Cheo cha Wanawake Chenye Maendeleo Je! Ni Baraka Yenye Mchanganyiko?
“KWA ujumla, wanawake katika miaka ya muda wa tangu 1980 wameelimishwa vizuri zaidi, wana afya nzuri zaidi, na wanaishi maisha marefu na yaliyo kamili zaidi.” Hayo ndiyo yaliyokuwa maneno ya kumalizia ya gazeti moja yenye makala: “Jinsi Tulivyokuwa; Jinsi Tulivyo Sasa.” Lakini je! ingeweza kuwa kwamba daraka la wanawake lenye maendeleo limekuwa baraka yenye mchanganyiko hasa kwa sababu ya matokeo yalo mabaya?
Matokeo kwa Ndoa na Jamaa
Kwa mfano, kuna pambano la kawaida baina ya maisha mazuri ya jamaa na kufuatia kazi ya kimwili ya maisha. Ripoti moja ilisema hivi: “Wanawake wenye vyeo vikubwa wanaelekea sana kutoyapa maisha yao ya nyumbani umuhimu kuliko wanaume wa vyeo vyao, na yaelekea kuna uwezekano maradufu kwa wanawake hao kupewa talaka.” Huenda ukashangaa kwa nini inakuwa hivyo. Profesa mmoja wa usimamizi katika Chuo Kikuu cha Mkoa wa Kalifornia anaeleza hivi: “Wanaume wanayaona mazingira yao ya kinyumbani kuwa mfumo wenye kutegemeza, hali wanawake wanayaona kuwa mzigo. Mwanamume anakuja nyumbani na kustarehe; hilo ndilo jambo amekuwa akifanyia kazi. Lakini kwa wanawake kuja nyumbani kunamaanisha furushi zaidi la kazi.”
Jambo hilo haliwahusu wanawake wenye vyeo vikubwa tu. Wanawake Warusi wamekuwa wakifanya kazi za kuajiriwa kwa kizazi kimoja zaidi ya wanawake walio katika nchi za Magharibi. Wangali wanaona kwamba kufanya kazi ya kuajiriwa na kutunza jamaa ni mzigo. Mhariri Mrusi wa Working Woman anasema hivi: “Wanawake ndiyo sehemu ya muhimu katika jamaa na lazima wawe wachangamfu ili kufanyiza hali yenye uchangamfu na upendo.” Kwa hiyo wao wanakabili furusi maradufu, hali wanaume wanashindwa kushiriki kazi za nyumbani.
Sababu nyingine ya pambano inaonyeshwa na mmojapo wanawake wenye mafanikio zaidi wa Wall Street. Yeye anajigamba hivi: “Kwangu mimi kazi ni tafrija,” kisha anaongezea hivi, “napenda ninachofanya, nami nafanya maachilio machache sana”—hata kwa jamaa yake. Hali njema yayo inategemea mumeye anayewatunza watoto wao wawili, ijapokuwa yeye ni mfanya biashara. Washiriki wa mwanamke huyo wanaeleza pendezi lake lenye kushughulisha sana kuwa “kwa wazi si zuri kwa mahusiano ya kijamaa.”
Ndivyo ilivyo kwa mmoja wa mawaziri wakuu wa kisasa. Jamaa ya mwanamke huyo haikuelekezewa fikira sana kwa sababu ya kutaka kwake cheo cha kisiasa. Walipokuwa wakikua, mara nyingi watoto wake walikaa nyumbani kwa mjomba wao kwa sababu, tunaambiwa, “mojawapo mambo [waliyo]penda sana ni kuketi tu chini kula chakula wakiwa jamaa, jambo ambalo halikuwa rahisi kamwe kupangia” nyumbani.
Katika mahoji ya hivi karibuni ya wanawake wanne wa Ulaya wenye vyeo vikubwa zaidi, mwanamke mmoja alifunua kwamba binti yake mwenye miaka 12 alikuwa karibu akilelewa kabisa na mumeye. Mwanamke mwingine mwenye cheo kikubwa alisema kwamba yeye aliweza kuwatunza watoto wake wakati wa miisho-juma tu. Kulingana na ripoti za habari, wasikilizaji walipata kuona kwamba watatu wa wanawake hao walielekea kukosa huruma ya kibinadamu.
Bila shaka, wanawake wengine wanafanya kazi za kuajiriwa kwa sababu ya uhitaji kabisa, labda kwa sababu mume alikufa au aliiacha jamaa. Kwa hiyo kwa wanawake hawa, kupata kazi huenda kwa sehemu kukawa baraka, lakini wapende au wasipende, inawapasa washindane na pande zisizofaa.
