Kupata Amani Pamoja na Mungu Kupitia Wakfu na Ubatizo
“[Yehova] akawaambia,.. Msimkaribie mtu ye yote mwenye hiyo alama.”—EZEKIELI 9:4, 6.
1, 2. (a) Ni kwa sababu gani watu kwa ujumla hawana amani pamoja na Mungu? (b) Ni kwa sababu gani ni jambo la muhimu kwa wote wapate amani hiyo?
KUPATA amani pamoja na Mungu? Lakini kwa sababu gani? Ni watu wachache sana wanaojiona kuwa wanahitilafiana na Mungu. Je! inawezekana, hata hivyo, kuwa adui halisi wa Mungu na usijue hilo? Mtume Paulo aliwaeleza Wakristo katika karne ya kwanza hivi: “Wakati mmoja sote tulijiendesha kwa kupatana na tamaa za mwili wetu, tukifanya mambo yanayotakwa na mwili na mawazo, nasi kwa asili tulikuwa watoto wa ghadhabu hata kama walivyo wengine.”—Waefeso 2:3, NW.
2 Vivyo hivyo leo, ingawa huenda ukapendezwa na kumpendeza Mungu, dhambi iliyorithiwa kutoka kwa Adamu inaathiri matazamio yako na inaweza kukufanya ufuatie “mambo yanayotakwa na mwili.” Hata kama wewe unajifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova au ni kijana asiyebatizwa ambaye wazazi wako ni Mashahidi, mwelekeo wa kujifikiria wa fanya kama wewe utakavyo unaweza kuwa ndiyo sifa kubwa maishani mwako na iendelee kukutenga mbali na Mungu. Mtu anayedumisha mwendo kama huo ‘anaweka akiba ghadhabu kwa ajili yake mwenyewe.’ (Warumi 2:5, NW; Wakolosai 1:21; 3:5-8) Mungu ataonyesha hasira yake kabisa wakati wa “siku ya ghadhabu na ya kufunuliwa kwa hukumu yenye uadilifu ya Mungu” inayokaribia kwa haraka sana. (Warumi 1:28–2:6, NW) Wewe unaweza kupataje amani pamoja na Mungu na kuiokoka hii “siku ya ghadhabu”?
Msingi wa Kupata Amani
3. Mungu aliandaaje msingi wa upatanisho?
3 Yehova alichukua hatua ya kwanza kusaidia. “Yeye alitupenda sisi, akamtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu.” (1 Yohana 4:10) Kifo cha dhabihu cha Yesu kinapatanisha, yaani, kinatuliza au kutosheleza haki ya Yehova. Hilo linaandaa msingi wa kisheria kwa ajili ya msamaha wa dhambi na, hatimaye, kwa ajili ya kuondolewa kabisa kwa uadui kati ya Mungu na mwanadamu. Ndiyo, inawezekana “kupatanishwa na Mungu kupitia kifo cha Mwana wake,” kama alivyoandika mtume Paulo.—Warumi 5:8-10, NW.
4. Ni njozi gani inayohusika hapa aliyopewa Ezekieli, na kwa sababu gani ni ya umaana kwetu?
4 Lakini ili tunufaike kibinafsi kutokana na dhabihu ya Kristo, ni lazima sisi tuchukue hatua fulani fulani. Hizo zinaonyeshwa katika njozi ya kitamasha iliyopewa kwa nabii Ezekieli, njozi inayotimizwa katika wakati wetu ambapo “siku ya ghadhabu” ya Mungu imekaribia sana. Majeshi ya kufisha ya Mungu yanafananishwa katika njozi hiyo na wanaume sita wenye silaha. Kabla ya hao kuonyesha ghadhabu ya Mungu, mwanamume wa saba, akibeba kidau cha wino cha mwaandishi, anaambiwa hivi: “Pita kati ya mji, kati ya Yerusalemu, ukatie alama katika vipaji vya nyuso vya watu wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanyika kati yake. Na hao wengine [wanaume sita wenye silaha] aliwaambia, nami nalisikia, Piteni kati ya mji nyuma yake, mkapige; . . . Lakini msimkaribie mtu ye yote mwenye hiyo alama.”—Ezekieli 9:1-6.
