Dini ya Ki-Siku-Hizi Ni Yenye Mafaa kwa Kadiri Gani?
“NILIITUPA Biblia katika chumba changu cha faragha huku nikielekea kwenye chumba changu cha kulala. Nilifikiri singeiokota tena wala kuhudhuria kanisa jingine. Nilikuwa nimekuwa nikitafuta kwa miaka yapata sita. Na bado sikupata msaada wo wote.”
Ronald, mwendesha-kompyuta, mwenye umri wa miaka 26, alikuwa amepita katika magumu fulani na aliogopa kwamba maisha yake yangebomoka-bomoka. Dini ilielekea kutokuwa yenye mafaa kwake. “Mimi nimeiacha kabisa,” yeye akasema.
Watu wengi, kama Ronald, wamekatishwa tamaa na dini. Namna gani wewe? Je! unafikiri dini imewapa watu msaada na mwongozo wenye mafaa ili wawe wenzi-wafanya kazi, jirani, waume, wake, wazazi, au watoto walio bora? Je! dini imekuwa kani ya kuleta amani na umoja miongoni mwa watu? Je! imewasaidia walifahamu kusudi la maisha? Je! imekaza kikiki katika akili na mioyo yao tumaini hakika kwa wakati ujao?
Mwongozo Wenye Mafaa Unakosekana
Katika ulimwengu huu wenye kutatanisha, watu wanahitaji mwongozo wa hekima, ulio wazi. Je! wanaweza kuutazamia kutokana na viongozi wa kiroho? Katika barua moja kwa mwanasafu wa gazeti, mwanamke mmoja alilalamika hivi:
“Jambo lote lile tunalosikia sasa katika kanisa letu . . . kwa muda mrefu sasa limekuwa ni upendo, upendo, upendo. . . . Yalienda wapi yale makatazo ‘Usifanye, usifanye’—‘usiue. Usiibe,’ na mengineyo yote? Sisi tunahitaji kukumbushwa mara nyingi kwamba mambo fulani yamekatazwa. .. . Lakini hata hatulisikii tena lile neno ‘Dhambi.’ Inaonekana wao wanaliepuka kama kwamba ni neno chafu. . . . “
Kwa wazi, watu fulani wanahisi kwamba washauri wao wa kidini wamekuwa walegevu mno, waendekevu mno. Waongozi hao wa kiroho ni dhaifu. Wao ni kama daktari anayefunika-funika tatizo la mgonjwa wake na kumwandikia dawa iliyoongezwa maji. Ni nini baadhi ya sababu za kushindwa hivyo?
Kazi Iliyo Katika Tatizo Kubwa
Mtu ambaye amelemewa mno na matatizo yake mwenyewe hataweza kutumia wakati na jitihada nyingi akisaidia wengine. Ripoti za vyombo vya habari zinaonyesha kwamba hesabu inayoongezeka ya viongozi wa kidini wanalemewa sana na matatizo yao wenyewe ya kikazi na kibinafsi. Hii ni baadhi ya mifano:
“Ingawa kupatwa na mikazo na kukosa uradhi kazini ni mambo ya kawaida katika kazi nyingi leo, hakuna mahali pengine ambapo mambo hayo yanatokea sana kuliko miongoni mwa viongozi wa kidini Wayahudi,” anasema msaikolojia wa matibabu Dakt. Leslie R. Freedman baada ya kufanya katika chuo kikuu uchunguzi wa viongozi wa kidini Wayahudi.
“Kama mimi ningekuwa na mwana, je! ningemtaka awe padri? Kwa kusikitisha, jibu langu lazima liwe hapana,” anashikilia padri mmoja, William Wells, katika ripoti moja inayohusu matatizo ya viongozi wa kidini. Kwa sababu gani sivyo? Yeye anasema hawezi kutia moyo kijana mwanamume afikirie kazi yenye kukumbwa sana na “uhitilafiano, msukosuko, na mashaka-mashaka kama vile upadri wa Roma Katoliki ulivyo leo.”
Mapadri katika Kanisa la Kilutheri la Sweden linaloungwa mkono na Serikali wamo katika taabu pia. Gazeti moja la kila siku la Sweden linasema: “Mapadri wana matatizo ya kisaikolojia, ambayo katika visa vya kupita kiasi yanaongoza kwenye kifo cha kujiua. . . . Kazi ya viongozi wa kidini imo katika tatizo kubwa.”
Ukosefu wa Umoja Unaosumbua Akili
Katika zile nchi ambako viongozi wa kidini wanahusika katika vita vinavyoleta hasara kubwa na migawanyiko, fikira zao zimetoka kwenye utoaji unaofaa wa mahitaji ya kiroho ya watu. Lazima wao washiriki pia lawama la upotevu wa watu na pesa ambazo zingaliweza kutumiwa kwa masilahi ya kimwili ya watu.
Kuna wale katika sehemu zote za dunia ambao wamepoteza tumaini lao katika dini wakawa wasiojali mambo ya kidini. Kupotezwa kwa washiriki na kupunguka kwa watu wanaoenda kanisani ni mambo yanayoripotiwa kutoka mahali kama Sweden, Finland, Ujeremani, Uingereza, Italia, Kanada, na United States.
Je! wewe umo miongoni mwa wale ambao, kama Ronald, wanafikiri kwamba amemaliza uhusiano wake na dini? Hata hivyo, je! ingeweza kuwa kwamba kuna dini fulani ambayo imethibitika kuwa yenye mafaa kwa wengi? Makala inayofuata itazungumzia hilo.