1 Wathesalonike 4:1, 2) Nyakati nyingi, wanaume hao wanaweza kukusaidia wewe uchunguze vichapo vya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi ili upate msaada katika kufanya uamuzi unaofaa au kukabiliana na tatizo fulani.

15. Ni kwa sababu gani Zaburi 34:18 inafariji?

15 Hata wakati moyo wetu unapotuhuzunisha kwa sababu ya udhaifu wetu wenyewe au kushindwa kwetu, tukiwa na mwelekeo unaofaa, tunaweza kudumisha amani yetu pamoja na Mungu. Daudi aliandika kwenye Zaburi 34:18, NW: “Yehova yu karibu kwa wale ambao wamevunjika moyo; na wale ambao wamepondwa-pondwa katika roho yeye anaokoa.” Tukiomba msamaha na kuchukua hatua zo zote zinazohitajiwa ili kusahihisha mambo (hasa kwa makosa mazito), Yehova atakaa karibu nasi. akitutegemeza kimoyoni​.—Mithali 28:13; Isaya 55:7; 2 Wakorintho 7:9-11.

Maarifa ya Kibinafsi Hutoa Amani

16. (a) Ni njia gani nyingine ya kupata maarifa sahihi ya kumjua Mungu? (b) Eleza usemi wa Daudi: “Onjeni na kuona kwamba Yehova ni mwema.”

16 Njia nyingine ambayo tunapata maarifa sahihi ya Mungu, zaidi ya kutwaa habari za kiroho ni kupitia kwa sisi kibinafsi kujionea usaidizi wake wenye upendo. (Zaburi 41:10, 11) Kukombolewa kutoka katika taabu hakumaanishi sikuzote kukoma kwa mara hiyo au kabisa kwa tatizo; huenda ukalazimika kuendelea kulivumilia. (1 Wakorintho 10:13) Ingawa uhai wa Daudi uliponywa huko Gathi, yeye alibaki akiwa mtoro kwa miaka kadha, akielekeana na hatari moja baada ya nyingine. Kupitia hayo yote, Daudi alihisi uangalizi na tegemezo la Yehova. Yeye alifuatia na akapata amani pamoja na Mungu, naye alijifunza kwamba wale wanaofanya hivyo ‘hawatapungukiwa na kitu’ cho chote kilicho chema. Akitambua kwa yale aliyojionea mwenyewe jinsi Yehova alivyomtegemeza wakati wa balaa, Daudi angeweza kusema hivi: “Onjeni na kuona kwamba Yehova ni mwema, O ninyi watu; mwenye furaha ni yule mwanamume kakawana ambaye hupata kimbilio katika yeye.”​—Zaburi 34:8-10, 14, 15, NW.

17. Kupata kimbilio katika Yehova wakati wa balaa, kulikuwa na matokeo gani juu ya jamaa moja?

17 Kupata kimbilio katika Yehova wakati wa magumu pia kutakuwezesha wewe ‘uonje na kuona kwamba Yehova ni mwema.’ Kwa sababu ya aksidenti, Mkristo mmoja katika magharibi ya kati ya United States alipoteza kazi yake yenye mshahara mzuri aliyokuwa amekuwa nayo kwa miaka 14. Kwa kuwa hawakuwa na pato lo lote, yeye pamoja na jamaa yake walimtolea Mungu sala ya kusihi. Ingawa hivyo, walipunguza matumizi yao, wakaokota-okota mavuno kwenye mashamba yaliyokuwa karibu, na wakavua samaki kwa ajili ya chakula. Kwa msaada wa wengine kundini na kazi ya kibarua ilipopatikana, jamaa hii ya watu wanne iliweza kuendelea. Mwaka mmoja baada ya aksidenti hiyo, huyo mama aliwaza hivi: “Sisi tunaweza kujidanganya wenyewe kwa kufikiri kwamba sisi tunamtegemea Yehova, hali kwa kweli sisi tunategemea uwezo wetu wenyewe, mwenzi wetu, au kazi yetu. Ingawa hivyo, sisi tulijifunza kweli kweli kumtumaini Yeye tu. Mambo hayo mengine yanaweza kuondolewa, lakini Yehova hakutuacha sisi kamwe—hata kwa kitambo kidogo. Ingawa sisi tuna ‘vile vitu vya lazima’ tu, uhusiano wetu pamoja na Yehova tukiwa jamaa ni wa karibu zaidi.”

