Je! Wewe Unathamini Mambo Matakatifu?
“Fuatieni amani pamoja na watu wote, na ule utakaso ambao bila huo hakuna mwanadamu atamwona Bwana, mkilinda kwa uangalifu . . . kwamba asiweko mwasherati wala mtu ye yote asiyethamini mambo matakatifu, kama Esau, ambaye kwa kubadilishana na mlo mmoja alitoa haki zake za kuwa mzaliwa wa kwanza zichukuliwe.”—WAEBRANIA 12:14-16, NW.
1. Ni ukosefu gani wa uthamini ambao wanadamu walio wengi wanaonyesha, lakini ni jinsi gani Wakristo walivyo tofauti?
YEHOVA Mungu wetu ni Mwandalizi mkarimu sana. Yeye anagawilia mahitaji ya uumbaji wake wote kwa wingi. Ingawa hivyo, walio wengi wa aina ya binadamu hawafikirii sana jambo hili. Wala wao hawapigii Yehova asante wala kukiri deni lao kubwa kwake. Wakristo, kwa upande ule mwingine, hawachukui wema wa Yehova kivivi-hivi. Wao wanamheshimu kwa ajili ya yale anayowafanyia. Kwa sababu ya bidii yao ya kujitolea yeye, Yehova ameitibarisha watu wake hesabu fulani ya mambo matakatifu yasiyofurahiwa na aina ya binadamu kwa ujumla. Haya ni mambo yenye thamani kubwa, yaliyowekwa kando kuwa matakatifu na yenye kuhusiana na ibada ya Yehova. Je! wewe unajua ni nini mambo haya matakatifu? Na je! wewe una uthamini wa kina kirefu, wenye kuhisiwa moyoni kwa ajili yayo?—Zaburi 104:10-28; Mathayo 5:45; Ufunuo 4:11.
2. Ni nani aliyeonyesha ukosefu wa uthamini wenye kuonekana wazi?
2 Si watu wote wa Mungu ambao wamethamini mambo matakatifu kwa njia inayofaa. Mathalani, Esau mwana wa Isaka alishindwa katika habari hii. Paulo alinena juu yake wakati alipoandikia Wakristo Waebrania wapakwa-mafuta. Baada ya kuwahimiza ‘wafuatie amani pamoja na watu wote,’ yeye aliwaonya wahakikishe kwamba katikati yao hangethibitika kuwako “mwasherati wala mtu ye yote asiyethamini mambo matakatifu, kama Esau, ambaye kwa kubadilishana na mlo mmoja alitoa haki zake za kuwa mzaliwa wa kwanza zichukuliwe.”—Waebrania 12:14-16, NW.
3, 4. Ni nini zilizokuwa haki takatifu za mzaliwa wa kwanza ambazo Esau aliuzia Yakobo kwa ajili ya bakuli moja la mchuzi?
3 Hizi haki za mzaliwa wa kwanza zilikuwa nini? Yehova aliahidi Abrahamu, babu ya Esau, kwamba kupitia yeye na wazao wake kuna mmoja ambaye angezaliwa awe ile Mbegu ya ahadi, Mesiya, au Kristo. Kwa njia ya Mbegu hii mataifa yote yangeweza kujibariki yenyewe, hiyo ikiyaongoza kukombolewa kutoka kwenye dhambi na kifo.—Mwanzo 22:15-18; Wagalatia 3:16.
4 Esau, mzaliwa wa kwanza wa Isaka, alikuwa na fursa ya kuwa sehemu ya ukoo ambao ungetokeza Mbegu hiyo. Hiyo ilikuwa sehemu ya haki yake ya uzaliwa. Lakini kwa aibu yake, kumbukumbu la maandishi ya Biblia linataarifu hivi: “Esau alidharau ile haki ya uzaliwa.” Kwa kiherehere yeye aliiuza kwa ajili ya mlo mmoja wa mchuzi wa dengu na mkate. Kwa uhakika, sisi hatutaki kuiga ukosefu wake wa uthamini. Badala ya hivyo, inatupasa sisi tukuze nia ile ya Yakobo, ndugu ya Esau. Ni yeye aliyefuata zamu ya kuwa katika ukoo wa haki ya uzaliwa, naye aliinunua kwa sababu ilionekana wazi kwamba ndugu yake alikosa uthamini. Hivyo Yakobo alihakikisha kwamba haki ya kuwa babu wa kale wa Mbegu iliyoahidiwa ilipitishwa mbele na mmoja aliyethamini kitu hiki kitakatifu kwa njia inayofaa.—Mwanzo 25:27-34.
