Shule Mpya Yafunguliwa!
Yaliyo katika makala hii ni mawazo makuu ya maneno ya kumalizia ya mwenyekiti wakati wa kuhitimu kwa darasa la 82 la Gileadi.
TANGU mwanzo wayo katika Februari 1943, Shule ya Biblia ya Gileadi ya Mnara wa Mlinzi imezoeza wahudumu waliojiweka wakfu wa Mashahidi wa Yehova zaidi ya 6,000 kwa ajili ya kazi ya misionari. Wakati wa miaka zaidi ya 40 ambayo wamisionari hao wamepelekwa nje, nchi nyingi zimefunguliwa ili kupokea ushuhuda kamili kuhusu Ufalme. Katika kutazama nyuma yale ambayo Yehova ametimiza, hakika watu wa Mungu wanafurahi kuona utimizo wa unabii wenye kutazamisha.
Katika Isaya sura ya 49, mistari 9-12, nabii alitabiri kufunguliwa kwa watu wenye elekeo la kufuata uadilifu waliokamatwa kama wafungwa katika Babuloni Mkuu. Kupitia jamii yake ya watumishi wapakwa-mafuta duniani, mwito huu wa Yehova wa kuamuru umetoka: “Kuwaambia waliofungwa, Haya, tokeni; na hao walio katika giza, Jionyesheni. Watajilisha katika njia, . . . Hawataona njaa, wala hawataona kiu; hari haitawapiga, wala jua; kwa maana yeye aliyewarehemu atawatangulia, naam, karibu na chemchemi za maji atawaongoza. . . . Tazama, hawa watakuja kutoka mbali.” Je! kumekuwako itikio? Ndiyo kumekuwako! Mamia ya maelfu ya watu wenye mioyo minyofu wamekuja, kutoka pande zote, wakijifunua wenyewe kuwa wana njaa ya ukweli, wakitamani kulishwa na kuelimishwa na Neno la Mungu, wakitafuta kukombolewa kiroho kutoka Babuloni Mkuu. Sasa wao wamo ndani ya milki ya kidunia ya tengenezo la Ufalme, wakila wingi wa chakula cha kiroho.
Ongezeko Lenye Kutokeza
Miaka ya katikati ya 1940, nchi zilizo katika Amerika ya Kilatini na eneo la Karibea zilikuwa miongoni mwa zile za kwanza kunufaika kutokana na wamisionari wa Gileadi. Kulikuwako wahubiri wachache sana katika maeneo hayo, jambo ambalo lilitokeza mwito wa ushindani kweli kweli juu ya kutoa ushuhuda wa Ufalme kikamili. Kwa mfano, Puerto Riko ilikuwa na wahubiri 25 tu katika 1944. Kosta Rika ilikuwa na 181. Meksiko ilikuwa na wahubiri 2,431 katika 1944 wakati wahitimu wa kwanza wa Gileadi walipowasili. Lakini kadiri watu wenye njaa ya kweli walivyotoka katika giza la kidini na kujitambulisha wenyewe kuwa watafutaji wa Ufalme wa Mungu, walihubiri kwa juhudi, na wengine wakajiandikisha katika utumishi wa painia. Wanaume walijitahidi wafikie madaraka. Matokeo yalikuwa nini? Leo, Puerto Riko imeripoti wahudumu watendaji 21,943, mara nne ya wale waliokuwa watendaji katika nchi 12 zilizoripoti katika eneo la Karibea katika 1947. Kosta Rika ina wahubiri wengi sasa kuliko wale waliokuwako katika Amerika ya Kati miaka 40 iliyopita. Januari mwaka huu, Meksiko iliripoti kilele kipya cha wahubiri zaidi ya 206,000, hesabu ambayo inakaribia ile ya wahubiri waliokuwa wakihubiri katika ulimwengu wote miaka 40 iliyopita.
Imekuwa vivyo hivyo katika Amerika ya Kusini. Mara ya kwanza wamisionari walipopelekwa Ajentina katika 1947, kulikuwa na wahubiri 790. Leo kuna wahudumu watendaji 63,613, mara 26 za hesabu ya wale waliokuwa wakihubiri katika nchi 12 tofauti-tofauti katika Amerika ya Kusini miaka 40 iliyopita. Na namna gani Brazili? Wamisionari wa kwanza walipopelekwa huko katika 1945, ni wahubiri 394 peke yao waliokuwa wakifanya kazi ya kutoa ushuhuda. Lakini wao walivumilia na sasa Brazili imepita hesabu ya wahubiri 200,000. Hiyo ni zaidi ya mara 80 za hesabu ya wale waliokuwa watendaji katika Amerika ya Kusini yote katika 1947. Nchi nyingine pia katika bara hilo zimepata pia maongezeko ya kutokeza yasiyopata kuwako wakati mwinginewo.
