Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Je! Yesu alikuwa akirejeza kwa Yuda alipomwambia Pilato kwamba: “Hii ndiyo sababu mwanamume aliyenipa mimi kwako ana dhambi kubwa”?—Yohana 19:11.
Haionekani kwamba Yesu alikuwa akirejeza kwa Yuda au mwanamume mwingine mahususi. Hesabu fulani ya wanaume wenye hatia walihusika katika matukio yaliyoongoza kwenye kuwa kwa Yesu mbele ya Pilato na kupatwa na kifo.
Yaelekea, Yuda anafikiriwa kwanza kwa sababu mtume huyo mfisadi aligeuka akawa msaliti. (Yohana 6:64, 71; 12:4-6) Yuda alikutana na makuhani wakuu, waliotaka “kumuua” Yesu. Walilipa Yuda vipande thelathini vya fedha ili amsaliti Yeye. (Luka 22:2-6) Basi, pasipo shaka, Yuda alikuwa na dhambi kubwa kuhusiana na kifo cha Yesu.
Lakini Yuda peke yake hakutokeza kifo cha Yesu. Kuhani mkuu Kayafa alikuwa amechochea wengine ili wafanye Yesu auawe. (Yohana 11:49, 50) Mathayo anasimulia kwamba mara “makuhani wakuu na Sanhedrini yote nzima” walipokuwa wamepasisha Yesu hukumu, walitenda kama kikundi: “Makuhani wakuu wote na wanaume wazee wa watu walifanya shauriano dhidi ya Yesu ili wamuue. Na, baada ya kumfunga yeye, wao waliongoza yeye na kumtoa kwa Pilato yule gavana.” (Mathayo 26:59-65; 27:1,2, NW) Zaidi ya hilo, baada ya Pilato kupata kwamba Yesu alikuwa hana hatia, “makutano” waliuliza Baraba afunguliwe. Kwa kutofautiana, kwa habari ya Yesu walipaaza sauti hivi: “Acheni yeye auawe!”—Mathayo 27:20-23; Yohana 18:40, NW.
Kwa hiyo yaelekea Yesu hakuwa akisema juu ya mtu mmoja mahususi alipomwambia Pilato: “Mwanamume aliyenipa mimi kwako ana dhambi kubwa.” (Yohana 19:11, NW) Ingawa Yuda, “mwana wa uharibifu,” alibeba hasa hatia kubwa, wengine wengi walishiriki hatia ya dhambi ya kumuua Yesu. (Yohana 17:12, NW) Hii ndiyo sababu katika siku ya Pentekoste mtume Petro aliwaambia Wayahudi watubu dhambi yao nzito dhidi ya Mwana wa Mungu. (Matendo 2:36-38) Wayahudi hao walikuwa sehemu ya taifa lililowekwa wakfu kwa Mungu wa Yesu, Yehova. Walikuwa na manabii yaliyomtambulisha Kristo akiwa Mesiya. Na wengi wao waliona miujiza ya Yesu. Kwa hiyo kwa hakika walikuwa na hatia zaidi ya dhambi kuliko afisa asiyekuwa Myahudi aliyemtangaza Yesu kuwa hana hatia.—Yohana 18:38.
■ Kulikuwa na maana gani Yehova kumwambia Ezekieli kwamba uso wake ungekuwa mgumu kama nyuso za Wayahudi?
Ezekieli alikuwa mnabii wa Mungu, aliyetumikia miongoni mwa Wayahudi ambao walikuwa wamechukuliwa mateka Babuloni. Yaelekea kwamba mateka hawa walifikiri kwamba kwa njia fulani Yehova angewaokoa upesi kwa sababu walikuwa watu wake wachaguliwa. Wao hawakukubali uhakika wa kwamba lililowapata lilitukia kwa sababu wao walistahili ukosefu wa upendeleo wake.
Kwa hiyo Yehova alipomwelekeza Ezekieli ‘awaambie maneno yangu,’ haukuwa mgawo mwepesi. Katika kutayarisha mnabii huyo, Mungu alionya kwamba “hawatakusikiliza wewe; kwa kuwa hawanisikilizi mimi; maana nyumba yote ya Israeli wana vipaji vigumu, na mioyo yenye ukaidi.”—Ezekieli 3:4, 7.
Kufikia hapo Mungu alimwambia Ezekieli: “Tazama niumeufanya uso wako kuwa mgumu juu ya nyuso zao, na kipaji cha uso chako kuwa kigumu juu ya vipaji vya nyuso vyao. Kama almasi ilivyo ngumu kuliko gumegume, ndivyo nilivyokifanya kipaji chako; usiwaogope.”—Ezekieli 3:8, 9.
Watu hao walikuwa wagumu na waasi. (Ezekieli 2:6) Je! wangeweza kushinda au kuogofya mjumbe wa Mungu? Hapana. Kwa kuwa aliungwa mkono na Mungu, Ezekieli hangekuwa mpole kuliko wao. Gumegume lilikuwa jiwe gumu sana, gumu kuliko chuma. Ikiwa Wayahudi washupavu, wasioitikia wangelinganishwa na gumegume, Ezekieli angekuwa hivyo pia. Hata zaidi, angekuwa kama almasi, jiwe lililo gumu sana kuliko mawe yote ni gumu sana hivi kwamba linaweza kutumiwa kukwaruza hata gumegume.—Yeremia 17:1,2.
Kwa hakika hilo halimaanishi kwamba watu wa Mungu leo wanapaswa kuliona kuwa jambo zuri kuwa wagumu, wasio wepesi kuona hisia za wengine, au hata wakali katika kufanya kile ambacho wanahisi kuwa sawa. Angalia yale ambayo mtume Petro alisihi kuhusu kushughulika na watu: “Mwe na akili iyo hiyo, mkionyesha hisia-mwenzi, mkiwa na shauku ya kidugu, wenye huruma nyororo, wanyenyekevu katika akili, msilipe umizo kwa umizo au tukano kwa tukano, bali, tofauti na hilo, mjaliwe na baraka.”—1 Petro 3:8, 9, NW.
Kuonyesha wengine huruma pia ni mojapo ya maelekeo ya kwanza katika kushiriki habari njema za Ufalme pamoja na wengine. (Mathayo 9:36-38) Lakini hata tunapokabili ubaridi, kukataliwa, au upinzani wa waziwazi, hatutakoma kutangaza ujumbe wa Mungu kwa wakati wetu. Hiyo inatia ndani kutangaza kwamba karibuni yeye ‘atawalipiza kisasi wao wasiomjua Mungu, na wao wasioitii Injili ya Bwana wetu Yesu.’ (2 Wathesalonike 1:6-9) Hatupasi kuogopa wala kushindwa. Katika maana hii tunaweza kuwa wenye ugumu kama ule wa almasi sawa na alivyokuwa Ezekieli.