5. Ni jambo gani linaloongoza kwenye toba?
5 Hao ‘waliotiwa alama’ kwa ulinzi walichukizwa kwa sababu watu waliodai kumwabudu yule Mungu wa kweli walikuwa ‘wameijaza nchi udhalimu,’ wakajiingiza katika ngono zisizo za adili, ibada ya sanamu, na kila namna nyingine ya mwenendo mbaya. (Ezekieli 8:5-18; Yeremia 7:9) Vivyo hivyo leo, wale ambao ‘wangetiwa alama’ lazima kwanza wajifunze, kupitia funzo la Biblia, waone thamani ya viwango vya Mungu na wahuzunishwe moyoni, ndiyo ‘waugue na kulia,’ juu ya mafundisho na mazoea yanayomvunjia yeye heshima. Pengine kwa sababu ya kutojua wengine walijiingiza katika kutenda mabaya au wakakubaliana na hayo kwa kutoa uungaji mkono wao. Lakini, sasa wanaanza kuuona utendaji huo kama auonavyo Mungu—kwa kuchukizwa sana! (Warumi 1:24-32; Isaya 2:4; Ufunuo 18:4; Yohana 15:19) Uthamini huo ulioongezeka unaongoza kwenye hatua ya kwanza ya kupata amani pamoja na Mungu: toba. Mtume Petro alisihi hivi: “Kwa hiyo, tubuni, na kugeuka ili mfutishe dhambi zenu, kwamba majira ya kuburudisha [badala ya ghadhabu] yapate kuja kutoka uso wa Yehova.” (Matendo 3:19, NW) Lo! ni wenye kuburudisha kama nini msamaha kama huo!
Kupata Ile “Alama”
6. Ni kwa sababu zipi watu fulani walitiwa alama katika nyakati za kale?
6 Ili waachiliwe wasipatwe na ghadhabu ya Mungu, wale waliokuwa ‘wakiugua na kulia’ walilazimika kutiwa alama juu ya vipaji vya nyuso zao. (Ezekieli 9:4) Katika nyakati za kale watumwa walikuwa mara nyingi wakitiwa alama katika kipaji cha uso ili kutambulishwa wazi. Alama zilizo wazi katika kipaji cha uso na sehemu nyinginezo zinaweza pia kuonyesha kwamba mtu aliabudu mungu fulani.a (Linganisha Isaya 44:5.) Kwa hiyo, katika siku zetu, ni nini alama iliyo wazi, yenye kuokoa uhai inayowatambulisha waziwazi wale wanaoibeba kuwa waabudu wa kweli na watumwa wa Yehova?
7. Ni nini alama hiyo ya mfano?
7 Ile alama ya mfano ni ule ushuhuda, kana kwamba unaonyeshwa mbele ya wote kwenye kipaji cha uso wako kinachofunuliwa, (1) kwamba wewe ni mwanafunzi wa Yesu Kristo aliye wakfu na kubatizwa na (2) kwamba wewe umevaa ule utu mpya ulio kama wa Kristo. (Waefeso 4:20-24) Kwa kuwa wale ‘wanaotiwa alama’ hivyo lazima kwanza wajitoe wakfu, tunahitaji kujua hilo linahusu nini. Yesu anaeleza: “Ikiwa ye yote anataka kuja nyuma ya mimi, acha yeye akane umwenywe na achukue mti wa mateso wake na afuate mimi kwa kuendelea.”—Marko 8:34,NW.
8, 9. (a) Ni nini maana ya ‘kukana umwenyewe’? (b) Linalotakwa na wakfu linaweza kufananishwaje?
