Jenga Itibari Katika Yehova kwa Kujifunza Neno Lake kwa Bidii-Endelevu
“Elekezeni kabisa mioyo yenu kwenye maneno yote ambayo mimi ninanena kwa kuonya ninyi leo . . . Kwa maana hilo si neno lisilo na thamani kwenu ninyi, bali hilo linamaanisha uhai wenu.”—KUMBUKUMBU 32:46, 47. NW.
1, 2. (a) Ni tazamio gani lililokabili Israeli walipokuwa wakipiga kambi katika nyanda za Moabu? (b) Ni himizo gani ambalo Musa alilipa taifa hilo?
MKAO wao mrefu jangwani ulikuwa umekaribia mwisho. Sasa ni Yordani wenye kujipinda-pinda tu ambao ulitenganisha taifa lile na Bara Lililoahidiwa walilolingojea muda mrefu. Hata hivyo, kwa kiongozi wa taifa hilo, Musa, tazamio la Israeli kuingia katika bara hilo kulitokeza mafikirio mazito. Yeye angeweza kukumbuka jinsi taifa lilivyokuwa limejikwaa wakati mmoja kwa sababu ya ukosefu walo wa itibari katika Yehova na hivyo likawa limenyimwa mwingio katika Kanaani.—Hesabu 13:25–14:30.
2 Hivyo Musa aliliita pamoja taifa hilo katika nyanda za Moabu zenye miinuko na vibonde. Baada ya kuipitia historia yao ya kitaifa na kurudia-rudia Sheria ya Mungu, Musa alitokeza kile ambacho kimeitwa insha yake iliyo bora zaidi. Kwa usemi wa ushairi bora kabisa, yeye alihimiza Israeli waitibari na kutii Yehova, “Mungu wa uaminifu, ambaye kwake hakuna ukosefu wa haki; mwadilifu na mnyoofu ni yeye.” Katika umalizio, Musa alihimiza hivi: “Elekezeni kabisa mioyo yenu kwenye maneno yote ambayo mimi ninanena kwa kuonya ninyi leo, kwamba ninyi mpate kuamuru wana wenu kufanya uangalifu kutenda maneno yote ya sheria hii. Kwa maana hilo si neno lisilo na thamani kwenu ninyi, bali linamaanisha uhai wenu.”—Kumbukumbu 32:4, 46, 47, NW.
‘Kuelekeza Kabisa Mioyo Yao’ Kwenye Neno la Mungu
3, 4. (a) Waisraeli walipaswa ‘kuelekeza kabisa mioyo yao’ kwenye kitu gani, na hiyo ilihusisha nini ndani? (b) Vizazi vya baadaye vilitumia shauri la Musa jinsi gani?
3 Musa aliwaonya Waisraeli kwa upole ‘waelekeze kabisa mioyo yao’ si kwenye wimbo wake wenye kusisimua tu, bali kwenye miandiko yote mitakatifu. Ilikuwa lazima wao ‘wafanye usikizi mwema’ (Knox), ‘wawe na uhakika wa kutii’ (Today’s English Version), au ‘watafakari juu ya’ (The Living Bible) Sheria ya Mungu. Ni kwa kujifahamisha nayo sana sana tu kwamba wangeweza ‘kuamuru wana wao wafanye uangalifu kutenda maneno yote ya sheria hii.’ Kwenye Kumbukumbu 6:6-8, NW, Musa aliandika hivi: “Maneno haya ambayo mimi ninaamuru wewe leo ni lazima yathibitike kuwa juu ya moyo wako; na ni lazima wewe uyakaze kikiki katika mwana wako . . . Na ni lazima wewe uyafunge yakiwa ishara juu ya mkono wako, na ni lazima yatumike kuwa kifungio cha mbele kati ya macho yako.”
4 Mwelezaji wa Biblia W. H. Davey anaeleza juu ya jinsi katika nyakati za baadaye, maneno haya “yalifasiriwa kihalisi na Wayahudi, na ule mwelekezo uliomo ukageuzwa kuwa wa matumizi ya kishirikina. Mistari fulani . . . iliandikwa juu ya hati ya ngozi ya kondoo au mbuzi, na kuvaliwa juu ya mkono na kipaji cha uso wakati wa sala.” Vifuko vidogo vyenye maandiko vilivyopambwa sana, au filaktari (hirizi za ulinzi), vilivaliwa wakati wa Yesu na bado vinatumiwa na mafarakano fulani ya Kiyahudi leo. (Mathayo 23:5) Lakini, Davey anaongezea hivi: “Wanadamu kwa upumbavu wao walijiridhisha wenyewe kwa kwenda-kwenda huku na huko wakiwa wamevaa miilini mwao nakala ya maneno matupu tu ya sheria, badala ya kuonyesha wazi katika maisha zao kwamba wanashika ile amri iliyo humo.”