5. Ni mambo matakatifu gani tutakayofikiria na ni jinsi gani sisi tunaweza kuepuka kuyachukua kivivi-hivi?
5 Ndani ya kundi la Kikristo, Yehova amefanya yapatikane mambo mengi matakatifu ili yatuendeleze tukiwa wenye imara kiroho na kutupa vifaa vya kutosha kwa ajili ya utumishi wake. Acheni tuzungumzie hesabu fulani ya mambo haya. Ndipo, sisi mmoja mmoja, tunaweza kutafakari juu yayo na kuimarisha uthamini wetu kwayo ili sisi tusije kamwe kuyachukua kivivi-hivi.
Jina la Yehova na Ukombozi —Ni Mambo Matakatifu Sana
6. Ni katika njia gani mbalimbali sisi tunaweza kuonyesha kwamba hatuchukui utakatifu wa jina la Yehova kivivi-hivi?
6 La kwanza katika orodha yetu ya mambo matakatifu ni jina la Yehova. Jina hili lina mtukuko wa jinsi gani katika akili na moyo wako wewe? Katika kutoa ile sala ya kielelezo, Yesu alisema hivi kwanza: “Acha jina lako litakaswe.” (Mathayo 6:9, NW) Wakati sisi tunapobatizwa, tunakuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. (Isaya 43:10, 11) Lo, ni heshima iliyoje! Na wakati sisi tunapoongea juu ya wema wa Yehova na makusudi yake makuu, wengine wanapata kumjua kwa jina lake la kibinafsi, na wao pia wanataka kumtumikia. Lakini ikiwa mmoja anapuuza kuongea juu yake au, kwa ubaya hata zaidi, anahusika katika kutenda kosa, hiyo inaleta suto juu ya jina jema na sifa ya Yehova. Mashahidi Wakristo wenye imani wa Yehova wanakazania sikuzote kutakasa jina takatifu lake mbele ya wengine kwa yale wanayosema na kutenda.—Walawi 22:31, 32; Kumbukumbu 5:11.
7. Kwa nini inatupasa sisi tuonyeshe uthamini wa upeo kwa ajili ya dhabihu ya ukombozi ya Kristo?
7 Lililo juu katika orodha ya mambo matakatifu ni dhabihu ya ukombozi. Dhabihu ya Kristo ni yenye thamani jinsi gani kwako wewe? Ni kwa kutegemea tu msingi wa imani kamili katika dhabihu hii kamilifu ya kibinadamu kwamba sisi tunaweza kusamehewa dhambi zetu. (1 Yohana 2:1, 2) Paulo ananena juu ya kundi lake lililopakwa mafuta kuwa “lilinunuliwa kwa damu ya Mwana [wa Mungu] mwenyewe.” (Matendo 20:28; linganisha 1 Petro 1:17-19, NW.) Yesu, Mwana-mzaliwa-pekee wa Mungu, aliacha cheo chake mbinguni, akaishi duniani miongoni mwa wanaume na wanawake wenye dhambi, na ndipo akatoa kabisa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu katika kifo chenye maumivu makali sana juu ya mti wa mateso ili sisi tuweze kuwa na uhai wa milele. (Mathayo 20:28) Mtu angekuwa na upeo wa ukosefu wa shukrani ikiwa hangeonyesha kila siku uthamini wa kina kirefu kwa ajili ya zawadi hii ya Mungu yenye thamani kubwa.—Waebrania 10:28, 29; Yuda 4, 5.
