Hatua Kubwa Nyingine Katika Elimu ya Biblia
ALHAMISI, Oktoba 1, 1987, ilikuwa hatua kubwa nyingine katika elimu ya Biblia kama inavyotolewa na ile Sosaiti ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova. Siku hiyo ilikuwa ya mzinduo wa ile Shule ya Mazoezi ya Kihuduma iliyo mpya. Darasa la kwanza la ndugu waseja 24 lilikuwa limepiga ripoti kwa ajili ya mazoezi maalum kwenye Jumba la Kusanyiko la Pittsburgh lililo na nafasi kubwa huko Coraopolis, Pennsylvania. Wenye nyumba wenye mioyo michangamfu miongoni mwa Mashahidi wa eneo hilo walikuwa wamefungua maskani zao ili kuwapa wanafunzi hao mahali pa kulala kwa ajili ya kipindi chao cha mazoezi ya majuma manane.
Wanafunzi hao walisajiliwa majina asubuhi, wakapokea vitabu vyao vya mafundisho na pia maagizo ya kufungua. Saa 1:30 jioni hiyo, hilo Jumba la Kusanyiko lilijaa pomoni Mashahidi 1,518 wenye kutaharuki, wakiwa na hamu nyingi ya kushiriki katika kufunguliwa rasmi kwa hiyo shule mpya.
Albert Schroeder, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alitumikia akiwa mwenyekiti. Baada ya wimbo na sala, yeye alitoa utangulizi wa kukaribisha Robert Dawson, mwangalizi wa jiji la Pittsburgh. Kwa uchangamfu yeye aliwakaribisha wale wanafunzi 24 na kusifu zile nyumba 13 zilizokuwa zimejitolea kuwaandalia mahali pa kulala. Ndugu Dawson alikumbusha wenye nyumba hao wakaribishaji kwamba litakuwa pendeleo lao kuonyesha upendo ambao unahimili, unaitikadi, unatumainia, na kuvumilia mambo yote. (1 Wakorintho 13:7, NW ) Yeye aliwakumbusha wanafunzi kwamba, wakiwa wageni, wanapaswa kudhihirisha shukrani, unyenyekevu, na kuwa wenye msaada. Kwa njia hiyo, kungeweza kutokea urafiki mwingi ambao ungeweza kudumu muda wa maisha yote.
Ndipo utangulizi ulipofanywa kujulisha wanafunzi hao ni akina nani, huku kila mmoja akitaja jina lake na kueleza ametoka wapi na nini iliyokuwa imekuwa kazi yake ya maisha katika utumishi wa Yehova. Baadhi yao walikuwa wamekuja kutoka Puerto Rico, Argentina, Kanada, na Hong Kong, na wale wengine wote wakiwa ni wa kutoka sehemu ya mashariki ya United States. Zaidi ya kusema Kiingereza, baadhi yao wanasema Kihispania, Kifaransa, Kiitalia, au Kichina.
Halafu mwenyekiti akafanya utangulizi wa kujulisha kwamba James Hinderer ni mmoja wa walimu. Akitegemeza maelezo yake juu ya Mathayo 7:24, 25, yeye alikazia umaana wa kufuatia mambo mpaka yawe yametendeka, kwa kuzoea mambo waliyojifunza. Hivyo, wanafunzi hao wangekuwa wakijenga “nyumba yao juu ya tungamo-mwamba badala ya kuijenga juu ya michanga yenye kuyumba-yumba.
Halafu Randall Davis, yule mwalimu mwingine, akawahutubia wanafunzi. Akitegemeza maelezo yake juu ya Isaya 54:13, yeye alitaja kwamba wao wangefundishwa na Yehova ili waweze kuwapa wengine maagizo. Wao wangehitaji kuegemea kwa uzito juu ya kile “msaidiaji” wa kweli, roho takatifu ya Yehova. —Yohana 14:26, NW.
Halafu Albert Schroeder akahutubu juu ya jinsi jioni hiyo ilivyomkumbusha yeye juu ya hatua kubwa nyingine katika elimu ya Biblia. Yeye alikumbuka Februari 1, 1943, wakati wanafunzi 100, walimu wanne (kutia ndani yeye), na wageni kutoka Brooklyn walipokusanyika huko South Lansing, New York, kwa ajili ya kufunguliwa kwa Shule ya Biblia ya Gileadi ya Mnara wa Mlinzi. Muda wa miaka 44 iliyopita tangu hapo, Shule ya Gileadi imekuwa na baraka ya Yehova, kama inavyoonwa katika kule kuwatawanya katika sehemu zote za dunia wamisionari zaidi ya 6,000 waliopewa mazoezi ya Biblia. Ndipo Ndugu Schroeder akayataja yale masomo mbalimbali yatakayofundishwa katika Shule ya Mazoezi ya Kihuduma. Miongoni mwayo ni Mafundisho ya Biblia, Tengenezo la Kitheokrasi (somo ambalo linakaza fikira juu ya madaraka ya waangalizi na watumishi wa huduma), Usimamizi wa Kazi ya Mungu, na Kutoa Hotuba za Watu Wote. Yeye alivuta fikira pia kwenye vitabu mbalimbali vya mafundisho, kutia ndani Reasoning From the Scriptures. Katika umalizio, Ndugu Schroeder alitaja utimizo wa Isaya 45:23, akitaarifu kwamba wapinzani wa kidini walikuwa ni kama wanapigia Mungu magoti yao kwa sababu wamelazimika kukiri kwamba Mashahidi wa Yehova wanasema mambo ya kweli katika nyanja za tiba, sheria, na tarehe za Biblia.