5. Ni nini uliokuwa utumizi unaofaa wa maneno ya Musa kwenye Kumbukumbu 6:6-8?
5 Sivyo, Sheria ya Mungu haikupasa kukaa juu ya mikono yao halisi wala vipaji vya nyuso halisi bali ‘juu ya mioyo yao.’ Kwa kupata si maarifa juu yayo tu bali pia uthamini wenye kina kirefu kwa maarifa hayo, ndipo Sheria hiyo ingewekwa ikionekana wazi, kama kwamba imeandikwa juu ya ubao mbele ya macho yao au imefungwa juu ya mikono yao.
Maandalizi ya Kujifunzia Sheria ya Mungu
6, 7. (a) Ni maandalizi gani ambayo Yehova alitoa kufanya Waisraeli wajifahamishe Sheria ya Musa? (b) Huenda ikawa pia iliwezekana jinsi gani watu wa Mungu katika nyakati za kale kuagizwa katika Neno la Mungu?
6 Ingawa hivyo, Waisraeli wangeweza jinsi gani kujifunza zile sheria-katiba za Sheria zipatazo 600? Nakala zayo bila shaka zilikuwa haba hapo kwanza. Mfalme wa wakati ujao wa Israeli alipaswa ‘kuandika katika kitabu kwa ajili yake mwenyewe nakala ya sheria hii, na ni lazima yeye asome katika hiyo siku zote za maisha yake, ili kwamba yeye apate kujifunza kuhofu Yehova Mungu wake ili kushika maneno yote ya sheria hii.’ (Kumbukumbu 17:18, 19, NW) Mungu alipanga ili Sheria hiyo isomwe kila mwezi wa saba kwenye Sikukuu ya Vibanda. (Kumbukumbu 31:10-13) Ingawa bila shaka pindi hiyo ilikuwa yenye kuburudisha, ilikuwa haitokei-tokei mara nyingi iweze kutia ndani ya watu maarifa ya kina kirefu.
7 Yehova alipanga pia kabila la Lawi liwe ‘likimwagiza Yakobo katika maamuzi ya kihukumu ya Mungu na Israeli katika sheria ya Mungu.’ (Kumbukumbu 33:8, 10; linganisha Malaki 2:7, NW.) Katika pindi fulani-fulani, Walawi waliendesha kampeni za kufundisha ambazo zilitumikia taifa zima. (2 Nyakati 17:7-9; Nehemia 8:7-9) Inaonekana kwamba, baada ya muda, angalau visehemu vya Neno la Mungu vilikuwapo pia ili watu kwa ujumla wawe navyo.a Kwa sababu hiyo, mtunga zaburi angeweza kuandika hivi: “Mwenye furaha ni mtu yule . . . [ambaye] upendezo wake ni katika sheria ya Yehova, na katika sheria yake yeye anasoma kwa sauti ya chinichini mchana na usiku.” (Zaburi 1:1, 2, NW) Hivyo himizo la Musa ‘kuelekeza kabisa mioyo yao kwenye Neno la Mungu’ lilikuwa kama amri ya kujifunza Biblia kwa bidii-endelevu.
‘Kuelekeza Kabisa Mioyo Yetu’ Kwenye Neno la Mungu Leo
8. Waisraeli walisikiza himizo la Musa kwa kadiri gani, na kwa matokeo gani?
8 Israeli hawakutii himizo la Musa. Wakati taifa lilipoanzisha umaliki wao hatimaye, inaonekana wazi kwamba walio wengi wa wafalme walo ‘hawakujiandikia wao wenyewe nakala ya ile sheria na kusoma katika hiyo siku zote za maisha zao.’ Kufikia karne ya saba K.W.K., katika siku za Mfalme Yosia, “kitabu kile chenyewe cha sheria” kilikuwa ni kama tu kimepotea kabisa. (2 Wafalme 22:8-13, NW) Bila shaka kielelezo kibaya kwa upande wa viongozi wa taifa kiliharakisha mtumbukio wa taifa katika uasi-imani. Kwa kupatana na onyo la Musa, kweli msiba wa kitaifa ulitukia katika 607 K.W.K.—Kumbukumbu 28:15-37; 32:23-35.