Uhusiano Wetu Pamoja na Yehova na Tengenezo Lake
8. Uhusiano wetu pamoja na Yehova ni wenye thamani kubwa jinsi gani?
8 Hii inatuleta kwenye jambo jingine lililo takatifu sana, uhusiano wetu pamoja na Yehova. Inatupasa sisi tutunze kwa upenzi mwingi usiri huu tulio nao pamoja na Baba yetu wa kimbingu. Ikiwa sisi ‘tunajivuta karibu na Mungu, yeye atajivuta karibu na sisi.’ (Yakobo 4:8, NW) Yeye anatupenda sana. Naye anatutaka tumpende kwa moyo wetu wote. (Mathayo 22:37, 38; Yohana 3:16) Daudi alimpa Sulemani mwanaye shauri timamu juu ya uhusiano wake pamoja na Yehova. Onyo moja lilitiwa ndani yalo: “Na wewe, Sulemani mwana wangu, jua yule Mungu wa baba yako na umtumikie ukiwa na moyo kamili na ukiwa na nafsi yenye kujaa upendezo; kwa maana Yehova anapekua mioyo yote, na yeye anatambua kila mwinamio wa ndani wa mawazo. Ikiwa wewe unamtafuta yeye, atajiacha yeye mwenyewe apatwe na wewe; lakini ikiwa wewe unamwacha, yeye atakutupa milele.” (1 Nyakati 28:9, NW) Kwa hiyo “jiendelezeni wenyewe katika upendo wa Mungu, huku ninyi mkiwa mnangojea ile rehema ya Bwana wetu Yesu Kristo kwa tazamio la uhai wa milele.”—Yuda 21, NW.
9. Ni katika njia gani mbalimbali sisi tunaonyesha kwamba hatuchukui kivivi-hivi lile pendeleo la kuwa sehemu ya tengenezo la Yehova?
9 Je! wewe unathamini pia ni pendeleo takatifu kama nini kuwa sehemu ya tengenezo la Yehova? Lazima sisi sote tukumbuke kwamba tumo ndani yalo kwa fadhili zisizostahiliwa tu za Yehova. Ikiwa mtu anathibitika kuwa asiyethamini na anakuwa mtenda kosa asiyetubu, yeye atapoteza pendeleo hili. Paulo alionya hivi: “Kwa hiyo anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.” (1 Wakorintho 10:6-12) Paulo alitoa onyo hili baada ya kusimulia juu ya Waisraeli 23,000 walioangamia kwa sababu ya ibada ya,sanamu na ukosefu wa adili. Sisi tunaweza kuonyesha uthamini wetu kwa ajili ya utakatifu wa tengenezo la Yehova kwa kila mmoja wetu kufanya sehemu yake ya kuliendeleza likiwa bila ukosefu wa usafi, ukosefu wa adili, mzozano, ubiashara, na hisia za kujiona bora kuliko wengine, na maoni mabaya ya kuhukumu watu kimapema. (2 Wakorintho 7:1; 1 Petro 1:14-16) Sisi tunaweza kuimarisha kifungo cha upendo wa kidugu huku tukiwa tunafuata kwa uangalifu utaratibu wa kitheokrasi na kuonyesha ushirikiano pamoja na wale wanaoongoza.—1 Wathesalonike 4:3-8; 5:12, 13.
Neno la Mungu, Sheria Zake, na Tumaini la Ufalme
10. Ni jinsi gani sisi tunaonyesha kwamba tunathamini kikamili Maandiko Matakatifu?
10 Neno la Mungu lenye uvuvio wake, Biblia Takatifu, ni takatifu pia. Hilo lina matamko rasmi ya kimungu, maagizo, mashauri, ahadi, mafunuo, ndiyo, mambo yote tunayohitaji ili ‘yatupe vifaa kwa ajili ya kila kazi njema.’ (2 Timotheo 3:16, 17, NW) Ni jinsi gani sisi tunavyoweza kuonyesha uthamini kwa ajili yalo? Kwanza, ni kwa kujifunza hilo na kutumia katika maisha zetu mambo tunayopata kujua. Halafu, kwa kutii ifaavyo ‘chakula kwa wakati unaofaa’ ambacho Yehova anaandaa kupitia “mtumwa mwenye imani na mwenye uangalifu.” (Mathayo 24:45, NW) Na kulingana na maoni yenye mafaa, sisi tunahitaji kuweka nakala zetu binafsi za Biblia, na pia vichapo vya Kikristo ambavyo tunatumia katika utendaji wetu wa kuhubiri, zikiwa nadhifu na safi. Huenda ikaleta suto kwa Yehova ikiwa sisi tunaenda nje kutoa ushuhuda na kutumia Biblia iliyochafuka-chafuka au isiyopendeza machoni.
11. Kwa nini haitupasi kuchukua kivivi-hivi sheria takatifu za Yehova?
11 Katika Neno la Yehova zimo sheria takatifu za Yehova. Je! sikuzote wewe unaziona kuwa takatifu, au wewe unaelekea nyakati nyingine kuzichukua kwa wepesi? Sheria za Yehova ni kama ishara, vitia-alama, na vizuizi vya usalama vilivyo kandokando ya sehemu kuu ya barabara inayoelekeza kwenye uhai. Ikiwa sisi tunazitii, tutasafiri kwa usalama na mwishowe tufike tunakoenda katika ulimwengu mpya wa Yehova; lakini ikiwa sisi tunachukua amri na vikumbusha vya Yehova kwa wepesi, sisi tunaelekea kwenye msiba.—Zaburi 119:10, 11, 35, 101, 102; Mithali 3:1-4, NW.
12. Ni jinsi gani tumaini letu la Ufalme lilivyo jambo takatifu?
12 Kupitia Biblia, sisi tunapata kujua pia juu ya jambo takatifu moja linalopasa kuwa la upenzi kwenye mioyo yetu: tumaini la Ufalme letu. Akinena juu ya Abrahamu mwaminifu, Paulo alisema kwenye Waebrania 11:10, NW: “Kwa maana yeye alikuwa anangojea jiji [Ufalme wa Mungu] lililo na misingi halisi, mjenzi na mfanyi wa jiji hilo akiwa ni Mungu.” Je! wewe una tumaini katika Ufalme wa Mungu, lililo imara na la kudumu kama hilo? Je! imani yako ina imara sana hivi kwamba moyo wako haukaribishi mashaka yo yote, na je! bidii yako inabaki bila kupungua unapokuwa ukingojea makusudi ya Mungu yatimizwe katika wakati wake unaofaa?—Mathayo 24:20-22, 33, 34, 42.
Mikusanyano na Mapendeleo Matakatifu
13. Kwa nini haitupasi kuchukua kivivi-hivi manufaa za mikutano ya Kikristo?
13 “Kuhimizana katika upendo na kazi nzuri; wala tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine,” akashauri Paulo. Hii inaonyesha kwamba mikutano ya Kikristo yetu ni uandalizi mwingine mtakatifu usio wa kuchukuliwa kwa wepesi. Kwenye mikutano, sisi tunapokea uagizo wa muhimu na uenzi mchangamfu tunaohitaji sana. Hapa sisi tunaweza pia kufanya “ungamo la tumaini letu” kwa kunena kutoka jukwaani kwa kadiri tupatavyo fursa, na kwa kutoa maelezo kwa ukawaida. (Waebrania 10:23-25) Na kwa kuwa Jumba la Ufalme ndipo panapofanyiwa mingi zaidi ya mikutano yetu, je! wewe unachanga michango kwa ukawaida na kufanya bidii ili kupadumisha ifaavyo?—Kutoka 35:21.