18. Ni nini kitakachokusaidia uvumilie hata matatizo yenye kuendelea?

18 Ndiyo, ugumu wa kifedha huenda ukaendelea. Au huenda mmoja akasumbuliwa na ugonjwa wa kimwili usioponyeka; pambano la kiutu pamoja na mwingine; hali ya kimoyoni yenye kuvurugika, kama vile mshuko wa moyo; au mojapo ya magumu yaliyo mengi sana. Lakini, kwa kumjua Mungu kikweli, utakuwa na imani katika tegemezo lake. (Isaya 43:10) Utumainifu huo usiovunjika utakusaidia kuvumilia na kuwa na “ile amani ya Mungu inayoshinda mawazo yote.​”—Wafilipo 4:7, NW.

19. Tunajuaje kwamba Yehova hachukui kuteseka kwetu kwa urahisi?

19 Unapopatwa na jambo lenye kusumbua, usisahau kamwe kwamba Yehova anajua mateso yanayokupata. Katika zaburi ambayo pia ilitungwa wakati alipofikiria jambo lililompata Gathi, Daudi alimsihi Yehova hivi: “Uyatie machozi yangu katika chupa yako. (Je! hayamo katika kitabu chako?)” (Zaburi 56:8) Hakika, Mungu alisikiliza ombi la Daudi. Ni jambo lenye kufariji kama nini kujua kwamba Mungu angekusanya machozi kama hayo yaliyosababishwa na dhiki na hangaiko, na kuyaweka, kana kwamba, katika chupa yake ya ngozi, kama vile mtu angemimina katika chombo hicho divai yenye thamani kubwa au maji ya kunywa! Machozi kama hayo yangekumbukwa sikuzote, ndiyo, yangeandikwa katika kitabu cha Mungu. Lo! ni jororo kama nini hangaikio la Yehova!

20. Sisi tunaweza kuongezaje amani yetu pamoja na Mungu?

20 Kwa hivyo ubatizo wako ni mwanzo tu wa uhusiano wenye amani pamoja na Mungu. Kwa kufahamiana vizuri zaidi na sifa za kibinafsi za Mungu na Yesu, na kujionea kibinafsi utegemezo wa Yehova wakati wa majaribu, wewe utazidisha amani yako pamoja na Mungu. Si kwamba tu uhusiano wako pamoja na Yehova utakuwa mahali pa kukimbilia kupata usalama sasa bali pia wewe utakuwa na lile tumaini lenye thamani kubwa la kuishi milele katika Paradiso, ambamo wewe ‘utajifurahisha kwa wingi wa amani.’​—Zaburi 37:11, 29.

[Maelezo ya Chini]

a Kulingana na Talmud, walimu wa kale walishauri hivi: “Acheni mtu ye yote asiongee na mwanamke katika barabara za mji.” Ikiwa desturi hii ilienea katika siku za Yesu, inaweza kuwa ndiyo sababu wanafunzi wake “wakastaajabu kwa sababu alikuwa akisema na mwanamke.”​—Yohana 4:27.

Je! Wewe Unakumbuka?

◻ Ni katika njia zipi tunaweza kupata maarifa sahihi ya Mungu na Yesu?

◻ Kuiga Mungu na Yesu kutatusukuma tufanye nini?

◻ Sisi tunaigaje uchukivu wa Mungu kwa yaliyo maovu?

◻ Sisi tunaweza kudumishaje amani yajapokuwapo magumu?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Yesu alikataa kuruhusu chuki za kijamii zisizo na msingi zizuie kutoa ushuhuda wake. Je! wewe unaiga bidii yake katika kuhubiri?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Alipokabiliwa na tatizo zito, Daudi alimtolea Yehova sala ya kusihi. . . . na akaubadilisha mwenendo wake apange njia ya kutorokea. Yehova alisikia sala za Daudi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki