Watangazaji wa Ufalme Waripoti
Ukweli wa Ufalme Wachanua Katika Sri Lanka
SRI LANKA, likimaanisha “Bara Lenye Kung’aa,” ni jina la kikale kililorudishiwa kisiwa hiki chenye kupendeza ambacho kingali kinajulikana na wengi kwa jina lacho la kikoloni, “Ceylon.” Kwa sababu ya mahali kilipo katika Bahari Hindi, kinaitwa pia Tone la Chozi la India; lakini machozi yacho yote hayajakuwa ya shangwe kwa kuwa katika nyakati za karibuni jeuri ya kikabila imetokea kwa ghafula, ikifanyiza habari kuu katika magazeti ulimwenguni pote.
Hata hivyo, ukweli wa Ufalme unachanua hapa pia. Wabudha, Wahindu, Waislamu, Wapasi, na Mkristo wa jina tu wanafundishwa kwamba Ufalme wa Yehova peke yake kupitia kwa Kristo Yesu ndio unaweza kuleta ponyo lenye kudumu kwa majeraha ya kikabila na kisiasa ambayo yanagawanya jamii ya watu. Mambo yafuatayo yaliyoonwa yanaonyesha kuchanua kwa ukweli wa Ufalme katika hili “Bara Lenye Kung’aa.”
◻ Salimoon alilelewa aitikadi kwamba Qurʼan ni Neno la Mungu. Lakini yeye hakukubali kikamili kwamba Mungu mwenye rehema zote angewatesa watu katika moto wa mateso. Siku moja Mashahidi wa Yehova walimwalika kwenye mkutano. Akiutambua ukweli mara moja, yeye hajarudi nyuma kamwe, na yeye sasa anatumikia kwa furaha akiwa mzee katika kundi la Kikristo.
◻ Harry, Mbuddha wa maisha ambaye alikuwa ameonyesha imani yake ya kidini kwa kutembea juu ya makaa yenye moto, alishindwa kufuata kanuni zilizomo katika fundisho la Kibuddha la kijia mara nane: (1) kufahamu kunakofaa, (2) kufikiri kunakofaa; (3) msemo unaofaa; (4) tendo linalofaa; (5) maisha yanayofaa; (6) jitihada inayofaa; (7) ufahamivu unaofaa, na (8) kukaza fikiri kunakofaa. Hatua hizi zapasa kujaza kila sehemu ya maisha ya mtu. Ijapokuwa yeye alijidhania kuwa Mbuddha mzuri, kuvuta kwake sigareti, kunywa vileo kupita kiasi na mwenendo mwingine usiofaa uliletea jamaa yake matatizo. Hatimaye, yeye aliamua kujifunza Biblia. Hata hivyo, hakuna mtu aliyejitoa kujifunza naye. Yeye alisikia kwamba huenda Mashahidi wa Yehova wakawa na nia ya kujifunza naye, kwa hiyo alihudhuria mkutano mmoja kwenye Jumba la Ufalme, na funzo likapangiwa. Mmoja wa Mashahidi mwenye malezi ya Kiislamu alimsaidia ajifunze yale ambayo Biblia inafundisha. Sasa amepata nguvu kutoka kwa Yehova ili kufuata kwa mafanikio kijia chenye kanuni nzuri. Yeye anafurahia kutumika akiwa mtumishi wa huduma naye anafanya mipango ili aingie katika huduma ya painia.
Kwa hiyo ukweli wa Ufalme unachanua katika Sri Lanka, na sasa kuna Mashahidi 1,086 katika bara hili zuri. Ukuzi huu unamaanisha kwamba vifaa zaidi vya tawi vinahitajiwa, na mahali pa tawi hilo panatafutwa. Pia akina ndugu wanajenga Majumba ya Ufalme mapya. Katika Puttalam kundi linalofanyizwa na jamaa 10 liliamua kujenga Jumba la Ufalme na kulijenga liwe kubwa vya kutosha kwa makusanyiko ya mzunguko. Jumba hilo lilimalizika kwa wakati kwa ajili ya kusanyiko la mzunguko, lililohudhuriwa na 107. Sasa kundi hilo limeongezeka maradufu, watu zaidi ya 75 wakihudhuria mikutano inayoongozwa katika Kitamil na Kisinhalese. Na kungali kuna nafasi kubwa kwa ukuzi zaidi.
Unabii wa Biblia uliotimizwa unaelekeza kwenye uhakika wa kwamba karibuni kila chozi la huzuni litapanguzwa kutoka macho yote kama alivyoahidi Mungu. Hata mawazo ya jeuri ya kikabila hayataingia moyoni kamwe. (Ufunuo 21:4; Isaya 65:17) Na katika “tone la chozi” la kisiwa chenye kupendeza, machozi ya shangwe yatatiririshwa matokeo ya tunda la kuamanika la Ufalme wa Mungu yanapoendelea kufurahiwa kwa umilele wote.