8 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘kukana umwenyewe’ lamaanisha “kukana kabisa kabisa” au “kuachilia haki.” Kwa hiyo, ‘kukana umwenyewe wako’ kunamaanisha zaidi ya kujinyima raha fulani au kujitia sana katika anasa mara kwa mara. Badala yake, kunamaanisha kuwa na nia ya kujiambia la inapohusu kuacha maisha yako yatawalwe na tamaa zako binafsi na kujitakia makuu. Sisi tunasaidiwa kuona kadiri kubwa ya maneno ya Yesu kwa kuangalia jinsi wazo hilo linavyotafsiriwa katika lugha tofauti tofauti: “Kuacha kufanya lile ambalo moyo wa mtu mwenyewe unataka kufanya” (Tzeltal, Meksiko), “kutokuwa wako mwenyewe tena” (K’anjobal, Guatemala), na “kujipa kisogo mwenyewe” (Javanese, Indonesia). Ndiyo, hilo lamaanisha wakfu wa kipekee, si ahadi tu ambayo ingeweza kufanywa kwa mambo mengine mengi.
9 Mkristo mmoja anayeitwa Susan, ambaye hapo kwanza alikuwa mwenye kujitegemea sana, anaeleza kile ambacho wakfu ulimaanisha kwake: “Mimi nilikuwa nikitoa nafsi yangu yote kwa mtu mwingine. Sasa Yehova anaamua mwendo wangu, ananiambia la kufanya, na anaweka mambo nitakayotanguliza.” Je! wewe una nia ya kujiweka wakfu kipekee hivyo kwa Yehova Mungu? Kumbuka, ile alama ya mfano inakutambulisha wewe kuwa ‘mali ya’ Mungu, kama mtumwa mwenye furaha kwa Bwana wake.—Linganisha Kutoka 21:5, 6; Warumi 14:8.
10. Ni mambo gani ambayo mmoja anapaswa kufikiria kabla ya kujiweka wakfu?
10 “Ni nani katika ninyi, kama akitaka kujenga mnara, asiyeketi kwanza na kuhesabu gharama, kwamba anavyo vya kuumalizia?” akauliza Yesu (Luka 14:28) Kwa hivyo wewe una nia ya: Kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida? (Waebrania 10:25) Kudumisha kiwango cha juu cha adili ambacho Mungu amewawekea watumishi wake? (1 Wathesalonike 4:3, 4, 7). Kuwa na ushirika kamili kadiri uwezavyo katika kazi ya kuhubiri Ufalme? Kuweka penzi la Mungu kwanza unapochagua kazi yako ya maisha au kuweka miradi maishani? (Mathayo 6:33; Mhubiri 12:1) Kuangalia wajibu wako mbalimbali wa jamaa? (Waefeso 5:22–6:4; 1 Timotheo 5:8) Ukiisha kufanya wakfu wa kibinafsi kupitia sala, hatua zaidi inaacha wengine wajue jambo hilo rasmi.
Ubatizo—kwa Nani?
11. Ubatizo unafananisha nini, na ni jambo gani linalotimizwa nao?
11 Yesu aliamuru kwamba wafuasi wake wabatizwe. (Mathayo 28:19, 20) Walipaswa wazamishwe kabisa chini ya maji na kuinuliwa kutoka ndani yayo. Kama vile kuzikwa na kufufuliwa. kwa kufaa hilo linafananisha mtu akifia njia ya maisha ya kujifikiria mwenyewe na kufanywa hai atende penzi la Mungu. Kwa ubatizo unajitambulisha mwenyewe kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova katika kushirikiana na kundi la Mungu la ulimwenguni pote.b Ubatizo unahalalisha mapatano mazito yanayowekwa pamoja na Mungu. (Linganisha Kutoka 19:3-8.) Lazima maisha yako yapatane na sheria zake. (Zaburi 15; l Wakorintho 6:9-11) Ubatizo, unaokuagiza rasmi kuwa mhudumu wa Mungu, unaonyesha pia “ombi linalotolewa kwa Mungu ili kupata dhamiri njema” kwa sababu unajua kwamba wewe una amani pamoja na Mungu.—1 Petro 3:21. NW.