9. Ni jinsi gani hali ya Wakristo leo inavyofanana na ile ya Waisraeli wa kale?
9 Kama Waisraeli wa kale, leo Wakristo wamesimama kwenye mpaka wa bara lililoahidiwa—ulimwengu mpya wa Mungu ulio mwadilifu. (2 Petro 3:13) Matukio ya kugutusha yanarundamana mbele kwenye upeo wa macho: lile tangazo la “amani na usalama,” anguko la “Babuloni Mkuu,” shambulio la ‘Gogu Wa Magogu.’ Matukio haya yatatia itibari yetu katika Yehova kwenye mtihani. Basi, ni jambo la haraka kwamba sisi ‘tuelekeze kabisa mioyo yetu kwenye neno la Mungu’ sasa!—1 Wathesalonike 5:3; Ufunuo sura ya 18; Ezekieli sura ya 38, NW.
10. Ni kwa nini huenda watu fulani wakalegea katika funzo la kibinafsi?
10 Hata hivyo, kufanya jambo hilo kunaweza kuwa mwito halisi wa ushindani katika hizi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1, NW) Kazi ya kimwili, malezi ya watoto, shule, na madaraka ya kundi yanaweza yote kutokeza madai makubwa juu ya wakati wetu. Tokeo ni kwamba, huenda sisi tukawa na elekeo la kujitolea udhuru na kulegea katika funzo letu la Biblia, tukiwaza kwamba ‘Mimi nafanya kiasi kinachotosha kuniwezesha kusonga mbele.’ Hata hivyo, Biblia inahimiza Wakristo hivi: “Fikiria sana vitu hivi; vama ndani yavyo.” (1 Timotheo 4:15, 16, NW) Acheni sisi tufikirie sasa sababu fulani zenye nguvu za kufanya hivyo.
Kuutia Imara Uhusiano Wetu Pamoja na Mungu
11, 12. (a) Kupata maarifa ya ndani zaidi juu ya Mungu kuliathiri Ayubu jinsi gani? (b) Kwa nini njozi yetu juu ya Mungu inaweza kuwa wazi zaidi ya ilivyokuwa katika siku ya Ayubu?
11 Ayubu alikuwa mmoja ‘mwenye kuhofu Mungu na mwenye kugeuka kando kutoka kwenye ubaya.’ Lakini baada ya Yehova kuzidi kujifunua katika dhoruba-upepo, Ayubu angeweza kusema hivi: “Nilikuwa nimesikia habari zako, kwa kusikia kwa masikio; bali sasa jicho langu linakuona.” (Ayubu 1:1; 42:5) Je! sisi leo tunaweza ‘kuona’ Mungu, yaani, kufanya zaidi ya kufahamiana naye kijuu-juu tu, kujua kwa undani zile nyuso nyingi za utu wake? Tunaweza kweli kweli! Kupitia kurasa za Biblia, Yehova amefunua mengi juu yake mwenyewe kuliko yale yaliyojulikana hata na Ayubu.
12 Sisi tuna rai iliyo wazi zaidi juu ya kina cha upendo wa Mungu, tukijua kwamba yeye “aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee.” (Yohana 3:16) Kupitia manabii ya Biblia, sisi tuna mpangilio wa utendaji wa Mungu—moja kwa moja mpaka kwenye mwisho wa ile Mileani! (Ufunuo, sura 18-22) Sisi tuna kumbukumbu lenye maandishi kuhusu shughuli za Mungu pamoja na kundi la Kikristo: kuleta ndani watu wasio Wayahudi, kuweka kwake “mtumwa mwaminifu na mwangalifu” alishe watu wake, kuita kwake “mkutano mkubwa” wenye tumaini la kuishi milele katika Paradiso duniani. (Mathayo 24:45; Ufunuo 7.9, 14-17; Waefeso 3:3-6) Baada ya kuchungulia yale mambo yenye kina kirefu ya Mungu na kufikiri sana juu ya kazi za ajabu ambazo amefanya kwa ajili yetu, sisi tunalazimika kupaaza mshangao huu: “Jinsi zilivyo kuu utajiri na hekima na maarifa ya Mungu!”—Warumi 11:33.