14. Ni nini kitakachotusaidia tuthamini kwamba huduma yetu ya Kikristo ni hazina takatifu?
14 Pendeleo ambalo Wakristo wanalo la kuzihubiri habari njema linafananishwa na Paulo na ‘hazina katika vyombo vya udongo.’ (2 Wakorintho 4:1, 7) Ndiyo, huduma ya Kikristo ni jambo takatifu pia ambalo sisi tunathamini kwa kina kirefu. Ingawa walio wengi wa wale tunaowahubiria ni wenye ubaridi, inatupasa tuendelee kujikumbusha wenyewe juu ya pendeleo lililotukuka tulilo nalo la kuambia wengine juu ya Yehova na makusudi yake. Hivyo sisi tutatimiza utume wetu wa kuzihubiri habari njema za Ufalme wa Mungu na kufanya wanafunzi. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Kutazama wanafunzi wapya wakifanya maendeleo ni kisababishi zaidi cha shangwe. (1 Wathesalonike 2:19, 20) Tukihazini huduma, sisi hatutakuwa wasio wa kawaida au wasio watendaji katika kuzitangaza habari njema.
15. Kwa nini utunzaji wa mapendeleo ndani ya tengenezo la Yehova si jambo la kuchukuliwa kwa wepesi?
15 Mapendeleo ndani ya tengenezo la Yehova ni matakatifu pia. Kwa kweli, mapendeleo hayo ni amana takatifu. (Linganisha Matendo 20:28.) Kama daraka lenyewe linahusisha ndani uangalizi, uchungaji, kufundisha, au utumishi fulani mwingine kwa Wakristo wenzetu, lipe uangalifu unaozidi ule wa kikawaida. Hata ikiwa furushi fulani la kikazi linaonekana kama lisilo la maana sana, usilichukue kwa wepesi, bali lifanye vizuri, bila kuchelewa, kama kwamba unafanyia Yehova. Kumbuka, “aliye mwaminifu katika lililo dogo sana, huwa mwaminifu katika lililo kubwa pia.”—Luka 16:10.
Ndoa na Jamaa
16. Ni katika njia gani mbalimbali sisi tunaweza kuonyesha kwamba tunafikiria ndoa na jamaa kuwa mambo matakatifu?
16 Katika kuorodhesha mambo matakatifu, usisahau kutia ndani ndoa na jamaa. Ni kweli kwamba watu wasio Wakristo wanafunga ndoa pia, lakini Wakristo wanaona ndoa kuwa takatifu, inayohusika katika ibada yao kwa Yehova. (Linganisha 1 Petro 3:1-7.) Ni jinsi gani wao wanavyoonyesha staha kwa jambo hili takatifu? Biblia inasema hivi kwenye Waebrania 13:4: “Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu.” Yesu alionya kwamba kuendelea kutazama mwanamke kwa kumfikiria-fikiria ili kuwa na harara kwa ajili yake kungekuwa sawa na kutenda uzinzi katika moyo. (Mathayo 5:27, 28, NW) Ikiwa wewe unachagua kufunga ndoa, fanya hivyo kwa njia yenye kuheshimika. Halafu usiichukue kamwe ndoa yako kivivi-hivi. Jenga upendo wa kweli na staha yenye kina kirefu kila siku. Ukiwa na watoto, ‘walee katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.’ Kwa njia hii jamaa yako itakuwa “takatifu.”—Waefeso 6:4; 1 Wakorintho 7:14, NW.
Roho Takatifu ya Yehova na Sala
17. Kwa nini sisi hatuwezi kuichukua kivivi-hivi roho takatifu ya Mungu?
17 Sisi tunahitaji yote ya maandalizi ya Yehova, na msaada mmoja ulio wa maana kutoka kwa Yehova ni roho takatifu yake. (Yohana 14:26) Si sikuzote ambapo sisi tunazijua njia ambazo Yehova anatumia roho takatifu yake kwa ajili yetu, lakini jambo moja ni hakika: Hatuwezi kusonga mbele bila hiyo. Inatupasa tusali kuomba roho takatifu itusaidie kuelewa mafundisho ya kweli na kuvumilia majaribu. Sisi tunaihitaji ili itusaidie kusitawisha matunda ya roho. (Wagalatia 5:22, 23, NW) Na tunaonywa kwenye Waefeso 4:30, NW, kwamba haitupasi ‘kuwa tukiitia kihoro’ roho takatifu, tukijihusisha ndani ya mambo yanayoizuia isitutiririkie. Sisi na tuithamini wakati wote roho takatifu ya Yehova.