12. Ni wakati gani watoto wanapolindwa na “alama” ya wazazi wao?
12 Je! hata vijana wafikirie ubatizo? Basi, kumbuka kwamba Yehova aliwaambia wale wanaume sita wenye, silaha katika njozi hivi: “Waueni kabisa, mzee, na kijana, na msichana, na watoto wachanga, na wanawake; lakini ‘ msimkaribie mtu ye yote mwenye hiyo alama.” (Ezekieli 9:6) Bila shaka, watoto walio wachanga sana wasiweze kujiweka wakfu wangelindwa na “alama” ya mzazi ikiwa mzazi huyo anajitahidi kuwalea wampende Yehova na ikiwa watoto wanaitikia kwa kutii. (1 Wakorintho 7:14) Lakini, ikiwa mtoto ana akili za kutosha kufanya uamuzi wa kibinafsi naye amefikia mahali ambapo ‘ajua kutenda mema’ usidhani kwamba yeye ataendelea mpaka wakati usiojulikana chini ya ustahili wa “alama” ya mzazi wake.—Yakobo 4:17?
13. Ni baadhi ya mambo gani ya kufikiriwa katika kuamua kama kijana yu tayari kubatizwa?
13 Kabla ya kujiweka wakfu, kijana apaswa awe na maarifa ya kutosha kufahamu yanayohusika naye apaswa awe akitafuta uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu. Yeye apaswa afahamu na awe anashikamana na kanuni za Biblia, akijua ya kwamba atatozwa hesabu kwa kuvunja yo yote yazo. Yeye apaswa pia awe na ujuzi wa kutosha katika kushiriki imani yake pamoja na wengine ajue kwamba hii ni sehemu ya muhimu ya ibada ya kweli; apaswa atake kikweli kumtumikia Mungu. Ni wazi, yeye hangetazamiwa aonyeshe ukomavu wa mtu mzima, lakini amepaswa kwa kadiri fulani azidi kufanya maendeleo ya kiroho.
14. Ni kwa sababu gani kijana mmoja aliuona ubatizo wake kuwa ulinzi?
14 Ikiwa mmoja ‘amehesabu gharama,’ haimletei mtu hasara kujiweka wakfu akiwa kijana. Baada ya ubatizo, uthamini unakuwa na kina kirefu zaidi kwa karibu Wakristo wapya wote. “Kubatizwa nikiwa kijana kulikuwa ulinzi kwangu,” akaeleza David. “Nilipoendelea kuwa na umri mkubwa zaidi, niliona jinsi matineja wengine wasiobatizwa kundini walivyojihisi kuwa huru na mamlaka ya wazee na matokeo ni kwamba waligeuka na kuingia katika mwenendo mbaya. Lakini sikuzote mimi nilikumbuka kwamba nilikuwa nimeweka maisha yangu wakfu kwa Mungu. Maisha yangu yalikuwa tayari yametwaliwa, kwa hiyo singeweza kufuata matineja kama hao.”
15. (a) Twajuaje kwamba inawezekana kwa vijana kudumisha maoni mazito juu ya ibada ya kweli? (b) Wazazi wanaweza kusaidiaje vizuri zaidi
15 ‘Lakini, namna gani ikiwa mwana au binti yangu anabatizwa akiwa mchanga kisha anapoa?’ wazazi wengine wanataka kujua. Hakika, kijana hapaswi kubatizwa ili kumpendeza mzazi tu au kwa sababu wengine wa rafiki zake wanabatizwa. Ingawa hivyo, Yusufu, Samweli, Mfalme Yosia, na Yesu walipokuwa matineja wote waliiona kwa uzito ibada ya Yehova na wakashikamana nayo. (Mwanzo 37:2; 39:1-3; 1 Samweli 1:24-28; 2:18-21; 2 Nyakati 34:3; Luka 2:42-49) Katika nyakati za kisasa, Mkristo aitwaye Jean alibatizwa alipokuwa na umri wa miaka kumi tu. Alipoulizwa miaka mingi baadaye kama alifahamu kweli kweli hatua hiyo, Jean alijibu: “Mimi nilijua nilimpenda Yehova, nilithamini alilofanya Yesu kwa ajili yetu, nami nilitaka kumtumikia Yehova.” Yeye ametumikia kwa uaminifu kwa miaka 40 hivi tangu ubatizo wake. Kila kijana ni mtu binafsi; hakuna awezaye kuweka kiwango cha mpaka wa umri. Wazazi wamepaswa wajitahidi kuufikia moyo wa mtoto wao, wakimsaidia asitawishe hali ya kujitolea Mungu.c Hawapaswi kuweka mbele ya watoto wao lile pendeleo la kujiweka wakfu na kubatizwa tu bali pia wawategemeze wawe waabudu walio imara.