Matokeo Yasiyofaa
Uhakika wa kwamba daraka la wanawake lililobadilika limekuwa baraka yenye mchanganyiko inaonyeshwa wazi na jambo linalotokea kwa kawaida wakati wanawake wanapowapita waume zao katika uwezo wa kuchuma pesa au katika cheo cha kazi. Kulingana na madaktari wanaowafanyisha wagonjwa mazoezi ya akili au ya mwili, mwelekeo huu “unaanza kutambuliwa kuwa hatua kubwa na yenye kuleta matatizo makubwa katika ndoa zaidi na zaidi.” Lalamiko la mume mmoja ni mfano mmoja: “Mimi ninajua kwamba kiakili ninasifu mafanikio yake. Lakini katika maono ya moyoni ninahisi vibaya. Ninahisi kwamba ninaachwa. Nami ninahisi nikiwa mwenye hatia kwa sababu ninafadhaika sana.” Ikiwa kwa sasa wenzi Wakristo wote wawili wanahitaji kufanya kazi ya kuajiriwa, mazungumzo na fikira zenye upendo vinaweza kusaidia kupunguza hisia na matokeo hayo yasiyofaa.—1 Petro 4:8.
Uhakika mwingine unayonyesha kwamba maendeleo yanayofanywa na wanawake ni baraka yenye mchanganyiko ni ule mkazo ambao wateteaji wengi wa haki za wanawake wanaweka katika kile ambacho ni kwa faida yao kwanza. The Coming Matriarchy kinaelekeza kwenye wakati ambao ulimwengu utaongozwa na wanawake wenye kujifikiria wenyewe tu na wanaouliza, “Ni nini kilichomo kwa ajili yangu?” Kwa kupendeza, mwanamke stadi na mwenye mafanikio katika mambo ya kifedha aliyetangulia kutajwa mwanzoni alisema maneno yanayokaribiana sana na hayo; yeye hakupendezwa na kuwasaidia wengine wapande cheo isipokuwa kama yeye angepata faida kwa kufanya hivyo. Yeye anakubali hivi: “Mimi nafikiria sana kupata faida.” Hilo ni jambo lenye hekima jinsi gani, kulingana na shauri la Yesu. Katika Mahubiri ya Mlimani yeye alisema hivi: “Sikuzote ni lazima mwatendee watu wengine kama vile mngependa wao wawatendee ninyi.” “Msihangaike kwa ajili ya kesho, kwa kuwa kesho itakuwa na wasiwasi wayo.” (Mathayo 7:12; 6:34, Goodspeed) Hakika, wanawake Wakristo wanajitahidi kudumisha maoni ya Yesu kuhusu mambo hayo.
Adili za Biblia Zinaweza Kudhabihiwa?
Bila shaka upande usiofaa sana wa cheo cha wanawake kilichobadilika ni mmomonyoko wa thamani za adili. Wale wanaotetea haki za wanawake wanataja Mungu na dini mara chache sana na wanapofanya hivyo huwa mara nyingi wanachambua tu. Mara nyingi wanawake wanaoahirisha ndoa kwa sababu ya kazi zao za kuajiriwa za maisha wanashikilia maoni ya kwamba ndoa si ya maana kabisa kabla ya kuwa na uhusiano wa kingono.
Mwelekeo mmoja usiofaa wa chama cha wanaotetea haki za wanawake ni kutegemeza kwacho tendo la kulalana kwa wanawake wao kwa wao. Katika 1971 mkutano wa kila mwaka wa NOW (Tengenezo la Kitaifa la Wanawake) lilifanya azimio hili: “Kwamba NOW linatambua udhalimu maradufu unaotendwa wanawake wanaolalana wao kwa wao, Kwamba haki ya mwanamke kwa utu wake mwenyewe inatia ndani haki ya kujiamulia mipaka ya na kufanya ngono zake mwenyewe na kuchagua mtindo wake mwenyewe wa maisha, Kwamba NOW inakiri kwamba udhalimu wanaotendwa wanawake wanaolalana wao kwa wao ni hangaikio halali la wale wanaotetea haki za wanawake.” Ingawaje, linganisha hukumu ya Mungu katika Warumi 1:26, 27. Mara nyingi unapatana na oni la wale wanaotetea haki za wanawake kuhusu kulalana wao kwa wao ni uungaji mkono wa mwanamke kutoa mimba wakati anapodai. Billups Percy, profesa katika Chuo Kikuu cha sheria cha Tulane alisema hivi kwa kufaa: “Kuona uangamizaji wa kijusu kuwa utaratibu mwingine tu wa upasuaji ni kudharau karne nyingi za uchunguzi wa uhalifu, theolojia na falsafa ya kiadili.”
