Je! Mimi Napaswa Kubadili Dini Yangu?
RUBANI wa ndege alikuwa tu ameruka kutoka Uwanja wa Ndege wa Okinawa Naha akiwa na abiria 101. Kwa ghafula akaona ndege tatu zenye kuchunguza hali ya anga zikielekea upande wake zikiwa katika mwendo wa kugongana. Akitenda kwa haraka sana, rubani huyo aligeuka upesi upande wa kushoto, hivyo akaepuka mgongano wa angani, akaokoa uhai wake mwenyewe na uhai wa abiria wake. Simulizi hilo la kupona chupuchupu, kama lilivyoripotiwa katika karatasi-habari ya kaskazini mwa Japani, linatoa kielezi kizuri kinachoonyesha kwamba badiliko kubwa sana katika mwendo linahitajiwa kabisa nyakati nyingine.
Hata hivyo, watu wengi wanahisi kwamba kubadili dini ya mtu ni jambo tofauti. Woga mkubwa unatokea. Kuna woga wa kushika kijia kisichozoelewa. Bi. Tachi, aliyekuwa akijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, alijieleza mwenyewe hivi: “Watu wengi ninaowafahamu wana mashaka mengi juu ya dini na inavyokazia pesa. Lakini mambo ambayo tumejua na yale ambayo tumeona tangu utoto na kuendelea ni sherehe na desturi za kidini. Hatufikirii sana kuhusu maana ya kiroho ya hoji [ile ibada ya ukumbusho ya Kibuddha inayofanywa kwa vipindi vyake kwa ajili ya mfu]. Tunafikiria hoji kuwa wakati wa furaha zaidi kuwa pamoja na watu wa ukoo na majirani. Lile wazo la kuacha yote hayo, au jambo baya zaidi kufukuzwa na jamaa liliniogopesha mimi.” Pengine watu wa eneo lako wanahisi vivyo hivyo kuhusu dini.
Kuna woga mwingine pia. Katika sehemu nyingi, watu wanaogopa aina fulani ya kisasi cha kimungu ikiwa wanabadili dini yao. Mwanamke mmoja aliyeanza kujifunza Biblia katika Japani aliambiwa na watu wa ukoo wake kwamba yeye alikuwa akipatwa na matatizo ya afya na ya jamaa kwa sababu alikuwa “amewadharau mababu wake waliokufa” naye akajiletea mwenyewe hasira-jeuri yao kwa kujifunza “dini ya kigeni.”
Woga mwingine unaowazuia watu wasibadili dini yao ni woga wa kutompendeza mwenzi au wazazi. Katika nchi nyingi za Mashariki, ambako ushikamanifu kwa wazazi na jamaa kunaonwa kuwa jambo la muhimu sana, kwa kawaida mke mpya anatazamiwa kuunga mkono oni la kidini la jamaa ambamo ameolewa. Hata ikiwa watu waliooana si watu wenye kupenda dini sana, kudumisha uhusiano mzuri pamoja na jamaa na kushika hali hiyo hiyo ya kidini yanaonwa kuwa mambo ya muhimu sana. Watu wawili vijana waliooana waliacha funzo lao la Biblia baada ya kuwekwa chini ya mkazo sana katika “kongamano la kijamaa.” “Kwa msingi, sisi tulikuwa na woga wa mwanadamu,” akaeleza mume, ambaye baadaye alianza kujifunza tena. “Sisi tulihisi kwamba tunapaswa kutii matakwa ya wazazi wetu, na hatukutaka kuwatia uchungu kwa kubadili dini yetu.”
Jambo hili linatukumbusha sababu nyingine inayowafanya wengi waogope kubadili dini yao: ile chuki ya watu wote ya kuonwa kuwa tofauti. Katika jamaa inayotajwa juu, mojapo ya sababu zilizotolewa na wazazi wa wale watu wawili vijana walioona kuacha funzo lao la Biblia ilikuwa kwamba wazazi hawakutaka watoto wao waonwe kuwa watu wa ajabu-ajabu au waondolewe katika utendaji wa jamii ya kimtaa.
Kwa hiyo, woga mkubwa sana unahusika katika swali, Je! mimi napaswa kubadili dini yangu? Kama tokeo, wengi wanakuwa na maoni matulivu: ‘Haidhuru mmoja ni wa dini gani, sivyo?’ ‘Je! dini zote si ni vijia tofauti-tofauti vyenye kuongoza kwenye kilele cha mlima ule ule?’ Kwa habari ya dini, wao wanakuwa kama wale nyani watatu wa kimithali, hawaona ubaya wo wote, hawasikii ubaya wo wote, hawaneni ubaya wo wote.
Lakini watu fulani wamebadili dini yao. Kwa nini? Kwa hesabu fulani kati yao lilikuwa tu jambo la kujiunga na dini nyingine ambayo iliahidi afya ya mara moja au manufaa ya kifedha, huku wakidumisha maoni na mazoea ya dini yao ya kimapokeo. Lakini kwa wengine, kumekuwa na badiliko halisi lililo kamili. Ingawaje, huenda wewe ukawa unashangaa, ‘Je! kweli kuna sababu za kunitosha mimi ili nibadili dini yangu? Kwa sababu gani watu fulani wamekuwa na nia ya kubadili? Je! badiliko linaweza kuwa na tokeo halisi katika maisha yangu?’ Tunakualika uchunguze makala inayofuata ili upate majibu.
[Picha katika ukurasa wa 3]
Ni kitu gani kinachowachochea watu washikilie desturi za dini yao ya kimapokeo?