Kushinda Vizuizi
16. Ni kwa sababu gani mengi zaidi ya maarifa ya kichwani tu yanatakwa?
16 Ingawa maarifa ya Biblia ni ya lazima, ile “alama” inatia ndani mengi zaidi ya maarifa ya kichwani tu. Kwa mfano, katika ile njozi aliyopewa Ezekieli, inawezekana kuwa wale wazee waliouawa kwa kufukiza uvumba kwa miungu isiyo ya kweli walikuwa na maarifa mengi ya Neno la Yehova lililoandikwa. Lakini mwenendo wao nyuma ya milango iliyofungwa ulionyesha kwamba hawakuwa waabudu wa kweli. (Ezekieli 8:7-12; 9:6) Kwa hiyo, ili ‘kutiwa alama’ kwa ajili ya kuokolewa kunataka kuvaa “utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.”—Waefeso 4:22-24, NW.
17. (a) Ni kizuizi gani kinachozuia wengine wasibatizwe? (b) Shauri katika Yakobo 4:8 linaweza kutumiwaje?
17 Kizuizi kikubwa ni uvutano wa mwili wako wenye dhambi. (Warumi 8:7, 8) Wengine hata wanajizuia kubatizwa kwa sababu ya kushindwa kuzuia udhaifu mkubwa wa kimwili au kwa sababu ya kutaka kujitia sana katika anasa zisizo halali za kilimwengu. (Yakobo 4:1, 4) Watu kama hao wanakosa uhusiano wenye thamani kubwa. Neno la Mungu linashauri hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi. Itakaseni mikono yenu, enyi wenye dhambi, na kuisafisha mioyo yenu, enyi wenye nia mbili.” (Yakobo 4:8) Tendo la kukata maneno linatakwa. .Kwa mfano, mwanamume mmoja aliyeanza kujifunza Biblia alikuwa ametumia vibaya kileo na dawa za kulevya kwa miaka 16 naye alikuwa mgonjwa karibu kufa kwa sababu ya jambo hilo. Kwa kupiga moyo konde yeye alishinda tabia hizo mbaya. “Lakini nilipokuwa tu ninafanya maendeleo kuelekea wakfu, mwanamke mmoja akaanza kunisihi nifanye ngono naye. Kilikuwa kishawishi kweli kweli” yeye akakiri. Ingawa mwanamke huyo alidhani nilikuwa na kichaa, mimi nilimwambia: ‘Mimi ninajifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, na mimi siwezi kufanya hivyo.’” Ni jambo gani lililomsukuma aitikie hivyo? “Mimi nilikuwa nimeona yale ambayo Yehova alikuwa amefanyia maisha yangu kwa kunisaidia niache kileo. Alinisaidia katika njia nyingine pia. Jambo hilo liliendelea kunivuta karibu zaidi na zaidi kwake. Singeweza kumkatisha tumaini.” Mwanamume huyu alikuwa amemkaribia Mungu.
18. Ni nini ufunguo wa kushinda vizuizi?
18 Lililo la maana si kwamba unajua mengi kadiri gani bali ni kwa kadiri gani unayapenda yale unayojua. Zaburi 119:165 yasema: “Wana amani nyingi waipendao [si kujua tu] sheria yako, wala hawana la kuwakwaza.” Ufunguo ni kupenda sheria ya Mungu, kuthamini kwa kina kirefu thamani yayo katika maisha yako.—Isaya 48:17, 18.
19, 20. (a) Ni vizuizi gani ambavyo ni lazima vishindwe, nasi tuna uhakikisho gani? (b) Kufaulu kushinda vizuizi vyote kutatokeza nini?