Ripoti moja inasema kwamba katika mwongo wa miaka uliopita uhalifu mbaya sana kwa upande wa wanawake umeongezeka haraka sana kuliko miongoni mwa wanaume. Kati ya 1974 na 1979, hesabu ya wanawake katika United States waliotiwa nguvuni kwa sababu ya udanganyifu iliongezeka kwa karibu asilimia 50, lakini ongezeko hilo lilikuwa asilimia 13 tu miongoni mwa wanaume. Wizi wa fedha walizoaminishwa uliongezeka vivyo hivyo kwa karibu asilimia 50 lakini asilimia 1.5 tu kwa wanaume. Kutiwa nguvuni miongoni mwa wanawake kwa sababu ya ubini na kufanyiza vitu vya bandia kulipanda kwa asilimia 27.7 lakini kulikuwa chini ya asimilia 10 miongoni mwa wanaume. Kwa wazi cheo cha wanawake kilichobadilika hakikutokeza uradhi kamili.
Matumizi ya tumbaku yameongezeka pia miongoni mwa wanawake. Kansa wa mapafu unaotokea kwa sababu ya kuvuta sigareti umechukua mahali pa kansa wa matiti kwa kuwa kisababishi namba 1 cha vifo vya kansa miongoni mwa wanawake. Katika mwaka mmoja hivi majuzi ulitokeza asilimia 25 ya vifo vyote vya kansa miongoni mwa wanawake na unaongezeka kwa kiasi cha asilimia 7 kila mwaka.
Wakati Ujao Wenye Kuridhisha —Jinsi Gani?
Je! kazi ya kuajiriwa au ya maisha inaweza kuwapa wanawake walio wengi zaidi uradhi kamili katika maisha? Yaelekea haiwezi, kama vile wengi zaidi na zaidi wanagundua. Hilary Cosell, mtungaji wa Woman on a Seesaw: The Ups and Downs of Making It, aliandika kuhusu tatizo hili katika makala moja, akiuliza hivi: “Ikiwa wanawake wamepata kukosea mbeleni upande wa ndoa na umama na kuwa mke nyumbani, je! wanaweza kuwa wanakosea tena kwa upande wa ujuzi wa kazi, kazi ya kuajiriwa ya maisha na mafanikio?” Mwanamke huyo anauliza hivi pia: “Je! kweli tunaweza kufanya mambo yote ambayo mama zetu walifanya, na mambo yote ambayo baba zetu walifanya pia?”
Vivyo hivyo, katika The Cost of Loving, Megan Marshall alifunua kwamba “utu wa nje wa kufanikiwa katika ujuzi wa kazi ulificha kidogo tu vidonda vya kisirisiri: mapenzi yaliyovunjika yanayoumiza moyo, kulazimika kufanya ngono za ovyo-ovyo, jaribio la tendo la kulalana wanawake kwa wanawake, kutoa mimba, talaka na upweke halisi.” Yeye anaeleza vile chama cha wanawake kilivyotokeza “hadithi ya uwongo ya kujitegemea,” lakini kwa walio wengi zaidi jambo hili halifanikiwi.
Marshall anamalizia kwa kusema kwamba “lazima sisi tusadiki katika upendo wa muda mrefu ambao ndoa nzuri inahifadhi,” kwamba “binadamu hawezi kuishi kwa kujitenga,” na kwamba “lazima tuwe na watu wengine wa kutunza, na wakututunza sisi.” Hilo linatukumbusha maneno ya mwalimu mkuu zaidi ambaye amepata kuishi duniani, Yesu Kristo. “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35, NW.
Kwa kweli, wanadamu wanaelekea kupita mpaka katika upande huu au ule. Uhakika wa kwamba cheo cha wanawake wa kisasa chenye maendeleo si baraka isiyo na mchanganyiko unakazia maneno ya nabii Yeremia: “Kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Wanawake Wakristo, kwa kujua mabadiliko ambayo yametukia (pamoja na baraka na matatizo yanayoambatana nayo), wanaweza kuthamini vizuri zaidi ubora wa kufuata shauri la Mungu. Mambo yaliyoonwa yameonyesha kwamba ni la “kutamanika kuliko dhahabu.” ‘Katika kulishika kuna thawabu nyingi.’—Zaburi 19:7-11.