Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Je! inafaa kusema juu ya “ulimwengu mpya” unaokuja?
Ulizo hilo linaweza kuulizwa kwa kufaa, kwa kuwa neno la Kigiriki ambalo linatafsiriwa mara nyingi kuwa “ulimwengu,” ko’smos, linamaanisha kwa msingi jamii ya wanadamu, na Mungu hatafanya aina mpya ya jamii ya wanadamu. Tena, katika Biblia hatuupati usemi kai·nos’ ko’smos (kwa uhalisi, “ulimwengu mpya”).
Lakini matumizi ya Kibiblia ya neno ko’smos linaruhusu Mkristo kusema juu ya “ulimwengu mpya” anapoelekeza kwenye Paradiso inayokuja itakayorudishwa duniani. Ka-musi The New International Dictionary of New Testament Theology inaeleza hivi: ‘Jina la kisarufi kosmos lilimaanisha hapo kwanza kujenga, lakini zaidi sana linamaanisha utaratibu.’ Kamusi hiyo inaongezea kwamba neno hilo pia lina maana fulani-fulani za kutaja mambo fulani ya wazi, kama vile “doido na pambo,” “urekebi wa maisha katika jamii ya kibinadamu,” na “wakaaji wa dunia, wanadamu kwa ujumla,”
Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno ko’smos linatumiwa mara nyingi katika maana ya jamaa nzima ya kibinadamu. Hivyo tunasoma kwamba “wote wamefanya dhambi [yaani, wote wa wazao wa Adamu wasio wakamilifu] na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Warumi 3:19, 23, NW) Kwa upande ule mwingine, “Mungu aliupenda ulimwengu [ko’smos] sana hata akamtoa Mwana wake mzaliwa wa pekee, ili kila mtu anayejizoeza imani katika yeye . . . awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16, NW) Ndiyo, dhabihu ya Kristo inapatikana kwa kila mtu aliye katika jamaa ya kibinadamu anayejizoeza imani.
Kama hayo tu ndiyo yangalikuwa matumizi ya Kibiblia ya neno ko’smos, ingalikuwa haifai kunena juu ya “ulimwengu mpya” unaokaribia. Kwa sababu gani? Kwa sababu baadhi ya jamii ya wanadamu wataiokoka dhiki kubwa inayokuja. Hao ndio watakaokuwa na nafasi ya kuishi katika Paradiso itakayorudishwa. Kwa hiyo Mungu hataumba aina mpya ya wanadamu, jamii mpya ya kibinadamu, ulimwengu mpya wa watu. Hata hivyo, Biblia hailitumii neno ko’smos kumaanisha tu jamii ya wanadamu wote.
Kwa mfano, nyakati nyingine neno la Kigiriki linamaanisha wanadamu wote waliotengwa mbali na Mungu. Waebrania 11:7 NW, inasema kwamba “kwa imani Noa . . . aliulaani ulimwengu [ko’smos].” Kwa wazi yeye hakulaani ki-i-la mtu, wote kati ya jamii ya wanadamu; Noa na saba kati ya jamaa yake waliiokoka Gharika. Vivyo hivyo, Yesu alisali hivi: “Mimi nafanya ombi, si kuuhusu ulimwengu [ko’smos], bali kuhusu wale ambao wewe umenipa mimi... ulimwengu umechukia wao, kwa sababu wao si sehemu ya ulimwengu, sawa na vile mimi nisivyo sehemu ya ulimwengu.”—Yohana 17:9, 14; linganisha 2 Petro 2:5; 3:6, NW.
Ingawa hivyo, acheni tukaze fikira juu ya maana nyingine bado ambayo Biblia inatumia neno ko’smos. Inafanya hivyo kumaanisha muundo, utaratibu, au eneo lenye mipaka la maisha ya kibinadamu.a Tunakuta matumizi kama hayo katika elezo la Yesu: “Kwani atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote [ko’smos], na kupata hasara ya nafsi yake?” (Mathayo 16:26) Kwa wazi Kristo hakuwa akieleza juu ya mtu ‘kuupata ulimwengu wote wa jamii ya wanadamu’ wala ‘ulimwengu wote wa watu waliotengwa mbali na Mungu.’ Si wanadamu ambao mtu mwenye kufuatia vitu vya kimwili angeweza kuwapata, bali ni vitu ambavyo watu wanavyo, mambo wanayofanya, au wanayopanga. Ndivyo pia ilivyokuwa juu ya maoneleo ya mtume Paulo kuhusu mtu aliyefunga ndoa ‘kuhangaishwa na tamaa ya vitu vya ulimwengu.’ Vilevile, haimpasi Mkristo awe ‘akiutumia ulimwengu sana.’—1 Wakorintho 7:31-33, NW.
Katika maana hiyo, neno ko’smos lina maana inayofanana na lile neno la Kigiriki ai-on’, linaloweza kufasiliwa kuwa “mfumo wa mambo’’ au “kipindi”. (Ona Aid to Bible Under-standing, kurasa 1671-74.) Tunapata katika visa fulani kwamba maneno hayo mawili yanaweza kukaribia kutumiwa-tumiwa kwa kubadilishana. Fikiria mifano miwili ya ufanani kati ya ko’smos na ai·on’: (1) Paulo aliandika kwamba yeye aliachwa na Dema, ambaye “aliupenda mfumo wa mambo wa sasa, [ai·on’].” Lakini mtume Yohana alishauri dhidi ya ‘kuupenda ulimwengu [ko’smos],’ ambao kwa huo inatoka “tamaa ya mwili na tamaa ya macho na kujionyesha kwa mtu mali yake.” (2 Timotheo 4:10; 1 Yohana 2:15-17, NW) (2) Yohana 12:31 NW, inasema juu ya “mtawala wa ulimwengu [ko’-smos] huu,” ambaye 2 Wakorintho 4:4 NW, linamtambulisha kuwa “mungu wa huu mfumo wa mambo [ai·on’].”
Kwa hiyo, ko’smos, au “ulimwengu,” linaweza kutumiwa kuhusu, si jamii ya wanadamu wote tu, bali pia kuhusu muundo wa eneo la utendaji wa kibinadamu. Kwa sababu hiyo tunaweza kwa kufaa na kwa usahihi unaolingana kusema juu ya “mfumo mpya wa mambo” unaokuja au “ulimwengu mpya.” Huo utakuwa muundo mpya, utaratibu wa ulimwengu, au eneo la utendaji wa maisha ya kibinadamu. Walio wengi kati ya wenye kuikaa Paradiso ya kidunia itakayorudishwa watakuwa wamekwisha kuishi katika mfumo wa kale wa mambo. Hata hivyo watakuwa wamekwisha kuuokoka au wakafufuliwa. Kwa hiyo watakuwa wanadamu wale wale kwa ujumla. Hata hivyo, bila ya kuwapo ulimwengu wa jamii ya wanadamu waliotengwa mbali na Mungu, na kukiwa na mpango mpya, au utaratibu mpya wenye kutegemea msingi wa mapenzi ya Mungu yaliyofunuliwa na yenye kutawala humo, Paradiso hiyo itakayorudishwa itakuwa ulimwengu mpya.
[Maelezo ya Chini]
a Kamusi iliyotajwa juu inaonyesha kwamba hata katika Kigiriki cha kale, kisicho cha Kibiblia, “kosmos ndilo neno la msingi kwa utaratibu wa ulimwengu, mfumo wa ulimwengu.”
[Picha katika ukurasa wa 31]
Jamii ya wanadamu waadilifu itarudisha paradiso katika ulimwengu mpya