19 Bila shaka, vizuizi vingine au vikwazo huenda vikazuka. “Lile lililokuwa gumu zaidi kwangu,” akasema ndugu huyo aliyetajwa hapo juu, lilikuwa “woga wa wanadamu. Mimi nilikuwa na ‘marafiki’ wa kilimwengu ambao nilikuwa nikinywa pamoja nao. Lilikuwa ndilo jambo gumu zaidi kwangu kuwaambia kwamba nilikuwa nikikata ushirika wangu kwa sababu nilikuwa ninaweka maisha yangu wakfu kwa Mungu.” (Mithali 29:25) Wengine wamekabili dhihaka ya washiriki wa jamaa. Shahidi mmoja aliyetoka tu kubatizwa ambaye alishinda upinzani wa mumeye, alisema: “Badala ya kizuizi kikubwa kimoja, kulikuwako vizuizi vidogo-vidogo vingi nilivyolazimika kushinda kimoja baada ya kingine.” Kushinda kila kizuizi kwa uaminifu kinapokuja kunakaza moyo wako. Uwe na uhakika wa kwamba hakuna kizuizi kisichoweza kushindwa na wale wanaoipenda sheria ya Mungu!—Luka 16:10.
20 Unaposhinda kila kikwazo, utapata “amani nyingi.” (Zaburi 119:165) Ndiyo, “utakwenda katika njia yako salama . . . Utalala na usingizi wako utakuwa mtamu. Usiogope hofu ya ghafula, wala uharibifu wa waovu utakapofika. Kwa kuwa [Yehova] atakuwa tumaini lako.”—Mithali 3:23-26.
[Maelezo ya Chini]
a Karibu miaka 150 baada ya njozi ya Ezekieli, mwanahistoria Mgiriki Herodotus, kwa kuona kwamba alama zilizokuwa juu ya waabudu wa mungu Hercules ziliwapa ulinzi, aliandika: “Ikiwa mtumwa wa mtu ye yote anakimbilia usalama [katika hekalu la Hercules], naye ametiwa alama takatifu juu yake, hivyo akijitoa kwa mungu huyo, ni kinyume cha sheria kumtia mikononi.”
b Hivi karibuni yale maswali mawili yanayoulizwa wale wanoenda kubatizwa yalirahisishwa ili waweze kuyajibu wakiwa na ufahamu kamili kwa yale yanayohusika katika kuja katika uhusiano wa karibu pamoja na Mungu na tengenezo lake la kidunia.
c Ona makala “Zoeza Mtoto Wako Asitawishe Utawa” katika toleo letu la Agosti 15, 1985.
Mambo ya Kurudia
◻ Mungu anatusaidiaje tupate amani pamoja naye?
◻ Alama ya kuokoa uhai ya mfano ni nini?
◻ Ni nini ulio umaana wa wakfu na ubatizo?
◻ Ni aina gani za vizuizi ambavyo ni lazima kukabiliwa, na hivi vinaweza kushindwaje?
[Sanduku katika ukurasa wa 13]
Kuzamishwa au Kunyunyiziwa Maji?
Simulizi juu ya ubatizo wa Yesu linataja ‘akipanda kutoka majini.’ (Marko 1:10) Kwamba Yesu alizamishwa inapatana na maana ya neno la Kigiriki linalotafsiriwa ubatizo (baʹpti·sma). Hilo linatokana na neno ba·ptiʹzo, linalomaanisha “chovya, zamisha.” Lilitumiwa nyakati nyingine kueleza kuzamishwa kwa merikebu. Mwandikaji wa karne ya pili Lusiani anatumia neno linalohusiana na hilo kueleza mtu mmoja akimfisha maji mwingine: “Akimtumbukiza kwenda chini kwenye kina kirefu sana [ba·ptiʹzon·ta] hivi kwamba hawezi kuja juu tena.” The New International Dictionary of New Testament Theology inamalizia hivi: “Yajapokuwa madai yaliyo kinyume, inaelekea kwamba baptizo, katika wazo la Kiyahudi na Kikristo pia, kwa kawaida lilinamaanisha ‘zamisha’, na kwamba hata lilipopata kuwa neno la kutumiwa kwa ajili ya ubatizo, lile wazo la uzamisho linabaki.”