Tukigeukia Mashariki ya Mbali, tunaona tena ushuhuda wa ajabu wa baraka za Yehova ujumbe wenye kukomboa wa ukweli wa Ufalme ulipowezesha maelfu kutoka gizani. Wamisionari wa kwanza walipopewa migawo kwenda Japani katika 1949, ni wahubiri wanane tu waliokuwa wakiripoti. Katika nchi nane za Kiesia zilizokuwa zikiripoti utendaji miaka 40 iliyopita, kulikuwa na jumla ya wahudumu watendaji 475. Leo, kuna wahudumu 116,272 katika Japani peke yake.
Katika Pasifiki ya Kusini kulikuwa na matawi mawili tu mpaka 1959. Kwa msaada wa wahubiri kutoka Australia ambao walihama ili kutumikia mahali ambako kuna uhitaji mkubwa, na kwa jitihada za wahubiri wengine wa kundi na wamisionari wachache, maelfu ya watu wamefikiwa na habari njema katika maeneo mbalimbali ya visiwa. Sasa kuna matawi sita zaidi katika sehemu hiyo ya shamba.
Historia ya ukuzi wa Afrika pia inasisimua sana. Nchi zile 17 zilizokuwa zikiripoti katika 1947 zilikuwa na jumla ya wahubiri 24,896. Lakini wamisionari wakisaidia ili habari njema zienee upesi, mamia ya maelfu wakajifunua kuwa wanamtafuta Yehova na uadilifu wake. Leo, katika Naijeria peke yake, karibu Mashahidi 130,000 wanatangaza ujumbe wa Ufalme kwa juhudi.
Hapana shaka kwamba Neno la Yehova la ukweli lenye kukomboa linatimiza lile limpendezalo. Linafanikiwa kwa uhakika katika jambo lililomfanya alipeleke. (Isaya 55:10, 11) Sasa kwa kuwa mavuno hayo makubwa yanakusanywa, Neno ilo hilo linatuhakikishia kwamba Yehova atainua wachungaji zaidi waliozoezwa. (Linganisha Yeremia 23:4.) Baraza Linaloongoza linajua sana uhitaji unaoongezeka wa wanaume wanaostahili ili watunze madaraka katika shamba na pia katika afisi mbalimbali za Sosaiti. Hatua zimechukuliwa ili kusaidia kutimiza uhitaji huo.
Shule ya Mazoezi ya Kihuduma
Ninyi wahitimu wa darasa la 82 la Gileadi, pamoja na wale ambao wamekuwapo hapa penye pindi hii yenye kujenga sana, mtafurahi kujua kwamba wakati wa vuli ya 1987, shule mpya itafunguliwa. Hiyo Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, kama itakavyoitwa, itakuwa sehemu ya Shule ya Biblia ya Gileadi ya Mnara ya Mlinzi, hivyo ikiwezesha akina ndugu kutoka nchi fulani nyingine waweze kuhudhuria. Darasa la kwanza linatazamiwa kuanza karibu Oktoba 1 mwaka huu katika mji wa Pittsburgh, Pennsylvania, U.S.A., kitovu kilichokuwa cha kwanza cha ukuzi wa Sosaiti mwanzoni-mwanzoni. Baada ya kumalizika kwa darasa la kwanza, madarasa mengine yataongozwa kwa vipindi vya kawaida katika sehemu tofauti-tofauti za United States.
Lazima matakwa fulani ya wazi ya Kimaandiko yatimizwe na wale watakaoandikishwa. Kwanza mazoezi yatatolewa kwa wazee waseja na watumishi wa huduma walio waseja ambao wana afya nzuri. Ni vizuri zaidi ikiwa wengine wao ni mapainia. Wale wanaoalikwa kwenye shule lazima wawe na nia ya kutumikia, baada ya mazoezi yao, mahali po pote ambapo pana uhitaji katika shamba la ulimwenguni pote. Jambo hili litahitaji roho ya Isaya, aliyejitoa mwenyewe kwa nia, akisema: “Mimi hapa, nitume mimi.” (Isaya 6:8) Ninyi wahitimu wa darasa hili la 82, pamoja na wamisionari ambao tayari wanatumika katika nchi zaidi ya mia moja, mnaweza kutazamia kuwa na ndugu wengine waliozoezwa wakifanya kazi bega kwa bega pamoja nanyi.
Mtaala mpya kabisa umetayarishwa kwa ajili ya Shule ya Mazoezi ya Kihuduma. Shule hiyo imeanzishwa kwa kusudi la kuwazoeza ndugu wanaostahili ambao wamekuwa na kadiri fulani ya ujuzi wa kitengenezo wakiwa wazee au watumishi wa huduma kundini.