13. Ni jinsi gani sisi tunaweza ‘kutafuta Mungu,’ na ni nini manufaa za kufanya hivyo?
13 Mtunga zaburi alisema: “Kwa moyo wangu mzima mimi nimekutafuta wewe.” Sisi tunaweza kutenda hivyo hivyo kwa kufanya mfikirio wa kila siku wa habari za Kimaandiko; hiyo inasaidia sana kuimarisha kifungo cha uhusiano wetu pamoja na Yehova. Funzo la bidii-endelevu linasaidia pia kufanya njia yetu iwe ‘iliyoimarika kwa uthabiti kushika virekebi-rekebi vya Mungu.’—Zaburi 119:5, 10, NW.
Funzo Hutusaidia Kukinga Imani Yetu
14. Toa kielezi juu ya thamani ya kuwa ‘tayari kufanya kinga’ ya tumaini letu la Kikristo.
14 “Mimi siwataki ninyi Mashahidi katika nyumba yangu!” akasema mwanamume mmoja Mghana akiwaambia wawili waliofika kwenye maskani yake. Zaidi ya hilo yeye aliwagombeza vikali Mashahidi kwa “kutokubali kutiwa damu mishipani na kutosalimu bendera ya taifa.” Vipingamizi hivyo vinakabiliwa kikawaida katika huduma ya shambani. Lingekuwa suto na mnyenyekezo kama nini kama hatungeweza “kufanya kinga mbele ya kila mmoja ambaye anadai kutoka kwenu ninyi sababu ya tumaini lililo ndani yenu ninyi”! (1 Petro 3:15, MW) Kwa nasibu, Mashahidi hawa waliweza kutumia Biblia kwa matokeo mazuri kueleza rai inayofaa juu ya damu na jinsi Mkristo anavyosawazisha staha ya vifananishi vya taifa na kuepuka kwake ibada ya sanamu. Tokeo likawa nini? Mwanamume huyo alivutiwa na majibu yao ya moja kwa moja. Leo, yeye na mke wake pia ni Mashahidi waliobatizwa.
15. Ni jinsi gani funzo la kibinafsi linavyotuweka sisi tayari kwa ajili ya huduma yetu?
15 Paulo anahimiza hivi: “Fanya yote yote uwezayo kujiweka mwenyewe mbele za Mungu katika hali ya kukubaliwa, mfanyi kazi asiye na lo lote la kuaibikia, ukitumia lile neno la ukweli sawasawa.” Funzo la kibinafsi litatusaidia si kubaki tu kwenye kijia cha uhai sisi wenyewe bali pia ‘kuwa na uwezo wa kutosha, tayari kabisa’ kusaidia wengine watende hivyo.—2 Timotheo 2:15; 3:17, NW.
Kukinza Mitego ya Shetani
16. Ni nini baadhi ya mitego ya Shetani inayokabili watu wa Yehova?
16 Leo, utangazaji unatuvamia kwa kuvutia-vutia “tamaa ya mnofu na tamaa ya macho na wonyesho mshaufu wa mali za maisha za mtu.” (1 Yohana 2:16, NW) Ukosefu wa adili katika ngono unatukuzwa na vyombo vya habari na unaendelezwa mara nyingi na wafanya kazi na wanashule wenzetu. Vitabu vya uchochezi wa kuasi imani huenda vikaletwa kwenye maskani zetu kwa njia ya posta bila sisi kuviomba. Kwa kuamshwa udadisi wao, ndugu fulani wamesoma habari hizo zenye kuchafua—kwa uangamivu wa imani yao. Pia kuna ile “roho ambayo inatenda kazi sasa katika wana wa kutotii,” ya ubinafsi na ya kufuata mambo ya mnofu. Ni rahisi kama nini kuambukizwa nayo na kusitawisha roho ya mwelekeo hasi, ya kuchambua-chambua mambo!—Waefeso 2:2, NW.
17, 18. Ni jinsi gani funzo la kibinafsi linavyoweza kutuzuia ‘kupeperukia mbali’?