“Mwe Waigaji wa Paulo” ndicho kichwa kilichochaguliwa na msemaji aliyefuata, Karl Klein wa Baraza Linaloongoza. Yeye alionyesha jinsi mtume Paulo alivyowaomba-omba wengine waige yeye. Yeye angeweza kufanya hivyo, kwa maana yeye alikuwa akiiga Kristo. (1 Wakorintho 11:1, NW ) Wanafunzi walishauriwa waige Paulo katika maarifa yake na utumizi stadi wa Maandiko, katika kuhubiri kwake kwa ujasiri na bidii, katika ukosefu wake wa ubinafsi, katika kiasi chake na unyenyekevu, na katika uvumilivu wake wenye subira.
Ndipo Theodore Jaracz, pia mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alipotoa ile hotuba ya mzinduo, “Shule Mpya—Kwa Ajili ya Kusudi Gani? ” Yeye alianza kwa kuonelea kwamba wale waliojitolea kwa ajili ya shule hii walifanya mwafaka kutumikia mahali ko kote ambako wangehitajiwa katika shamba la ulimwenguni pote. Kwa kuwa Mashahidi ni zaidi ya milioni tatu na robo katika makundi zaidi ya 54,000, kuna uhitaji mkubwa wa wanaume wanaostahili kuchunga, kufundisha, na kuchukua uongozi katika ile kazi kubwa ya kueneza evanjeli. Zamani za kale, Yehova alitabiri kwamba yeye angeandaa “zawadi katika namna ya wanaume.” (Zaburi 68:18,NW ) Yeye alifanya hivyo katika nyakati za kimitume, hata kama vile ilivyoelezwa na mtume Paulo kwenye Waefeso 4:8-11, NW. Leo, Yehova anaandaa pia ‘zawadi katika wanaume’ na anazoeza baadhi yao kupitia hii shule mpya.
Ndugu Jaracz alizidi kutaja kwamba ingawa wanafunzi wote wana uwezo mbalimbali waliozaliwa nao, Kristo anaweza kuuongezea. Lakini hiyo inahitaji jitihada, na msemaji alieleza ana uhakika kwamba wanafunzi hao 24 wangefanya jitihada hiyo. Alionyesha wazi kwamba hakuwezi kuwako ukengeufu wa kuacha viwango vya uadilifu vya Yehova, na akasema kwamba wale wanaochukua uongozi wanaweza kusaidia kwa kielelezo na mavutano yao ya kibinafsi. Katika sehemu nyingi za dunia, kuna uhitaji mkubwa wa wanaume wanaostahili kukubali daraka la kitengenezo. Hiyo inatia ndani hata makundi makubwa ambayo huenda yakawa yana mzee mmoja tu au wawili na hesabu ndogo ya watumishi wa huduma. Kwa hiyo ni wazi kwa nini Shule ya Mazoezi ya Kihuduma ilihitaji kuanzishwa. Hiyo inakusudiwa kuzoeza wazee na watumishi wa huduma wasiofunga ndoa watumikie mahali ko kote katika lile shamba la ulimwenguni pote. Kutokana na mazoezi yao, wao watakuwa wametayarika kwa njia bora kulitunza ongezeko wakiwa wachungaji.
Mashahidi wa Yehova wote wanaweza kuzitoa asante kwa Mungu kwa sababu ya kufanya Shule ya Mazoezi ya Kihuduma iwezekane. Katika umalizio, Ndugu Jaracz alitaarifu hivi: “Mimi nina uhakika kwamba sisi sote tunaweza kuungana kwa umoja na fikira na hisia zinazoelekezwa kwa Yehova kama zinavyoelezwa kwenye Zaburi 79:13, NW; ‘Kwa habari ya sisi watu wako na kundi la machunga yako, sisi tutazitoa asante kwako wewe mpaka wakati usio dhahiri; kutoka kizazi mpaka kizazi sisi tutatangaza sifa yako.’ ” Ndipo, kwa wimbo na sala, pindi hiyo yenye kukumbukika na kufurahisha sana ikafikia mwisho.