Uhitaji wa Kufanya Maendeleo
Baada ya sikukuu ya Pentekoste katika 33 W.K., kundi la Kikristo lilikuwa lenye kutenda sana katika kueneza habari njema katika Yerusalemu, katika Yudea yote na Samaria, na ndipo, baadaye, kwenye sehemu za mbali zaidi za dunia. (Matendo 1:8) Karibu na mwaka 60 W.K. mtume Paulo, ambaye alikuwa ametanguliza utendaji wa kueneza evanjeli miongoni mwa mataifa, aliwaandikia Wakolosai, akisema: “Tumaini hili ninyi mlisikia juu yalo kabla ya hapa kwa kusimuliwa ukweli wa habari njema hizo ambazo zimejitokeza zenyewe kwa ninyi, hata kama vile zilivyozaa tunda na kuongezeka katika ulimwengu wote.” Kisha, yeye aliongezea kwamba hao waamini wenzake ‘hawapaswi kuhamishwa kutoka tumaini la habari njema zile walizosikia, na ambazo zilihubiriwa katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.’—Wakolosai 1:5, 6, 23, NW.
Katika muda mfupi kiasi, Wakristo wa kwanza walikuwa wameeneza habari njema kwa mapana na marefu. Yehova alikuwa amewapa ongezeko, hesabu za wanafunzi zikizidika sana. Jambo hilo lilihitaji wanaume waliostahili zaidi ili wafundishe kundini na kulichunga kundi. Mmoja wa waangalizi vijana aliyewekewa daraka hilo alikuwa Timotheo. Mtume Paulo alimsihi Timotheo afanye nini? Hakungekuwa na kuacha mazoezi yake: “Kwa kuwapa akina ndugu mashauri hayo utakuwa mhudumu mzuri sana wa Kristo Yesu, mmoja aliyekuzwa kwa ulishaji wa maneno ya imani na ya fundisho zuri sana ambalo wewe umefuata . . . Uwe ukijizoeza mwenyewe huku shabaha yako ikiwa bidii ya kujitolea Mungu.” (1 Timotheo 4:6-8, NW) Hilo lingekuwa jambo la maana kuliko kuelekeza fikira kwenye jambo au shughuli fulani unayopenda kibinafsi, kutia ndani hata mazoezi ya mwili. Ili kutimiza huduma yake kikamili, Timotheo alihitaji kujiangalia yeye mwenyewe na mafundisho yake.
Ninyi wahitimu wa darasa hili la Gileadi mmepokea mazoezi kwa utendaji wenu wa umisionari. Zawadi nzuri za kiroho zimepewa kwenu na waangalizi wanaostahili kufundisha. Sasa katika akiba kuna programu ya kufundisha iliyo nzuri sana kwa ajili ya wanaume wanaostahili wenye ujuzi fulani katika kutunza madaraka ya kundi ambao watazoezwa kwa tazamio la kuwa na bidii ya kujitolea Mungu. Jambo hilo litawasaidia wadumishe usawa wa maoni na kuwaandaa wakazie fikira jambo zaidi ambalo Paulo alimwandikia Timotheo: “Mtu awaye yote asiudharau ujana wako, bali uwe kielelezo kwao waaminio, katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi. . . . Ufanye bidii katika kusoma na kuonya na kufundisha . . . Uyatafakari hayo; ukae katika hayo; ili kuendelea kwako kuwe dhahiri kwa watu wote.”—1 Timotheo 4:12, 13, 15.
Kama katika kisa cha Timotheo, akina ndugu ambao wamewekwa rasmi kutunza madaraka ya kundi leo, kutia na wanaume vijana, inawapasa watambue kwamba huu ni wakati unaofaa na wenye uharaka ili wao wadhihirishe maendeleo yao. Kwa kufanya hivyo, wao watatoa ushuhuda katika njia yenye kutoka moyoni wa kwamba wanafikia viwango vya kimungu na wa kwamba wana nia ya kweli ya kutunza masilahi za kiroho, hivyo wakistahili kupewa mapendeleo zaidi ya utumishi.—Wafilipi 2:20, 21.
Kwa sababu ya uhitaji uliopo katika hatua hii ya utimizo wa kusudi la kimungu, ni pendeleo kutumiwa na Yehova mahali po pote ndani ya tengenezo lake. Tuna shukrani kwake jinsi gani akiwa Mchungaji Mkuu wetu, na kwa yule Mchungaji Bora, Yesu Kristo, kwa uandalizi huu mpya wa kitengenezo wa wakati wake, hiyo Shule ya Mazoezi ya Kihuduma!