17 Bila shaka, si watu wengi wanaojiondokea wenyewe ili wakatiwe na Shetani katika mtego. Bali, kwa kutojali funzo la kibinafsi, kama mashua iliyofunguliwa minyororo, wao ‘wanapeperukia mbali’ pole kwa pole na kuwa shabaha za kushambuliwa na Shetani. (Waebrania 2:1, NW) Mathalani, ndugu mmoja kijana alikuja kuhusika kwa njia isiyo ya adili pamoja na msichana mmoja shuleni. “Mimi niligundua,” yeye anakumbuka, “kwamba kisababishi kikuu cha jambo hili kilikuwa uhakika wa kwamba nilikuwa ninakufa njaa kiroho. Mimi sikufanya funzo la kibinafsi. Hiyo ndiyo sababu sikuweza kupinga kishawishi hicho.” Hata hivyo, programu ya funzo la kibinafsi ilisaidia ndugu huyo kuwa imara kiroho.
18 Shetani amepiga moyo konde aharibu wengi wa watu wa Mungu kwa kadiri awezayo. Kwa kulisha akili yetu daima mambo mema yanayotokana na Neno la Mungu na wakili wake mwaminifu, sisi tunaweza kuepuka kutiwa katika mtego. (Wafilipi 4:8) Vikumbusho vya kuepuka ufuatiaji wa vitu vya kimwili, ukosefu wa adili katika ngono, fikira za uasi imani, na roho ya mwelekeo hasi ni tele katika Biblia na pia katika vichapo vya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi. Tukifanya uangalifu unaozidi ule wa kikawaida, sisi hatutapeperukia mbali kamwe.
Maandalizi Kutokana na Tengenezo la Yehova Ili Kutusaidia
19. Yule towashi Mwethiopia anatoa kielezi cha jambo gani juu ya uhitaji wetu wa mwongozo wa kiroho?
19 Funzo ni kazi ngumu. Kwa hiyo sisi tunaweza kushukuru kwamba tengenezo la Yehova linatupa usaidizi mwingi. Katika miaka ya majuzi kuna wengine ambao wamedai kwamba watu mmoja mmoja wanapaswa kuruhusiwa wajifasirie wenyewe maana ya Biblia. Hata hivyo, yule towashi Mwethiopia alikiri wazi uhitaji wake wa mwongozo wa kiroho. Kwa maana alikuwa mwongofu asiyetahiriwa, bila shaka yeye alikuwa na maarifa ya kadiri fulani juu ya Biblia. Ule uhakika wenyewe wa kwamba alikuwa akijaribu kujifunza kitu kilicho cha kina kirefu kama unabii wa Isaya 53 unaonyesha hivyo. Hata hivyo, alipoulizwa kama alielewa aliyokuwa akisoma, yeye alikubali wazi hivi: “Nitawezaje kuelewa, mtu asiponiongoza?”—Matendo 8:26-33.
20. (a) Ni nini baadhi ya maandalizi ambayo tengenezo la Yehova limefanya kutusaidia katika funzo letu la kibinafsi la Biblia? (b) Wewe unahisi jinsi gani juu ya maandalizi hayo?
20 Watu wa Yehova leo wanahitaji vivyo hivyo mwongozo wa kiroho. Kwa kutamani “kunena kwa mwafaka” wakati mambo ya kiroho yanapohusika, wao wanakaribisha msaada unaotolewa na tengenezo la Yehova—na huo ni msaada mkubwa kama nini! (1 Wakorintho 1-10, NW) Sisi tunapata mtiririko-habari wa daima kupitia magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Tuna vitabu vingi sana na broshua zinazozungumzia vichwa mbalimbali vya habari za Biblia. Wasomaji wa Kiingereza hasa wamebarikiwa kuwa na Watch Tower Publications Index 1930-1985, chombo kinachoweza kusaidia mtu ‘afulize kutafuta hekima kama kutafuta fedha na kama kutafuta hazina iliyofichwa.’—Mithali 2:2-4, NW.
21. (a) Ni jinsi gani mtume Paulo alivyodhihirisha upendezi katika funzo la kibinafsi? (b) Ni nini baadhi ya madokezo ya kurahisisha funzo la kibinafsi?