18. Kwa nini sala ni pendeleo takatifu?
18 Jambo takatifu la mwisho tutakalozungumzia, sala, kwa uhakika silo lenye umaana mdogo zaidi. Ni pendeleo kubwa kama nini tulilo nalo la kuwasiliana pamoja na Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote mzima, Yehova! Kwa uwazi, inatupasa sisi tumfikie kwa staha, kwa kicho, si kamwe kwa kuchukua mambo kwa wepesi. Sisi tunaweza kuwa na uhakika wa kwamba yeye atatusikia na kujibu sala zetu zinazotolewa kwa upatano na mapenzi yake. “Msisumbuke juu ya jambo lo lote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-asante acheni mambo rasmi yenu yajulishwe kwa Mungu.” (Wafilipi 4:6, NW) Sala itatuendeleza tukiwa na uthamini wa mambo matakatifu.
19. Ni baraka gani zinazowajia wale wanaothamini mambo matakatifu ifaavyo?
19 Tumezungumzia mambo matakatifu 13 tu ambayo hatupaswi kamwe kuyachukua kivivi-hivi. Mengi zaidi yangeweza kutajwa. Ikiwa sisi tunathamini mambo hayo, tutaendeleza uhusiano mwema pamoja na Mungu wetu, Yehova, na kuwa na baraka yake ya kila siku. Hii inaleta amani ya akili iliyoje, pamoja na dhamiri njema! Usiuchukue uhusiano huo mwema hivivi-hivi kamwe! Penda Yehova kwa moyo wako wote, akili, nafsi, na nguvu, na sikuzote yeye atakupenda wewe. (1 Yohana 4:16) Hakuna kitu kinachoweza kuvunja kifungo hicho cha upendo isipokuwa ukosefu wa imani wako mwenyewe.—Warumi 8:38, 39.
20. Ni jinsi gani sisi tunaweza kutembea kwa mafanikio katika ile barabara inayoelekea kwenye uhai katika ulimwengu mpya wa Yehova?
20 Acheni sisi tuendelee kuwa wenye shughuli katika utumishi wa Ufalme pia, tukitunza vizuri mapendeleo yote na kuthamini maandalizi yote ya kiroho. Tukiwa na mioyo yenye kujaa shukrani wakati wote, sisi na tuwe chonjo kutii sheria na vikumbusha vyote vya Yehova vilivyo vitakatifu, tukithamini kwamba vimeandikwa ili kutuongoza kwa usalama katika ile barabara ya kuelekea kwenye uhai. Na, wakati tunapoendelea kutembea katika barabara hiyo nyembamba inayoelekea kwenye uhai, inaelekea kwamba licha ya Yehova kutuhifadhi hai tuipite ile dhiki kubwa atatupa uhai wa milele pamoja na baraka zisizo na mwisho katika ulimwengu mpya wake, ambao sasa uko karibu sana. Yote haya yatakuwa ni kwa sababu sisi tulithamini mambo matakatifu.
Ni Jibu Gani Ambalo Wewe Ungetoa?
◻ Ni jinsi gani sisi tunaweza kuepuka kuchukua jina la Yehova na dhabihu ya ukombozi kivivi-hivi?
◻ Ni jambo gani huenda likatokeza wazo la kwamba sisi hatuthamini uhusiano wetu pamoja na Yehova na tengenezo lake?
◻ Ni nini baadhi ya mambo yanayoonyesha uthamini wetu kwa Neno la Mungu na sheria zake, na tumaini la Ufalme?
◻ Ni jinsi gani sisi tunaweza kuonyesha kwamba hatuchukui mikutano ya Kikristo na mapendeleo ya kitheokrasi kivivi-hivi?
◻ Ni nini baadhi ya mambo matakatifu ya ziada ambayo kwa ajili yayo inatupasa tusitawishe uthamini wa kina kirefu?