21 Je! wewe unajifaidi kikamili na vichapo vya Sosaiti kwa kuvitumia kwa ajili ya funzo na utafiti? Au vichapo hivyo vinakuwa kidogo ni kama vitu vya kupambia rafu ya vitabu? Jambo la kupendeza ni kwamba, mtume Paulo alimwagiza Timotheo wakati mmoja ‘alete zile hatikunjo, hasa zile ngozi’ kwake kule Roma; kwa uwazi, Paulo alikuwa akirejeza kwenye visehemu vya Maandiko ya Kiebrania. (2 Timotheo 4:13, NW) Bila shaka yeye alivitaka viwe karibu mkononi ili virahisishe funzo na utafiti. Ikiwa wewe hujafanya hivyo, kwa nini usianze kujikusanyia maktaba yako mwenyewe ya vichapo vya kitheokrasi ili kwamba uweze kufanya utafiti? Weka vichapo hivyo katika hali ya kupatikana kwa urahisi, katika utaratibu, unadhifu, na usafi. Weka kando mahali pa kujifunza penye utulivu na mwangaza wa kutosha. Ratibisha nyakati za ukawaida za funzo la kibinafsi.
22. Kwa nini ‘kuelekeza kabisa mioyo yetu kwenye neno la Mungu’ ni kwa maana leo kuliko katika wakati mwinginewo wote?
22 Kama vile Waisraeli wenye kupiga kambi katika nyanda za Moabu zenye rutuba, sisi tumesimama kwenye ukingo wa ulimwengu mpya. Zaidi ya wakati mwinginewo wote, sisi tunahitaji kujifunza Neno la Mungu kwa bidii-endelevu na ‘kununua kabisa wakati wenye fursa’ ili kujifunza, labda tukidhabihu mapendezi mengine, kama vile kutazama televisheni. (Waefeso 5:16, NW) “Fanyizeni mtamanio wa yale maziwa yasiyotoholewa ya lile neno,” anahimiza Petro, “ili kwamba kupitia hayo mpate kukua” si kufikia ukomavu tu bali “kufikia wokovu.” (1 Petro 2:2; linganisha Waebrania 5:12-14, NW.) Uhai wetu wenyewe unahusika. Kwa hiyo kinza elekeo lo lote la kulegea katika funzo la kibinafsi. Litumie kama njia ya kuongeza kina cha upendo wako kwa Mungu na itibari yako katika yeye; hiyo pia ni njia ya kuongeza kimo cha uthamini wako kwa tengenezo analotumia kutusaidia. Ndiyo, ‘elekeza kabisa moyo wako’ kwenye Neno la Mungu, kwa bidii-endelevu, kwa ukawaida. “Hilo si neno lisilo na thamani kwenu ninyi, bali hilo linamaanisha uhai wenu.”
[Maelezo ya Chini]
a Vigae vya vyungu vilivyovunjika vilitumiwa sana katika nyakati za Biblia kuwa mahali pa kuandikia pasipo pa bei kubwa. Inasema hivi International Standard Bible Encyclopedia (1986): “Vigae vya vyungu vilivyovunjika vingeweza kutumiwa hata na tabaka zilizo za umaskini kabisa, ambazo hazingeweza kupata kitu kinginecho chote cha kuandikia.” Haijulikani ni kwa kadiri gani vigae vya vyungu vilivyovunjika vilitumiwa na Waisraeli wa kale kuandika maandiko ya Biblia. Ingawa hivyo, jambo la kupendeza ni kwamba vigae vya vyungu vilivyovunjika vya karne ya saba W.K., vyenye maandiko ya Biblia, vimegunduliwa katika Misri, hiyo ikidokeza njia moja ambayo watu wa kikawaida waliweza kuwa na visehemu vya Biblia.
Mambo ya Kupitia
◻ Kwa nini Musa alihimiza Waisraeli ‘waelekeze kabisa mioyo yao kwenye Neno la Mungu,’ nao wangefanya hivyo jinsi gani?
◻ Ni jinsi gani funzo la kibinafsi linavyoimarisha uhusiano wetu pamoja na Mungu na kutusaidia tukinge imani yetu?
◻ Ni fungu gani ambalo funzo la kibinafsi linatimiza katika kukinza kwetu mitego ya Shetani?
◻ Tengenezo la Yehova limefanya maandalizi gani ili kurahisisha funzo letu la Neno la Mungu?
[Picha katika ukurasa wa 11]
Badala ya kuandika sheria ya Mungu juu ya mioyo yao, Wayahudi waliifunga juu ya vifuko vyenye maandiko